Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wasaidie Wanaume Wafanye Maendeleo ya Kiroho
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Novemba 15
    • Wasaidie Wanaume Wafanye Maendeleo ya Kiroho

      “Tangu sasa na kuendelea utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.”—LUKA 5:10.

      1, 2. (a) Wanaume waliitikiaje mahubiri ya Yesu? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

      YESU na wanafunzi wake walipokuwa wakihubiri kotekote Galilaya, walipanda mashua na kwenda mahali pasipo na watu. Lakini umati uliwafuata kwa miguu. Watu ambao walikuja siku hiyo walikuwa “wanaume karibu elfu tano, bila kuhesabu wanawake na watoto wachanga.” (Mt. 14:21) Pindi nyingine, umati wa watu ulimjia Yesu ili uponywe na kumsikiliza. Umati huo ulitia ndani “wanaume elfu nne, bila kuhesabu wanawake na watoto wachanga.” (Mt. 15:38) Ni wazi kwamba wanaume wengi walikuwa miongoni mwa watu waliomjia Yesu na kupendezwa na mafundisho yake. Kwa kweli, alitazamia wengine wengi wakubali kweli, kwa kuwa baada ya kuwasaidia wanafunzi wake kuvua samaki kimuujiza, Yesu alimwambia Simoni hivi: ‘Tangu sasa na kuendelea mtakuwa mkiwavua watu wakiwa hai.’ (Luka 5:10) Wanafunzi wake walipaswa kushusha nyavu zao ndani ya bahari ya wanadamu na kutazamia kwamba ‘wangevua’ watu kutia ndani wanaume wengi.

      2 Leo, wanaume pia wanapendezwa na ujumbe unaotegemea Maandiko ambao tunahubiri na wanaukubali. (Mt. 5:3) Hata hivyo, wanaume wengi wanasitasita na hawafanyi maendeleo ya kiroho. Tunaweza kuwasaidiaje? Ingawa Yesu hakuanzisha huduma ya pekee ya kuwatafuta wanaume, bila shaka alizungumzia mambo ambayo yaliwahusu wanaume katika siku zake. Tukitumia mfano wake, acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kuwasaidia wanaume kushughulikia mambo matatu ya kawaida yanayowahangaisha leo: (1) kutafuta riziki, (2) kuogopa maoni ya watu wengine, na (3) kuhisi kwamba hawastahili.

      Kutafuta Riziki

      3, 4. (a) Wanaume wengi wanahangaikia nini hasa? (b) Kwa nini wanaume fulani wanatanguliza utafutaji wa riziki badala ya mambo ya kiroho?

      3 Mwandishi mmoja alimwambia Yesu hivi: “Mwalimu, mimi nitakufuata mahali popote unapoenda.” Lakini Yesu alipomwambia kwamba “Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake,” mwandishi huyo alibadili nia. Inaonekana kwamba mwandishi huyo alikuwa na mahangaiko kuhusu chakula na mahali ambapo angeishi kwa kuwa Biblia haisemi kwamba alikuja kuwa mfuasi wa Kristo.—Mt. 8:19, 20.

      4 Kwa kawaida, wanaume wanatanguliza vitu vya kimwili badala ya mambo ya kiroho. Jambo muhimu kwa wengi wao ni kupata elimu ya juu zaidi na kazi yenye mshahara mnono. Wanafikiri kwamba ni muhimu zaidi kutafuta pesa kwa sababu zitawasaidia kupata riziki kuliko kujifunza Biblia na kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Huenda wakavutiwa na mambo ambayo Biblia inafundisha, lakini “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu za utajiri” zinasonga upendezi wowote kuelekea Biblia ambao wanaweza kuwa nao. (Marko 4:18, 19) Fikiria jinsi Yesu alivyowasaidia wanafunzi wake kurekebisha maoni yao kuhusu mambo waliyohitaji kutanguliza.

      5, 6. Ni nini kilichowasaidia Andrea, Petro, Yakobo, na Yohana kurekebisha maoni yao kuhusu kutanguliza kazi ya kuhubiri badala ya kutanguliza utafutaji wa riziki?

      5 Andrea na ndugu yake Simoni Petro walikuwa wakifanya pamoja biashara ya uvuvi. Yohana, na ndugu yake Yakobo, walikuwa pia wakifanya biashara hiyo na baba yao, Zebedayo. Biashara yao ilikuwa imesitawi sana hivi kwamba waliwaajiri wafanyakazi. (Marko 1:16-20) Andrea na Yohana waliposikia kwa mara ya kwanza habari za Yesu kutoka kwa Yohana Mbatizaji, walisadiki kwamba walikuwa wamempata Masihi. Andrea akamwambia ndugu yake Simoni Petro habari hizo, na labda Yohana alimwambia Yakobo, ndugu yake. (Yoh. 1:29, 35-41) Katika miezi iliyofuata, wote wanne walikuwa pamoja na Yesu alipokuwa akihubiri katika Galilaya, Yudea, na Samaria. Kisha hao wanafunzi wanne wakarudia biashara yao ya kuvua samaki. Walipendezwa na mambo ya kiroho, lakini kazi ya kuhubiri haikuwa muhimu sana kwao.

      6 Baadaye, Yesu aliwaalika Petro na Andrea wamfuate na kuwa “wavuvi wa watu.” Wanafunzi hao wawili waliitikiaje? “Mara moja wakaziacha nyavu, wakamfuata.” Yakobo na Yohana walifanya vivyo hivyo. “Mara moja wakaacha ile mashua na baba yao, wakamfuata.” (Mt. 4:18-22) Ni nini kilichowasaidia wanaume hao kuanza huduma ya wakati wote? Je, ulikuwa uamuzi wa ghafula uliotegemea hisia? Hapana! Katika miezi iliyotangulia, wanaume hao walimsikiliza Yesu, wakaona akifanya miujiza, wakaona bidii yake kwa ajili ya uadilifu, na kushuhudia watu wengi sana wakikubali ujumbe ambao alihubiri. Mambo hayo yaliwasaidia kuwa na imani yenye nguvu zaidi katika Yehova na kumtegemea zaidi!

      7. Tunaweza kuwasaidiaje wanafunzi wa Biblia wajifunze kutegemea uwezo wa Yehova wa kuwatunza watu wake?

      7 Tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani katika kuwasaidia wanafunzi wa Biblia wajifunze kumtegemea Yehova? (Met. 3:5, 6) Jambo hilo linategemea sana njia yetu ya kufundisha. Tunapofundisha, tunaweza kukazia kwamba Mungu anaahidi kuwa atatubariki sana ikiwa tutatanguliza mambo ya Ufalme. (Soma Malaki 3:10; Mathayo 6:33.) Ingawa tunaweza kutumia maandiko mbalimbali kukazia jinsi Yehova anavyowatunza watu wake, hatupaswi kusahau kwamba mfano wetu wenyewe unaweza kuwachochea. Kuwasimulia mambo ambayo tumejionea maishani mwetu kunaweza kuwasaidia sana wanafunzi wa Biblia wajifunze kumtegemea Yehova. Tunaweza pia kuwasimulia mambo yanayotia moyo tunayosoma katika machapisho yetu.a

      8. (a) Kwa nini ni muhimu kwa mwanafunzi wa Biblia ‘kuonja na kuona kwamba Yehova ni mwema’? (b) Tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi wetu ajionee mwenyewe kwamba Yehova ni mwema?

      8 Mwanafunzi wa Biblia hawezi kusitawisha imani yenye nguvu kwa kusoma tu na kusikiliza jinsi ambavyo wengine wamebarikiwa na Yehova. Mwanafunzi wa Biblia anahitaji pia kujionea wema wa Yehova katika maisha yake binafsi. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema; mwenye furaha ni mwanamume ambaye humkimbilia.” (Zab. 34:8) Tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi aone kwamba Yehova ni mwema? Tuseme kwamba mwanafunzi ambaye ana mahangaiko ya kifedha anajaribu pia kuacha zoea fulani baya, kama vile kuvuta sigara, kucheza kamari, au kunywa kupita kiasi. (Met. 23:20, 21; 2 Kor. 7:1; 1 Tim. 6:10) Kumfundisha mwanafunzi huyo kusali na kuomba msaada wa Mungu ili kushinda zoea baya, je, hakutamsaidia kuona kwamba Yehova ni mwema? Fikiria pia jambo linaloweza kutokea ikiwa tutamtia moyo mwanafunzi atangulize mambo ya kiroho kwa kutenga wakati wa kujifunza Biblia kila juma, kutayarisha na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Bila shaka, imani yake itakuwa na nguvu zaidi anapojionea mwenyewe Yehova akibariki jitihada zake!

      Kuogopa Maoni ya Wengine

      9, 10. (a) Kwa nini Nikodemo na Yosefu, mwenyeji wa Arimathea, walikuwa wanafunzi wa Yesu kwa siri? (b) Kwa nini wanaume fulani leo wanasitasita kumfuata Kristo?

      9 Huenda wanaume fulani wakasitasita kumfuata Kristo kikamili kwa sababu ya kusongwa na wengine. Nikodemo na Yosefu, mwenyeji wa Arimathea, walikuwa wanafunzi wa Yesu kwa siri kwa sababu waliogopa mambo ambayo Wayahudi wengine wangesema au kufanya ikiwa wangejua. (Yoh. 3:1, 2; 19:38) Walikuwa na sababu ya kuogopa. Viongozi wa kidini walimchukia sana Yesu hivi kwamba mtu yeyote aliyemwamini alifukuzwa kutoka katika sinagogi.—Yoh. 9:22.

      10 Katika sehemu fulani leo, mwanamume akipendezwa sana na mambo ya Mungu, Biblia, au dini, anaweza kusumbuliwa na wafanyakazi wenzake, marafiki, au watu wa ukoo. Katika sehemu nyingine, huenda hata ikawa hatari kusema kwamba unabadili dini yako. Mwanamume anaweza kushutumiwa vikali zaidi hasa ikiwa anatumika katika jeshi, anajihusisha sana na siasa, au ana cheo kikubwa katika jamii. Kwa mfano, mwanamume fulani huko Ujerumani alikiri hivi: “Mambo ambayo ninyi Mashahidi mnahubiri kuhusu Biblia ni ya kweli. Lakini nikiamua kuwa Shahidi leo, kesho kila mtu atakuwa amejua jambo hilo. Wengine watanionaje kazini, katika ujirani, na katika klabu ambacho mimi na familia yangu tunashiriki? Siwezi kuvumilia hali hiyo.”

      11. Yesu aliwasaidiaje wanafunzi wake kutowaogopa wanadamu?

      11 Ingawa mitume wote wa Yesu walikuwa jasiri, nyakati nyingine waliwaogopa wanadamu. (Marko 14:50, 66-72) Yesu aliwasaidiaje kufanya maendeleo hata ingawa walisongwa sana na watu wengine? Yesu alichukua hatua ili kuwatayarisha wanafunzi wake kukabiliana na upinzani ambao wangepata baadaye. Alisema hivi: “Wenye furaha ni ninyi wakati wowote ule watu wanapowachukia ninyi, na wakati wowote ule watu wanapowatenga ninyi na kuwashutumu na kulitupa nje jina lenu kuwa ovu kwa ajili ya Mwana wa binadamu.” (Luka 6:22) Yesu aliwaonya wafuasi wake kwamba wanapaswa kutazamia kushutumiwa. Shutuma yoyote ambayo wangepata ingekuwa ni “kwa ajili ya Mwana wa binadamu.” Yesu aliwahakikishia pia kwamba Mungu angewatunza ikiwa tu wangemtegemea Yeye ili awasaidie na kuwapa nguvu. (Luka 12:4-12) Zaidi ya hayo, Yesu aliwaalika wapya ili washirikiane kwa uhuru na wanafunzi wake na kuanzisha urafiki nao.—Marko 10:29, 30.

      12. Ni katika njia gani tunaweza kuwasaidia wapya ili wasiwaogope wanadamu?

      12 Sisi pia tunahitaji kuwasaidia wanafunzi wa Biblia kutowaogopa wanadamu. Mara nyingi ni rahisi zaidi kushinda tatizo tunapojua mapema jinsi ya kukabiliana nalo. (Yoh. 15:19) Kwa mfano, kwa nini usimsaidie mwanafunzi kutayarisha majibu rahisi yenye kusadikisha yanayotegemea Biblia kwa maswali na vipingamizi ambavyo huenda wafanyakazi wenzake na wengine wakatokeza? Zaidi ya kuwa rafiki yake wa karibu, tunaweza kumtambulisha kwa washiriki wengine wa kutaniko, hasa wale ambao huenda wana mapendezi kama yake. Zaidi ya yote, tunapaswa kumfundisha kusali kwa ukawaida na kutoka moyoni. Jambo hilo linaweza kumsaidia amkaribie Mungu na kumfanya Yehova kuwa Kimbilio na Mwamba wake.—Soma Zaburi 94:21-23; Yakobo 4:8.

      Kujihisi Kwamba Hawastahili

      13. Hisia za kutostahili zinaweza jinsi gani kuwafanya wengine wakatae mambo ya kiroho?

      13 Wanaume fulani wanakataa mambo ya kiroho kwa sababu hawasomi vizuri au hawawezi kujieleza vizuri au kwa sababu tu wanaona haya. Wanaume wengine wanaogopa kutoa maoni yao au kueleza hisia zao hadharani. Huenda wakaona kwamba ni vigumu kujifunza, kutoa maelezo katika mikutano ya Kikristo, au kuwaeleza wengine kuhusu imani yao. Ndugu mmoja Mkristo anakiri hivi: “Nilipokuwa na umri mdogo, nilikuwa nikienda haraka mlangoni, nilijifanya kuwa ninapiga kengele, halafu nilitoka polepole na kwenda nikitumaini kwamba hakuna mtu ambaye angenisikia au kuniona. . . . Wazo la kuhubiri nyumba kwa nyumba lilinifanya niwe mgonjwa kihalisi.”

      14. Kwa nini wanafunzi wa Yesu walishindwa kumponya mvulana fulani aliyekuwa na roho waovu?

      14 Fikiria jinsi ambavyo wanafunzi wa Yesu walivyokosa uhakika waliposhindwa kumponya mvulana fulani aliyekuwa na roho waovu. Baba ya mwana huyo alimjia Yesu na kusema: ‘Mwanangu, ana kifafa na ni mgonjwa, kwa maana yeye huanguka ndani ya moto na ndani ya maji mara nyingi; nami nilimleta kwa wanafunzi wako, lakini hawakuweza kumponya.’ Yesu alimfukuza huyo roho mwovu na kumponya mvulana huyo. Baadaye wanafunzi walimjia Yesu na kumuuliza: “Kwa nini sisi hatukuweza kumfukuza?” Yesu akawajibu hivi: “Ni kwa sababu ya imani yenu kidogo, kwa maana kwa kweli ninawaambia, Mkiwa na imani inayotoshana na mbegu ya haradali, mtauambia mlima huu, ‘Ondoka hapa uende pale,’ nao utaondoka, na hakuna jambo litakalowashinda.” (Mt. 17:14-20) Imani katika Yehova inahitajiwa ili kushinda matatizo ambayo ni kama mlima. Ni nini kinachotokea mtu anapokosa kukazia fikira jambo hilo na badala yake anaanza kukazia fikira uwezo wake mwenyewe? Atakosa kufanikiwa na hilo litafanya akose uhakika.

      15, 16. Tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi wa Biblia ashinde hisia ya kwamba hastahili?

      15 Njia nzuri ya kumsaidia mtu anayepambana na hisia za kutostahili ni kumtia moyo amfikirie Yehova badala ya kujifikiria mwenyewe. Petro aliandika hivi: “Jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue ninyi katika wakati unaofaa; huku mkitupa mahangaiko yenu yote juu yake.” (1 Pet. 5:6, 7) Hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kumsaidia mwanafunzi wetu wa Biblia asitawishe hali ya kiroho. Mtu anayependa mambo ya kiroho anathamini sana mambo ya kiroho. Anapenda Neno la Mungu na kuonyesha ‘tunda la roho’ katika maisha yake. (Gal. 5:22, 23) Ni mwanamume anayedumu katika sala. (Flp. 4:6, 7) Zaidi ya hayo, anamwomba Mungu ampe ujasiri na nguvu anazohitaji ili kupambana na hali yoyote au kutimiza mgawo wowote kwa mafanikio.—Soma 2 Timotheo 1:7, 8.

      16 Huenda wanafunzi fulani pia wakahitaji kusaidiwa inavyofaa kuboresha uwezo wao wa kusoma na kuzungumza. Huenda wengine wakahisi kwamba hawastahili kumtumikia Mungu kwa sababu ya mambo mabaya ambayo walitenda kabla ya kumjua Yehova. Katika hali yoyote ile, huenda wanahitaji tu tuwasaidie kwa upendo na kwa subira. Yesu alisema hivi: “Watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua ndio wanaomhitaji.”—Mt. 9:12.

      ‘Wavue’ Wanaume Wengi Zaidi

      17, 18. (a) Tunaweza kuwasaidia jinsi gani wanaume wengi zaidi katika huduma yetu? (b) Tutajifunza nini katika makala inayofuata?

      17 Tunatumaini kwamba wanaume wengi zaidi watakubali ujumbe wenye kuridhisha sana ambao unapatikana tu katika Biblia. (2 Tim. 3:16, 17) Basi tunaweza kuwasaidia jinsi gani wanaume wengi zaidi katika huduma yetu? Kwa kutumia wakati mwingi zaidi kuhubiri jioni, Jumamosi na Jumapili alasiri, au siku za sikukuu wakati ambapo wanaume wengi wako nyumbani. Inapowezekana, tunaweza kuomba kuzungumza na mwanamume mwenye-nyumba. Acheni tuwahubirie isivyo rasmi wafanyakazi wenzetu wanaume inapofaa na kuwasaidia waume ambao si waamini katika kutaniko.

      18 Tunapomhubiria kila mtu tunayekutana naye, tunaweza kuwa na hakika kwamba watu wenye mioyo minyoofu watakubali kweli. Acheni tuwasaidie kwa subira wote ambao wanapendezwa na kweli kwa unyoofu. Hata hivyo, tunaweza kuwasaidia jinsi gani wanaume waliobatizwa kutanikoni wajitahidi kustahili kupata mapendeleo katika tengenezo la Mungu? Makala inayofuata itajibu swali hilo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ona Vitabu vya Mwaka vya Mashahidi wa Yehova na pia masimulizi ya maisha yanayochapishwa katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni!

  • Wazoeze Wengine ili Wajitahidi Kufikia Mapendeleo
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Novemba 15
    • Wazoeze Wengine ili Wajitahidi Kufikia Mapendeleo

      “Kila mtu aliyefundishwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake.”—LUKA 6:40.

      1. Wakati wa huduma yake duniani, Yesu aliwekaje msingi wa kutaniko la pekee?

      AKIMALIZIA simulizi lake la Injili, mtume Yohana aliandika hivi: “Kwa kweli, kuna mambo mengine mengi pia aliyofanya Yesu, ambayo, kama yangeandikwa kirefu, nadhani ulimwengu wenyewe haungeweza kuwa na nafasi ya kuviweka vitabu vya kukunjwa ambavyo vingeandikwa.” (Yoh. 21:25) Kati ya mambo yote ambayo Yesu alitimiza wakati wa huduma yake ya muda mfupi lakini yenye matokeo mazuri sana ni kuwatafuta, kuwazoeza, na kuwapanga wanaume ambao wangeongoza kazi baada ya yeye kurudi mbinguni. Aliporudi mbinguni mwaka wa 33 W.K., Yesu aliacha msingi wa kutaniko la pekee ambalo lingeongezeka haraka na kuwa na maelfu ya watu.—Mdo. 2:41, 42; 4:4; 6:7.

      2, 3. (a) Kwa nini kuna uhitaji mkubwa sana wa wanaume waliobatizwa kujitahidi kufikia mapendeleo? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala hii?

      2 Kukiwa na wahubiri wa Ufalme wenye bidii zaidi ya milioni saba katika makutaniko zaidi ya 100,000 ulimwenguni pote leo, bado kuna uhitaji wa wanaume wa kuongoza katika mambo ya kiroho. Kwa mfano, kuna uhitaji mkubwa sana wa wazee Wakristo. Wale ambao wanajitahidi kufikia pendeleo hilo la utumishi wanastahili kupongezwa, kwa kuwa ‘wanatamani kazi njema.’—1 Tim. 3:1.

      3 Hata hivyo, ni lazima wanaume watimize matakwa fulani ili wastahili kupata mapendeleo katika kutaniko. Kuwa tu na elimu ya ulimwengu au uzoefu maishani hakumtayarishi mwanamume kwa ajili ya kazi hiyo. Ili atumikie ifaavyo katika pendeleo hilo, ni lazima mwanamume astahili kiroho. Zaidi ya kuwa na uwezo au kutimiza mambo mbalimbali, ni lazima awe na sifa za kiroho. Wanaume katika kutaniko wanaweza kusaidiwa jinsi gani ili wastahili? Yesu alisema hivi: “Kila mtu aliyefundishwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake.” (Luka 6:40) Katika makala hii, tutazungumzia baadhi ya njia ambazo yule Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo, alitumia kuwasaidia wanafunzi wake wastahili kupata mapendeleo makubwa zaidi, na tutaona mambo tunayoweza kujifunza kutokana na yale aliyofanya.

      “Nimewaita Ninyi Rafiki”

      4. Yesu alionyeshaje kwamba alikuwa rafiki wa kweli kwa wanafunzi wake?

      4 Yesu aliwatendea wanafunzi wake kama marafiki, wala si kama watu wa hali ya chini. Alitumia wakati pamoja nao, aliwaamini, na ‘kuwajulisha mambo yote ambayo alikuwa amesikia kutoka kwa Baba yake.’ (Soma Yohana 15:15.) Wazia jinsi walivyosisimka Yesu alipojibu swali lao: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mt. 24:3, 4) Pia, aliwaambia wafuasi wake mawazo na hisia zake. Kwa mfano, usiku ambao alisalitiwa, Yesu alimchukua Petro, Yakobo, na Yohana pamoja naye katika bustani ya Gethsemane, ambako alisali kwa bidii akiwa na mahangaiko mengi moyoni. Huenda mitume hao watatu hawakusikia maneno ambayo Yesu alikuwa akisema katika sala, lakini bila shaka waliona jinsi alivyokuwa akiteseka sana. (Marko 14:33-38) Fikiria pia jinsi mitume hao watatu walivyotiwa nguvu awali walipomwona Yesu akigeuka sura. (Marko 9:2-8; 2 Pet. 1:16-18) Urafiki wa karibu ambao Yesu alisitawisha pamoja na wanafunzi wake uliwatia nguvu ili kutimiza migawo mizito baadaye.

      5. Wazee Wakristo wanaweza kusitawisha urafiki na wengine katika njia zipi?

      5 Kama Yesu, wazee Wakristo leo wanasitawisha urafiki na wengine na kuwasaidia. Wanasitawisha urafiki mchangamfu na wa karibu pamoja na waamini wenzao kwa kutumia wakati kuwaonyesha upendezi wa kibinafsi. Ingawa wazee wanatambua umuhimu wa kutunza siri, kuna mambo fulani wanayoweza kuzungumza na wengine. Wazee wanawaamini ndugu zao na wanazungumza nao kuhusu kweli za Kimaandiko ambazo wao wenyewe wamejifunza. Wazee hawamdharau kamwe mtumishi wa huduma mwenye umri mdogo. Badala yake, wanamwona kuwa mwanamume wa kiroho mwenye uwezo ambaye anatimiza utumishi wenye thamani kwa faida ya kutaniko.

      “Niliweka Kielelezo kwa Ajili Yenu”

      6, 7. Yesu aliwawekea wanafunzi wake kielelezo gani na kilikuwa na uvutano gani juu yao?

      6 Ingawa wanafunzi wa Yesu walithamini mambo ya kiroho, nyakati nyingine fikira zao ziliongozwa na malezi na utamaduni wao. (Mt. 19:9, 10; Luka 9:46-48; Yoh. 4:27) Hata hivyo, Yesu hakuwafokea au kuwatisha wanafunzi wake. Wala hakuwalemea kwa kuwaambia wafanye mambo ambayo hawangeweza kufanya au kuwashauri wafanye jambo fulani huku yeye mwenyewe akifanya jambo tofauti. Badala yake, Yesu aliwafundisha kupitia mfano wake.—Soma Yohana 13:15.

      7 Yesu aliwaachia wanafunzi wake kielelezo gani? (1 Pet. 2:21) Aliishi maisha rahisi ili aweze kuwahudumia wengine kwa uhuru. (Luka 9:58) Yesu alikuwa mwenye kiasi na sikuzote mafundisho yake yalitegemea Maandiko. (Yoh. 5:19; 17:14, 17) Alikuwa mwenye urafiki na mwenye fadhili. Alichochewa na upendo katika mambo yote aliyofanya. (Mt. 19:13-15; Yoh. 15:12) Mfano wa Yesu ulikuwa na uvutano mzuri juu ya mitume wake. Kwa mfano, Yakobo hakuogopa alipokabili kifo, badala yake aliendelea kumtumikia Mungu kwa ushikamanifu mpaka alipouawa. (Mdo. 12:1, 2) Yohana alifuata kwa uaminifu hatua za Yesu kwa miaka zaidi ya 60.—Ufu. 1:1, 2, 9.

      8. Wazee wanawawekea wanaume vijana na wengine mfano gani?

      8 Wazee ambao wanajidhabihu, ni wanyenyekevu, na wenye upendo, wanaweka mfano ambao wanaume vijana wanahitaji. (1 Pet. 5:2, 3) Isitoshe, wazee ambao ni mfano mzuri katika imani, kufundisha, maisha ya Kikristo, na katika huduma, wanaridhika wanapojua kwamba wengine wanaweza kuiga imani yao.—Ebr. 13:7.

      ‘Yesu Aliwapa Maagizo, Akawatuma’

      9. Tunajuaje kwamba Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kufanya kazi ya kueneza injili?

      9 Baada ya kuhubiri kwa bidii kwa miaka miwili hivi, Yesu alipanua kazi ya kuhubiri kwa kuwatuma mitume wake 12 ili wahubiri. Hata hivyo, aliwapa maagizo kwanza. (Mt. 10:5-14) Kabla ya kuulisha umati wa maelfu ya watu kimuujiza, Yesu aliwaambia wanafunzi wake jinsi alivyotaka wawapange watu na kugawa chakula. (Luka 9:12-17) Basi, ni wazi kwamba Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kwa kuwapa mwongozo hususa na ulio wazi. Kielelezo chake katika kuwazoeza wengine, pamoja na uvutano wenye nguvu wa roho takatifu, uliwawezesha baadaye mitume kupanga kazi kubwa sana ya kuhubiri ambayo ilifanywa mwaka wa 33 W.K. na kuendelea.

      10, 11. Wapya wanaweza kuzoezwa jinsi gani hatua kwa hatua?

      10 Leo, mwanamume anaanza kupokea maagizo ya kiroho anapokubali funzo la Biblia. Huenda tukahitaji kumsaidia kujua kusoma vizuri. Tunaendelea kumsaidia tunapojifunza Biblia pamoja naye. Anapoanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, mazoezi yake ya kiroho yataendelea anaposhiriki katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, anapokuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, na kadhalika. Baada ya kubatizwa, anaweza kuzoezwa pia katika mambo kama vile kushiriki katika kutunza Jumba la Ufalme. Baada ya muda, ndugu anaweza kusaidiwa kuona mambo anayohitaji kufanya ili astahili kuwa mtumishi wa huduma.

      11 Mzee anapompa ndugu aliyebatizwa mgawo, anahitaji kumweleza vizuri utaratibu unaofaa wa kitengenezo na kumpa maagizo anayohitaji. Ni muhimu ndugu anayezoezwa aelewe jambo analotazamiwa kufanya. Ikiwa kazi aliyopewa ni ngumu kwake, mzee mwenye upendo haamui haraka-haraka kwamba ndugu huyo hastahili. Badala yake, mzee huyo anamweleza tena kwa fadhili mambo hususa anayohitaji kufanya na utaratibu wa kufuata. Wazee wanafurahi wanapoona wanaume wakiitikia vizuri jitihada kama hizo na kupata shangwe ya kuwatumikia wengine.—Mdo. 20:35.

      “Anayesikiliza Shauri Ni Mwenye Hekima”

      12. Ni nini kilichofanya mashauri ya Yesu yawe yenye matokeo mazuri?

      12 Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kwa kumpa kila mmoja mashauri kulingana na uhitaji wake. Kwa mfano, aliwakemea Yakobo na Yohana kwa kutaka kuomba moto ushuke kutoka mbinguni na kuwaangamiza Wasamaria fulani ambao hawakumpokea. (Luka 9:52-55) Mama ya Yakobo na Yohana alipomfikia Yesu kwa niaba yao na kuomba kwamba wapewe vyeo vikubwa katika Ufalme, Yesu aliwaambia hivi ndugu hao moja kwa moja: “Kuketi upande wangu wa kuume na upande wangu wa kushoto sina haki ya kutoa, bali wataketi wale ambao Baba yangu amewatayarishia.” (Mt. 20:20-23) Nyakati zote, Yesu alitoa mashauri yaliyo wazi, yanayofaa, na yanayotegemea kabisa kanuni za Mungu. Aliwafundisha wanafunzi wake kufikiria na kutenda kupatana na kanuni hizo. (Mt. 17:24-27) Yesu alitambua pia udhaifu wa wafuasi wake na hakutazamia watende kwa njia kamilifu. Mashauri yake yalichochewa na upendo wa kweli.—Yoh. 13:1.

      13, 14. (a) Ni nani anayehitaji shauri? (b) Toa mifano inayoonyesha shauri ambalo mzee anaweza kumpa mtu ambaye hafanyi maendeleo ya kiroho.

      13 Kila mwanamume anayejitahidi kufikia mapendeleo katika kutaniko la Kikristo anahitaji mashauri ya Kimaandiko mara kwa mara. Andiko la Methali 12:15 linasema hivi: “Anayesikiliza shauri ni mwenye hekima.” Ndugu mmoja kijana anasema hivi: “Niligundua kwamba tatizo langu kubwa zaidi lilikuwa kupambana na udhaifu wangu. Mzee mmoja alinishauri na kunisaidia kuelewa kwamba sikuhitaji kuwa mkamilifu ili kutumika.”

      14 Wazee wakiona kwamba mwenendo fulani usiofaa unamzuia mwanamume kufanya maendeleo ya kiroho, wanachukua hatua ya kumrekebisha upya katika roho ya upole. (Gal. 6:1) Nyakati nyingine, wazee wanahitaji kumshauri mtu ili arekebishe tabia fulani isiyofaa. Kwa mfano, ikiwa ndugu fulani anaonekana hapendi kujitoa sana, huenda ikafaa kwa mzee kumwonyesha kwamba Yesu alikuwa mhubiri wa Ufalme mwenye bidii na aliwapa wafuasi wake kazi ya kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20; Luka 8:1) Ikiwa ndugu anaonekana kuwa na kimbelembele, mzee anaweza kumwonyesha jinsi Yesu alivyowasaidia wanafunzi Wake kuona hatari za kutafuta umashuhuri. (Luka 22:24-27) Namna gani ikiwa ndugu ana mwelekeo wa kutosamehe? Mfano wa yule mtumwa ambaye alikataa kusamehe deni dogo hata ingawa yeye mwenyewe alikuwa amesamehewa deni kubwa zaidi unaweza kumsaidia sana. (Mt. 18:21-35) Shauri linapohitajiwa, ni vizuri wazee walitoe haraka iwezekanavyo.—Soma Methali 27:9.

      “Uwe Ukijizoeza”

      15. Familia ya mwanamume inaweza kumsaidiaje ili awatumikie wengine?

      15 Wazee wanaongoza katika kuwazoeza wanaume wajitahidi kufikia mapendeleo, lakini wengine wanaweza kuwasaidia wazee katika jitihada hizo. Kwa mfano, familia ya mwanamume inaweza na inapaswa kumsaidia ajitahidi kufikia mapendeleo. Na ikiwa yeye tayari ni mzee, atafaidika akiungwa mkono na mke mwenye upendo na watoto wasio na ubinafsi. Utayari wao wa kumruhusu alitumikie pia kutaniko ni muhimu ili afanikiwe kutimiza madaraka yake. Roho yao ya kujidhabihu inamletea shangwe na inathaminiwa sana na wengine.—Met. 15:20; 31:10, 23.

      16. (a) Ni nani aliye na daraka la msingi la kujitahidi kufikia mapendeleo? (b) Mwanamume anaweza kujitahidi jinsi gani kufikia mapendeleo katika kutaniko?

      16 Ingawa wengine wanaweza kumsaidia na kumuunga mkono, mwanamume mwenyewe ndiye aliye na daraka la msingi la kujitahidi kufikia mapendeleo. (Soma Wagalatia 6:5.) Bila shaka, si lazima ndugu awe mtumishi wa huduma au mzee ili awasaidie wengine na kushiriki kikamili katika huduma. Hata hivyo, kujitahidi kufikia mapendeleo katika kutaniko kunamaanisha kujitahidi kutimiza matakwa ya kustahili ambayo yameonyeshwa katika Maandiko. (1 Tim. 3:1-13; Tito 1:5-9; 1 Pet. 5:1-3) Kwa hiyo, ikiwa mwanamume anatamani kutumika akiwa mtumishi wa huduma au mzee lakini bado hajawekwa rasmi, anapaswa kukazia fikira mambo anayohitaji kurekebisha ili afanye maendeleo ya kiroho. Hilo linamaanisha kusoma Biblia kwa ukawaida, kujifunza kibinafsi kwa bidii, kutafakari kwa uzito, kusali kutoka moyoni, na kushiriki kwa bidii katika huduma ya Kikristo. Kwa kufanya mambo hayo, anaweza kutumia kibinafsi shauri hili ambalo Paulo alimpa Timotheo: “Uwe ukijizoeza ujitoaji-kimungu ukiwa ni shabaha yako.”—1 Tim. 4:7.

      17, 18. Ndugu aliyebatizwa anaweza kufanya nini ikiwa mahangaiko, hisia za kutostahili, au kukosa tamaa ya kuwatumikia wengine kunamzuia asijitahidi kufikia mapendeleo?

      17 Lakini namna gani ikiwa mwanamume hajitahidi kufikia mapendeleo kwa sababu ya mahangaiko au kuhisi kwamba hastahili? Itakuwa vizuri akifikiria mambo mengi sana ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wanatufanyia. Kwa kweli, Yehova “hutubebea mzigo wetu kila siku.” (Zab. 68:19) Kwa hiyo, Baba yetu wa mbinguni anaweza kumsaidia ndugu akubali madaraka katika kutaniko. Ndugu ambaye hatumikii akiwa mtumishi wa huduma au mzee atafaidika pia akifikiria uhakika wa kwamba kuna uhitaji mkubwa wa wanaume wakomavu ambao wanaweza kukubali mapendeleo ya utumishi katika tengenezo la Mungu. Kutafakari kuhusu mambo hayo kunaweza kumchochea ndugu ajitahidi kushinda hisia zisizofaa. Anaweza kusali ili apate roho takatifu, akikumbuka kwamba tunda la roho linatia ndani sifa ya amani na kujizuia, sifa ambazo zinahitajiwa ili kushinda mahangaiko na hisia za kutostahili. (Luka 11:13; Gal. 5:22, 23) Na anaweza kuwa na hakika kabisa kwamba Yehova anawabariki wote wanaojitahidi kufikia mapendeleo wakiwa na nia nzuri.

      18 Je, inawezekana kwamba kukosa tamaa ya kutumika kunamzuia mwanamume aliyebatizwa asijitahidi kufikia mapendeleo? Ni nini kinachoweza kumsaidia ndugu ambaye hana tamaa ya kutumika? Mtume Paulo aliandika hivi: “[Mungu], kwa ajili ya mapenzi yake mema, anatenda ndani yenu ili ninyi muwe na nia na kutenda pia.” (Flp. 2:13) Tamaa ya kuwatumikia wengine inatoka kwa Mungu, na roho ya Yehova inaweza kumwimarisha mtu ili aweze kutoa utumishi mtakatifu. (Flp. 4:13) Zaidi ya hayo, Mkristo anaweza kusali ili Mungu amchochee kufanya jambo linalofaa.—Zab. 25:4, 5.

      19. Kusimamishwa kwa “wachungaji saba, ndiyo, watawala wadogo wanane” kunatuhakikishia nini?

      19 Yehova anabariki jitihada za wanaume wazee za kuwazoeza wengine. Pia, anawabariki wale ambao wanakubali kuzoezwa na kujitahidi kufikia mapendeleo katika kutaniko. Maandiko yanatuhakikishia kwamba kati ya watu wa Mungu “wachungaji saba, ndiyo, watawala wadogo wanane,” yaani, idadi inayohitajiwa ya wanaume wenye uwezo, watasimamishwa ili waongoze katika tengenezo la Yehova. (Mika 5:5) Ni baraka kama nini kwamba wanaume wengi sana Wakristo wanazoezwa na kwa unyenyekevu wanajitahidi kufikia mapendeleo ya utumishi ili kumletea Yehova sifa!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki