-
Unaweza Kuboresha Kumbukumbu YakoFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Ni muhimu pia kukumbuka mambo unayosoma. Unawezaje kukumbuka vizuri zaidi mambo unayosoma? Inafaa kuwa na upendezi na ufahamu. Lazima upendezwe sana na mambo unayosoma ili uyazingatie kabisa. Huwezi kukumbuka kitu ikiwa akili yako iko mbali unapojaribu kusoma. Unaweza kuboresha ufahamu wako unapolinganisha habari hizo na mambo ambayo tayari unayajua. Jiulize: ‘Naweza kutumia habari hii maishani mwangu jinsi gani na wakati gani? Naweza kutumiaje habari hii kumsaidia mtu mwingine?’ Pia unaweza kuboresha ufahamu wako unaposoma mafungu ya maneno badala ya kusoma neno moja-moja. Utafahamu kwa urahisi zaidi mawazo yanayotokezwa na kutambua mambo makuu na hiyo itafanya yawe rahisi kukumbuka.
Tafuta Nafasi Kupitia Habari
Wataalamu wa elimu wanasisitiza kwamba ni muhimu kupitia habari uliyosoma. Profesa mmoja wa chuo kikuu alifanya uchunguzi, akathibitisha kwamba ukitumia dakika moja kupitia haraka habari uliyosoma, utazidisha mara mbili uwezo wako wa kukumbuka mambo hayo. Basi, baada tu ya kumaliza kusoma habari fulani—au sehemu yake kuu—jikumbushe mambo makuu ili uyakaze akilini mwako. Fikiria jinsi unavyoweza kueleza kwa maneno yako mwenyewe mambo mapya ambayo umejifunza. Ukijikumbusha jambo punde tu baada ya kulisoma, utalikumbuka kwa muda mrefu.
Kisha katika siku chache zijazo, tafuta nafasi za kujikumbusha mambo uliyosoma kwa kumweleza mwingine habari hiyo. Unaweza kumweleza mtu wa familia, mtu wa kutaniko, mfanyakazi mwenzako, mwanafunzi mwenzako, jirani, au mtu unayekutana naye katika huduma ya shambani. Jaribu kuwatajia mambo makuu na vilevile Maandiko yanayohusika. Kufanya hivyo kutakufaidi kwa kukaza mambo muhimu akilini na kuwafaidi wengine pia.
Tafakari Mambo Muhimu
Mbali na kujikumbusha habari ambayo umesoma na kuwaeleza wengine juu yake, kuna faida ya kutafakari mambo muhimu ambayo umesoma. Waandishi wa Biblia Asafu na Daudi walifanya hivyo. Asafu alisema: “Nitayakumbuka matendo ya BWANA; naam, nitayakumbuka maajabu yako ya kale. Pia nitaitafakari kazi yako yote; nitaziwaza habari za matendo yako.” (Zab. 77:11, 12) Pia Daudi aliandika hivi: “Nakutafakari Wewe makesha yote ya usiku,” na “nimezikumbuka siku za kale, nimeyatafakari matendo yako yote.” (Zab. 63:6; 143:5) Je, wewe hufanya hivyo?
Kutafakari sana matendo ya Yehova, sifa zake, na mapenzi yake kutakusaidia sana kukumbuka mambo. Ukiwa na mazoea ya kutafakari, kwa kweli moyo wako utazingatia mambo muhimu. Hiyo itajenga utu wako wa ndani. Kumbukumbu zako zitaonyesha mambo yaliyo moyoni mwako kabisa.—Zab. 119:16.
-