-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
‘WAPIGENI MARUFUKU MASHAHIDI’
Wapinzani wetu hawakufurahia maendeleo hayo. Kuanzia 1960 na kuendelea, muungano wa makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo, shirika la kuwategemeza wanajeshi waliostaafu na wanajeshi wengine wa Australia (Returned Services League, RSL), na vyombo vya habari vilianza kampeni iliyopangwa ya kuwavunjia heshima na kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova.
Mambo yalifikia kilele wakati ambapo karatasi iliyochapishwa kuhusu msimamo wetu juu ya kutiwa damu mishipani iliposambazwa kwa madaktari, makasisi, na maofisa wa serikali. Kama kawaida, makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo ndio waliokuwa wa kwanza kusema. Agosti 30, 1960, gazeti South Pacific Post lilikuwa na kichwa “Makanisa Yakasirishwa na Suala la Damu.” Katika makala inayokuwa ndani, viongozi wa kanisa walisema kuwa Mashahidi ni “wapinga-Kristo [na] maadui wa Kanisa.”
Makala zilizofuata zilidai kwa uwongo kwamba Mashahidi wa Yehova ni wachochezi na kwamba mafundisho yao yaliwachochea watu wasiende shuleni, wasilipe kodi, wajiunge na madhehebu ya waabudu-mali, na wasidumishe usafi. Ripoti nyingine za uwongo ziliwashtaki kwa kutumia vibaya kupatwa kwa jua ili kuwaogopesha na “kuwadhibiti wenyeji wasio na elimu.” Gazeti moja hata liliwazomea Mashahidi kwa “kuishi, kula, na kufanya kazi pamoja na wanakijiji.” Gazeti South Pacific Post liliwachambua kwa kufundisha kwamba “watu wote wako sawa” na likadai kwamba Mashahidi ni “tisho kubwa kuliko Ukomunisti.”
Mwishowe, Machi 25, 1962, RSL iliwaomba wenye mamlaka wakoloni wawapige Mashahidi marufuku. Hata hivyo, serikali ya Australia ilikataa waziwazi ombi hilo. “Tangazo hilo lilikuwa na matokeo mazuri katika nchi yote,” anasema Don Fielder. “Watu wenye akili zilizofunguka wangeweza kuona kwamba madai ya wapinzani hayakuwa ya kweli.”
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Baada tu ya watu hao waliokuwa wakitafuta dhahabu, wamishonari wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walifuata. “Wamishonari hao waliposikia kwamba tunaenda huko, waliwaamuru wanakijiji wasitusikilize,” anasema Rowena. “Lakini onyo lao lilitusaidia sana. Watu hao wa nyanda za juu—ambao kwa kawaida ni wadadisi—walikuwa wakitusubiri kwa hamu tufike.”
Tom na Rowena walifungua duka dogo huko Wabag, kilomita 80 kaskazini-magharibi ya mji wa Mlima Hagen. “Makasisi waliwaagiza wafuasi wao wasinunue chochote kutoka kwetu, wasituuzie, au hata kuzungumza nasi na wakawashinikiza waombe tunyang’anywe ardhi yetu,” anasema Tom. “Hata hivyo, baada ya muda, wanakijiji hao waliona kwamba tulikuwa tofauti na wazungu wengine ambao waliwafahamu. Jambo lililoonekana wazi ni kwamba tuliwatendea kwa fadhili. Kwa kweli, mara nyingi matendo yetu ya fadhili yaliwafanya walie machozi na wakasema kwamba walitaka tuendelee kuishi huko!”
-