Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ni Daraka la Kikristo Kuwatunza Walio Wazee
    Mnara wa Mlinzi—2004 | Mei 15
    • Daraka Letu Tukiwa Watoto

      4. Watoto Wakristo wana daraka gani kuelekea wazazi wao?

      4 “Mheshimu baba yako na mama yako.” (Waefeso 6:2; Kutoka 20:12) Mtume Paulo alitumia andiko hilo rahisi lakini muhimu ambalo limenukuliwa kutoka katika Maandiko ya Kiebrania, ili kuwakumbusha watoto daraka lao kwa wazazi wao. Lakini maneno hayo yanahusianaje na kuwatunza walio wazee? Ili kujibu swali hilo acheni tufikirie kielelezo chenye kuchangamsha moyo cha kabla ya Ukristo.

      5. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yosefu hakuwa amesahau madaraka yake kuelekea wazazi? (b) Inamaanisha nini kuwaheshimu wazazi wetu, naye Yosefu aliweka kielelezo gani kizuri kuhusiana na hilo?

      5 Kwa miaka zaidi ya 20, Yosefu hakuwasiliana na Yakobo, babake mzee aliyekuwa mzee wa ukoo. Hata hivyo, ni wazi kwamba bado Yosefu alimpenda babake Yakobo. Kwa kweli, Yosefu alipojitambulisha kwa ndugu zake, aliuliza: “Je, baba yangu angali hai?” (Mwanzo 43:7, 27; 45:3) Wakati huo, nchi ya Kanaani iliathiriwa na njaa kali. Hivyo, Yosefu alituma ujumbe kwa babake, na kusema: “Njoo kwangu. Usikawie. Ukae katika nchi ya Gosheni, uishi karibu nami . . . Nami nitakupa chakula huko.” (Mwanzo 45:9-11; 47:12) Naam, kuwaheshimu wazazi waliozeeka hutia ndani kuwalinda na kuwaandalia mahitaji ya kimwili ikiwa hawawezi kufanya hivyo. (1 Samweli 22:1-4; Yohana 19:25-27) Yosefu alikubali kwa furaha daraka hilo.

      6. Yosefu alionyeshaje upendo wa kweli kwa babake, nasi tunawezaje kuiga kielelezo chake?

      6 Yosefu alisaidiwa na Yehova kuwa mmoja wa watu tajiri na wenye uwezo mkubwa zaidi nchini Misri. (Mwanzo 41:40) Lakini hakujiona kuwa mtu wa maana sana au mwenye shughuli nyingi sana asiweze kumheshimu babake mwenye umri wa miaka 130. Alipojua kwamba Yakobo (au Israeli) alikuwa anakaribia, ‘Yosefu alitayarisha gari lake, akaenda kumpokea babake Israeli huko Gosheni. Alipomtokea, alimwangukia shingoni mara moja, akalia shingoni pake tena na tena.’ (Mwanzo 46:28, 29) Makaribisho hayo hayakuwa wonyesho wa heshima wa kidesturi tu. Yosefu alimpenda sana babake mzee na hakuaibika kumwonyesha upendo. Ikiwa tuna wazazi wazee, je, sisi pia huwaonyesha upendo mwingi?

      7. Kwa nini Yakobo alitaka akazikwe Kanaani?

      7 Yakobo aliendelea kujitoa kwa Yehova hadi kifo chake. (Waebrania 11:21) Kwa kuwa aliamini ahadi za Mungu, Yakobo aliomba mwili wake ukazikwe Kanaani. Yosefu alimheshimu babake kwa kukubali ombi lake licha ya gharama na jitihada kubwa zilizohusika.—Mwanzo 47:29-31; 50:7-14.

      8. (a) Ni nini hasa hutuchochea kuwatunza wazazi wetu wazee? (b) Mtumishi mmoja wa wakati wote alifanya nini ili kuwatunza wazazi wake wazee? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 17.)

      8 Ni nini kilichomchochea Yosefu amtunze babake? Ni tamaa yake kubwa ya kumpendeza Yehova na pia upendo na hisia kwamba alikuwa na deni kwa babake kwa sababu ya kumzaa na kumlea. Tunapaswa kuwa na tamaa hiyohiyo. Paulo aliandika: “Ikiwa mjane yeyote ana watoto au wajukuu, acha hao wajifunze kwanza kuzoea ujitoaji-kimungu nyumbani kwao wenyewe na kuendelea kuwalipa wazazi na wazazi wa wazazi wao malipo yanayowastahili, kwa maana hilo linakubalika machoni pa Mungu.” (1 Timotheo 5:4) Naam, kumpenda Yehova na woga wenye heshima kwake utatuchochea kuwatunza wazazi wetu wazee, bila kujali magumu yanayohusika katika kufanya hivyo.a

  • Ni Daraka la Kikristo Kuwatunza Walio Wazee
    Mnara wa Mlinzi—2004 | Mei 15
    • [Sanduku katika ukurasa wa 17]

      Wazazi Wake Walipohitaji Msaada

      Philip alikuwa mjenzi wa kujitolea huko Liberia mwaka wa 1999 wakati alipopata habari kwamba babake alikuwa mgonjwa sana. Akiwa na uhakika kwamba mamake hangeweza kushughulikia hali hiyo akiwa peke yake, aliamua kurudi nyumbani ili kufanya mipango ya matibabu kwa ajili ya babake.

      “Haikuwa rahisi kurudi nyumbani,” akumbuka Philip, “lakini nilihisi kwamba daraka langu la kwanza ni kwa wazazi wangu.” Katika miaka mitatu iliyofuata, aliwahamisha wazazi wake kwenda katika nyumba nzuri zaidi na kwa msaada wa Wakristo wenzake, alirekebisha nyumba hiyo ili ifae kwa mahitaji ya pekee ya babake.

      Sasa mama ya Philip anaweza kukabiliana ifaavyo na matatizo mabaya ya afya ya babake. Hivi karibuni, Philip alikubali mwaliko wa kuwa mfanyakazi wa kujitolea katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Makedonia.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki