-
Je, “Hekima ya Kutoka Juu” Inakuongoza Maishani?Mkaribie Yehova
-
-
“Yenye Kujaa Rehema na Matunda Mema”
15. Rehema ni nini, na kwa nini inafaa kwamba andiko la Yakobo 3:17 linataja “rehema” pamoja na “matunda mema”?
15 “Yenye kujaa rehema na matunda mema.”c Rehema ni sifa muhimu ya hekima ya kutoka juu, kwa sababu inasemekana kwamba hekima hiyo ‘imejaa rehema.’ Ona kwamba “rehema” inatajwa pamoja na “matunda mema.” Jambo hilo linafaa kwa sababu katika Biblia, mara nyingi rehema humaanisha kuwajali sana wengine na kuwatendea mambo mengi ya fadhili kwa huruma. Kichapo kimoja cha marejeo chafafanua rehema kuwa “hali ya kuhuzunishwa na hali mbaya ya mtu mwingine na kujaribu kumsaidia.” Kwa hiyo, hekima ya Mungu si baridi wala haitegemei akili tu. Badala yake, ni yenye upendo na huruma, na inawajali wengine. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tumejaa rehema?
16, 17. (a) Mbali na kumpenda Mungu, ni nini kinachotuchochea tushiriki kazi ya kuhubiri, na kwa nini? (b) Ni katika njia zipi tunaweza kuonyesha kwamba tumejaa rehema?
16 Bila shaka njia bora ya kuonyesha sifa hiyo ni kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Ni nini kinachotuchochea kufanya kazi hiyo? Hasa ni kwa sababu tunampenda Mungu. Tunachochewa pia na rehema, au huruma. (Mathayo 22:37-39) Watu wengi leo ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ (Mathayo 9:36) Wamepuuzwa na kupofushwa kiroho na wachungaji wa uwongo wa kidini. Ndiyo sababu hawajui mwongozo wenye hekima ulio katika Neno la Mungu wala hawajui baraka zitakazoletwa duniani na Ufalme huo hivi karibuni. Kwa hiyo, tunapozingatia mahitaji ya kiroho ya jirani zetu, tunachochewa na huruma kutoka moyoni kujitahidi kadiri tuwezavyo kuwaambia kusudi la Yehova lenye upendo.
Tunapowaonyesha wengine rehema, au huruma, tunadhihirisha “hekima ya kutoka juu”
17 Ni katika njia zipi nyingine tunaweza kuonyesha kwamba tumejaa rehema? Kumbuka mfano wa Yesu wa yule Msamaria aliyemkuta msafiri fulani aliyelala kando ya barabara baada ya kupigwa na kuporwa. Msamaria huyo alimhurumia na ‘akatenda kwa rehema.’ Alimfunga majeraha na kumtunza. (Luka 10:29-37) Mfano huo waonyesha kwamba kuwa na rehema kwahusisha kuwasaidia wenye uhitaji. Biblia inatuambia “tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Fikiria mifano kadhaa. Huenda mwamini mwenzako aliye mzee kwa umri anahitaji kusaidiwa kusafiri kwenda kwenye mikutano ya Kikristo na kurudi. Huenda mjane fulani kutanikoni anahitaji kusaidiwa kurekebisha nyumba yake. (Yakobo 1:27) Huenda mtu fulani aliyeshuka moyo anahitaji kuambiwa “neno jema” la kumfariji. (Mithali 12:25) Tunapoonyesha rehema katika njia hizo, tunathibitisha kwamba tunaongozwa na hekima ya kutoka juu.
-
-
Je, “Hekima ya Kutoka Juu” Inakuongoza Maishani?Mkaribie Yehova
-
-
c Biblia Habari Njema inatafsiri hivi maneno hayo: “Imejaa huruma na huzaa matunda ya matendo mema.”
-