-
Tunaazimia Kutimiza Huduma YetuMnara wa Mlinzi—2007 | Juni 1
-
-
Mimi na John tulifunga ndoa Juni (Mwezi wa 6) 1955. Tulinunua basi tukiwa na nia ya kulibadili ili liwe nyumba. Kusudi letu lilikuwa kulitumia basi hilo ili kuhubiri maeneo ya mbali ya Australia. Mwaka uliofuata, ombi lilitolewa ili Mashahidi wahamie New Guinea, sehemu ya kaskazini-mashariki ya kisiwa kikubwa kilicho kaskazini ya Australia.a Ujumbe wa Ufalme haukuwa umehubiriwa katika sehemu hiyo ya ulimwengu. Tulijitolea mara moja kwenda huko.
Wakati huo, njia pekee ya kuingia New Guinea ilikuwa kupata kazi ya wakati wote. Hivyo, John alianza kutafuta kazi. Muda si muda, akapata kazi katika kiwanda cha mbao huko New Britain, kisiwa kidogo zaidi ambacho ni sehemu ya New Guinea. Majuma kadhaa baadaye, tulifunga safari ya kwenda kwenye mgawo wetu mpya. Tulifika Rabaul, New Britain, mnamo Julai 1956. Tulikaa huko siku sita tukingoja mashua ambayo ingetupeleka Waterfall Bay.
Huduma Yetu Huko Waterfall Bay
Baada ya siku kadhaa za safari hatari ya mashua, tulifika Waterfall Bay, ghuba kubwa iliyo kilomita 240 hivi kusini mwa Rabaul. Huko, kulikuwa na kiwanda kikubwa cha mbao katika uwanja fulani msituni. Jioni hiyo wafanyakazi wote walipokuwa wameketi kuzunguka meza ya chakula, msimamizi alisema hivi: “Bwana na Bibi Davison, ni sheria ya kampuni hii kwa wafanyakazi wote kusema wao ni wa dini gani.”
Tulikuwa na hakika kabisa kwamba hakukuwa na sheria kama hiyo, lakini kwa kuwa tulikuwa tumekataa kuvuta sigara, walikuwa na mashaka kutuelekea. Kwa vyovyote vile, John alisema: “Sisi ni Mashahidi wa Yehova.” Kisha, kukawa na kimya cha ajabu. Wanaume hao walikuwa wamepigana Vita vya Pili vya Ulimwengu na waliwachukia Mashahidi kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo wakati wa vita hivyo. Tangu hapo na kuendelea, walitafuta nafasi za kutuletea matatizo.
Mwanzoni msimamizi alikataa kutupa friji na jiko, ijapokuwa tulikuwa na haki ya kupewa vitu hivyo. Vyakula fulani tulivyokuwa navyo viliharibika haraka, nasi tulilazimika kupika chakula kwa kutumia jiko bovu tulilopata msituni. Baadaye, wanakijiji walikatazwa kutuuzia vyakula walivyotoka kuvuna, kwa hiyo, tulikula tu mboga tulizopata. Pia, walituita wapelelezi na walichunguza ikiwa tulikuwa tunamfundisha mtu yeyote Biblia. Kisha nikapata malaria.
Hata hivyo, tuliazimia kutimiza huduma yetu. Kwa hiyo, tuliwaomba vijana wawili wenyeji waliokuwa wakifanya kazi katika kiwanda hicho cha mbao ambao walijua Kiingereza watufundishe lugha ya Pijini ya Melanesia, ambayo ni lugha ya taifa. Na sisi tuliwafundisha Biblia. Mwishoni mwa juma tulikuwa tukifunga safari nyingi za kitalii ili “kujionea” nchi. Tukiwa safarini, tuliwahubiria kwa busara wanavijiji ambao tulikutana nao. Tulitumia wanafunzi wetu wa Biblia kama watafsiri wetu. Tulivuka mito yenye maji yanayotiririka kwa nguvu na pembeni kulikuwa na mamba wengi waliokuwa wakiota jua. Ijapokuwa pindi moja tuliponea chupuchupu, kwa kawaida hatukusumbuliwa na wanyama hao hatari.
Kutengeneza Vifaa vya Kufundishia
Kadiri huduma yetu ilivyopanuka, tuliamua kuchapisha ujumbe mfupi wa Biblia ili tuwape watu waliopendezwa. Wanafunzi wetu wa Biblia waliofanya kazi kiwandani walitusaidia kutafsiri ujumbe wa kwanza wa aina hiyo. Kwa siku nyingi, tulichapisha mamia ya trakti wakati wa usiku na kuzisambaza kwa wanavijiji na wafanyakazi wa mashua ambazo zilikuwa zikipita.
Mwaka wa 1957, John Cutforth, mhudumu anayesafiri mwenye uzoefu, alitutembelea na kututia moyo.b Alisema kwamba huenda kutumia picha kukawa njia yenye matokeo ya kuwafundisha kweli za Biblia watu ambao hawakujua kusoma. Yeye na mume wangu walichora, au kubandika picha fulani rahisi ili kueleza mafundisho ya msingi ya Biblia. Baadaye, tulitumia saa nyingi sana kuchora kwenye vitabu picha hizo ambazo tulitumia katika mahubiri. Kila mwanafunzi wa Biblia alipata nakala ambayo aliitumia kuwahubiria watu wengine. Mwishowe, njia hiyo ya kufundisha ilitumiwa nchini kote.
Baada ya kukaa huko Waterfall Bay kwa miaka miwili na nusu, tulikamilisha muda wetu wa kufanya kazi na tukakubaliwa kukaa nchini. Hivyo, tulipoombwa tuwe mapainia wa pekee tulikubali.
Tunarudi Rabaul
Tulipokuwa tukisafiri kaskazini kwenda Rabaul, mashua yetu ilisimama usiku wote huko Wide Bay karibu na shamba la minazi na kakao. Wenzi wa ndoa wazee ambao walimiliki shamba hilo, walitaka kustaafu na kuhamia Australia, nao walimwomba John asimamie shamba hilo. Kazi hiyo ilivutia sana, lakini tulipozungumzia jambo hilo usiku huo, tulikubaliana kwamba hatukuja New Guinea kutafuta mali za kimwili. Tuliazimia kutimiza huduma yetu tukiwa mapainia. Hivyo, siku iliyofuata tuliwajulisha wenzi hao wa ndoa uamuzi wetu na tukapanda tena mashua yetu.
Baada ya kufika Rabaul, tulijiunga na kikundi kidogo cha Mashahidi kutoka nchi nyingine waliokuwa wamehamia eneo hilo. Watu wa eneo hilo walipendezwa sana na ujumbe wa Ufalme, nasi tulianzisha mafunzo mengi ya Biblia. Wakati huohuo, tulifanya mikutano ya Kikristo katika jumba la kukodi, na watu 150 hivi walihudhuria. Wengi wao walikubali kweli na wakasaidia kueneza habari njema ya Ufalme wa Mungu katika sehemu nyingine nchini.—Mathayo 24:14.
Pia, tulitembelea Vunabal, kijiji kidogo kilicho kilomita 50 kutoka Rabaul. Watu kadhaa katika kijiji hicho walipendezwa sana na kweli ya Biblia. Muda si muda, Mkatoliki fulani mashuhuri alitambua jambo hilo. Akiwa pamoja na marafiki wake wa kanisani, alivunja funzo letu la Biblia la kila juma na kutufukuza katika kijiji hicho. Tulipojua kwamba kungekuwa na matatizo zaidi juma lililofuata, tuliwaomba polisi watusindikize.
Siku hiyo Wakatoliki wenye dhihaka walisimama kando ya barabara kwa umbali wa kilomita kadhaa. Wengi wao walikuwa tayari kutupiga kwa mawe. Wakati huo, kasisi mmoja alikuwa amekusanya kijijini mamia ya wanaume wa kabila fulani. Polisi walituhakikishia kwamba tulikuwa na haki ya kufanya mkutano wetu, hivyo waliwatawanya watu ili tuweze kupita. Hata hivyo, punde tu tulipoanza mkutano wetu, yule kasisi aliwachochea watu waanze fujo. Polisi walishindwa kuuzuia umati huo wa watu; hivyo, mkuu wa polisi akatusihi tuondoke na akatupeleka haraka kwenye gari letu.
Watu hao walituzunguka, wakitutukana, kututemea mate, na kutikisa ngumi zao huku kasisi akiwa amesimama, amekunja mikono yake, na kutabasamu. Baada ya sisi kukimbia, mkuu wa polisi alisema kwamba hajawahi kamwe kuona tukio baya kama hilo. Ingawa watu wengi huko Vunabal waliogopa kujifunza kweli kwa sababu ya jeuri ya umati huo, mwanafunzi mmoja wa Biblia alikubali kwa ujasiri kweli ya Ufalme. Tangu wakati huo, mamia ya watu wengine kotekote katika New Britain wamechukua msimamo wao upande wa kweli.
Eneo la New Guinea Linafunguka
Mnamo Novemba (Mwezi wa 11) 1960, tulitumwa Madang, mji mkubwa ulio katika pwani ya kaskazini ya New Guinea, ambacho ndicho kisiwa kikuu. Katika mji huo, mimi na John tulipewa nafasi nyingi sana za kuajiriwa kazi ya muda wote. Kampuni moja iliniomba nisimamie duka la nguo. Kampuni nyingine ilitaka nifanye kazi ya kurekebisha nguo. Wanawake fulani wa kigeni walijitolea kunisaidia kufungua duka langu mwenyewe la kushona nguo. Kwa kuwa tuliendelea kukumbuka mradi wetu, tulikataa kwa fadhili nafasi hizo na nyinginezo.—2 Timotheo 2:4.
Eneo la Madang lilikuwa na matokeo mazuri, na muda si muda kutaniko lenye kusitawi likaanzishwa. Tulisafiri kwa miguu na kwa pikipiki ili kuhubiri kwa siku kadhaa katika vijiji vilivyokuwa kandokando ya mji huo. Tulilala katika nyumba za misonge zilizohamwa, nasi tulilalia marundo ya nyasi tulizokata porini. Tulibeba tu chakula cha mikebe, biskuti, na chandarua ili kujikinga na mbu.
Pindi moja, tulitembelea kikundi cha watu waliopendezwa huko Talidig, kijiji kilicho kilomita 50 hivi kaskazini mwa Madang. Kwa kuwa watu hao walikuwa wakifanya maendeleo ya kiroho, mwalimu mkuu wa shule ya eneo hilo aliwakataza wasijifunzie Biblia tena kwenye uwanja wa watu wote. Baadaye, alichochea polisi waharibu nyumba za watu hao na kuwafukuza waishi porini. Hata hivyo, chifu wa eneo jirani alikubali watu hao waishi katika eneo lake. Baada ya muda, chifu huyo mwenye fadhili alikubali kweli ya Biblia, na Jumba jipya la Ufalme likajengwa katika eneo hilo.
Kazi ya Kutafsiri na ya Kusafiri
Miaka miwili tu baada ya kufika New Britain mwaka wa 1956, mimi na John tuliombwa tutafsiri vichapo mbalimbali vya Biblia katika lugha ya Pijini ya Melanesia. Tulifanya kazi hiyo kwa miaka mingi. Kisha mwaka wa 1970, tulialikwa katika ofisi ya tawi ya Port Moresby, mji mkuu wa Papua New Guinea, ili tufanye kazi ya wakati wote ya kutafsiri. Pia tuliwafundisha wengine lugha.
Mwaka wa 1975 tulirudi huko New Britain ili kufanya kazi ya kusafiri. Kwa miaka 13 iliyofuata, tulisafiri kwa ndege, mashua, gari, au miguu kwenda karibu kila sehemu ya nchi. Tulikabili hatari nyingi njiani, kutia ndani lile tukio lililotajwa mwanzoni mwa simulizi hili. Wakati huo, tulipokuwa tukikaribia uwanja mdogo wa ndege wa Kandrian huko New Britain, rubani alizimia kwa sababu ya vidonda vibaya sana vya tumbo. Tulizunguka juu ya jangwa huku ndege ikiwa katika mfumo wa kujiendesha yenyewe, naye John alikuwa akijaribu sana kumwamsha rubani aliyezimia. Mwishowe, rubani alirudiwa na fahamu, naye akaona vizuri kidogo na hivyo akaweza kutua, lakini alitua kwa shida. Kisha akazimia tena.
Mlango Mwingine wa Utendaji Unafunguka
Mwaka wa 1988, tulipewa mgawo wa kurudi tena Port Moresby ili kusaidia katika kazi ya kutafsiri iliyokuwa ikiongezeka kwenye ofisi ya tawi. Tukiwa watu 50 hivi tuliishi na kufanya kazi kama familia katika ofisi ya tawi, na pia tuliwazoeza watafsiri wapya. Sote tuliishi katika nyumba yenye vyumba vingi vidogo. Mimi na John tuliamua kuacha mlango wa chumba chetu ukiwa wazi ili kuwatia moyo washiriki wa familia yetu na wageni wengine waingie na kufahamiana nasi. Hivyo, tukawa na uhusiano wa karibu sana pamoja na familia yetu, tulipendana na kutegemezana sana.
Mwaka wa 1993, John alikufa kutokana na mshtuko wa moyo. Nilihisi kana kwamba sehemu fulani ya mwili wangu ilikuwa imekufa pia. Tuliishi pamoja katika ndoa kwa miaka 38 na tulitumia wakati huo wote pamoja katika huduma. Bado niliazimia kuendelea kwa nguvu za Yehova. (2 Wakorintho 4:7) Mlango wa chumba changu ulibaki wazi, na vijana waliendelea kunitembelea. Ushirika huo mzuri ulinisaidia kudumisha mtazamo mzuri.
-
-
Tunaazimia Kutimiza Huduma YetuMnara wa Mlinzi—2007 | Juni 1
-
-
Simulizi la Maisha
Tunaazimia Kutimiza Huduma Yetu
Kama lilivyosimuliwa na Lena Davison
“Ninapoteza uwezo wangu wa kuona. Siwezi kuona,” akasema rubani wetu kwa sauti isiyosikika vizuri. Muda mfupi baadaye, aliacha kushikilia usukani wa ndege ndogo tuliyokuwa tukisafiria, akazimia kwenye kiti chake. Mume wangu ambaye hakujua kuendesha ndege, alijaribu awezavyo kumwamsha. Kabla sijawaeleza jinsi tulivyoponea chupuchupu, acheni nieleze kilichofanya tusafiri kwa ndege hiyo iliyokuwa katika anga la Papua New Guinea, mojawapo ya sehemu za mbali zaidi za dunia.
-