Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Musa Ashambuliwa
    Amkeni!—2004 | Aprili 8
    • Musa Ashambuliwa

      MARA nyingi Wayahudi, Wakristo, na Waislamu hawakubaliani kuhusu mambo mengi. Hata hivyo, licha ya tofauti zao, dini hizo hukubaliana kuhusu jambo moja: zinamheshimu sana mwanamume anayeitwa Musa. Wayahudi wanamtambua kuwa “mwalimu mkuu zaidi kati ya walimu wote Wayahudi,” yaani, mwanzilishi wa taifa la Kiyahudi. Wakristo wanamwona kuwa mtangulizi wa Yesu Kristo. Na Waislamu wanamtambua Musa kuwa mmoja wa manabii wao wa kwanza wakuu zaidi.

      Musa

      Kwa hiyo, Musa ni mmojawapo wa watu wenye uvutano mkubwa sana katika historia ya wanadamu. Hata hivyo, kwa zaidi ya miaka mia moja, Musa ameshambuliwa na wasomi na makasisi. Mbali na kutilia shaka kwamba Musa alifanya miujiza na kuwaongoza Waisraeli kutoka Misri, wengi hupinga hata kuwapo kwake. Kitabu Moses—A Life cha Jonathan Kirsch kinasema: “Yale tunayoweza kusema kumhusu Musa ni kwamba huenda mtu fulani kama yule anayezungumziwa katika Biblia aliishi wakati na mahali pasipojulikana zamani za kale, na huenda mambo machache aliyofanya ndiyo yametumiwa kutunga hadithi ambayo imesimuliwa kwa karne nyingi hivi kwamba amekuwa mtu maarufu na anayezua ubishi ambaye anazungumziwa katika Biblia.”

      Kwa kuona mambo kijuujuu, ubishi huo unaweza kuonekana kuwa wa kweli. Kwa mfano, wahakiki wanasema kwamba uthibitisho wa kiakiolojia umegunduliwa unaoonyesha kwamba watu fulani katika nyakati za Biblia waliishi, kama vile Mfalme Yehu wa Israeli. Lakini hakuna uthibitisho wowote wa kiakiolojia uliogunduliwa kuonyesha kwamba Musa aliishi. Hata hivyo, hiyo haithibitishi kwamba Musa ni mtu wa kuwaziwa tu. Wakati mmoja, wapinzani walisema kwamba watu fulani wanaotajwa katika Biblia, kama vile Mfalme Belshaza wa Babiloni na Mfalme Sargoni wa Ashuru, walikuwa watu wa kuwaziwa mpaka akiolojia ilipothibitisha kwamba waliishi.

      Mwandishi Jonathan Kirsch anasema hivi: “Vitu vya kale vya Waisraeli vilivyosalia ni vichache sana hivi kwamba kukosekana kwa uthibitisho wa kwamba Musa aliishi isipokuwa ule ulio katika Biblia hakushangazi wala hakuthibitishi jambo lolote.” Kulingana na Kirsch, watu fulani husema kwamba haielekei kuwa Musa ni mtu wa kuwaziwa tu, kwa sababu “haingewezekana . . . , kubuni hadithi tata yenye matukio mengi na mazungumzo mengi sana kadiri hiyo.”

      Uwe unafuata dini au la, yaelekea unajua mambo fulani muhimu kumhusu Musa: jinsi alivyozungumza na Mungu kwenye mti uliokuwa ukiwaka moto, jinsi Waisraeli walivyotoka utumwani Misri, na kugawanyika kwa Bahari Nyekundu. Lakini je, tuna sababu ya kuamini kwamba mambo hayo yalitokea? Au Musa ni mtu anayesimuliwa katika hadithi tu? Makala ifuatayo itazungumzia maswali hayo yenye kusisimua.

  • Musa—Mtu Halisi au wa Hadithi?
    Amkeni!—2004 | Aprili 8
    • Musa Mtu Halisi au wa Hadithi?

      MUSA alizaliwa wakati wa hatari. Familia yao ilikuwa kati ya familia ambazo zilihamia Misri pamoja na baba yao Yakobo, au Israeli, ili kuepuka njaa. Waliishi kwa amani na jirani zao Wamisri kwa miaka mingi. Lakini kukawa na badiliko lenye kuogopesha sana. Ripoti moja ya historia inayoheshimika inasema: “Mfalme mpya . . . akainuka juu ya Misri. Naye akawaambia watu wake: ‘Tazama! Watu wa wana wa Israeli ni wengi zaidi na wenye nguvu kuliko sisi. Haya! Na tuwatendee kwa werevu, wasije wakaongezeka.’” Wamisri walipanga kufanya nini? Kuwafanya Waisraeli kuwa “watumwa chini ya uonevu” ili wasiongezeke na kuwaamuru wazalishaji Waebrania kuwaua watoto wote wa kiume wanaozaliwa. (Kutoka 1:8-10, 13, 14) Licha ya dhuluma hiyo, Waisraeli waliongezeka kwa sababu ya ujasiri wa wazalishaji wao waliokataa kutii amri hiyo. Hivyo, mfalme wa Misri akaamuru: “Kila mwana anayezaliwa mtamtupa kwenye mto Nile.”—Kutoka 1:22.

      Wenzi wawili Waisraeli, Amramu na Yokebedi, “hawakuliogopa agizo la mfalme.” (Waebrania 11:23) Yokebedi akamzaa mwana ambaye baadaye alisemwa kuwa “mwenye sura nzuri machoni pa Mungu.”a (Matendo 7:20) Huenda walitambua kwamba mtoto huyo alikuwa na kibali cha Mungu. Vyovyote vile, walikataa kumtoa mtoto wao auawe. Huku wakihatarisha uhai wao, waliamua kumficha.

      Baada ya miezi mitatu, wazazi wa Musa hawangeweza kuendelea kumficha. Basi, waliamua kuchukua hatua. Yokebedi alimweka mtoto huyo katika safina ya mafunjo na kuiweka kwenye Mto Nile. Bila kujua, hatua hiyo ya Yokebedi ilimfanya Musa kuwa mtu maarufu katika historia!—Kutoka 2:3, 4.

      Je, Matukio Hayo Ni ya Kweli?

      Wasomi wengi leo husema kwamba matukio hayo ni hadithi tu. Gazeti Christianity Today linasema “ukweli ni kwamba hakuna uthibitisho wowote wa kiakiolojia unaoonyesha kwamba wana wa Israeli waliishi Misri kwa muda.” Ingawa hakuna uthibitisho wa moja kwa moja unaoonyesha jambo hilo, kuna uthibitisho mwingi usio wa moja kwa moja unaoonyesha kwamba simulizi hilo la Biblia ni la kweli. Katika kitabu chake Israel in Egypt, James K. Hoffmeier, mtaalamu wa vitu vya kale vya Misri, anasema: “Habari za kiakiolojia zinaonyesha kwamba watu wa upande wa mashariki wa Mediterania walitembelea Misri mara nyingi hasa kwa sababu ya ukame . . . Hivyo, kuanzia mwaka wa 1800 mpaka 1540 K.W.K. hivi, Wasemiti kutoka magharibi mwa Asia waliiona nchi ya Misri kuwa mahali pazuri pa kuhamia.”

      Isitoshe, kwa muda mrefu imekubaliwa kwamba masimulizi ya Biblia kuhusu utumwa wa Waisraeli huko Misri ni sahihi. Kitabu Moses—A Life kinasema: “Masimulizi ya Biblia kuhusu kudhulumiwa kwa Waisraeli yanaungwa mkono na picha moja ya kaburi la Misri ya kale ambayo imechorwa mara nyingi inayoonyesha waziwazi kikundi cha watumwa kikitengeneza matofali.”

      Masimulizi ya Biblia kuhusu safina ndogo ambayo Yokebedi alitumia ni ya kweli pia. Biblia inasema kwamba ilitengenezwa kwa mafunjo ambayo kulingana na kitabu Commentary cha Cook, “yalitumiwa sana na Wamisri kutengeneza mashua nyepesi zinazoenda mbio.”

      Hata hivyo, je, kweli kiongozi wa nchi angeamuru watoto wachanga wauawe bila huruma? Msomi George Rawlinson anatukumbusha hivi: “Mauaji ya watoto . . . yametukia wakati na mahali mbalimbali, na yameonwa kuwa jambo dogo.” Ama kweli, hata katika nyakati zetu kumekuwa na mauaji ya watu wengi. Huenda simulizi la Biblia likahuzunisha, lakini ni la kweli kabisa.

      Je, Kuokolewa kwa Musa​—Ni Hadithi ya Kipagani?

      Musa akiwa mtoto mchanga

      Wahakiki wanasema kwamba kuokolewa kwa Musa kutoka Mto Nile kunafanana sana na hadithi ya kale ya Mfalme Sargoni wa Akkad—ambayo wengine wanasema ni ya kale zaidi kuliko hadithi ya Musa. Hadithi hiyo inasimulia pia kuhusu mtoto aliyeokolewa kutoka mtoni akiwa ndani ya kikapu.

      Hata hivyo, historia ina mambo mengi yanayofanana. Na kumweka mtoto mtoni hakukuwa jambo la ajabu. Kitabu Biblical Archaeology Review kinasema: “Watu wa Babilonia na Misri waliishi kando-kando ya mito na kumweka mtoto katika kikapu kisichopenya maji kungekuwa afadhali kuliko kumtupa kwenye rundo la takataka ambalo lilikuwa zoea la kawaida. . . . Si ajabu kusikia hadithi juu ya mtoto aliyepatikana majini na baadaye akawa mashuhuri kwa kuwa hilo ni jambo la kawaida maishani.”

      Katika kitabu chake, Exploring Exodus, Nahum M. Sarna, anasema kwamba ijapokuwa kuna mambo fulani yanayofanana, hadithi ya kuzaliwa kwa Musa inatofautiana na “Hadithi ya Sargoni” kwa “njia nyingi.” Madai ya kwamba simulizi la Biblia lilitokana na hadithi ya kipagani, ni ya uwongo.

      Alelewa Nyumbani mwa Farao

      Yokebedi hakuacha mtoto wake apotee tu. Aliiweka “[safina] katikati ya matete kando ya mto Nile.” Huenda aliiweka hapo kwa sababu alitarajia kwamba itagunduliwa. Huenda hapo ndipo binti ya Farao alipokuwa akioga kwa ukawaida.b—Kutoka 2:2-4.

      Safina hiyo ndogo iligunduliwa haraka. “[Binti ya Farao] alipoifungua akamwona yule mtoto, na tazama, mvulana huyo alikuwa akilia. Kwa hiyo akamwonea huruma, ingawa alisema: ‘Huyu ni mmoja wa watoto wa Waebrania.’” Binti huyo wa Mfalme wa Misri aliamua kumlea. Jina ambalo wazazi wake walimpa lilisahauliwa. Leo, anajulikana duniani pote kwa jina alilopewa na mama yake mlezi, yaani, Musa.c—Kutoka 2:5-10.

      Hata hivyo, je, haishangazi kwamba binti ya Mfalme wa Misri angemlea mtoto kama huyo? Sivyo, kwa kuwa dini ya Wamisri ilifundisha kwamba matendo ya fadhili yalikuwa takwa la kwenda mbinguni. Kuhusiana na hatua ya kumlea mtoto huyo, mwanaakiolojia Joyce Tyldesley anasema: “Wanawake Wamisri walikuwa na usawa na wanaume Wamisri. Walipaswa kuwa na haki sawa kisheria na kiuchumi, na . . . wanawake wangewalea watoto wa wengine.” Hati moja ya kale ya mafunjo inayohusu kuwalea watoto wa wengine inasema kuhusu mwanamke Mmisri aliyewalea watumwa wake. Kuhusu jinsi mama ya Musa alivyopewa kazi ya kumnyonyesha, kitabu The Anchor Bible Dictionary kinasema: “Mpango wa kumlipa mama ya Musa amtunze Musa . . . unafanana na mipango ya kuwalea watoto huko Mesopotamia.”

      Kwa kuwa Musa alilelewa na mtu mwingine, je, angefichwa asili yake ya Kiebrania? Sinema fulani za Hollywood zimewafanya watu wafikiri hivyo. Hata hivyo, Maandiko yanasema tofauti. Kwa hekima, dada ya Musa, Miriamu, alipanga Musa alelewe na mama yake mwenyewe, Yokebedi. Bila shaka, mwanamke huyo mcha-Mungu angemweleza mwana wake ukweli kuhusu asili yake! Kwa kuwa watoto katika nyakati za kale walinyonyeshwa kwa miaka kadhaa, Yokebedi alikuwa na wakati wa kutosha kumfundisha Musa kumhusu ‘Mungu wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo.’ (Kutoka 3:6) Msingi huo wa kiroho ulimsaidia Musa kwa sababu baada ya kupelekwa kwa binti ya Farao, “Musa akafundishwa hekima yote ya Wamisri.” Dai la mwanahistoria Josephus kwamba Musa alipanda cheo na kuwa jenerali katika vita dhidi ya Ethiopia haliwezi kuthibitishwa. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba Musa “alikuwa mwenye nguvu katika maneno na matendo.”d—Matendo 7:22.

      Alipofikisha umri wa miaka 40, Musa angeweza kuwa mtawala mashuhuri wa Misri. Ikiwa angebaki nyumbani mwa Farao angepata mamlaka na utajiri. Kisha jambo fulani likatukia lililobadili maisha yake.

      Akimbilia Midiani

      Siku moja Musa ‘alimwona Mmisri fulani akimpiga Mwebrania fulani, mmoja wa ndugu zake.’ Kwa miaka mingi Musa alifurahia faida za kuwa Mwebrania na kuwa Mmisri. Lakini alipomwona Mwisraeli mwenzake akipigwa, labda kiasi cha kuuawa, Musa aliamua kuchukua hatua kubwa. (Kutoka 2:11) “Alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao, akachagua kutendewa vibaya pamoja na watu wa Mungu.”—Waebrania 11:24, 25.

      Musa alichukua hatua ya haraka na ya kukata maneno: ‘Alimpiga Mmisri huyo na kumuua, halafu akamficha ndani ya mchanga.’ (Kutoka 2:12) Hilo halikuwa tendo la mtu “mwenye mazoea ya kukasirika haraka,” kama mhakiki mmoja alivyodai. Ingawa halikufaa, hilo lilikuwa tendo la imani kwamba Mungu angewakomboa Waisraeli kutoka Misri. (Mwanzo 15:13, 14) Labda kwa kukosa hekima, Musa aliamini kwamba matendo yake yangewachochea watu wake kuasi. (Matendo 7:25) Hata hivyo, alikata tamaa Waisraeli wenzake walipokataa uongozi wake. Farao alipopata habari kuhusu mauaji hayo, Musa alilazimika kukimbia. Alikimbilia Midiani, akamwoa mwanamke anayeitwa Sipora, binti ya Yethro, mkuu wa kabila la wahamaji.

      Kwa miaka 40, Musa alikuwa mchungaji tu, na tumaini lake la kuwa mkombozi lilikuwa limedidimia. Hata hivyo, siku moja aliwapeleka kondoo wa Yethro karibu na Mlima Horebu. Akiwa hapo, malaika wa Yehova akamtokea Musa katika mti uliokuwa ukiwaka moto. Hebu wazia ilivyokuwa. Mungu anamwamuru: ‘Watoe watu wangu wana wa Israeli kutoka Misri.’ Lakini Musa anasitasita, hajiamini, na ana wasiwasi. Anauliza hivi: “Mimi ni nani hata niende kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli kutoka Misri?” Hata anafunua udhaifu wake ambao watengenezaji fulani wa sinema wameficha: Kwamba ana tatizo la kusema. Jinsi Musa alivyo tofauti na mashujaa wa hadithi za kale! Ile miaka 40 akiwa mchungaji ilimnyenyekeza. Ingawa Musa hajiamini, Mungu ana uhakika kwamba anafaa kuwa kiongozi!—Kutoka 3:1–4:20.

      Kukombolewa Kutoka Misri

      Musa anaondoka Midiani na kumwendea Farao, akitaka awaachilie watu wa Mungu. Mtawala huyo mkaidi anapokataa, nchi ya Misri inakumbwa na mapigo kumi makali. Pigo la kumi linawaua wazaliwa wa kwanza wa Misri, na Farao mwenye huzuni anawaachilia Waisraeli.—Kutoka, sura ya 5-13.

      Watu wengi wanayajua matukio hayo. Lakini je, ni matukio ya kweli? Wengine wanadai kwamba kwa kuwa jina la Farao huyo halijatajwa, basi simulizi hilo si la kweli.e Hata hivyo, Hoffmeier, aliyenukuliwa awali, anasema kwamba mara nyingi waandishi Wamisri hawakuyataja majina ya adui za Farao kimakusudi. Anasema: “Wanahistoria hawawezi kusema kwamba Mfalme Thutmose wa 3 hakupigana huko Megido eti kwa sababu majina ya wafalme wa Kadeshi na Megido hayakutajwa.” Hoffmeier anasema kwamba Farao huyo hakutajwa “kwa sababu nzuri za kidini.” Sababu moja ni kwamba kwa kutotaja jina la Farao huyo, simulizi hilo linaelekeza uangalifu kwa Mungu, wala si kwa Farao.

      Hata hivyo, wahakiki hawaamini kwamba Wayahudi wengi walitoka Misri. Msomi Homer W. Smith alisema kwamba uhamaji mkubwa kama huo “ungejulikana sana katika historia ya Misri au Siria . . . Yaelekea hadithi ya kuhama ni simulizi lililopotoshwa na la kuwaziwa la watu wachache waliokimbia kutoka Misri hadi Palestina.”

      Ni kweli kwamba maandishi ya Kimisri kuhusu tukio hilo hayajapatikana. Lakini Wamisri wangeweza kubadilisha maandishi yao ya kihistoria yalipowaaibisha au kuhatarisha masilahi yao ya kisiasa. Thutmose wa 3 alipoanza kutawala, alijaribu kufuta maandishi yote kumhusu Hatshepsut, mtawala aliyemtangulia. Mtaalamu wa vitu vya kale vya Misri John Ray anasema: “Maandishi yake yalifutwa, piramidi zake zikazungushiwa ukuta, na sanamu zake za ukumbusho zikasahauliwa. Jina lake halipatikani katika maandishi ya baadaye.” Jitihada kama hizo za kufuta au kuficha mambo yenye kuaibisha zimefanywa katika nyakati za sasa.

      Kwa kuwa Wayahudi walikuwa wanahamahama, hakuna uthibitisho wa kiakiolojia unaoonyesha maisha yao nyikani. Hawakujenga majiji wala kupanda mimea. Inaelekea kuna mambo machache yanayoonyesha kwamba waliishi huko. Hata hivyo, uthibitisho wa kutosha kuhusu maisha yao nyikani unaweza kupatikana katika Biblia. Kitabu hicho kitakatifu kinazungumzia sana maisha yao ya nyikani. (1 Samweli 4:8; Zaburi 78; Zaburi 95; Zaburi 106; 1 Wakorintho 10:1-5) Jambo muhimu ni kwamba Yesu Kristo pia alitoa ushahidi kwamba matukio ya nyikani yalifanyika.—Yohana 3:14.

      Basi, bila shaka simulizi la Biblia kumhusu Musa ni la kweli kabisa. Lakini aliishi zamani sana. Je, Musa ana umuhimu wowote maishani mwako?

      a Kihalisi, “mzuri machoni pa Mungu.” Kulingana na The Expositor’s Bible Commentary, maneno hayo yanaweza kumaanisha “sifa za moyoni” za mtoto huyo, wala si sura ya nje tu.

      b Kitabu Commentary cha Cook kinasema kwamba “ilikuwa kawaida katika Misri ya kale” kuoga katika Mto Nile. “Mto Nile ulionwa kuwa . . . ulitokana na Osiris na maji yake yalionwa kuwa yenye nguvu za ajabu za kutokeza uhai na uzazi.”

      c Asili ya jina hilo imezua ubishi miongoni mwa wasomi. Katika Kiebrania, jina Musa linamaanisha “Kuchotwa; Kuokolewa Kutoka Majini.” Mwanahistoria Flavius Josephus alisema kwamba jina Musa limeundwa kwa maneno mawili ya Kimisri yanayomaanisha “maji” na “kuokolewa.” Leo vilevile, wasomi fulani wanaamini kwamba jina Musa ni la asili ya Kimisri lakini wanaona kwamba huenda linamaanisha “Mwana.” Hiyo ni kwa sababu neno “Musa” linatamkwa sawa na majina fulani ya Kimisri. Kwa kuwa hakuna anayejua jinsi Kiebrania au Kimisri cha kale kilivyotamkwa, dhana hizo ni za kukisia tu.

      d Kitabu Israel in Egypt kinasema: “Dhana ya kwamba Musa alilelewa katika jumba la kifalme la Misri inaonekana kuwa hadithi tu. Lakini uchunguzi wa makini wa jumba la kifalme wakati wa falme za kati ya mwaka wa 1550 mpaka 1070 K.W.K. hivi, hauungi mkono dhana hiyo. Mfalme Thutmose wa 3 . . . alianzisha zoea la kuwapeleka Misri wana wa wafalme vibaraka wa mataifa ya magharibi mwa Asia ili wazoezwe desturi za Misri . . . Hivyo, wana na binti za wafalme wa mataifa mengine walikuwapo katika jumba la kifalme la Misri.”

      e Wanahistoria fulani wanasema kwamba Farao aliyetawala wakati Waisraeli walipotoka Misri ni Thutmose wa 3. Wengine wanasema alikuwa Amenhotep wa 2, Ramses wa 2, na kadhalika. Kwa sababu ya mvurugo wa rekodi za ukoo za Misri, ni vigumu kujua kwa hakika jina la Farao huyo.

      Ni Nani Aliyeandika Vitabu Vitano vya Kwanza vya Biblia?

      Inasemekana kwamba Musa ndiye mwandishi wa vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, vinavyoitwa Pentateuki. Huenda alipata habari alizoandika kutoka kwa vyanzo vya kale vya historia. Hata hivyo, wahakiki wengi wanasema kwamba Musa hakuandika vitabu hivyo kamwe. Spinoza, mwanafalsafa wa karne ya 17, alisema: “Ni wazi kabisa kwamba Musa hakuandika Pentateuki.” Katika sehemu ya mwisho ya karne ya 19, msomi Mjerumani Julius Wellhausen, alisambaza dhana ya kwamba vitabu vitano vya kwanza vya Biblia ni mkusanyo wa maandishi ya waandishi kadhaa au vikundi vya waandishi.

      Kwa unyenyekevu, Musa aliandika jinsi alivyoshindwa kumtukuza Mungu

      Wellhausen alisema kwamba mwandishi mmoja alitumia jina la Mungu, Yehova, kila mahali. Mwandishi mwingine alimwita Mungu “Elohimu.” Inasemekana kwamba mwandishi mwingine aliandika sheria na kanuni za ukuhani katika Mambo ya Walawi, na mwingine akaandika Kumbukumbu la Torati. Ijapokuwa wasomi fulani wamekubali dhana hiyo kwa miaka mingi, kitabu The Pentateuch cha Joseph Blenkinsopp, kinasema kwamba dhana ya Wellhausen ni hadithi iliyo “hatarini.”

      Kitabu Introduction to the Bible, cha John Laux, kinaeleza: “Dhana ya waandishi wengi inategemea madai yasiyo na msingi maalumu au ya uwongo kabisa. . . . Ikiwa dhana hiyo ni ya kweli, basi Waisraeli walidanganywa walipokubali kufanya kazi ngumu ya kuishi kulingana na Sheria. Huo ungekuwa uwongo mkubwa zaidi katika historia ya ulimwengu.”

      Wengine wanasema kwamba Pentateuki iliandikwa na waandishi wengi kwa sababu ya mitindo tofauti ya uandishi. Hata hivyo, K. A. Kitchen, anasema hivi katika kitabu chake Ancient Orient and Old Testament: “Mitindo tofauti ya uandishi si hoja na inaonyesha tu tofauti katika habari zinazozungumziwa.” Tofauti kama hizo za mitindo ya uandishi zinapatikana pia “katika maandishi ya kale ambayo hayakuandikwa na waandishi tofauti-tofauti.”

      Dai la kwamba matumizi ya majina mbalimbali ya Mungu ni uthibitisho kwamba kulikuwa na waandishi tofauti-tofauti halina msingi. Katika sehemu ndogo ya kitabu cha Mwanzo, Mungu anaitwa “Mungu Aliye Juu Zaidi,” “Yeye aliyezitokeza mbingu na dunia,” “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova,” “Mungu mwenye kuona,” “Mungu Mweza-Yote,” “Mungu,” “Mungu wa kweli,” na “Mwamuzi wa dunia yote.” (Mwanzo 14:18, 19; 15:2; 16:13; 17:1, 3, 18; 18:25) Je, waandishi tofauti-tofauti waliandika sehemu hizo za Biblia? Au vipi kuhusu Mwanzo 28:13, ambapo maneno “Elohimu” (Mungu) na “Yehova” yanatumiwa pamoja? Je, waandishi wawili walishirikiana kuandika mstari huo mmoja?

      Dhana hiyo huonekana waziwazi kuwa haina msingi inapotumiwa kuchunguza maandishi ya kisasa. Katika kitabu kimoja cha karibuni kuhusu Vita vya Pili vya Ulimwengu, mtawala wa Ujerumani anaitwa “Führer,” “Adolf Hitler,” na “Hitler” katika kurasa chache. Je, yeyote anaweza kudai kwamba hilo linathibitisha kiliandikwa na waandishi watatu tofauti?

      Hata hivyo, aina mbalimbali za dhana ya Wellhausen zinaongezeka. Mojawapo ni dhana iliyobuniwa na wasomi wawili kuhusu yule mwandishi aliyetumia jina Yehova. Zaidi ya kusema kwamba mwandishi huyo hakuwa Musa, wanasema pia kwamba mwandishi huyo alikuwa mwanamke.

  • Musa—Jinsi Maisha Yake Yanavyokuhusu
    Amkeni!—2004 | Aprili 8
    • Musa—Jinsi Maisha Yake Yanavyokuhusu

      WASOMI na wahakiki wengi wanamwona Musa kuwa mtu wa kuwaziwa tu. Wanakataa masimulizi ya Biblia, wakitoa madai ambayo yangekanusha kwamba watu kama Plato na Socrates waliishi.

      Hata hivyo, kama tulivyoona, hakuna sababu inayofaa kukanusha masimulizi ya Biblia yanayomtaja Musa. Badala yake, watu wenye imani wana uthibitisho wa kutosha kwamba Biblia nzima ni “neno la Mungu.”a (1 Wathesalonike 2:13; Waebrania 11:1) Kwa watu kama hao, kuchunguza maisha ya Musa si kazi ya usomi tu bali ni njia ya kujenga imani.

      Musa Halisi

      Mara nyingi watengenezaji wa sinema hukazia jinsi Musa alivyokuwa shujaa na jasiri—sifa ambazo huwavutia watazamaji. Ni kweli kwamba Musa alikuwa jasiri. (Kutoka 2:16-19) Lakini jambo muhimu zaidi ni kwamba alikuwa mwenye imani. Mungu alikuwa halisi kwake, hivi kwamba baadaye mtume Paulo alisema kwamba Musa “aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.”—Waebrania 11:24-28.

      Kwa hiyo, kupitia Musa tunajifunza kwamba tunahitaji kusitawisha uhusiano pamoja na Mungu. Katika maisha yetu ya kila siku, sisi pia tunaweza kutenda kana kwamba tunamwona Mungu! Tukifanya hivyo, hatutatenda jambo linalomchukiza. Kumbuka pia kwamba imani ya Musa ilianza kujengwa alipokuwa mtoto. Imani yake ilikuwa yenye nguvu sana hivi kwamba haikuathiriwa na “hekima yote ya Wamisri.” (Matendo 7:22) Wazazi wanatiwa moyo kama nini kuanza kufundisha watoto wao juu ya Mungu tangu utotoni!—Methali 22:6; 2 Timotheo 3:15.

      Unyenyekevu wa Musa unapendeza pia. Alikuwa “mpole zaidi kuliko watu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hesabu 12:3) Hivyo, Musa alikuwa tayari kukubali makosa yake. Anaandika jinsi alivyopuuza kumtahiri mwana wake. (Kutoka 4:24-26) Anaeleza kwa unyofu jinsi ambavyo hakumtukuza Mungu wakati fulani na hukumu kali ambayo Mungu alitoa. (Hesabu 20:2-12; Kumbukumbu la Torati 1:37) Pia, Musa alikuwa tayari kukubali mashauri ya wengine. (Kutoka 18:13-24) Je, haifai waume, akina baba, na wanaume wengine wenye mamlaka kumwiga Musa?

      Ni kweli kwamba wahakiki fulani wanatilia shaka upole wa Musa wakitaja matendo ya jeuri aliyofanya. (Kutoka 32:26-28) Mwandishi Jonathan Kirsch anasema: “Musa wa Biblia hakuwa mnyenyekevu wala mpole, na mwenendo wake haukuwa mwadilifu nyakati zote. Nyakati nyingine, . . . Musa anaonekana kuwa mjeuri, mwenye hamu ya kumwaga damu, na mkatili.” Uchambuzi wa aina hiyo hauna msingi hata kidogo. Hautilii maanani uhakika wa kwamba Musa alitenda kwa kupenda sana haki na kwa kuchukia uovu wala si kwa ukatili. Leo ambapo watu wengi wanapenda ukosefu wa adili, kielelezo cha Musa kinatukumbusha umuhimu wa kutovunja kanuni za maadili.—Zaburi 97:10.

      Yesu Alikuwa Nabii Kama Musa

      Zifuatazo ni njia zinazoonyesha jinsi Yesu alivyokuwa kama Musa:

      • Musa na Yesu waliokoka mauaji ya watoto wavulana yaliyoamriwa na watawala wa wakati wao.—Kutoka 1:22; 2:1-10; Mathayo 2:13-18.

      • Musa aliitwa kutoka Misri pamoja na ‘mzaliwa wa kwanza’ wa Yehova, taifa la Israeli. Yesu aliitwa kutoka Misri akiwa Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu.—Kutoka 4:22, 23; Hosea 11:1; Mathayo 2:15, 19-21.

      • Musa na Yesu walifunga kula kwa siku 40 nyikani.—Kutoka 34:28; Mathayo 4:1, 2.

      • Musa na Yesu walikuwa watu wapole na wanyenyekevu zaidi.—Hesabu 12:3; Mathayo 11:28-30.

      • Musa na Yesu walifanya miujiza. —Kutoka 14:21-31; Zaburi 78:12-54; Mathayo 11:5; Marko 5:38-43; Luka 7:11-15, 18-23.

      • Musa na Yesu walikuwa wapatanishi wa maagano kati ya Mungu na watu Wake.—Kutoka 24:3-8; 1 Timotheo 2:5, 6; Waebrania 8:10-13; 12:24.

      Maandishi ya Musa Yalihifadhiwa

      Musa aliandika mambo mengi ajabu. Maandishi hayo yanatia ndani mashairi (Ayubu, Zaburi 90), maelezo ya kihistoria (Mwanzo, Kutoka, Hesabu), maelezo kuhusu ukoo (Mwanzo, sura ya 5, 11, 19, 22, 25), na sheria nyingi sana zinazoitwa Sheria ya Musa (Kutoka, sura ya 20-40; Mambo ya Walawi; Hesabu; Kumbukumbu la Torati). Sheria hiyo iliyoongozwa na roho ya Mungu ilikuwa na sera, sheria, na kanuni za uongozi ambazo zilikuwa za hali ya juu kuliko nyingine za wakati huo.

      Katika nchi ambapo mtawala ndiye mkuu wa Kanisa, mara nyingi hakuna uhuru wa ibada, dini nyingine hudhulumiwa, na mamlaka hutumiwa vibaya. Sheria ya Musa ilitia ndani kanuni ya kutenganisha Kanisa na Serikali. Mfalme hakuruhusiwa kufanya kazi za makuhani.—2 Mambo ya Nyakati 26:16-18.

      Sheria ya Musa pia ilikuwa na kanuni za usafi na za kuzuia magonjwa, kama vile kuwatenga wagonjwa na kuondoa mavi, ambazo zinapatana na sayansi ya leo. (Mambo ya Walawi 13:1-59; 14:38, 46; Kumbukumbu la Torati 23:13) Hilo linapendeza kwani matibabu mengi ya Wamisri katika siku za Musa yalikuwa hatari kwa kuwa yalikuwa duni na yalihusisha ushirikina. Leo katika nchi zinazoendelea, mamilioni wanaweza kuepuka magonjwa na kifo wakitumia kanuni za usafi ambazo Musa alifundisha.

      Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa. (Wakolosai 2:13, 14) Lakini kujifunza sheria hiyo ni muhimu sana. Sheria hiyo iliwaamuru Waisraeli wajitoe kwa Mungu kikamili na kuepuka ibada ya sanamu. (Kutoka 20:4; Kumbukumbu la Torati 5:9) Iliwaamuru watoto wawaheshimu wazazi wao. (Kutoka 20:12) Pia, Sheria ilishutumu uuaji, uzinzi, wizi, uwongo, na kutamani. (Kutoka 20:13-17) Kanuni hizo zinaheshimiwa sana na Wakristo leo.

      Kanuni za usafi zinazopatikana katika Sheria ya Musa zinaweza kusaidia kuzuia magonjwa

      Nabii Aliye Kama Musa

      Yesu akiwa na wanafunzi wake

      Yesu ndiye nabii aliyekuwa kama Musa

      Tunaishi nyakati za taabu. Wanadamu wanahitaji kiongozi aliye kama Musa—mtu aliye na uwezo na mamlaka na anayeshikamana na kanuni za maadili, kiongozi jasiri, mwenye huruma, na anayependa sana haki. Musa alipokufa, huenda Waisraeli walijiuliza, ‘Je, ulimwengu utamwona mtu kama yeye tena?’ Musa mwenyewe alijibu swali hilo.

      Maandishi ya Musa yanaeleza jinsi magonjwa na kifo yalivyotokea na kwa nini Mungu ameruhusu uovu. (Mwanzo 3:1-19; Ayubu, sura ya 1, 2) Unabii wa kwanza wa Mungu unaopatikana katika Mwanzo 3:15, unaahidi kwamba uovu utakomeshwa hatimaye! Jinsi gani? Unabii huo ulionyesha kwamba mtu fulani angezaliwa ambaye angeleta wokovu. Ahadi hiyo iliwafanya watu wawe na tumaini kwamba Masihi angetokea na kuwakomboa wanadamu. Lakini Masihi huyo angekuwa nani? Musa anatusaidia kumtambua waziwazi.

      Alipokaribia kufa, Musa aliandika maneno haya ya kinabii: “Nabii kutoka katikati yako mwenyewe, kutoka kwa ndugu zako, kama mimi, ndiye ambaye Yehova Mungu wako atakuinulia—ninyi mnapaswa kumsikiliza yeye.” (Kumbukumbu la Torati 18:15) Baadaye mtume Petro alionyesha waziwazi kwamba maneno hayo yanamhusu Yesu.—Matendo 3:20-26.

      Wasomi wengi Wayahudi wanapinga vikali uhusiano kati ya Musa na Yesu. Wanadai kwamba maneno hayo yanamhusu nabii yeyote wa kweli aliyetokea baada ya Musa. Hata hivyo, kulingana na Tanakh—The Holy Scriptures cha Jewish Publication Society, andiko la Kumbukumbu la Torati 34:10 linasema: “Hapakuinuka tena kamwe katika Israeli nabii kama Musa—ambaye BWANA aliteua, uso kwa uso.”

      Naam, manabii wengi waaminifu kama vile Isaya na Yeremia, walitokea baada ya Musa. Lakini hakuna yeyote kati yao aliyekuwa na uhusiano wa pekee pamoja na Mungu kama vile Musa, yaani kuzungumza naye “uso kwa uso.” Kwa hiyo ahadi ya Musa kuhusu nabii aliye ‘kama yeye’ ilimhusu mtu mmoja, yaani, Masihi! Inapendeza kwamba kabla ya Ukristo kuanzishwa na kabla ya mnyanyaso wa kidini kutoka kwa Wakristo wa uwongo, wasomi Wayahudi walikuwa na maoni hayohayo. Uthibitisho wa hilo unapatikana katika maandishi ya Kiyahudi kama vile kitabu Midrash Rabbah, kinachomtaja Musa kuwa mtangulizi wa “Mkombozi wa baadaye,” au Masihi.

      Uhakika wa kwamba Yesu alikuwa kama Musa hauwezi kukanushwa. (Ona sanduku “Yesu Alikuwa Nabii Kama Musa.”) Yesu ana nguvu na mamlaka. (Mathayo 28:19) Yesu ni “mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni.” (Mathayo 11:29) Yesu anachukia uasi-sheria na ukosefu wa haki. (Waebrania 1:9) Basi anaweza kutuongoza vizuri sana! Yeye ndiye atakayekomesha uovu hivi karibuni na kufanya dunia iwe Paradiso ambayo Biblia inazungumzia.b

      a Ona kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      b Ikiwa unataka kujifunza zaidi kuhusu ahadi ya Biblia ya dunia Paradiso chini ya Ufalme wa Kristo, tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova. Watafurahi kujifunza Biblia pamoja nawe bila malipo.

      Kweli na Uwongo Kumhusu Musa

      Sinema zinazomhusu Musa zimeonyesha mambo fulani yasiyo ya kweli kumhusu. Mifano michache imeonyeshwa hapa chini:

      Uwongo: Musa hakujua asili yake ya Kiyahudi.

      Kweli: Musa alilelewa na mama yake Myahudi, labda kwa miaka michache. Matendo 7:23-25 inaonyesha kwamba Musa aliwaona watumwa Wayahudi kuwa “ndugu zake.”

      Uwongo: Musa alitaka kuwa mtawala wa Misri.

      Kweli: Biblia haisemi hivyo. Kichapo Daily Bible Illustrations, cha John Kitto, kinasema kwamba hakuna sababu inayoonyesha kwamba “malezi ya Musa yalimfanya awe mrithi wa ufalme. . . . Haionekani kwamba kulikuwa na ukosefu wa wavulana ambao wangerithi ufalme.”

      Uwongo: Musa alirudi Misri ili kumkabili adui yake.

      Kweli: Biblia inasema kwamba adui zake wote walikuwa wamekufa aliporudi.—Kutoka 4:19.

      Uwongo: Mungu alitoa Amri Kumi kwa mara ya kwanza baada ya Musa kupanda Mlima Sinai.

      Kweli: Amri Kumi zilitolewa na Mungu kwa taifa lote la Israeli kupitia malaika wake. Baadaye, Waisraeli wenye woga walimwomba Musa aende mlimani ili azungumze kwa niaba yao.—Kutoka 19:20–20:19; 24:12-14; Matendo 7:53; Waebrania 12:18, 19.

      Uwongo: Farao aliokoka wakati majeshi yake yalipoharibiwa kwenye Bahari Nyekundu.

      Kweli: “Farao na jeshi lake” waliangamia katika Bahari Nyekundu.—Kutoka 14:28; Zaburi 136:15.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki