-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
KUHUBIRI KWENYE NYANDA ZA JUU
Katika mwezi huohuo, Tom na Rowena Kitto walitoka Port Moresby na kufunga safari ngumu ya majuma kadhaa. Walikuwa wakielekea maeneo ambayo hayajahubiriwa kwenye nyanda za juu za New Guinea.
Miaka 30 mapema, Waaustralia waliokuwa wakitafuta dhahabu waliingia kwenye nyanda hizo na kugundua karibu watu milioni moja ambao hawakuwa wamewahi kuwasiliana na sehemu nyingine za dunia. Wenyeji hao waliopigwa na butwaa walidhani wanaume hao wazungu walikuwa roho za mababu wao waliokuwa wamefufuka.
Baada tu ya watu hao waliokuwa wakitafuta dhahabu, wamishonari wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walifuata. “Wamishonari hao waliposikia kwamba tunaenda huko, waliwaamuru wanakijiji wasitusikilize,” anasema Rowena. “Lakini onyo lao lilitusaidia sana. Watu hao wa nyanda za juu—ambao kwa kawaida ni wadadisi—walikuwa wakitusubiri kwa hamu tufike.”
Tom na Rowena walifungua duka dogo huko Wabag, kilomita 80 kaskazini-magharibi ya mji wa Mlima Hagen. “Makasisi waliwaagiza wafuasi wao wasinunue chochote kutoka kwetu, wasituuzie, au hata kuzungumza nasi na wakawashinikiza waombe tunyang’anywe ardhi yetu,” anasema Tom. “Hata hivyo, baada ya muda, wanakijiji hao waliona kwamba tulikuwa tofauti na wazungu wengine ambao waliwafahamu. Jambo lililoonekana wazi ni kwamba tuliwatendea kwa fadhili. Kwa kweli, mara nyingi matendo yetu ya fadhili yaliwafanya walie machozi na wakasema kwamba walitaka tuendelee kuishi huko!”
KUHUBIRI KWA SUBIRA KUNALETA MATOKEO
Kuanzia mwaka wa 1963 na kuendelea, Mashahidi kutoka nchi nyingine walihamia kwenye nyanda za juu ili kusaidia katika upanuzi wa kazi ya kuhubiri. Wakisonga polepole kutoka mashariki hadi magharibi, hao akina ndugu na dada walihubiri katika eneo lote, wakianzisha vikundi na makutaniko katika maeneo mengi.
Huko Goroka, kwenye Mkoa wa Nyanda za Juu za Mashariki, kutaniko dogo lilikutana nyumbani kwa mtu fulani. Baadaye, walijenga mahali pa kukutania kwa kutumia vifaa walivyopata msituni. Kisha, mnamo 1967, walijenga Jumba la Ufalme lenye kuvutia lililokuwa na viti 40. “Nilitania kwamba tutajaza viti hivyo wakati wa Har–Magedoni,” anasema George Coxsen, aliyetumika kwenye nyanda za juu kwa miaka kumi. “Nilikosea kama nini! Katika muda wa miezi 12, watu wengi sana walikuwa wakihudhuria mikutano hivi kwamba tulihitaji kuanzisha kutaniko la pili!”
Mbali zaidi upande wa mashariki, karibu na Kainantu, Norm Sharein alijifunza Biblia na zaidi ya wanakijiji 50 ambao walikuja nyumbani kwake kila siku. Baadaye, mapainia Berndt na Erna Andersson walitunza kikundi hicho kwa muda wa miaka miwili na nusu. “Mara nyingi watu hawakuoga, walivalia mavazi machache, hawakujua kusoma na kuandika, na walijihusisha sana na uchawi,” anaeleza Erna. “Hata hivyo, kwa sababu ya kusaidiwa kwa subira na upendo, baadhi yao walianza kukariri na kueleza maandiko 150.”
Berndt na Erna walikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na kikundi hicho. “Tulipopewa mgawo wa kwenda Kavieng, wanawake walinizunguka wakilia, na kuomboleza kwa sauti kubwa!” anasema Erna. “Mmoja baada ya mwingine, walishika mikono yangu na kunigusa usoni huku machozi yao yakitiririka. Tena na tena, nilirudi ndani ya nyumba na kulia huku Berndt akijaribu kuwatuliza, lakini hawangeweza kufarijika. Mwishowe, tulipoanza kuondoka, umati mkubwa ulifuata gari letu lilipokuwa likiteremka mlimani, wanawake wakilia kwa sauti kubwa. Bado mimi hushindwa na hisia ninapoeleza jinsi nilivyohisi siku hiyo. Tunatamani kama nini kuwaona watu hao tuliowapenda sana katika ulimwengu mpya!” Mapainia wengine waliendeleza kazi ya Berndt na Erna, na kutaniko zuri likaanzishwa huko Kainantu.
MBEGU YA UFALME ILIYOPANDWA YATOKEZA MATUNDA
Kufikia mwanzoni mwa miaka ya 1970, kikundi kidogo cha Mashahidi kilikuwa kimeanza kwenye mji wa Mlima Hagen, kilomita 130 hivi magharibi ya Goroka. Mji huo ulijulikana sana kwa ajili ya soko lake la kila juma, ambalo liliwakusanya pamoja maelfu ya watu kutoka vijiji vya mbali. “Tuliwaachia watu vichapo vingi sana katika soko hilo,” anasema Dorothy Wright painia asiye na woga. Watu hao waliporudi kwenye vijiji vyao, ujumbe wa Ufalme ulienda pamoja nao, na ukapenya katika maeneo ya mbali ambayo wahubiri hawangeweza kufika wakati huo.
Baadaye, Jim Wright, mwana wa Dorothy, pamoja na painia mwenzake, Kerry Kay-Smith walipewa mgawo wa kwenda Banz, wilaya ya kukuza chai na kahawa katika bonde maridadi la Wahgi mashariki ya Mlima Hagen. Huko walikabili upinzani mkali kutoka kwa makanisa, ambayo yaliwachochea watoto wawatupie mawe na kuwafukuza kutoka vijijini mwao. Kerry alipohamia kwenye mgawo mwingine, Jim alibaki Banz, akifanya upainia akiwa peke yake. Anakumbuka hivi: “Mara nyingi nilijilaza kitandani usiku katika nyumba yangu ndogo ya nyasi nikisali, ‘Yehova, ninafanya nini hapa?’ Miaka mingi baadaye ndipo tu nilipopata jibu la swali hilo.
“Katika mwaka wa 2007, nilisafiri kutoka Australia kwenda Banz ili nihudhurie kusanyiko la wilaya,” Jim anasema. “Karibu na mahali ambapo ile nyumba yangu ya nyasi ilikuwa, sasa kulikuwa na Jumba jipya la Ufalme ambalo lingeweza kupanuliwa na kuwa Jumba la Kusanyiko ambalo lingeweza kutoshea watu 1,000. Nilipoingia katika eneo hilo, ndugu mmoja alinikimbilia, akanishika, na kuanza kulia begani mwangu. Mwishowe, ndugu huyo anayeitwa Paul Tai, alipoacha kulia, alinieleza kwamba nilikuwa nimejifunza na baba yake miaka 36 iliyopita. Baadaye Paul alisoma vitabu ambavyo baba yake alitumia kujifunza na akaikubali kweli. Aliniambia kwamba anatumika akiwa mzee.
“Wakati wa kusanyiko hilo, nilihojiwa jukwaani na nikaeleza mateso ambayo tulivumilia zamani huko Banz,” akasema Jim. “Karibu kila mtu aliyekuwa akisikiliza alitokwa na machozi. Baada ya programu baadhi ya akina ndugu walikuja wakanikumbatia na kuomba msamaha huku wakitokwa na machozi. Walipokuwa wavulana, walikuwa wamenifukuza kutoka kijijini mwao huku wakinitupia mawe na kunitusi. Isitoshe, mmoja wao, Mange Samgar—ambaye sasa ni mzee—ndiye kasisi wa Kilutheri aliyekuwa amewachochea wafanye hivyo! Kusanyiko hilo lilikuwa wakati mzuri kama nini wa kukutana tena!”
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 112]
‘Je, Wamekula Moyo Wako?’
AIOKOWAN
ALIZALIWA 1940
ALIBATIZWA 1975
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Mmoja kati ya watu wa kwanza kutoka Enga kujifunza kweli.
◼ WAKATI Tom na Rowena Kitto walipofika Wabag, Mkoa wa Enga, wamishonari wenyeji walieneza habari za uwongo kuwahusu. Kwa mfano, wamishonari hao walidai kwamba Tom na Rowena waliifukua miili ya wafu na kuila. Uvumi huo uliniogopesha sana.
Siku moja Tom alimwuliza baba yangu ikiwa alijua msichana fulani ambaye angeweza kumsaidia mke wake kufanya kazi za nyumbani. Baba alimweleza kwamba ningekuwa tayari kufanya hivyo. Niliogopa sana, lakini baba alinilazimisha nifanye kazi hiyo.
Baadaye, Tom na Rowena waliniuliza, “Unafikiri ni nini huwapata watu wanapokufa?”
“Watu wazuri huenda mbinguni,” nilijibu.
“Je, ulisoma hivyo katika Biblia?” waliuliza.
“Sijawahi kwenda shule, kwa hiyo sijui kusoma,” nikajibu.
Walianza kunifundisha kusoma, na pole kwa pole nilianza kuelewa kweli za Biblia. Nilipoacha kuhudhuria Kanisa Katoliki, mmoja wa viongozi wa kanisa hilo aliniuliza: “Kwa nini uliacha kuja kanisani? Je, wazungu hao wawili wamekula moyo wako?”
“Ndiyo,” nikajibu, “nimewapa moyo wangu wa mfano kwa sababu ninajua kwamba wananifundisha kweli.”
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 109]
Nyanda za juu
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 110]
Tom na Rowena Kitto wakiwa mbele ya duka lao dogo na nyumba yao huko Wabag
-