-
Maoni ya Mungu Juu ya Usafi wa KiadiliMnara wa Mlinzi—2000 | Novemba 1
-
-
Maoni ya Mungu Juu ya Usafi wa Kiadili
“Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.”—ISAYA 48:17.
1, 2. (a) Kwa ujumla watu huonaje maadili ya ngono? (b) Wakristo wana maoni gani kuhusu maadili ya ngono?
KATIKA sehemu nyingi za dunia leo, mwenendo wa kiadili unaonwa kuwa suala la kibinafsi. Watu huona kufanya ngono kuwa njia ya kawaida ya kuonyesha upendo na kwamba watu waweza kufanya hivyo wakati wowote wanapotaka, wala si wenzi wa ndoa peke yao walio na haki ya kufanya ngono. Wanahisi kwamba ikiwa hakuna anayeumizwa, basi si vibaya mtu kujiamulia atakavyojiendesha. Kwa maoni yao, watu hawapaswi kuamuliwa mambo ya kiadili, hasa ngono.
2 Wale ambao wamemjua Yehova wana maoni tofauti. Wanafurahia kufuata miongozo ya Maandiko kwa sababu wanampenda Yehova na wanataka kumpendeza. Wanatambua kwamba Yehova anawapenda na huwapa mwongozo wenye kuwafaidi, mwongozo ambao utawanufaisha kikweli na kuwafurahisha. (Isaya 48:17) Kwa kuwa Mungu ndiye Chanzo cha uhai, inafaa wamtegemee ili wapate mwongozo wa jinsi ya kutumia miili yao, hasa katika suala hili linalohusiana sana na kupitisha uhai.
Zawadi Kutoka kwa Muumba Mwenye Upendo
3. Wengi katika Jumuiya ya Wakristo wamefundishwa nini kuhusu kufanya ngono, na maoni hayo yanatofautianaje na yale ambayo Biblia hufundisha?
3 Tofauti na ulimwengu wa sasa, baadhi ya watu katika Jumuiya ya Wakristo wamefundisha kwamba ni aibu na ni dhambi kufanya ngono, na kwamba “dhambi ya awali” katika bustani ya Edeni ilitokea baada ya Hawa kumtongoza Adamu wafanye ngono. Maoni hayo yanapingana na Maandiko yaliyopuliziwa. Biblia hurejezea wanadamu wawili wa kwanza kuwa “mwanamume na mkewe.” (Mwanzo 2:25, Biblia Habari Njema) Mungu aliwaambia wazae watoto, kwa kusema hivi: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi.” (Mwanzo 1:28) Ni jambo ambalo halingepatana na akili Mungu kuwaamuru Adamu na Hawa wazae watoto kisha awaadhibu kwa kutekeleza maagizo hayo.—Zaburi 19:8.
4. Kwa nini Mungu aliwapa wanadamu uwezo wa kufanya ngono?
4 Katika amri hiyo iliyotolewa kwa wazazi wetu wa kwanza, na kurudiwa kwa Noa na watoto wake, twaona kusudi kuu la uhusiano wa ngono: kuzaa watoto. (Mwanzo 9:1) Hata hivyo, Neno la Mungu laonyesha kwamba watumishi wake waliofunga ndoa wanaweza kufanya ngono hata wasipotaka kuzaa watoto. Uhusiano huo waweza kutimiza ifaavyo mahitaji ya kihisia-moyo na ya kimwili na waweza kuwafurahisha wenzi waliooana. Ni njia moja ya kuonyeshana upendo wenye kina.—Mwanzo 26:8, 9; Mithali 5:18, 19; 1 Wakorintho 7:3-5.
Vizuizi Vilivyowekwa na Mungu
5. Ni vizuizi gani ambavyo Mungu amewekea wanadamu kuhusu ngono?
5 Ingawa ngono ni zawadi kutoka kwa Mungu, yapasa kuwa na mipaka. Kanuni hiyo yatumika hata katika ndoa. (Waefeso 5:28-30; 1 Petro 3:1, 7) Kufanya ngono kumekatazwa nje ya ndoa. Biblia husema mambo wazi kuhusu suala hili. Katika Sheria ambayo Mungu alilipa taifa la Israeli, ilisemwa hivi: “Usizini.” (Kutoka 20:14) Baadaye, Yesu alitia ndani “uasherati” na “uzinzi” pamoja na “mawazowazo mabaya” ambayo hutoka moyoni na kumchafua mtu. (Marko 7:21, 22) Mtume Paulo alipuliziwa kuwashauri Wakristo katika Korintho hivi: “Ukimbieni uasherati.” (1 Wakorintho 6:18) Na katika barua yake kwa Waebrania, Paulo aliandika hivi: “Acheni ndoa iwe yenye kuheshimika miongoni mwa wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila kutiwa unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.”—Waebrania 13:4.
6. Katika Biblia, neno “uasherati” latia ndani nini?
6 Neno “uasherati” lamaanisha nini? Latokana na neno la Kigiriki por·neiʹa, ambalo nyakati nyingine hutumiwa kurejezea ngono kati ya watu wasiofunga ndoa. (1 Wakorintho 6:9) Kwingineko, kama vile katika Mathayo 5:32 na Mathayo 19:9, neno hilo lina maana zaidi na hurejezea uzinzi, ngono ya maharimu, na ngono na mnyama. Mazoea mengine ya ngono kati ya watu wasiofunga ndoa, kama vile ngono inayohusisha mdomo na mkundu, na kushika-shika viungo vya uzazi vya mtu mwingine, yaweza kuitwa por·neiʹa pia. Mazoea hayo yote hulaumiwa—ama waziwazi ama kwa kugusiwa tu—katika Neno la Mungu.—Mambo ya Walawi 20:10, 13, 15, 16; Waroma 1:24, 26, 27, 32.a
Kunufaika na Sheria za Mungu za Kiadili
7. Tunanufaikaje kwa kudumisha usafi wa kiadili?
7 Linaweza kuwa jambo gumu kwa wanadamu wasiokamilika kutii mwongozo wa Yehova kuhusu mwenendo wa kingono. Maimonides, mwanafalsafa mashuhuri Myahudi wa karne ya 12, aliandika hivi: “Hakuna katazo katika Torati [Sheria ya Kimusa] nzima lililo gumu kutii kama lile la ngono ya maharimu na ngono haramu.” Lakini iwapo tunatii mwongozo wa Mungu tunanufaika sana. (Isaya 48:18) Kwa mfano, kuonyesha utii katika mambo hayo hutulinda na maradhi ya kuambukizwa kingono, ambayo baadhi yake hayana dawa na yanaweza kuua.b Tunalindwa tusipate mimba nje ya ndoa. Kutumia hekima ya Mungu pia huchangia dhamiri safi. Kufanya hivyo huchangia kujistahi na kufanya tuheshimiwe na wengine, kutia ndani watu wetu wa jamaa, wenzi wetu, watoto wetu, na ndugu na dada zetu Wakristo. Pia hutufanya tuwe na mtazamo unaofaa kuhusu ngono ambao utatokeza furaha katika ndoa. Mwanamke mmoja Mkristo aliandika hivi: “Kweli ya Neno la Mungu ndiyo ulinzi bora kabisa. Ninangoja kuolewa, na nitakapoolewa, nitafurahi sana kumwambia mwanamume Mkristo atakayenioa kwamba nimedumisha usafi wa kiadili.”
8. Ni katika njia zipi mwenendo wetu wa kiadili huchangia ibada safi?
8 Kwa kudumisha mwenendo safi wa kiadili, twaweza pia kuvutia watu kwa Mungu tunayeabudu na kufanya wengi wasiielewe vibaya ibada safi. Mtume Petro aliandika hivi: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa bora miongoni mwa mataifa, ili, katika jambo ambalo katika hilo wao wanasema dhidi yenu kuwa watenda-maovu, likiwa tokeo la kazi zenu bora ambazo wamekuwa mashahidi wa kujionea wapate kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.” (1 Petro 2:12) Hata ikiwa wale wasiomtumikia Yehova hawatambui wala hawaungi mkono mwenendo wetu safi kiadili, twaweza kuwa na hakika kwamba Baba yetu wa kimbingu, anaona, anapendezwa nasi, na hata anafurahia jitihada zetu za kufuata mwongozo wake.—Mithali 27:11; Waebrania 4:13.
9. Kwa nini twapaswa kuwa na uhakika katika mwongozo wa Mungu, hata ingawa huenda tusielewe kabisa sababu za kutoa mwongozo huo? Fafanua.
9 Kumwamini Mungu kwatia ndani kuwa na uhakika kwamba anajua yale yanayotufaa zaidi, hata kama hatuelewi kabisa sababu zote za kutuongoza kama afanyavyo. Fikiria kielelezo kimoja katika Sheria ya Kimusa. Kanuni moja kuhusu kambi za kijeshi ilisema kwamba kinyesi chapasa kufukiwa nje ya kambi. (Kumbukumbu la Torati 23:13, 14) Labda Waisraeli walijiuliza ni kwa nini mwongozo huo ulitolewa; labda wengine walifikiri haukuwa wa lazima. Hata hivyo, tangu wakati huo, sayansi ya kitiba imegundua kwamba sheria hiyo ilisaidia kuzuia maji yasichafuliwe na kuzuia maradhi mengi yanayopitishwa na wadudu. Vivyo hivyo, kuna sababu za kiroho, kijamii, kihisia-moyo, kimwili, na kiakili zinazofanya Mungu akataze kufanya ngono nje ya ndoa. Acheni sasa tuchunguze mifano michache ya Biblia ya watu waliodumisha usafi wa kiadili.
Yosefu—Alibarikiwa kwa Sababu ya Mwenendo Wake wa Kiadili
10. Ni nani aliyejaribu kumtongoza Yosefu, naye alijibuje?
10 Yaelekea unafahamu mfano unaotajwa katika Biblia wa Yosefu, mwana wa Yakobo. Akiwa na umri wa miaka 17, alijikuta akiwa mtumwa wa Potifa, mkuu wa walinzi wa Farao wa Misri. Yehova alimbariki Yosefu, na baada ya muda akawekwa kuwa msimamizi wa nyumba ya Potifa. Alipofikisha umri wa miaka 20, Yosefu alikuwa “mtu mzuri, na mwenye uso mzuri.” Mke wa Potifa alivutiwa naye na kujaribu kumtongoza. Yosefu alitangaza waziwazi msimamo wake, akisema kwamba kukubali ombi hilo hakungekuwa kumsaliti tu bwana wake bali pia kungekuwa ni “kumkosea Mungu.” Kwa nini Yosefu alisababu hivyo?—Mwanzo 39:1-9, BHN.
11, 12. Ingawa hakukuwa na sheria yoyote ya Mungu iliyoandikwa ambayo ilikataza uasherati na uzinzi, kwa nini Yosefu alisababu jinsi hiyo?
11 Kwa wazi, Yosefu hakufikia uamuzi huo kwa sababu ya kuogopa kugunduliwa na watu. Familia ya Yosefu iliishi mbali sana, na baba yake alifikiri kwamba alikuwa amekufa. Ikiwa Yosefu angejihusisha na ukosefu wa adili katika ngono, familia yao haingejua kamwe. Labda Potifa na watumishi wake wa kiume wangeweza kufichwa dhambi hiyo, kwa kuwa kuna nyakati ambazo hawakuwa nyumbani. (Mwanzo 39:11) Lakini Yosefu alijua kwamba hangeweza kumficha Mungu mwenendo huo.
12 Lazima Yosefu awe alitafakari juu ya mambo aliyojua kuhusu Yehova. Bila shaka alijua yale aliyosema Yehova katika bustani ya Edeni: “Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Zaidi ya hayo, yaelekea Yosefu alijua yale ambayo Yehova alimwambia mfalme Mfilisti aliyejaribu sana kumtongoza Sara mama ya nyanya ya Yosefu. Yehova alimwambia hivi mfalme huyo: “Umekuwa mfu wewe kwa sababu ya mwanamke huyu uliyemtwaa, maana ni mkewe mtu. . . . Nami nikakuzuia usinitendee dhambi, kwa hiyo sikukuacha umguse.” (Mwanzo 20:3, 6, Italiki ni zetu.) Kwa hiyo ingawa Yehova hakuwa ameandika sheria yoyote kufikia wakati huo, Yosefu alifahamu waziwazi maoni ya Yehova kuhusu ndoa. Uwezo wa Yosefu wa kupambanua mema na mabaya pamoja na tamaa ya kumpendeza Yehova, vilimfanya akatae ukosefu wa adili.
13. Yaelekea ni kwa nini Yosefu hangeweza kumkwepa mke wa Potifa?
13 Hata hivyo, mke wa Potifa aliendelea kumwomba “siku baada ya siku” alale naye. Kwa nini Yosefu hakumkwepa tu? Kwa kuwa alikuwa mtumwa, alikuwa na kazi za kufanya na hivyo hangeweza kubadili hali yake. Uthibitisho wa kiakiolojia wadokeza kwamba kwa sababu ya mtindo wa ujenzi wa nyumba za Wamisri ilikuwa lazima mtu apite katikati ya sehemu kuu ya nyumba ili kufika kwenye maghala. Kwa hiyo, labda Yosefu hangeweza kumwepuka mke wa Potifa.—Mwanzo 39:10.
14. (a) Ni nini kilichompata Yosefu alipomkimbia mke wa Potifa? (b) Yehova alimbarikije Yosefu kwa uaminifu wake?
14 Siku ikafika walipojikuta peke yao nyumbani. Mke wa Potifa akamshika Yosefu huku akisema kwa sauti: “Lala nami.” Yosefu akakimbia. Mke wa Potifa aliumia sana kihisia-moyo alipokataliwa na akamshtaki Yosefu kuwa alijaribu kumbaka. Matokeo yakawa nini? Je, Yehova alimthawabisha papo hapo kwa sababu ya mwendo wake wa kushika uaminifu-maadili? La. Yosefu alitupwa gerezani na kufungwa kwa pingu. (Mwanzo 39:12-20; Zaburi 105:18) Yehova aliona udhalimu aliotendewa Yosefu na hatimaye akamkweza kutoka gerezani hadi kwenye nyumba ya mfalme. Akawa mtu wa pili mwenye uwezo mkubwa zaidi nchini Misri na kubarikiwa kupata mke na watoto. (Mwanzo 41:14, 15, 39-45, 50-52) Zaidi ya hayo, masimulizi ya uaminifu-maadili wa Yosefu yaliandikwa miaka 3,500 iliyopita ili watumishi wa Mungu waendelee kuyasoma tangu wakati huo. Ni baraka zilizoje zinazopatikana kwa kufuata sheria za Mungu za uadilifu! Vivyo hivyo, huenda sisi leo tusione manufaa ya papo hapo ya kudumisha uaminifu-maadili, lakini twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaona na atatubariki kwa wakati wake.—2 Mambo ya Nyakati 16:9.
‘Agano [la Yobu] na Macho Yake’
15. ‘Agano la Yobu na macho yake’ lilikuwa gani?
15 Yobu pia alishika uaminifu-maadili. Wakati wa majaribu aliyoletewa na Ibilisi, Yobu alichunguza maisha yake na kusema kwamba alikuwa tayari kuadhibiwa vikali iwapo, miongoni mwa kanuni nyingine, alikuwa amekiuka kanuni ya Yehova ya adili za ngono. Yobu alisema hivi: “Nilifanya agano na macho yangu; basi nawezaje kumwangalia msichana?” (Ayubu 31:1) Kwa kusema hivyo, Yobu alimaanisha kwamba katika uamuzi wake wa kushika uaminifu-maadili kwa Mungu, alikuwa ameazimia kuepuka kumwangalia mwanamke kwa kumtamani. Bila shaka, angeona wanawake kila siku na labda kuwasaidia walipohitaji msaada. Lakini hakuwatazama akiwa na lengo la kutafuta mahaba. Kabla ya majaribu yake, alikuwa na mali mengi, “mkuu sana kuliko watu wote wa upande wa mashariki.” (Ayubu 1:3) Hata hivyo, hakutumia mali yake kuvutia wanawake wengi. Ni wazi kwamba hakucheza-cheza na wazo la kujihusisha katika ngono haramu na wasichana.
16. (a) Kwa nini Yobu ni kielelezo kizuri kwa Wakristo waliofunga ndoa? (b) Tabia ya wanaume walioishi siku za Malaki ilitofautianaje na ya Yobu, na hali ikoje leo?
16 Hivyo, katika nyakati zifaazo hali kadhalika nyakati ngumu, Yobu alidhihirisha uaminifu-maadili. Yehova aliona jambo hilo na kumbariki sana. (Ayubu 1:10; 42:12) Yobu ni kielelezo kizuri kama nini kwa wanaume na wanawake Wakristo waliofunga ndoa! Si ajabu kwamba Yehova alimpenda kadiri hiyo! Tofauti na Yobu, tabia ya watu wengi leo inafanana sana na ya watu wa siku za Malaki. Nabii huyo alilaumu jinsi waume wengi walivyoacha wake zao, na mara nyingi kuoa wasichana. Madhabahu ya Yehova ilifunikwa kwa machozi ya wake walioachwa, na Mungu alilaumu wale ‘waliotenda mambo ya hiana’ dhidi ya wake zao.—Malaki 2:13-16.
Msichana Aliye Safi Kiadili
17. Mshulami alikuwaje kama “bustani iliyofungwa”?
17 Mtu wa tatu aliyeshika uaminifu-maadili ni msichana Mshulami. Alivutia mvulana mchungaji na pia Solomoni, mfalme tajiri wa Israeli, kwa kuwa alikuwa mchanga tena mrembo. Katika masimulizi yote yenye kuvutia yapatikanayo katika Wimbo Ulio Bora, Mshulami alidumisha usafi wa kiadili, na kuheshimiwa na watu walioishi karibu naye. Ingawa Solomoni alikataliwa naye, alipuliziwa kuandika simulizi juu yake. Mchungaji aliyempenda pia aliheshimu msimamo wake safi kiadili. Pindi moja aliwaza kwamba Mshulami alikuwa kama “bustani iliyofungwa.” (Wimbo Ulio Bora 4:12) Katika Israeli la kale, bustani nzuri zilikuwa na mboga zenye kupendeza za namna mbalimbali, maua yenye harufu nzuri, na miti ya fahari. Bustani hizo zilizingirwa ua au ukuta na mtu angeweza kuingia tu kupitia lango lililofungwa. (Isaya 5:5) Mchungaji aliona usafi wa kiadili na uzuri wa Mshulami huyo kuwa kama bustani hiyo yenye umaridadi adimu. Alikuwa safi kabisa kiadili. Angedhihirisha upendo mwororo tu kwa yule ambaye angekuja kumwoa.
18. Masimulizi ya Yosefu, Yobu na Mshulami yatukumbusha nini?
18 Mshulami aliwekea wanawake Wakristo leo kielelezo bora kabisa cha uaminifu-maadili. Yehova aliona na kuthamini wema wa adili wa msichana Mshulami na kumbariki kama alivyombariki Yosefu na Yobu. Matendo yao ya uaminifu-maadili yameandikwa katika Neno la Mungu ili kutuongoza. Ingawa jitihada zetu za kudumisha uaminifu-maadili leo haziandikwi katika Biblia, Yehova ana “kitabu cha ukumbusho” kwa wale wanaojitahidi kufanya mapenzi yake. Na tusisahau kamwe kwamba Yehova “anasikiliza” na kushangilia tunapojitahidi kwa uaminifu kudumisha usafi wa kiadili.—Malaki 3:16.
19. (a) Twapaswa kuuonaje usafi wa kiadili? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala ifuatayo?
19 Ijapokuwa wasio na imani huenda wakatudhihaki, tunafurahi kumtii Muumba wetu mwenye upendo. Tuna maadili ya kiwango cha juu zaidi, maadili ya Mungu. Tunajivunia hayo, tunayaona kuwa hazina. Kwa kudumisha msimamo safi wa kiadili, twaweza kufurahia baraka za Mungu na kudumisha tumaini hakika la baraka za wakati ujao zisizo na kikomo. Hata hivyo, twaweza kufanya nini ili kudumisha usafi wa kiadili? Makala ifuatayo itazungumzia swali hilo muhimu.
[Maelezo ya Chini]
b Kwa kusikitisha, kuna hali ambazo Mkristo asiye na hatia hupatwa na maradhi yanayoambukizwa kingono kutoka kwa mwenzi asiyeamini ambaye hafuati mwongozo wa Mungu.
-
-
Unaweza Kudumisha Usafi wa KiadiliMnara wa Mlinzi—2000 | Novemba 1
-
-
Unaweza Kudumisha Usafi wa Kiadili
“Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake.”—1 YOHANA 5:3.
1. Kuna tofauti gani ya mwenendo kati ya watu leo?
ZAMANI za kale, nabii Malaki alipuliziwa kutabiri juu ya wakati ambapo mwenendo wa watu wa Mungu ungetofautiana kabisa na wa watu wasiomtumikia Mungu. Nabii huyo aliandika hivi: “Ndipo mtakaporudi, nanyi mtapambanua kati ya wenye haki na waovu, na kati ya yeye amtumikiaye Mungu na yeye asiyemtumikia.” (Malaki 3:18) Unabii huo unatimizwa leo. Kushika amri za Mungu, kutia ndani zile zinazodai usafi wa kiadili, ndio mwendo unaofaa na wa busara maishani. Hata hivyo, kwa kawaida huo si mwendo rahisi. Yesu alikuwa na sababu nzuri aliposema kwamba lazima Wakristo wajikakamue wenyewe kisulubu ili kupata wokovu.—Luka 13:23, 24.
2. Kuna msongo gani kutoka nje unaofanya iwe vigumu kwa wengine kudumisha usafi wa kiadili?
2 Kwa nini ni vigumu kudumisha usafi wa kiadili? Sababu moja ni kwamba kuna mkazo kutoka nje. Biashara ya vitumbuizo huonyesha ngono haramu kuwa yenye kusisimua, yenye kupendeza, inayofanya mmoja aonekane kuwa mtu mzima, huku ikipuuza kabisa matokeo yake yenye kudhuru. (Waefeso 4:17-19) Uhusiano wa kingono unaoonyeshwa mara nyingi huwa kati ya wenzi wasiofunga ndoa. Mara nyingi sinema na vipindi vya televisheni huonyesha uhusiano wa kingono katika hali ambayo watu hawawajibiki. Kwa kawaida hakuna uchangamfu na kustahiana. Wengi wameona vipindi hivyo tangu utotoni. Isitoshe, kuna mkazo mkubwa sana wa marika wa kujipatanisha na maadili malegevu ya kisasa, na wale wasiofanya hivyo nyakati nyingine hudhihakiwa au hata kutukanwa.—1 Petro 4:4.
3. Ni zipi baadhi ya sababu zinazofanya wengi ulimwenguni wajihusishe na ukosefu wa adili?
3 Mkazo kutoka ndani pia hufanya iwe vigumu kudumisha usafi wa kiadili. Yehova aliwaumba wanadamu wakiwa na tamaa ya ngono, na tamaa hiyo yaweza kuwa kubwa. Tamaa inahusiana na yale tunayofikiri, na ukosefu wa adili unahusiana na kufikiri juu ya mambo yasiyopatana na mawazo ya Yehova. (Yakobo 1:14, 15) Kwa mfano, kulingana na uchunguzi wa hivi majuzi uliochapishwa katika British Medical Journal, watu wengi waliofanya ngono mara ya kwanza walitaka tu kujua mtu huhisije. Wengine waliamini kwamba wengi wa marika wao walikuwa wakifanya ngono, kwa hiyo wao pia wakataka kuanza. Na bado wengine walisema kwamba walishindwa kudhibiti hisia zao au walikuwa “wamelewa kidogo wakati huo.” Tukitaka kumpendeza Mungu, lazima tufikiri kwa njia tofauti. Ni kufikiri kwa aina gani ambako kutatusaidia kudumisha usafi wa kiadili?
Sitawisha Msimamo Thabiti
4. Yatupasa kufanya nini ili tudumishe usafi wa kiadili?
4 Ili tudumishe usafi wa kiadili, lazima tutambue kwamba inafaa kuishi maisha ya kiadili. Hiyo yapatana na yale ambayo mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wa Roma: “[Jithibitishieni] wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Kutambua kwamba usafi wa kiadili unafaa kwahusisha mengi zaidi kuliko kujua tu ukosefu wa adili unakatazwa katika Neno la Mungu. Kwahusisha kuelewa sababu zinazofanya ukosefu wa adili ukatazwe na jinsi tunavyonufaika kwa kuuepuka. Baadhi ya sababu hizo zilizungumziwa katika makala iliyotangulia.
5. Ni kwa nini hasa Wakristo wanapaswa kudumisha usafi wa kiadili?
5 Hata hivyo, kwa kweli sababu kubwa zinazofanya Wakristo waepuke ukosefu wa adili katika ngono zategemea uhusiano wetu na Mungu. Tumejifunza kwamba anajua yale yanayotufaa zaidi. Kumpenda kutatusaidia tuchukie lililo baya. (Zaburi 97:10) Mungu ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu.” (Yakobo 1:17) Anatupenda. Kwa kumtii, twaonyesha kwamba twampenda na kuthamini yote ambayo ametufanyia. (1 Yohana 5:3) Hatutaki kamwe kumtamausha wala kumwumiza Yehova kwa kuvunja amri zake za uadilifu. (Zaburi 78:41) Hatungependa kujiendesha kwa njia ambayo itafanya ibada yake takatifu na adilifu itukanwe. (Tito 2:5; 2 Petro 2:2) Kwa kudumisha usafi wa kiadili, tunamfurahisha Aliye Mkuu Kabisa.—Mithali 27:11.
6. Kujulisha wengine viwango vyetu vya kiadili kunasaidiaje?
6 Tuazimiapo kudumisha usafi wa kiadili, tutapata ulinzi zaidi kwa kuwaeleza wengine msimamo huo. Wajulishe watu kwamba wewe ni mtumishi wa Yehova Mungu na kwamba umeazimia kudumisha viwango vyake vya juu. Ni maisha yako, mwili wako, uchaguzi wako. Ni nini kimo hatarini? Uhusiano wako wenye thamani pamoja na Baba yako wa kimbingu. Kwa hiyo onyesha waziwazi kwamba huwezi kamwe kubadili msimamo wako wa uaminifu-maadili. Jivunie kumwakilisha Mungu kwa kutegemeza kanuni zake. (Zaburi 64:10) Usiaibike kamwe kuzungumza juu ya msimamo wako wa maadili na wengine. Kusema waziwazi kwaweza kukuimarisha, kukulinda, na kuwatia moyo wengine wafuate kielelezo chako.—1 Timotheo 4:12.
7. Tunaweza kudumishaje azimio letu la kubaki safi kiadili?
7 Kisha, baada ya kuazimia kudumisha viwango vya juu vya adili na kujulisha msimamo wetu, lazima tuchukue hatua za kushikamana na azimio letu. Njia moja ya kufanya hivyo ni kuwa waangalifu tunapochagua marafiki. “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima,” yasema Biblia. Shirikiana na wale wanaofuata kanuni sawa na wewe; watakuimarisha. Pia andiko hilo lasema hivi: “Bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Kwa kadiri uwezavyo, epuka watu wanaoweza kudhoofisha azimio lako.—1 Wakorintho 15:33.
8. (a) Kwa nini twapaswa kulisha akili zetu mambo yanayofaa? (b) Twapaswa kuepuka nini?
8 Zaidi ya hayo, twahitaji kulisha akili zetu mambo yaliyo ya kweli, mazito, ya uadilifu, yaliyo safi kiadili, ya kupendeka, yanayosemwa vema, yenye wema wa adili, na yanayostahili sifa. (Wafilipi 4:8) Tunafanya hivyo kwa kuteua yale tunayotazama na kusoma na muziki tunaosikiliza. Kusema kwamba vichapo visivyo vya adili havipotoshi mtu ni sawa na kusema kwamba vichapo vyenye mambo ya adili haviathiri mtu ifaavyo. Kumbuka kwamba wanadamu wasiokamilika wanaweza kutumbukia kwa urahisi katika ukosefu wa adili. Kwa hiyo, vitabu, magazeti, sinema, na muziki unaochochea nyege utaongoza kwenye tamaa mbaya ambazo hatimaye zaweza kuongoza kwenye dhambi. Ili tudumishe usafi wa kiadili lazima tujaze akili zetu hekima ya Mungu.—Yakobo 3:17.
Hatua Zinazoongoza Kwenye Ukosefu wa Adili
9-11. Kama ilivyosimuliwa na Solomoni, ni hatua zipi zilizomwongoza kijana fulani kutumbukia katika ukosefu wa adili?
9 Mara nyingi, kuna hatua dhahiri ambazo huongoza kwenye ukosefu wa adili. Hatua moja inapopigwa inakuwa vigumu sana kurudi nyuma. Ona jinsi jambo hilo linavyoelezwa katika Mithali 7:6-23. Solomoni aona “kijana asiyekuwa na akili,” au asiyekuwa na nia njema. Kijana huyo ‘anapita njiani karibu na pembe yake [ya kahaba], akiishika njia iendayo nyumbani kwake, wakati wa magharibi, wakati wa jioni.’ Anafanya kosa la kwanza. Wakati wa jioni, “moyo” wake umemwelekeza, si katika barabara yoyote ile, bali katika barabara ambayo anajua kwa kawaida inaweza kuwa na kahaba.
10 Kisha twasoma hivi: “Tazama, mwanamke akamkuta, ana mavazi ya kikahaba, mwerevu wa moyo.” Sasa kijana anamwona! Anaweza kugeuka na kurudi nyumbani, lakini sasa ni vigumu zaidi kuliko hapo awali, hasa kwa kuwa yeye ni dhaifu kiadili. Huyo mwanamke anamshika na kumbusu. Baada ya kukubali busu, sasa anasikiliza utongozi wake: “Kwangu ziko sadaka za amani,” asema. “Leo hivi nimeziondoa nadhiri zangu.” Sadaka za amani zilitia ndani nyama, unga, mafuta, na divai. (Mambo ya Walawi 19:5, 6; 22:21; Hesabu 15:8-10) Kwa kutaja vitu hivyo, labda alikuwa akimdokezea kwamba hali yake ya kiroho haikuwa mbaya, na wakati huohuo, labda alikuwa akimjulisha kwamba kulikuweko vyakula na vinywaji vingi tena vizuri nyumbani mwake. “Haya,” anamsihi “na tushibe upendo hata asubuhi, tujifurahishe nafsi zetu kwa mahaba.”
11 Si vigumu kujua matokeo yalikuwaje. “Kwa ubembelezi wa midomo yake akamshinda.” Kijana akamfuata kahaba nyumbani “kama vile ng’ombe aendavyo machinjoni” na “kama ndege aendaye haraka mtegoni.” Solomoni amalizia kwa maneno yenye kuamsha fikira: “Wala hajui ya kuwa ni hasara ya nafsi yake.” Nafsi, au uhai wake wahusika kwa sababu “Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Waebrania 13:4) Ni somo lenye maana kubwa kama nini kwa wanaume na wanawake! Twapaswa kuepuka kuchukua hatua za kwanzakwanza zitakazotuongoza kukosa kibali cha Mungu.
12. (a) Usemi “asiyekuwa na akili” wamaanisha nini? (b) Twaweza kuimarishaje nguvu za kiadili?
12 Ona kwamba kijana anayesimuliwa ‘hakuwa na akili.’ Usemi huo watuonyesha kwamba mawazo, tamaa, shauku, hisia-moyo, na miradi yake maishani haikupatana na yale ambayo Mungu hukubali. Udhaifu wake wa kiadili ulitokeza mambo yenye kuhuzunisha. Katika “siku [hizi] za mwisho” zenye hatari, jitihada inahitajiwa ili kusitawisha nguvu za kiadili. (2 Timotheo 3:1) Mungu ametuandalia misaada. Huandaa mikutano ya kutaniko la Kikristo ili kututia moyo tuendelee kufuata njia inayofaa na kuwa na ushirika na wale walio na miradi kama yetu. (Waebrania 10:24, 25) Kuna wazee wa kutaniko wanaotuchunga na kutufundisha njia za uadilifu. (Waefeso 4:11, 12) Tuna Neno la Mungu, Biblia, ili kutuongoza. (2 Timotheo 3:16) Na nyakati zote, tuna fursa ya kusali kupata roho ya Mungu ili itusaidie.—Mathayo 26:41.
Kujifunza Kutokana na Dhambi za Daudi
13, 14. Mfalme Daudi alihusikaje katika dhambi nzito?
13 Ingawa hivyo, inasikitisha kwamba watumishi wa Mungu wenye kutokeza wamehusika katika ukosefu wa adili katika ngono. Mmoja wa watumishi hao ni Mfalme Daudi, ambaye alikuwa amemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miongo mingi. Bila shaka alimpenda Mungu sana. Hata hivyo, alitumbukia hatua kwa hatua katika dhambi. Kama ilivyokuwa na yule kijana aliyesimuliwa na Solomoni, kuna hatua zilizomwongoza Daudi kwenye dhambi kisha zikafanya dhambi hiyo iwe mbaya hata zaidi.
14 Wakati huo Daudi alikuwa na umri wa makamo, labda miaka 50 hivi. Akiwa juu ya paa lake, alimwona Bath-sheba mrembo akioga. Aliulizia habari zake na kupata kujua mwanamke huyo alikuwa nani. Akagundua kwamba mume wake, Uria, alikuwa katika kampeni ya kuzingira Raba, jiji la Waamoni. Daudi alifanya mpango mwanamke huyo aletwe kwenye jumba la mfalme na kulala naye. Baadaye, mambo yakatatanika—Bath-sheba akagundua kwamba ana mimba ya Daudi. Daudi alimwita Uria arudi kutoka vitani akitumaini kwamba angelala na mke wake usiku huo. Kwa njia hiyo, ingeonekana kwamba Uria ndiye baba ya mtoto wa Bath-sheba. Lakini Uria hakwenda nyumbani kwake. Akitaka sana kuficha dhambi yake, Daudi alimtuma Uria arudi Raba akiwa na barua ya mkuu wa jeshi iliyosema kwamba Uria awekwe mahali ambapo angeuawa. Hivyo Uria akauawa, na Daudi akamwoa mjane huyo kabla watu hawajajua kwamba alikuwa mjamzito.—2 Samweli 11:1-27.
15. (a) Dhambi ya Daudi ilifichuliwaje? (b) Daudi aliitikiaje karipio la Nathani lililotolewa kwa ustadi?
15 Ilionekana kana kwamba njama ya Daudi ya kuficha dhambi yake ilikuwa imefaulu. Miezi kadhaa ikapita. Mtoto wa kiume akazaliwa. Ikiwa Daudi alikuwa akikumbuka kisa hiki alipoandika Zaburi ya 32, basi ni wazi kwamba dhamiri yake ilimsumbua sana. (Zaburi 32:3-5) Hata hivyo, Mungu hakufichwa dhambi hiyo. Biblia husema: “Jambo lile alilolitenda Daudi likamchukiza BWANA.” (2 Samweli 11:27) Yehova alimtuma nabii Nathani, aliyemkabili Daudi kwa ustadi kuhusu yale aliyokuwa amefanya. Daudi aliungama mara moja na kumwomba Yehova msamaha. Toba yake ya kweli ilimpatanisha na Mungu. (2 Samweli 12:1-13) Daudi hakuchukia karipio. Badala yake, alionyesha mtazamo unaoelezwa katika Zaburi 141:5: “Mwenye haki na anipige, itakuwa fadhili; anikemee, itakuwa kama mafuta kichwani; kichwa changu kisikatae.”
16. Solomoni alitoa onyo na shauri gani kuhusu ukiukaji-sheria?
16 Huenda Solomoni, aliyekuwa mwana wa pili wa Daudi na Bath-sheba alikumbuka tukio hilo lenye kuhuzunisha katika maisha ya baba yake. Baadaye aliandika hivi: “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema.” (Mithali 28:13) Tukitumbukia katika dhambi nzito, twapaswa kutii shauri hilo lililopuliziwa, ambalo ni onyo na shauri pia. Twapaswa kuungama kwa Yehova na kuwafikia wazee wa kutaniko ili watusaidie. Daraka moja muhimu la wazee ni kusaidia kuwarekebisha upya wale ambao wametenda kosa.—Yakobo 5:14, 15.
Kuvumilia Matokeo ya Dhambi
17. Ingawa Yehova husamehe dhambi, yeye hatukingi na mambo gani?
17 Yehova alimsamehe Daudi. Kwa nini? Kwa sababu Daudi alishika uaminifu-maadili, aliwarehemu wengine, na alionyesha toba ya kweli. Hata hivyo, Daudi hakukingwa na matokeo yenye msiba. (2 Samweli 12:9-14) Ndivyo ilivyo leo. Ingawa Yehova hasababishi uovu kwa watu wanaotubu, hawakingi wasipatwe na mambo ambayo hutokea kwa sababu ya makosa yao. (Wagalatia 6:7) Ukosefu wa adili katika ngono waweza kutokeza talaka, mimba isiyotakiwa, maradhi yanayoambukizwa kingono, na kukosa kuaminiwa na kustahiwa.
18. (a) Paulo aliambia kutaniko la Korintho lishughulikieje kisa cha mwenendo mbaya sana wa ngono? (b) Yehova huonyeshaje upendo na rehema kwa watenda-dhambi?
18 Ikiwa sisi wenyewe tumetenda kosa zito, ni rahisi kuvunjika moyo tunapopatwa na matokeo ya makosa ambayo tumefanya. Hata hivyo, tusiruhusu kitu chochote kituzuie kutubu na kupatanishwa na Mungu. Katika karne ya kwanza, Paulo aliandikia Wakorintho kwamba walipaswa kumwondoa kutoka kutanikoni mtu aliyekuwa amezoea kufanya ngono ya maharimu. (1 Wakorintho 5:1, 13) Mtu huyo alipotubu kikweli, Paulo aliagiza kutaniko hilo hivi: “[Msameheni] kwa fadhili na kumfariji [na] kumthibitishia upendo wenu.” (2 Wakorintho 2:5-8) Katika shauri hilo lililopuliziwa, twaona upendo wa Yehova na rehema yake kuelekea watenda-dhambi wanaotubu. Malaika mbinguni hufurahi mtenda-dhambi anapotubu.—Luka 15:10.
19. Twaweza kupata manufaa gani tukihuzunishwa ifaavyo na mwenendo usiofaa?
19 Ijapokuwa tunahuzunishwa na mwenendo usiofaa, majuto tunayohisi yaweza kutusaidia ‘tujitunze tusiutazame uovu.’ (Ayubu 36:21) Kwa kweli, matokeo mabaya ya dhambi yapasa kutuzuia tusirudie kosa. Isitoshe, Daudi alitumia jambo lenye kuhuzunisha lililompata kwa sababu ya mwenendo wake wa dhambi, kuwashauri wengine. Alisema hivi: “Nitawafundisha wakosaji njia zako, na wenye dhambi watarejea kwako.”—Zaburi 51:13.
Furaha Huja kwa Kumtumikia Yehova
20. Tunapata manufaa gani kwa kutii matakwa ya Mungu ya uadilifu?
20 “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!” akasema Yesu. (Luka 11:28) Kutii matakwa ya Mungu ya uadilifu hutokeza baraka sasa na wakati ujao usio na mwisho. Ikiwa tumedumisha usafi wa kiadili, na tuendelee vivyo hivyo kwa kutumia maandalizi yote ambayo Yehova ametupa ili kutusaidia. Ikiwa tumetumbukia katika ukosefu wa adili, na tutiwe moyo kujua kwamba Yehova yuko tayari kusamehe wale wanaotubu kikweli, na acheni tuazimie kutorudia dhambi hiyo kamwe.—Isaya 55:7.
21. Tunaweza kudumisha usafi wa kiadili kwa kutumia shauri gani la mtume Petro?
21 Karibuni ulimwengu huu usio mwadilifu utapitilia mbali, pamoja na mitazamo na mazoea yake yasiyo ya adili. Kwa kudumisha usafi wa kiadili tutanufaika sasa na milele. Mtume Petro aliandika hivi: “Wapendwa, kwa kuwa mnangojea mambo haya, fanyeni kabisa yote mwezayo ili mwishowe mpatikane naye mkiwa bila doa na bila waa na katika amani. . . . Mkiwa mnakuwa na ujuzi huu wa kimbele, iweni wenye kulinda ili msipate kuongozwa kando pamoja nao kwa kosa la watu wanaokaidi sheria na kuanguka kutoka kwenye uimara wenu wenyewe.”—2 Petro 3:14, 17.
-