-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Na tuambatane na mwangalizi mmoja pamoja na mke wake wanapotembelea makutaniko yaliyo kandokando ya mto huo mkubwa.
Warren Reynolds anaandika hivi: “Asubuhi na mapema, mimi na mke wangu, Leann, tunaelekea mji wa Wewak tukiwa tumefunga boti yetu ya alumini yenye urefu wa mita 3.5 juu ya gari letu. Baada ya kusafiri kwa saa tatu katika gari linaloendeshwa kwa magurudumu yote manne, tunaegesha gari hilo kando ya mto kwa siku chache na kusafiri sehemu ya juu ya mto huo ili kuwatembelea wahubiri 30 hivi wanaoishi katika vijiji vinne kando ya vijito vya Mto Sepik.
“Huku boti yetu ikiwa imepakiwa vitu, tunawasha injini yake na kuelekea upande wa juu wa mto. Baada ya saa moja, tunageuka na kuingia Mto Yuat, ambao ni kijito cha Mto Sepik, na kusafiri kwa saa mbili nyingine kabla ya kufika kijiji cha Biwat. Tunakaribishwa kwa uchangamfu na akina ndugu na wanafunzi wao wa Biblia, baadhi yao wanavuta boti yetu ufuoni na mmoja anaiweka nyumbani kwake. Baada ya kufurahia mlo wa ndizi na tui, sote tunafunga safari ya saa mbili kwa miguu kupitia msitu wenye vinamasi, wahubiri hao wakituongoza huku wakiwa wamebeba mizigo yetu. Hatimaye tunafika kwenye kijiji kidogo kinachoitwa Dimiri, ambapo tunakata kiu kwa tui, kisha katika nyumba iliyotengenezwa kwa vitu vinavyopatikana msituni na iliyojengwa juu ya nguzo za mbao, tunatayarisha mahali pa kulala na kuweka chandarua cha kujikinga na mbu. Baada ya kula viazi vikuu vilivyopikwa, tunaenda kulala.
“Wahubiri 14 wanaishi katika vijiji vitatu katika eneo hilo. Kwa siku chache zinazofuata, tunahubiri kila kijiji na kupata watu wengi wanaopendezwa. Pia tunafurahia kuona wanafunzi wawili wa Biblia wakihalalisha ndoa yao na kustahili kuwa wahubiri wa Ufalme. Wale wahubiri wengine wanaandaa karamu ya harusi ya viazi vikuu, sago, mboga fulani za majani, na kuku wawili.
“Siku ya Jumapili tunafurahia kuwa na hudhurio la wanakijiji 93 kwenye hotuba ya watu wote! Baada ya mkutano, saa za adhuhuri, mikoba yetu ikiwa imejaa, tunafunga safari ya kurudi Biwat, tunaacha mizigo yetu katika nyumba ya mwanafunzi fulani wa Biblia na kuanza kuhubiri. Watu wengi wanakubali vichapo vyetu; na baadhi yao wanakubali kujifunza Biblia. Usiku huo, katika nyumba ya mwanafunzi mmoja wa Biblia, tunaketi karibu na moto huku moshi ukifukuza mbu.
“Mapema siku inayofuata, tunarudi kwenye boti yetu, tunaisukuma mtoni na kuanza safari katika ukungu wa asubuhi huku tukifurahia ndege na samaki wanaoruka majini. Tunapishana na familia kwenye vyelezo vya mianzi wakienda kuuza bidhaa zao sokoni.
“Tunaporudi kwenye gari letu, tunajaza mafuta kwenye injini ya boti na kujaza maji ya kunywa ndani ya mitungi yetu na kupakia vitu vingine tutakavyohitaji. Kisha tukaelekea mtoni tena kuanza safari ya kuwatembelea wahubiri 14 huko Kambot. Tunawasili saa mbili baadaye tukiwa tumelowa kabisa kwa sababu ya mvua. Kutoka Kambot, tunaelekea upande wa juu wa mto huo, kwenye kijiji kimoja kikubwa kilichokuwa pande zote mbili za mto. Wakati huu boti yetu imejaa wahubiri. Tunawahubiria watu hao wenye uthamini hadi jioni. Tunapokuwa tukirudi, tunawahubiria watu ambao wamesimama kwenye gati za mianzi zilizokuwa zikielea majini. Walituona asubuhi tukielekea upande wa juu kwa hiyo wamekuwa wakitusubiri turudi. Kwa kuwa watu wengi katika eneo hili la mbali hawana pesa, wanakijiji wanatushukuru kwa kuwatembelea na kwa trakti ambazo tumewapa, kwa kutupa vyakula mbalimbali—nazi, maboga, samaki waliokaushwa, na ndizi. Jua linaposhuka, tunarudi Kambot na kuanza kupika vyakula hivyo.
“Huko Kambot, mahali pa kukutania pamejengwa juu ya nguzo ndefu za mbao kama nyumba zote katika eneo hilo zinavyojengwa. Wakati wa majira ya mvua, eneo hilo lote linapofurika, watu huendesha mitumbwi yao hadi kwenye mlango wa mahali pa mkutano. Katika siku ya mwisho ya ziara yetu, watu 72, kutia ndani wengine ambao wametembea kwa saa tano ili kufika mahali hapo, wanahudhuria hotuba ya watu wote.
“Baada ya kurudi kwenye gari letu na kufunga boti juu ya paa, tunaanza safari ya saa tatu kurudi nyumbani. Tukiwa njiani, tunatafakari kuhusu ndugu na dada zetu wapendwa wanaoishi kandokando ya Mto Sepik. Pia tunafikiria kuhusu jinsi Yehova anavyowapenda, kama inavyoonyeshwa kupitia jitihada ambazo tengenezo lake linafanya ili walishwe vizuri kiroho. Ni pendeleo kama nini kuwa sehemu ya familia hii nzuri!”
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 132, 133]
Kushoto: Mwangalizi wa mzunguko Warren Reynolds na mke wake, Leann, wakitembelea kijiji cha Biwat; juu: akitoa hotuba ya watu wote alipotembelea kijiji cha Dimiri
-