-
Jinsi Tunavyoonyesha Tunampenda MunguMnara wa Mlinzi—2004 | Machi 1
-
-
Jinsi Tunavyoonyesha Tunampenda Mungu
KUSITAWISHA upendo kwa Mungu hakumaanishi kujifunza tu kumhusu. Kama watumishi wa Mungu duniani wanavyoweza kushuhudia, upendo wa kweli kwa Mungu hukua mtu anapojua utu wake, na hata huwa wenye nguvu zaidi anapofahamu matakwa yake na mambo ambayo yeye hupenda na kuchukia.
Kwa upendo, Yehova ametupatia Neno lake, Biblia, naye hujifunua kupitia Neno hilo. Kutokana na Biblia, tunajifunza jinsi Yehova alivyoshughulika na hali mbalimbali. Kama vile tu barua kutoka kwa mpendwa hutufurahisha, vivyo hivyo Biblia hutufurahisha inapotufunulia mambo mapya kuhusu utu wa Yehova.
Hata hivyo, nyakati nyingine tunapokuwa katika huduma ya shambani tunaona kuwa si lazima mtu aanze kumpenda Mungu kwa kuwa tu amejifunza juu yake. Yesu alisema hivi kuhusu Wayahudi fulani wasio na uthamini wa siku zake: “Ninyi mnayachunguza Maandiko, kwa sababu mnafikiri kwamba kwa njia yake mtakuwa na uzima wa milele; . . . lakini ninajua vizuri kwamba ninyi hammpendi Mungu ndani yenu.” (Yohana 5:39, 42) Wengine hutumia miaka mingi wakijifunza matendo yenye upendo ya Yehova na bado hawampendi sana. Kwa nini? Wanashindwa kutafakari maana ya yale wanayojifunza. Kinyume cha hilo, mamilioni ya watu wanyoofu tunaojifunza Biblia pamoja nao huona kwamba upendo wao kwa Mungu huendelea kukua. Kwa nini? Kwa sababu, kama vile sisi wenyewe tulivyofanya, wao hufuata kielelezo cha Asafu. Katika njia gani?
Tafakari kwa Uthamini
Asafu aliazimia kusitawisha upendo kwa Yehova moyoni mwake. Aliandika: “Nitaonyesha hangaiko moyoni . . . Nitavikumbuka vitendo vya Yah; kwa maana nitayakumbuka matendo yako ya ajabu ya zamani za kale. Nami hakika nitautafakari utendaji wako wote, nami nitajishughulisha mwenyewe na matendo yako.” (Zaburi 77:6, 11, 12) Upendo kwa Mungu utakua katika moyo wa mtu anayetafakari njia za Yehova kama mtunga-zaburi alivyofanya.
Isitoshe, uhusiano wetu na Mungu huimarika tunapokumbuka mambo tuliyofurahia katika utumishi wa Yehova. Mtume Paulo alisema kwamba sisi ni “wafanyakazi wenzi” wa Mungu, na urafiki unaoweza kusitawi kati ya wafanyakazi wenzi ni wa pekee sana. (1 Wakorintho 3:9) Tunapomwonyesha Yehova upendo, yeye hufurahi na kuthamini. (Methali 27:11) Hivyo, tunapomwomba Yehova atusaidie kutatua tatizo fulani naye anafanya hivyo, tunajua kwamba yupo pamoja nasi, na upendo wetu kwake huongezeka.
Urafiki kati ya watu wawili husitawi wanapoonyeshana hisia. Vivyo hivyo, tunapomweleza Yehova sababu inayofanya tujitoe kwake, upendo wetu kwake huimarika. Tutajikuta tukitafakari maneno haya ya Yesu: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30)
-
-
Jinsi Tunavyoonyesha Tunampenda MunguMnara wa Mlinzi—2004 | Machi 1
-
-
Upendo utakua ukisitawishwa kwa njia inayofaa. Kwa hiyo, tunaendelea kutumia wakati ili kutafakari. Tunakumbuka mambo ambayo Yehova ametufanyia na kwa nini anastahili ujitoaji wetu. Tukiwa wazao wa Adamu wasio wakamilifu, hatuwezi kamwe kustahili kupokea “mambo ambayo Mungu amewatayarishia wale wanaompenda,” lakini tunaweza kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kwa nafsi yetu yote. Na tuendelee kufanya hivyo!—1 Wakorintho 2:9.
-