-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
KAZI YA KUTAFSIRI INASONGA MBELE
“Katika nchi iliyo na zaidi ya lugha 800, ni muhimu kuwa na lugha moja au zaidi ambazo watu wanaweza kutumia kuwasiliana,” anasema Timo Rajalehto, ambaye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi na msimamizi wa Idara ya Tafsiri. “Lugha rahisi zinazotumiwa katika biashara, kama vile Kitok Pisin na Kihiri Motu zinafaa kwa kusudi hilo. Ni rahisi kujifunza lugha hizo, na pia zinatumiwa katika shughuli za kila siku. Lakini haziwasilishi kwa njia inayofaa hoja ngumu. Kwa hiyo, mara nyingi watafsiri wetu hushindwa kueleza maneno mengine magumu.
“Kwa mfano, tuligundua kwamba hakuna neno la Kitok Pisin linaloweza kutafsiri kwa kufaa neno ‘kanuni.’ Kwa hiyo, watafsiri wetu waliunganisha maneno mawili ya lugha ya Tok Pisin ili kufanyiza neno stiatok (maneno ya kuelekeza), ambalo hufafanua jinsi ambavyo kanuni zinafanya kazi kwa kuwaelekeza watu katika njia inayofaa. Neno hilo lilianza kutumiwa na vyombo vya habari na sasa linatumiwa na watu wengi wanaozungumza Kitok Pisin.”
Gazeti Mnara wa Mlinzi lilianza kuchapishwa katika lugha ya Motu mwaka wa 1958, na katika lugha ya Tok Pisin mwaka wa 1960. Makala za funzo zilichapishwa huko Sydney, Australia, kwenye kurasa mojamoja ambazo ziliunganishwa kwa kibanio na kisha kusafirishwa kwa meli hadi Port Moresby. Katika mwaka wa 1970, kurasa ziliongezwa zikawa 24, na nakala zaidi ya 3,500 zilichapishwa. Gazeti Amkeni! lenye kurasa 24 lilichapishwa kwa mara ya kwanza katika lugha ya Tok Pisin mnamo Januari 1972. Kwa sasa, ofisi ya tawi hutayarisha gazeti Mnara wa Mlinzi mara mbili kwa mwezi na gazeti Amkeni! mara nne kwa mwaka katika lugha ya Tok Pisin na toleo la funzo la Mnara wa Mlinzi kila mwezi na toleo la watu wote mara nne kwa mwaka katika lugha ya Hiri Motu.
“Hivi majuzi, tulitafsiri baadhi ya trakti katika lugha mpya, kutia ndani lugha ya Enga, Jiwaka, Kuanua, Melpa, na Orokaiva,” anasema Timo Rajalehto. “Kwa kuwa watu wanaozungumza lugha hizo huzungumza pia lugha ya Tok Pisin au Kiingereza, au lugha zote mbili, kwa nini hilo lilifanywa? Tulitaka kuona jinsi ambavyo watu wataitikia ujumbe wa Ufalme katika lugha yao ya kienyeji. Je, watavutiwa na kweli na wawe na maoni yanayofaa kuwaelekea Mashahidi?
“Jibu la wazi ni ndiyo! Kwa kweli, kumekuwa na maelezo mengi mazuri kuhusu jambo hilo. Mafunzo ya Biblia yameanzishwa, na hata watu fulani ambao hapo awali walitupinga wamebadili mtazamo wao kuwaelekea Mashahidi. Watu wanapopata kichapo katika lugha yao ya kienyeji, jambo hilo huwa na matokeo mazuri.”
Kwa sasa, Idara ya Tafsiri ina watu 31, kutia ndani vikundi vya kutafsiri lugha ya Hiri Motu na Tok Pisin. Mnamo Desemba 2009, wote walifurahia kuhamia ofisi mpya za utafsiri.
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 155]
Kikundi cha watafsiri, 2010
-