-
Ukweli Kuhusu EkaristiMnara wa Mlinzi—2008 | Aprili 1
-
-
Kanisa Katoliki linafundisha kwamba mkate na divai zinageuka kimuujiza na kuwa mwili na damu halisi ya Kristo. Fundisho hilo lilitokea hatua kwa hatua.
-
-
Ukweli Kuhusu EkaristiMnara wa Mlinzi—2008 | Aprili 1
-
-
Kuanzishwa kwa “Mlo wa Jioni wa Bwana”
Yesu mwenyewe alianzisha “mlo wa jioni wa Bwana” au Ukumbusho wa kifo chake. (1 Wakorintho 11:20, 24) Hata hivyo, je, alianzisha desturi ya kifumbo ambayo wafuasi wake wangekula mwili wake na kunywa damu yake?
Yesu alikuwa tu amemaliza kuadhimisha Pasaka ya Kiyahudi na kumfukuza Yuda Iskariote, yule mtume ambaye alikuwa karibu kumsaliti. Mathayo, mmoja wa mitume 11 waliokuwapo, anaripoti hivi: “Walipokuwa wakiendelea kula, Yesu alichukua mkate na, baada ya kutoa baraka, akaumega, akawapa wanafunzi, akasema: ‘Chukueni, mle. Huu unamaanisha mwili wangu.’ Pia, akachukua kikombe na, akiisha kushukuru [Kigiriki, eu·kha·ri·ste΄sas], akawapa, akisema: ‘Kinyweeni, ninyi nyote; kwa maana hii inamaanisha “damu yangu ya agano,” ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi.’”—Mathayo 26:26-28.
Sawa na kwa watumishi wote wa Mungu, lilikuwa jambo la kawaida kwa Yesu kutoa baraka kwa ajili ya chakula. (Kumbukumbu la Torati 8:10; Mathayo 6:11; 14:19; 15:36; Marko 6:41; 8:6; Yohana 6:11, 23; Matendo 27:35; Waroma 14:6) Je, kuna sababu yoyote ya kuamini kwamba alipotoa shukrani, Yesu alikuwa pia akifanya muujiza, na hivyo kuwafanya wafuasi wake wale mwili wake na kunywa damu yake?
“Huu Unamaanisha” Ama “Huu Ndio”?
Kwa kweli, Biblia fulani zinatafsiri hivi maneno ya Yesu: “Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu,” na, “Nyweni nyote katika hiki; kwa maana hii ndiyo damu yangu.” (Mathayo 26:26-28, Union Version) Pia, ni kweli kwamba neno la Kigiriki e·stin΄, ambalo ni namna ya kitenzi cha Kigiriki “kuwa,” linamaanisha “ndio.” Lakini kitenzi hichohicho kinaweza kumaanisha “kuwakilisha.” Inapendeza kwamba katika Biblia nyingi, mara nyingi kitenzi hicho kinatafsiriwa “maana ya” au “mfano wa.”b Muktadha ndio unaoamua jinsi kitenzi hicho kitakavyotafsiriwa. Kwa mfano katika Biblia nyingi, neno e·stin΄ katika Mathayo 12:7 linatafsiriwa kuwa “maanisha.” Andiko hilo linasema hivi: “Kama mngalijua maana yake [Kigiriki, e·stin΄] maneno haya, nataka rehema, wala si sadaka, msingaliwalaumu wasio na hatia.”—UV; Zaire Swahili Bible.
Kwa sababu hiyo, wasomi wengi wa Biblia wanaoheshimiwa wamekubaliana kwamba neno “ndio” halitoi maana sahihi ya wazo la Yesu. Kwa mfano, Jacques Dupont alifikiria utamaduni na jamii ambamo Yesu aliishi na akakata kauli kwamba “njia ya kawaida zaidi” ya kutafsiri mstari huo inapaswa kuwa: “Huu unamaanisha mwili wangu.”
Vyovyote vile, Yesu hangeweza kumaanisha kwamba wafuasi wake walipaswa kula mwili wake na kunywa damu yake. Kwa nini? Baada ya Gharika ya siku za Noa, Mungu alipowaruhusu wanadamu wale nyama ya wanyama, hakuwapa ruhusa ya kula nyama ya wanadamu. Zaidi ya hilo, aliwakataza waziwazi wasile damu. (Mwanzo 9:3, 4) Amri hiyo ilirudiwa katika Sheria ya Musa, ambayo Yesu alitii kabisa. (Kumbukumbu la Torati 12:23; 1 Petro 2:22) Na mitume waliongozwa na roho takatifu warudie tena amri hiyo iliyokataza kula damu, na hivyo kuifanya iwahusu Wakristo wote. (Matendo 15:20, 29) Je, Yesu angeanzisha maadhimisho ambayo yangehitaji wafuasi wake wavunje sheria takatifu ya Mungu Mweza-Yote? Hilo ni jambo lisilowezekana!
Hivyo basi, ni wazi kwamba Yesu alitumia mkate na divai kama mifano. Mkate usiotiwa chachu, ulimaanisha, au uliwakilisha, mwili wake usio na dhambi ambao ungetolewa kama dhabihu. Divai nyekundu inawakilisha damu yake ambayo ingemwagwa “kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi.”—Mathayo 26:28.
-