Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Maajabu ya Hekima ya Kisilika
    Amkeni!—2007 | Julai
    • Uwezo Unaozidi Silika

      Wanadamu, ambao waliumbwa kwa njia ya kustaajabisha na Mungu, hawaongozwi hasa na silika. Badala yake, sisi ni viumbe wenye uwezo wa kujiamulia mambo kwani tuna dhamiri na uwezo wa kuwapenda watu. (Mwanzo 1:27; 1 Yohana 4:8) Kwa sababu ya kuwa na zawadi hizo zote, tunaweza kufanya maamuzi ya haki na yanayotegemea maadili ambayo nyakati nyingine huonyesha upendo mwingi na kujidhabihu.

      Bila shaka, mtazamo na tabia ya mtu hutegemea hasa kanuni za maadili na za kiroho ambazo alifundishwa au hakufundishwa alipokuwa mchanga. Kwa sababu hiyo, watu wanaweza kuwa na maoni yanayotofautiana kuhusu lililo sawa na lililo kosa, kuhusu linalofaa na lisilofaa. Tofauti hizo zinaweza kutokeza kutoelewana, kutovumiliana na hata kuchukiana, hasa ikiwa mambo kama utamaduni, uzalendo, na dini yanahusika.

      Ulimwengu ungekuwa bora zaidi ikiwa familia yote ya wanadamu ingefuata viwango vilevile ambavyo vinapatana na maadili na kanuni za Biblia, kama tu sote tunavyofuata sheria zilezile za kiasili zinazoongoza ulimwengu wote! Lakini je, kuna mtu yeyote aliye na uwezo na ujuzi wa kuweka viwango vya kufuatwa ulimwenguni pote? Ikiwa yupo, je, atafanya hivyo? Je, tayari amefanya hivyo? Maswali hayo yatajibiwa katika makala inayofuata.

  • Mwongozo Bora Kuliko Silika
    Amkeni!—2007 | Julai
    • Mwongozo Bora Kuliko Silika

      “Ikiwa kila mtu ataruhusiwa kujichagulia maadili yake, bila kuwa na kanuni za kuamua ikiwa maadili hayo ni sawa, basi lazima sheria itatumiwa kuhakikisha kwamba kuna tabia nzuri.” —DAKT. DANIEL CALLAHAN.

      TUNAWEZA kuona ukweli wa maneno ya Callahan kwani watu wanazidi kupuuza kanuni za maadili hivi kwamba katika sehemu nyingi ulimwenguni, serikali zimelazimika kuweka sheria nyingi ili kuzuia uhalifu. Katika mkutano wa kwanza kabisa wa Kongamano la Akina Mama wa Nigeria, rais wa Nigeria alieleza mahangaiko yake kuhusu wakati ujao wa taifa hilo. Hakuwa akifikiria siasa au umaskini, bali “tatizo zito zaidi,” yaani, “kumomonyoka kwa . . . maadili ya msingi katika familia, kazini, katika jamii na hata katika taifa zima.”

      Uchunguzi uliofanyiwa akina mama 1,736 nchini Uingereza ulionyesha kwamba “familia zinazorota kwa sababu ya kuporomoka kwa maadili na kuongezeka kwa familia zenye mzazi mmoja.” Vilevile, maadili yanaporomoka kwa kasi nchini China. Gazeti Time linaripoti kwamba watu wanaanza kufanya ngono mapema zaidi maishani na wana wapenzi wengi kuliko zamani. “Haya ni maisha yangu, nami naweza kufanya chochote ninachotaka,” akasema msichana mmoja Mchina ambaye alijivunia kuwa na zaidi ya wapenzi 100.

      Kuporomoka kwa maadili kumewaathiri pia wenye mamlaka. “Watu hawawaoni viongozi wao kuwa mifano ya kuigwa kiadili,” akasema Javed Akbar katika gazeti la Kanada Toronto Star. Aliongezea kusema kwamba wanasiasa, wasimamizi wa mashirika, na pia viongozi wa kidini “wanaonekana kuwa hawana maadili mazuri.”

      Kwa Nini Maadili Yameporomoka?

      Mambo kadhaa yamechangia hali hiyo. Jambo moja ni roho ya kuasi kanuni ambazo zimekuwepo kwa muda mrefu. Kwa mfano, uchunguzi uliofanywa Kusini mwa Marekani ulionyesha kwamba wanafunzi wengi wa chuo kikuu waliamini “mtu anapaswa kujiamulia mwenyewe tofauti kati ya mema na mabaya.”

      Mwandishi wa mambo ya kisiasa Zbigniew Brzezinski alitaja sababu nyingine. Aliandika kwamba watu leo “hukazia kutosheleza tamaa zao, na kwamba anasa ndilo jambo linaloamua jinsi tabia za watu zitakavyokuwa.” Uhuru na uwezo wa kufanya maamuzi yanayopatana na maadili, ubinafsi, na kujitosheleza tu kunaweza kukuvutia, lakini je, kunasaidia uwe na furaha ya kweli, uradhi, na uhusiano mzuri zaidi pamoja na wengine?

      “Hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake,” akasema Yesu. (Mathayo 11:19) Je, kuporomoka kwa maadili kumewafanya watu wawe na furaha na uradhi zaidi? Fikiria matokeo kadhaa: kiwango cha kutowaamini wengine kimeongezeka, hakuna usalama, uhusiano unavunjika, watoto wanakua bila baba au mama, magonjwa ya kuambukiza yanayopitishwa kingono, mimba zisizotakiwa, uraibu wa dawa za kulevya, na jeuri. Mambo haya hayaonyeshi uradhi na kufanikiwa badala yake ni huzuni na kushindwa.—Wagalatia 6:7, 8.

      Baada ya kuona matatizo kama hayo katika siku zake, nabii wa Mungu, Yeremia, alisema hivi: “Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Ndiyo, Mungu hakutuumba tujiongoze, yaani, tujiamulie mema na mabaya. Kinachoonekana kuwa kizuri kwetu kinaweza kudhuru. Methali 14:12 inasema: “Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.”

      Adui Aliye Ndani Yetu!

      Kwa nini tunahitaji mwongozo kuhusiana na maadili? Kwa sababu mioyo yetu inaweza kutudanganya. Biblia inasema hivi katika Yeremia 17:9: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?” Ukijua mtu ni mwenye hila na hatari, ungemwamini? La hasha! Hata hivyo, kila mmoja wetu ana moyo ambao una sifa hizohizo. Kwa hiyo, Mungu anatupa onyo hili: “Anayetegemea moyo wake mwenyewe ni mjinga, lakini yeye anayetembea katika hekima ndiye atakayeponyoka.”—Methali 28:26.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki