-
Imani Yako Katika Ufufuo Ni Yenye Nguvu Kadiri Gani?Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
-
-
Mwili na Nafsi
18. Wanafalsafa fulani Wagiriki waliitikiaje taarifa ya Paulo ya kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa, na kwa nini?
18 Alipokuwa Athene, mtume Paulo alihubiri habari njema kwa umati uliotia ndani wanafalsafa Wagiriki. Walisikiliza mazungumzo hayo kuhusu Mungu mmoja wa kweli na mwito wake wa toba. Lakini ni nini kilichotukia baadaye? Paulo alimalizia hotuba yake kwa kusema hivi: “[Mungu] ameweka siku ambayo katika hiyo akusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kwa njia ya mwanamume ambaye ameweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.” Maneno hayo yalitokeza mvurugo. “Waliposikia juu ya ufufuo wa wafu, wengine wao wakaanza kudhihaki.” (Matendo 17:22-32) Mwanatheolojia Oscar Cullmann asema hivi: “Kwa Wagiriki walioamini kwamba nafsi haiwezi kufa, huenda lilikuwa jambo gumu zaidi kwao kukubali yale Wakristo waliyohubiri kuhusu ufufuo kuliko ilivyokuwa kwa wengine. . . . Fundisho la Socrates na Plato, waliokuwa wanafalsafa wakuu, haliwezi kwa vyovyote kupatanishwa [kukubaliana] na fundisho la Agano Jipya.”
19. Wanatheolojia wa Jumuiya ya Wakristo walijaribu kupatanishaje fundisho la ufufuo na fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa?
19 Ijapokuwa hivyo, kufuatia uasi mkubwa baada ya kifo cha mitume, wanatheolojia walijitahidi kuunganisha fundisho la Wakristo juu ya ufufuo, na imani ya Plato katika nafsi isiyoweza kufa. Baada ya muda, baadhi yao walikubaliana juu ya utatuzi huu mpya: Wakati wa kufa, nafsi hutenganishwa (“huwekwa huru,” kama vile wengine husema) na mwili. Kisha kulingana na kichapo Outlines of the Doctrine of the Resurrection, cha R. J. Cooke, Siku ya Hukumu “kila mwili utaunganishwa tena na nafsi yake wenyewe, na kila nafsi na mwili wake yenyewe.” Kuunganishwa wakati ujao kwa mwili na nafsi yake isiyoweza kufa, kwasemekana kuwa ndio ufufuo.
20, 21. Ni nani ambao wamefundisha kweli kuhusu ufufuo kwa upatano, na hilo limewanufaishaje?
20 Nadharia hiyo bado ni fundisho rasmi la makanisa mashuhuri. Ingawa dhana hiyo yaweza kuonekana kuwa jambo la akili kwa mwanatheolojia, waenda-kanisani wengi hawaifahamu. Wao huamini tu kwamba wataenda mbinguni moja kwa moja watakapokufa. Kwa sababu hiyo, katika makala ya Mei 5, 1995, ya Commonweal, mwandishi John Garvey alidai kwamba: “Imani ya Wakristo walio wengi [kuhusu uhai baada ya kifo] yaonekana yakaribiana zaidi na ile imani ya Uplato mpya kuliko inavyokaribiana na imani yoyote ambayo kwa kweli ni ya Kikristo, na haina msingi wowote wa Biblia.” Kwa kweli, kwa kubadilisha Biblia na imani ya Plato, makasisi wa Jumuiya ya Wakristo walifuta tumaini la Biblia la ufufuo kwa makundi yao.
-
-
Imani Yako Katika Ufufuo Ni Yenye Nguvu Kadiri Gani?Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
-
-
12. Jumuiya ya Wakristo ilipata wapi fundisho lake kuhusu nafsi isiyoweza kufa?
12 Kwa nini Jumuiya ya Wakristo hufundisha mambo tofauti na yale Biblia husema? Kichapo New Catholic Encyclopedia, katika makala yake ya “Kutoweza Kufa kwa Nafsi na kwa Binadamu,” chasema kwamba Waandishi wa Kanisa walitegemeza imani yao juu ya nafsi isiyoweza kufa, katika “washairi na wanafalsafa na dhana ya kimapokeo ya Kigiriki wala si katika Biblia . . . Baadaye, wasomi walipendelea kutumia imani ya Plato au kanuni za Aristotle.” Kichapo hicho chataarifu kwamba “uvutano wa dhana ya Uplato na Uplato mpya”—kutia na imani katika nafsi isiyoweza kufa—hatimaye ziliingizwa “katika mambo ya msingi ya theolojia ya Kikristo.”
13, 14. Kwa nini si jambo la akili kutumaini kuelimishwa na wanafalsafa wapagani Wagiriki?
13 Je, wanaodai kuwa Wakristo wangalipaswa kugeukia wanafalsafa wapagani Wagiriki kujifunza jambo la msingi kama vile tumaini la uhai baada ya kifo? Bila shaka la. Paulo alipowaandikia Wakristo walioishi Korintho, Ugiriki, alisema hivi: “Hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu kwa Mungu; kwa maana imeandikwa: ‘Yeye hunasa wenye hekima katika ujanja wao wenyewe.’ Na tena: ‘Yehova ajua kwamba mawazowazo ya watu wenye hekima ni ya ubatili.’” (1 Wakorintho 3:19, 20) Wagiriki wa kale walikuwa waabudu-sanamu. Hivyo basi, wangeweza kuwaje chanzo cha ile kweli? Paulo aliwauliza Wakorintho hivi: “Hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu? Kwa maana sisi ni hekalu la Mungu aliye hai; kama vile Mungu alivyosema: ‘Mimi nitakaa miongoni mwao na kutembea miongoni mwao, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.’”—2 Wakorintho 6:16.
14 Ufunuo wa kupata kweli takatifu ulitolewa mara ya kwanza kupitia taifa la Israeli. (Waroma 3:1, 2) Baada ya mwaka wa 33 W.K., ulitolewa kupitia kutaniko la Kikristo la watiwa-mafuta la karne ya kwanza. Akizungumza kuhusu Wakristo wa karne ya kwanza, Paulo alisema hivi: “Ni kwetu sisi Mungu ameyafunua [mambo yaliyotayarishwa kwa ajili ya wale wampendao] kupitia roho yake.” (1 Wakorintho 2:10; ona pia Ufunuo 1:1, 2.) Fundisho la Jumuiya ya Wakristo juu ya kutokufa kwa nafsi limetolewa katika falsafa za Kigiriki. Haikufunuliwa kupitia ufunuo mbalimbali wa Mungu kwa Waisraeli au kupitia kutaniko la karne ya kwanza la Wakristo watiwa-mafuta.
-