-
Norway2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
WASAMI WAKUBALI HABARI NJEMA
Kwa miaka mingi, mapainia wengi pamoja na wahubiri wengine wamewahubiria Wasami, kutia ndani wachungaji wa mbawala katika nyanda za mlima Finnmarksvidda. Ingawa Wasami wengi huzungumza Kinorway, wakati mwingine wahubiri wamelazimika kutumia wakalimani. Mmoja wa Mashahidi wa kwanza kuhubiri kwa mapana na marefu katika Kisami alikuwa Aksel Falsnes, mwenye asili ya Sami na aliyezungumza Kisami, Kinorway, na Kifini. Dada yake aliyeishi kusini mwa Norway, ambaye alikuwa amejifunza kweli, alimtumia kitabu chetu kimoja alichokisoma kwa hamu kubwa. Hakukuwa na Mashahidi katika eneo la Troms, ambamo aliishi, lakini katika mwaka wa 1968 mapainia kadhaa pamoja na mwangalizi wa mzunguko walimtembelea Aksel na kumsaidia kufanya maendeleo ya kiroho.
Aksel alikuwa mhubiri mwenye bidii. Mara nyingi aliibeba baiskeli yake katika mtumbwi wake mapema asubuhi, akavuka mkono wa bahari, na kisha akatumia baiskeli kutembelea jamii moja hadi nyingine. Kwa kuwa alijua Kisami, Aksel aliwahubiria Wasami kwa mafanikio katika sehemu za mbali za Finnmark.
Aksel alikuwa mtu mkakamavu, na alisafiri sana akitumia viatu vya kuteleza kwenye theluji ili kufika maeneo ya mbali. Kwa mfano, wakati fulani mwishoni mwa majira ya baridi kali, alisafiri kwa kuteleza kwenye theluji kutoka Karasjok akipitia nyanda za mlima hadi Kautokeino na kisha akaelekea Alta. Kile tu alichoweza kubeba ni mfuko wa kubeba mgongoni uliokuwa na vitu vichache vya kibinafsi pamoja na machapisho kadhaa. Baada ya majuma machache, alifika Alta, kwa rafiki zake, akiwa amesafiri umbali wa kilomita 400 akitumia viatu vya kuteleza kwenye theluji!
Mwanzoni mwa miaka ya 1970, Wasami kadhaa waliikubali kweli. Mjini Hammerfest, mwanamke mmoja Msami pamoja na mume wake walianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Baada ya muda mfupi, baadhi ya watu wake wa ukoo walioishi Alta wakapendezwa pia. Arne na Marie Ann Milde, waliokuwa mapainia wa pekee huko Alta, wakaanza kujifunza Biblia na watu hao wanyoofu na mara nyingi watu 10 au 12 walihudhuria funzo. Hatimaye, karibu nusu ya watu hao wakawa Mashahidi.
Hartvig Mienna, painia Msami huko Alta, ambaye hutumia kigari kinachoendeshwa juu ya theluji ili kuwafikia watu walio mbali asema: “Si rahisi kuhubiri katika eneo la Wasami. Maeneo yao yako mbali sana na wengi wanashikilia desturi zao. Lakini wao ni wakarimu sana, na tumefanikiwa kuanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia.”
-
-
Norway2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 142]
Hartvig Mienna na wahubiri wengine wakitumia magari yanayoendeshwa juu ya theluji wanapowahubiria Wasami
-