-
“Imeandikwa”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
“Leo andiko hili . . . limetimizwa”
1-3. Yesu anawataka watu wa Nazareti watambue jambo gani, naye anatoa uthibitisho gani?
NI MAPEMA katika huduma ya Yesu. Amerudi Nazareti, mji wa nyumbani. Anakusudia kuwasaidia watu watambue jambo hili: Yeye ndiye Masihi aliyeahidiwa tangu zamani za kale! Anatoa uthibitisho gani?
2 Haikosi wengi wangetazamia afanye muujiza. Wamesikia mambo ya ajabu ambayo Yesu amefanya. Hata hivyo, hatoi ishara yoyote ya aina hiyo. Badala yake, anaingia katika sinagogi kama ilivyo desturi yake. Anasimama ili asome, naye anapewa kitabu cha kukunjwa cha Isaya. Ni kitabu kirefu ambacho inaelekea kimekunjwa katika vijiti viwili, naye Yesu anakikunjua kwa makini kutoka upande mmoja hadi mwingine mpaka anapopata fungu la maneno anayotafuta. Kisha anasoma kwa sauti maneno ambayo sasa yanapatikana katika Isaya 61:1-3.—Luka 4:16-19.
3 Lazima wasikilizaji hao wawe wanayajua maneno hayo. Ni unabii kumhusu Masihi. Kila mtu katika sinagogi anamkazia Yesu macho. Kumetulia tuli. Kisha, Yesu anaanza kufafanua waziwazi: “Leo andiko hili ambalo mmesikia sasa hivi limetimizwa.” Wasikilizaji wanastaajabia maneno yake yenye kuvutia sana, lakini inaonekana kwamba bado wengi wanataka kuona ishara fulani ya pekee. Hata hivyo, kwa uhodari Yesu anatumia mfano wa Kimaandiko kufunua ukosefu wao wa imani. Muda si muda, watu wa Nazareti wanajaribu kumuua!—Luka 4:20-30.
4. Yesu alituwekea mfano gani katika huduma yake, nasi tutachunguza nini katika sura hii?
4 Katika kisa hicho, Yesu alifanya jambo ambalo aliendelea kufanya katika huduma yake yote. Alitegemea sana Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Ni kweli, miujiza yake ilisaidia sana kuthibitisha kwamba roho ya Mungu ilikuwa pamoja naye. Hata hivyo, hakuna chochote machoni pa Yesu kilichokuwa cha maana kuliko Maandiko Matakatifu.
-