-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Baadaye, Jim Wright, mwana wa Dorothy, pamoja na painia mwenzake, Kerry Kay-Smith walipewa mgawo wa kwenda Banz, wilaya ya kukuza chai na kahawa katika bonde maridadi la Wahgi mashariki ya Mlima Hagen. Huko walikabili upinzani mkali kutoka kwa makanisa, ambayo yaliwachochea watoto wawatupie mawe na kuwafukuza kutoka vijijini mwao. Kerry alipohamia kwenye mgawo mwingine, Jim alibaki Banz, akifanya upainia akiwa peke yake. Anakumbuka hivi: “Mara nyingi nilijilaza kitandani usiku katika nyumba yangu ndogo ya nyasi nikisali, ‘Yehova, ninafanya nini hapa?’ Miaka mingi baadaye ndipo tu nilipopata jibu la swali hilo.
“Katika mwaka wa 2007, nilisafiri kutoka Australia kwenda Banz ili nihudhurie kusanyiko la wilaya,” Jim anasema. “Karibu na mahali ambapo ile nyumba yangu ya nyasi ilikuwa, sasa kulikuwa na Jumba jipya la Ufalme ambalo lingeweza kupanuliwa na kuwa Jumba la Kusanyiko ambalo lingeweza kutoshea watu 1,000. Nilipoingia katika eneo hilo, ndugu mmoja alinikimbilia, akanishika, na kuanza kulia begani mwangu. Mwishowe, ndugu huyo anayeitwa Paul Tai, alipoacha kulia, alinieleza kwamba nilikuwa nimejifunza na baba yake miaka 36 iliyopita. Baadaye Paul alisoma vitabu ambavyo baba yake alitumia kujifunza na akaikubali kweli. Aliniambia kwamba anatumika akiwa mzee.
“Wakati wa kusanyiko hilo, nilihojiwa jukwaani na nikaeleza mateso ambayo tulivumilia zamani huko Banz,” akasema Jim. “Karibu kila mtu aliyekuwa akisikiliza alitokwa na machozi. Baada ya programu baadhi ya akina ndugu walikuja wakanikumbatia na kuomba msamaha huku wakitokwa na machozi. Walipokuwa wavulana, walikuwa wamenifukuza kutoka kijijini mwao huku wakinitupia mawe na kunitusi. Isitoshe, mmoja wao, Mange Samgar—ambaye sasa ni mzee—ndiye kasisi wa Kilutheri aliyekuwa amewachochea wafanye hivyo! Kusanyiko hilo lilikuwa wakati mzuri kama nini wa kukutana tena!”
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 114]
Kerry Kay-Smith na Jim Wright
-