Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Papua New Guinea
    2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • MAKUSANYIKO YASIYOSAHAULIKA

      Mnamo Julai 1955, John Cutforth, mmishonari Mkanada aliyekuwa akitumika huko Australia, aliwasili Port Moresby na kuwa mwangalizi wa kwanza wa mzunguko. Mara moja, John alipenda eneo hilo, utamaduni, na watu wake. Hakujua kwamba angetumika nchini Papua New Guinea kwa zaidi ya miaka 35.

      John alifika akiwa na sinema inayoitwa The New World Society in Action, masimulizi yaliyoonyesha utaratibu wa tengenezo na makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Wakati wa ziara yake ya majuma matatu, alionyesha sinema hiyo mara 14 nyakati nyingine mbele ya mamia ya wahudhuriaji au hata mbele ya watu 2,000 hivi. Watu wengi sana waliifurahia, hiyo ikiwa mara ya kwanza kwa wengine wao kutazama sinema yoyote.

      Ziara ya John ilifikia mwisho wakati wa kusanyiko la mzunguko la siku moja huko Haima. “Wanaotaka kubatizwa walipoombwa wasimame, . . . watu 70 walisimama!” anakumbuka Tom Kitto. “Mioyo yetu ilijawa na shangwe tulipoona ndugu 40 na dada 30 wakisimama msituni kwenye ukingo wa mto wakiwa tayari kuonyesha wakfu wao kwa Yehova.”

      Mwaka uliofuata, akina ndugu walipanga kuwa na kusanyiko la pili la mzunguko huko Haima. Bobogi, chifu wa kijiji, alipewa mgawo wa kutayarisha mahali pa kusanyiko na chakula kwa ajili ya wote waliotazamiwa kuhudhuria. Siku tatu kabla ya kusanyiko, John (Ted) Sewell, mwangalizi mpya wa mzunguko kutoka Australia, alikutana na Bobogi kuzungumzia matayarisho hayo.

      “Umejenga nini?” akauliza Ted moja kwa moja.

      “Hakuna,” Bobogi akamjibu.

      “Bobogi, leo ni Alhamisi (Siku ya 4) na kusanyiko ni Jumapili!” Ted akasema kwa mshangao.

      “Ni kweli, ndugu,” akajibu Bobogi. “Tutatayarisha kila kitu Jumamosi.”

      Ted alishangaa na kurudi Port Moresby akiwa na uhakika kwamba hakutakuwa na utaratibu wowote katika kusanyiko hilo.

      Jumapili hiyo alielekea Haima akiwa na wasiwasi kuona ni nini ambacho kingetukia. Kulikuwa na mabadiliko makubwa kama nini! Chini ya mti mkubwa kulikuwa na jukwaa la mbao mbele ya eneo kubwa lililokuwa limefyekwa. Mbali kidogo kulikuwa na maeneo ya kupikia, ambako nguruwe, wallaby, mbawala, hua, samaki, viazi vikuu, na viazi vitamu vilikuwa vikichomwa. Birika za chai zilikuwa zikichemka. Watu walichangamana kwa furaha katika eneo la kula lililotengenezwa kwa vifaa vilivyopatikana msituni. Bobogi alisimama katikati ya hekaheka hizo zote, bila wasiwasi wowote. Ted alistaajabu sana!

      “Bobogi, ulijifunzia wapi kufanya mambo haya yote?” akamwuliza.

      “Oh, niliona mambo yote haya katika sinema ile ambayo John Cutforth alituonyesha mwaka uliopita,” Bobogi akajibu.

      Zaidi ya watu 400 kutoka katika makabila manane walihudhuria kusanyiko hilo, na 73 wakabatizwa. Miaka iliyofuata, kusanyiko hilo likaja kuitwa kusanyiko la Bobogi.

  • Papua New Guinea
    2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • KUTUMIA PICHA KUHUBIRI

      Mnamo 1957, John Cutforth alihamia kabisa Papua New Guinea na kuwa mwangalizi anayesafiri huko. Tangu ziara yake ya kwanza, alikuwa amefikiria sana njia bora zaidi ya kuwahubiria wenyeji, kwa kuwa wengi wao hawakujua kusoma na kuandika. Sasa alikuwa tayari kutumia mbinu yake.

      Alipokuwa akitoa hotuba mbele ya kutaniko au kikundi cha mbali, John aliandika jina lake na la mtafsiri kwenye ubao mweusi. Kisha, akaelekeza kidole mbinguni, na kuwauliza wasikilizaji, “Mungu, jina lake nani?” Akaandika jibu lao, “Yehova” na “Zaburi 83:18” juu ya ubao huo. Chini yake upande wa kushoto, aliandika kichwa “Ulimwengu wa Kale” na kuchora wanaume wawili wakipigana, mtu akilia, kaburi, na “Waroma 5:12.” Upande wa kulia, akaandika kichwa “Ulimwengu Mpya” na kuchora wanaume wawili wakisalimiana kwa mikono, mtu akitabasamu, kaburi lililofutwa, na “Ufunuo 21:4.” Baadaye, alitoa hotuba yenye kusisimua ili kueleza michoro yake. Kisha akawakaribisha wasikilizaji wasimame mbele na kurudia hotuba yake. Walipokuwa wameelewa, aliwaambia wachore picha hizo kwenye karatasi na kuzitumia katika kazi ya kuhubiri.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki