Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jitihada za Kutafuta Majibu
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Februari 1
    • Ikiwa unataka kupata amani ya kweli ya akili, unahitaji kupata majibu ya maswali matatu muhimu sana.

      Tulitoka wapi?

      Ni nini kusudi la maisha?

      Ni nini kitakachotokea wakati ujao?

      Unaweza kupata wapi majibu yenye kutegemeka ya maswali hayo muhimu? Badala ya kutoa falsafa au majibu ya kukisiwa tu, habari inayofuata itatoa majibu ya Neno la Mungu, Biblia. Tunakuomba ufungue Biblia yako na kujisomea mambo inayosema.

  • Tulitoka Wapi?
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Februari 1
    • Tulitoka Wapi?

      KWA NINI JIBU LA SWALI HILO NI LA MAANA? Watu wengi wanafundishwa kwamba uhai ulitokea duniani kimuujiza tu. Wanaambiwa kwamba matukio fulani yalitukia yenyewe tu bila mpango na kutokeza wanadamu kupitia mageuzi, wakiwa na uwezo wao wa kihisia, kiakili, na tamaa ya kujua kusudi la maisha.

      Lakini fikiria hili: Kwa kweli ikiwa tulitokana na mageuzi na hakuna Muumba, kwa njia fulani wanadamu wangekuwa mayatima. Wanadamu hawangekuwa na mtu mwenye hekima ya juu zaidi wa kumwomba mashauri. Hatungekuwa na mtu wa kutusaidia kusuluhisha matatizo yetu. Tungelazimika kutegemea hekima ya wanadamu ili kuepuka misiba ya kimazingira, kusuluhisha migogoro ya kisiasa, na kushughulikia matatizo ya kibinafsi.

      Je, wazo hilo linakuletea amani ya akili? Ikiwa sivyo, fikiria kuhusu kumtegemea mtu mwenye hekima inayozidi ya wanadamu. Wazo hilo halituvutii tu bali pia linapatana na akili.

      Yale Ambayo Biblia Inasema

      Biblia inafundisha kwamba wanadamu waliumbwa moja kwa moja na Mungu. Hatukutokana na mageuzi ambayo hayategemei akili. Badala yake, sisi ni watoto wa Baba mwenye upendo na mwenye akili. Ona habari zifuatazo ambazo zinasemwa wazi katika Biblia.

      Mwanzo 1:27. “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.”

      Zaburi 139:14. “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha. Kazi zako ni za ajabu, kama vile nafsi yangu inavyojua vema.”

      Mathayo 19:4-6. “Je, hamkusoma kwamba yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”

      Matendo 17:24, 25. “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, akiwa, kama Huyu alivyo, Bwana wa mbingu na dunia, hakai katika mahekalu yaliyofanywa kwa mikono, wala hatumikiwi kwa mikono ya binadamu kana kwamba anahitaji kitu chochote, kwa sababu yeye mwenyewe huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.”

      Ufunuo 4:11. “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.”

      Jinsi Jibu la Biblia Linavyoleta Amani ya Kweli ya Akili

      Kujua kwamba “kila familia . . . duniani hupata jina kutokana” na Mungu kunabadili maoni yetu kuhusu watu wengine. (Waefeso 3:15) Kuwa na ujuzi huo pia kunaongoza jinsi tunavyojiona na kuona matatizo yetu. Fikira zetu zitabadilika katika njia zifuatazo.

      Tunapokabili maamuzi mazito, hatutahangaishwa kupita kiasi na maoni ya watu yenye kupingana. Badala yake, tutategemea kabisa mashauri ya Biblia. Kwa nini? Kwa sababu “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17.

      Ni kweli kwamba ili kufuata mashauri ya Biblia tunapaswa kujitahidi na kujitia nidhamu. Nyakati nyingine huenda mwongozo wake ukatulazimu kutenda kwa njia ambazo zinaonekana hazipatani na mwelekeo wetu. (Mwanzo 8:21) Hata hivyo, tukikubali kwamba tuliumbwa na Baba wa mbinguni mwenye upendo, ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba anajua njia bora zaidi ambayo tunapaswa kufuata. (Isaya 55:9) Neno lake linatuhakikishia hivi: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” (Methali 3:5, 6) Tukitumia shauri hilo, mahangaiko mengi tunayopata tunapokabili matatizo na maamuzi yatakwisha.

      Tunapobaguliwa, hatutalemewa na hisia za kujiona hatufai, na kufikiri kwamba kwa njia fulani hatuna thamani kama watu wa rangi au jamii nyingine. Badala yake, tutajiheshimu kwa usawaziko. Kwa nini? Kwa sababu Baba yetu, Yehova Mungu, “hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” —Matendo 10:34, 35.

      Tukijua hivyo, hatutaruhusu ubaguzi utufanye tuwe na mtazamo mbaya kuelekea watu wengine. Tutaelewa kwamba hatuna sababu yoyote halali ya kujiona kuwa bora kuliko watu wa jamii nyingine, kwa kuwa Mungu “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, ili wakae juu ya uso wa dunia nzima.”—Matendo 17:26.

      Bila shaka, kujua kwamba tuliumbwa na kwamba Muumba wetu anatujali ni msingi wa kupata amani ya kweli ya akili. Lakini tunahitaji kufanya mengi zaidi ili tudumishe amani ya ndani.

      [Blabu katika ukurasa wa 4]

      Je, wanadamu walitokana na mageuzi?

      [Picha katika ukurasa wa 5]

      Kujua kwamba Muumba wetu anatujali kunaweza kutuletea amani ya akili

  • Ni Nini Kusudi la Maisha?
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Februari 1
    • Ni Nini Kusudi la Maisha?

      KWA NINI JIBU LA SWALI HILO NI LA MAANA? Ni mambo machache sana yanayomhangaisha mwanadamu kama wazo la kwamba maisha hayana maana wala kusudi. Kwa upande mwingine, mtu ambaye ana kusudi halisi maishani anavumilia matatizo mengi. Viktor E. Frankl, mtaalamu wa mishipa ambaye aliokoka Maangamizi Makubwa, aliandika hivi: “Hakuna kitu chochote ulimwenguni ambacho ninaweza kusema kinaweza kumsaidia sana mtu kuokoka hata hali mbaya zaidi, kama kujua kwamba maisha yake yana kusudi.”

      Lakini kuna maoni mengi yanayopingana kuhusu jambo hilo. Wengi wanahisi kwamba mtu mwenyewe ndiye anayepaswa kujiamulia kusudi la maisha yake. Kinyume chake, wengine wanaoamini mageuzi wanafundisha kwamba maisha hayana kusudi lolote.

      Hata hivyo, kwa kweli njia nzuri zaidi ya kujua kusudi la maisha ni kujifunza kutoka kwa Yehova Mungu ambaye ni Mpaji-Uhai. Fikiria yale ambayo Neno lake linasema kuhusu jambo hilo.

      Yale Ambayo Biblia Inasema

      Biblia inafundisha kwamba Yehova Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke ili watimize kusudi fulani. Yehova aliwapa wazazi wetu wa kwanza amri ifuatayo.

      Mwanzo 1:28. “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.”

      Mungu alikusudia Adamu na Hawa na watoto wao waifanye dunia yote kuwa paradiso. Hakukusudia wanadamu wazeeke na kufa; wala hakutaka wanadamu wayaharibu mazingira. Hata hivyo, tumerithi dhambi na kifo kwa sababu ya maamuzi mabaya ambayo wazazi wetu wa kwanza walifanya. (Mwanzo 3:2-6; Waroma 5:12) Lakini, kusudi la Yehova halijabadilika. Hivi karibuni dunia itakuwa paradiso.—Isaya 55:10, 11.

      Yehova alituumba tukiwa na uwezo wa kimwili na kiakili wa kutimiza kusudi lake. Hakutuumba ili tuishi bila kumtegemea. Ona jinsi kusudi la Mungu kwa ajili yetu linavyoelezwa na maandiko yafuatayo ya Biblia.

      Mhubiri 12:13. “Huu ndio mwisho wa mambo, kila jambo limekwisha sikiwa: Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.”

      Mika 6:8. “Yehova anataka ni kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?”

      Mathayo 22:37-39. “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza. Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’”

      Jinsi Jibu la Biblia Linavyoleta Amani ya Kweli ya Akili

      Ili mashini yoyote ya hali ya juu ifanye kazi vizuri, ni lazima itumiwe kwa kusudi na kwa njia ambayo mtengenezaji alikusudia. Vivyo hivyo, ili tuepuke kujiumiza wenyewe kiroho, kiakili, kihisia, au kimwili, tunahitaji kutumia maisha yetu kwa njia ambayo Mtengenezaji wetu alikusudia. Fikiria jinsi kujua kusudi la Mungu kunavyoweza kutuletea amani ya akili katika mambo yafuatayo maishani.

      Wanapochagua mambo ya kutanguliza, watu wengi leo wanatumia maisha yao kukusanya mali. Hata hivyo, Biblia inaonya hivi: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru.”—1 Timotheo 6:9, 10.

      Kwa upande mwingine, wale wanaojifunza kumpenda Mungu badala ya pesa wanagundua siri ya kutosheka. (1 Timotheo 6:7, 8) Wanaelewa umuhimu wa kufanya kazi kwa bidii na wanajua kwamba wana wajibu wa kutosheleza mahitaji yao ya kimwili. (Waefeso 4:28) Lakini pia wanachukua kwa uzito onyo hili la Yesu: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda yule mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau yule mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.”—Mathayo 6:24.

      Kwa hiyo, badala ya kutanguliza kazi ya kimwili au utafutaji wa mali maishani, wale wanaompenda Mungu wanaona kufanya mapenzi yake kuwa jambo kuu zaidi maishani mwao. Wanajua kwamba wakitanguliza mapenzi ya Mungu maishani, Yehova Mungu atawatunza. Kwa kweli, Yehova anaona kwamba ana wajibu wa kuwatunza.—Mathayo 6:25-33.

      Wanaposhughulika na wengine, watu wengi wanajitanguliza. Leo, ulimwengu hauna amani, hasa kwa sababu watu wengi sana wamekuwa “wenye kujipenda wenyewe, . . .  wasio na upendo wa asili.”  (2  Timotheo 3:2,  3) Mtu fulani anapowaudhi au kukataa maoni yao, wanamwaga “hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano.” (Waefeso 4:31) Kutojizuia kama huko “huchochea ugomvi” tu badala ya kuleta amani ya akili.— Methali  15:18.

      Kinyume chake, wale wanaotii amri ya Mungu ya kumpenda jirani yao kama wanavyojipenda ni ‘wenye fadhili wao kwa wao, wenye huruma nyororo, wanasameheana kwa hiari.’ (Waefeso 4:32; Wakolosai 3:13) Hata wengine wanapowatendea kwa njia isiyo ya fadhili, wanajitahidi kumwiga Yesu, ambaye alipokuwa akitukanwa “hakujibu kwa matukano.” (1 Petro 2:23) Kama Yesu, wanaelewa kwamba kuwatumikia wengine kunaleta uradhi, hata kuwatumikia wale ambao hawathamini mambo wanayofanyiwa. (Mathayo 20:25-28; Yohana 13:14, 15; Matendo 20:35) Yehova Mungu anawapa roho yake wale wanaomwiga Mwana wake, na roho hiyo inatokeza amani ya kweli katika maisha yao.—Wagalatia 5:22.

      Hata hivyo, maoni yako kuhusu wakati ujao yanaweza kuwa na matokeo gani kwa amani yako ya akili?

      [Blabu katika ukurasa wa 6]

      Mtu anahitaji kuwa na kusudi la wazi maishani

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Yesu anatufundisha jinsi ya kupata amani ya akili

  • Ni Nini Kitakachotokea Wakati Ujao?
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Februari 1
    • Ni Nini Kitakachotokea Wakati Ujao?

      KWA NINI JIBU LA SWALI HILO NI LA MAANA? Matarajio ya mtu ya wakati ujao yanaweza kuongoza jinsi anavyotenda leo. Kwa mfano, wale ambao hawana tumaini la wakati ujao wanaweza kuwa na mtazamo huu: “Na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:32) Mara nyingi mtazamo kama huo hauleti amani ya kweli ya akili, badala yake unawafanya watu wawe walafi, wanywe kupindukia, na wahangaike.

      Kwa kweli, ikiwa wanadamu wangeachiwa kabisa daraka la kujiamulia kuhusu wakati ujao, hatungekuwa na tumaini lolote. Hewa, maji, na udongo wa dunia unachafuliwa kuliko wakati mwingine wowote. Tishio la vita vya nyuklia na mashambulizi ya kigaidi yanaongezeka. Mabilioni ya watu ulimwenguni pote ni wagonjwa na maskini. Hata hivyo, tuna sababu nzuri za kuwa na tumaini.

      Ingawa wanadamu hawawezi kutabiri kwa usahihi wakati ujao, Yehova Mungu anasema yeye ndiye “anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho, na kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa.” (Isaya 46:10) Yehova anasema nini kuhusu kitakachotukia wakati ujao?

      Yale Ambayo Biblia Inasema

      Yehova hataruhusu dunia iharibiwe kabisa au uhai uliomo uangamizwe. Kwa kweli, Biblia inaahidi kwamba Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Kupitia Ufalme wake, au serikali yake ya kimbingu, Yehova ataondoa kabisa uovu duniani na hali ziwe kama alivyokusudia mwanzoni. (Mwanzo 1:26-31; 2:8, 9; Mathayo 6:9, 10) Mistari inayofuata ya Biblia inatusaidia kuelewa wakati ujao. Inaeleza matukio ambayo hivi karibuni yatamgusa kila mtu duniani.

      Zaburi 46:8, 9. “Njooni, tazameni matendo ya Yehova, jinsi ambavyo ameweka matukio ya kushangaza duniani. Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mkuki vipande-vipande; magari ya kukokotwa anayateketeza motoni.”

      Isaya 35:5, 6. “Wakati huo macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Wakati huo kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha. Kwa maana maji yatakuwa yamebubujika katika nyika, na mito katika nchi tambarare ya jangwani.”

      Isaya 65:21, 22. “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale.”

      Danieli 2:44. “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”

      Yohana 5:28, 29. “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Yesu] na kutoka.”

      Ufunuo 21:3, 4. “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”

      Jinsi Jibu la Biblia Linavyoleta Amani ya Kweli ya Akili

      Mwanzoni, huenda mtu akafikiri kwamba hali zinazoelezwa katika maandiko hayo ni ndoto tu. Lakini Mungu ndiye anayetoa ahadi hizo, si wanadamu. Na Yehova Mungu ‘hawezi kusema uwongo.’—Tito 1:2.

      Ukijifunza kutegemea ahadi za Mungu na kuishi kupatana na sheria zake, utakuwa na amani ya akili hata ukikabili hali ngumu zaidi. Vita, umaskini, magonjwa, kifo, na hata matatizo ya uzee hayawezi kukunyang’anya kabisa amani yako. Kwa nini? Kwa sababu una hakika kwamba Ufalme wa Mungu utaondoa kabisa madhara ya matatizo hayo yote.

      Unaweza jinsi gani kuwa na tumaini kama hilo la wakati ujao? Ni lazima ‘ufanye upya akili yako’ na kujihakikishia mwenyewe “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Inaelekea kwamba utahitaji uthibitisho zaidi wa kwamba ahadi za Biblia zinategemeka. Utafaidika ukijitahidi kuchunguza uthibitisho huo. Ni mambo machache sana maishani ambayo yanaweza kukuletea amani nyingi ya akili kuliko jambo hilo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki