-
Musa—Mtu Halisi au wa Hadithi?Amkeni!—2004 | Aprili 8
-
-
Musa Mtu Halisi au wa Hadithi?
MUSA alizaliwa wakati wa hatari. Familia yao ilikuwa kati ya familia ambazo zilihamia Misri pamoja na baba yao Yakobo, au Israeli, ili kuepuka njaa. Waliishi kwa amani na jirani zao Wamisri kwa miaka mingi. Lakini kukawa na badiliko lenye kuogopesha sana. Ripoti moja ya historia inayoheshimika inasema: “Mfalme mpya . . . akainuka juu ya Misri. Naye akawaambia watu wake: ‘Tazama! Watu wa wana wa Israeli ni wengi zaidi na wenye nguvu kuliko sisi. Haya! Na tuwatendee kwa werevu, wasije wakaongezeka.’” Wamisri walipanga kufanya nini? Kuwafanya Waisraeli kuwa “watumwa chini ya uonevu” ili wasiongezeke na kuwaamuru wazalishaji Waebrania kuwaua watoto wote wa kiume wanaozaliwa. (Kutoka 1:8-10, 13, 14) Licha ya dhuluma hiyo, Waisraeli waliongezeka kwa sababu ya ujasiri wa wazalishaji wao waliokataa kutii amri hiyo. Hivyo, mfalme wa Misri akaamuru: “Kila mwana anayezaliwa mtamtupa kwenye mto Nile.”—Kutoka 1:22.
Wenzi wawili Waisraeli, Amramu na Yokebedi, “hawakuliogopa agizo la mfalme.” (Waebrania 11:23) Yokebedi akamzaa mwana ambaye baadaye alisemwa kuwa “mwenye sura nzuri machoni pa Mungu.”a (Matendo 7:20) Huenda walitambua kwamba mtoto huyo alikuwa na kibali cha Mungu. Vyovyote vile, walikataa kumtoa mtoto wao auawe. Huku wakihatarisha uhai wao, waliamua kumficha.
Baada ya miezi mitatu, wazazi wa Musa hawangeweza kuendelea kumficha. Basi, waliamua kuchukua hatua. Yokebedi alimweka mtoto huyo katika safina ya mafunjo na kuiweka kwenye Mto Nile. Bila kujua, hatua hiyo ya Yokebedi ilimfanya Musa kuwa mtu maarufu katika historia!—Kutoka 2:3, 4.
Je, Matukio Hayo Ni ya Kweli?
Wasomi wengi leo husema kwamba matukio hayo ni hadithi tu. Gazeti Christianity Today linasema “ukweli ni kwamba hakuna uthibitisho wowote wa kiakiolojia unaoonyesha kwamba wana wa Israeli waliishi Misri kwa muda.” Ingawa hakuna uthibitisho wa moja kwa moja unaoonyesha jambo hilo, kuna uthibitisho mwingi usio wa moja kwa moja unaoonyesha kwamba simulizi hilo la Biblia ni la kweli. Katika kitabu chake Israel in Egypt, James K. Hoffmeier, mtaalamu wa vitu vya kale vya Misri, anasema: “Habari za kiakiolojia zinaonyesha kwamba watu wa upande wa mashariki wa Mediterania walitembelea Misri mara nyingi hasa kwa sababu ya ukame . . . Hivyo, kuanzia mwaka wa 1800 mpaka 1540 K.W.K. hivi, Wasemiti kutoka magharibi mwa Asia waliiona nchi ya Misri kuwa mahali pazuri pa kuhamia.”
Isitoshe, kwa muda mrefu imekubaliwa kwamba masimulizi ya Biblia kuhusu utumwa wa Waisraeli huko Misri ni sahihi. Kitabu Moses—A Life kinasema: “Masimulizi ya Biblia kuhusu kudhulumiwa kwa Waisraeli yanaungwa mkono na picha moja ya kaburi la Misri ya kale ambayo imechorwa mara nyingi inayoonyesha waziwazi kikundi cha watumwa kikitengeneza matofali.”
Masimulizi ya Biblia kuhusu safina ndogo ambayo Yokebedi alitumia ni ya kweli pia. Biblia inasema kwamba ilitengenezwa kwa mafunjo ambayo kulingana na kitabu Commentary cha Cook, “yalitumiwa sana na Wamisri kutengeneza mashua nyepesi zinazoenda mbio.”
Hata hivyo, je, kweli kiongozi wa nchi angeamuru watoto wachanga wauawe bila huruma? Msomi George Rawlinson anatukumbusha hivi: “Mauaji ya watoto . . . yametukia wakati na mahali mbalimbali, na yameonwa kuwa jambo dogo.” Ama kweli, hata katika nyakati zetu kumekuwa na mauaji ya watu wengi. Huenda simulizi la Biblia likahuzunisha, lakini ni la kweli kabisa.
Alelewa Nyumbani mwa Farao
Yokebedi hakuacha mtoto wake apotee tu. Aliiweka “[safina] katikati ya matete kando ya mto Nile.” Huenda aliiweka hapo kwa sababu alitarajia kwamba itagunduliwa. Huenda hapo ndipo binti ya Farao alipokuwa akioga kwa ukawaida.b—Kutoka 2:2-4.
Safina hiyo ndogo iligunduliwa haraka. “[Binti ya Farao] alipoifungua akamwona yule mtoto, na tazama, mvulana huyo alikuwa akilia. Kwa hiyo akamwonea huruma, ingawa alisema: ‘Huyu ni mmoja wa watoto wa Waebrania.’” Binti huyo wa Mfalme wa Misri aliamua kumlea. Jina ambalo wazazi wake walimpa lilisahauliwa. Leo, anajulikana duniani pote kwa jina alilopewa na mama yake mlezi, yaani, Musa.c—Kutoka 2:5-10.
Hata hivyo, je, haishangazi kwamba binti ya Mfalme wa Misri angemlea mtoto kama huyo? Sivyo, kwa kuwa dini ya Wamisri ilifundisha kwamba matendo ya fadhili yalikuwa takwa la kwenda mbinguni. Kuhusiana na hatua ya kumlea mtoto huyo, mwanaakiolojia Joyce Tyldesley anasema: “Wanawake Wamisri walikuwa na usawa na wanaume Wamisri. Walipaswa kuwa na haki sawa kisheria na kiuchumi, na . . . wanawake wangewalea watoto wa wengine.” Hati moja ya kale ya mafunjo inayohusu kuwalea watoto wa wengine inasema kuhusu mwanamke Mmisri aliyewalea watumwa wake. Kuhusu jinsi mama ya Musa alivyopewa kazi ya kumnyonyesha, kitabu The Anchor Bible Dictionary kinasema: “Mpango wa kumlipa mama ya Musa amtunze Musa . . . unafanana na mipango ya kuwalea watoto huko Mesopotamia.”
Kwa kuwa Musa alilelewa na mtu mwingine, je, angefichwa asili yake ya Kiebrania? Sinema fulani za Hollywood zimewafanya watu wafikiri hivyo. Hata hivyo, Maandiko yanasema tofauti. Kwa hekima, dada ya Musa, Miriamu, alipanga Musa alelewe na mama yake mwenyewe, Yokebedi. Bila shaka, mwanamke huyo mcha-Mungu angemweleza mwana wake ukweli kuhusu asili yake! Kwa kuwa watoto katika nyakati za kale walinyonyeshwa kwa miaka kadhaa, Yokebedi alikuwa na wakati wa kutosha kumfundisha Musa kumhusu ‘Mungu wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo.’ (Kutoka 3:6) Msingi huo wa kiroho ulimsaidia Musa kwa sababu baada ya kupelekwa kwa binti ya Farao, “Musa akafundishwa hekima yote ya Wamisri.”
-
-
Musa—Mtu Halisi au wa Hadithi?Amkeni!—2004 | Aprili 8
-
-
d Kitabu Israel in Egypt kinasema: “Dhana ya kwamba Musa alilelewa katika jumba la kifalme la Misri inaonekana kuwa hadithi tu. Lakini uchunguzi wa makini wa jumba la kifalme wakati wa falme za kati ya mwaka wa 1550 mpaka 1070 K.W.K. hivi, hauungi mkono dhana hiyo. Mfalme Thutmose wa 3 . . . alianzisha zoea la kuwapeleka Misri wana wa wafalme vibaraka wa mataifa ya magharibi mwa Asia ili wazoezwe desturi za Misri . . . Hivyo, wana na binti za wafalme wa mataifa mengine walikuwapo katika jumba la kifalme la Misri.”
-