Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kukopesha na Kukopa Kati ya Marafiki
    Amkeni!—1999 | Aprili 8
    • Kukopesha na Kukopa Kati ya Marafiki

      “ASIYE HAKI HUKOPA WALA HALIPI, BALI MWENYE HAKI HUFADHILI, HUKIRIMU.”—ZABURI 37:21.

      “USIWE mkopaji wala mkopeshaji; kwa sababu mara nyingi fedha hupotea na urafiki kuharibika.” Akaandika William Shakespeare mwandishi Mwingereza wa tamthilia, aliporudia kutaja ile hekima ya muda mrefu. Kwa hakika, ni mambo machache sana katika mahusiano ya kibinadamu ambayo huelekea kuzusha ugomvi kama ukopaji au ukopeshaji wa fedha. Hata kukiwa na mipango madhubuti na mielekeo iliyo minyoofu kabisa, sikuzote mambo hayawi kama yalivyotarajiwa.—Mhubiri 9:11, 12.

      Huenda hali zikatokea ambazo hufanya iwe vigumu au hufanya isiwezekane kwa mkopaji kutimiza wajibu wake. Au huenda mkopeshaji akahitaji zile fedha alizozikopesha kwa sababu ya hali ya ghafula. Mambo kama hayo yatokeapo, urafiki na mahusiano yaweza kuhatarishwa, sawa na alivyosema Shakespeare.

      Bila shaka, huenda mtu akawa na sababu halali za kukopa kiasi fulani cha fedha. Huenda mtu akaona ukopaji kuwa njia pekee ya kupata msaada, anapokabiliwa na tatizo la kifedha lililosababishwa na kugharimia aksidenti mbaya au kufutwa kazi. Biblia hutia moyo wale walio na uwezo wawasaidie wale walio na uhitaji ikiwa katika uwezo wa mkono wao kufanya hivyo. (Mithali 3:27) Huenda hili likatia ndani kukopesha fedha. Ingawa hivyo, Wakristo wanaoingia katika mpango wa namna hiyo wanapaswa kuonaje wajibu wao?

      Kanuni za Kufikiria

      Biblia si kitabu kinachotoa mwongozo wa mambo ya kifedha. Haizungumzii mambo yote yanayohusika katika ukopaji na ukopeshaji. Mambo kama vile kutoza au kutokutoza riba na kiasi cha riba kinachoweza kutozwa huachiwa wale wanaohusika.a Hata hivyo, Biblia huandaa kanuni zenye upendo na zilizo wazi, ambazo zapaswa kuongoza mitazamo na tabia ya mtu yeyote anayekopa au kukopesha.

  • Kukopesha na Kukopa Kati ya Marafiki
    Amkeni!—1999 | Aprili 8
    • Mkopeshaji

      Ingawa wajibu ulio mkubwa ni wa mkopaji, pia kuna kanuni zinazomhusu mkopeshaji. Biblia yaonyesha kwamba ikiwa tuna uwezo wa kuwasaidia wenye uhitaji, twapaswa kufanya hivyo. (Yakobo 2:14-16) Lakini hiyo haimaanishi kwamba mtu awaye yote ana wajibu wa kukopesha fedha, hata kama anayeomba ni ndugu wa kiroho. “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha,” yasema Biblia.—Mithali 22:3.

      Anapotambua na kuelewa hatari halisi za ukopaji na ukopeshaji, mtu mwenye utambuzi atafikiria kwa uangalifu mikopo yoyote ambayo huenda akaombwa. Je, ombi hilo ni halali? Je, yule anayeomba amefikiria kwa uangalifu jambo hilo? Je, yule anayekopa ana utaratibu mzuri na sifa njema? Je, yuko tayari kutia sahihi hati inayoonyesha masharti ya mapatano hayo? (Linganisha Yeremia 32:8-14.) Je, kwa kweli yuko tayari kulipa?

      Hii haidokezi kwamba Mkristo hapaswi kumpa mkopo mtu aliye na uhitaji na ambaye yaonekana huenda asiweze kulipa. Wajibu wa kibinafsi wa Mkristo kuelekea watu wengine unapita ule wa shughuli za kibiashara. “Yeyote yule aliye na njia ya ulimwengu huu ya kutegemeza maisha na amwona ndugu yake akiwa na uhitaji na bado amfungia mlango wa huruma zake nyororo, ni katika njia gani kumpenda Mungu hukaa katika yeye?” auliza mtume Yohana. Ndiyo, ni lazima Wakristo waonyeshe ‘upendo, si katika neno wala kwa ulimi, bali katika kitendo na kweli.’—1 Yohana 3:17, 18.

      Katika visa fulani mtu aweza kuamua kutomkopesha fedha ndugu yake mhitaji. Huenda akapendelea kumpa zawadi au kumpa msaada wa namna nyingine. Katika kuonyesha roho iyo hiyo, huenda mkopeshaji akatenda kwa rehema matatizo yanapozuka katika shughuli ya kutoa mkopo. Huenda akapenda kuzingatia kubadilika kwa hali ya mkopaji na kuongeza muda wa malipo ya deni, au akapunguza malipo, au hata kufuta hilo deni kabisa. Haya ni maamuzi ya kibinafsi ambayo lazima kila mtu ajifanyie.

      Lazima Wakristo wakumbuke kwamba Mungu anaona kila jambo na kwamba tutatoa hesabu ya jinsi ambavyo tunajiendesha wenyewe na kwa njia ambayo tunatumia mali zetu. (Waebrania 4:13) Shauri la Biblia la kuacha ‘mambo yetu yote yatendeke kwa upendo’ bila shaka linatumika katika kukopesha na kukopa kati ya marafiki.—1 Wakorintho 16:14.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki