-
Kwa Nini Namba Zinavutia?Amkeni!—2002 | Septemba 8
-
-
Wabashiri wanaotumia namba siku hizi wanatumia mbinu hiyohiyo. Mara nyingi, wao huanza na jina lako na tarehe uliyozaliwa. Namba fulani huambatanishwa na kila herufi ya jina lako. Mbashiri huongeza namba hizo na namba za mwezi na za tarehe uliyozaliwa ili kupata namba zako kuu. Kisha anatoa fasiri ya pekee ya namba hizo ambazo anadhani zinaeleza kila jambo kukuhusu—kutia ndani utu wako, mambo unayotamani, na mambo yatakayokupata wakati ujao.
-
-
Je, Inafaa Kutafuta Mwongozo Katika Namba?Amkeni!—2002 | Septemba 8
-
-
Je, Inafaa Kutafuta Mwongozo Katika Namba?
JE, KUBASHIRI kwa kutumia namba kunapatana na akili na sayansi? Je, namba zinaweza kufunua wakati wetu ujao? Je, inafaa kupanga maisha yako ya baadaye kwa kutegemea mafumbo na ubashiri wa namba?
Wabashiri wengi wanaotumia namba wametatizwa na kipingamizi kimoja. Kipingamizi hicho ni kwamba tamaduni mbalimbali zinatumia kalenda tofauti. Kwa mfano, vipi ikiwa mtu anaishi nchi inayotumia kalenda ya Kichina? Fikiria tarehe ile iliyotajwa kwenye makala ya kwanza—Septemba 11, 2001. Kulingana na kalenda ya Kichina, tarehe hiyo ilikuwa siku ya 24 ya mwezi wa saba, mwaka wa 18 wa mzunguko wa 78. Kalenda ya Julian inaonyesha tarehe hiyo ni Agosti 29, 2001. Kulingana na kalenda ya Waislamu, ilikuwa tarehe 22 Jumada II 1422, na kwenye kalenda ya Waebrania ilikuwa 23 Eluli 5761. Tarehe inayoandikwa kwa njia nyingi hivyo inawezaje kuwa na ujumbe muhimu? Jambo jingine ni hili: Mara nyingi majina huandikwa kwa njia maalumu katika lugha mbalimbali. Kwa mfano, herufi zilizo katika jina la Kiingereza John zinawakilishwa na namba 2, lakini herufi za jina hilohilo katika Kihispania—Juan—zinawakilishwa na namba 1.
Ingawa vitu vingi katika ulimwengu vinategemea fomyula za hesabu, fomyula hizo zinaweza kujaribiwa na kuthibitishwa. Lakini kudai kwamba jina lako lilichaguliwa kimbele lifaane na tarehe yako ya kuzaliwa na kwamba lingeweza kuambatanishwa na namba fulani ili ujue wakati wako ujao ni jambo tofauti kabisa.
Mkataa ni wazi: Si jambo la kiakili kuamini kwamba kubashiri kwa kutumia namba ni sahihi kwa kuwa kunategemea mambo mbalimbali yanayotofautiana sana kama vile kalenda na lugha.
“Wakati na Tukio Lisilotazamiwa”
Baadhi ya watu huvutiwa na ubashiri huo kwa sababu wana hamu ya kujua mambo yao ya wakati ujao. Hata hivyo, Biblia inasema waziwazi kwamba maisha ya mwanadamu hayawezi kupangwa kimbele. Tunasoma hivi: “Si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati [“tukio lisilotazamiwa,” “NW”] huwapata wote.” (Mhubiri 9:11, italiki ni zetu.) Naam, mambo mengi hutukia ghafula. Hatuwezi kamwe kubashiri mambo kulingana na tarehe ya kuzaliwa au namba zinazowakilisha jina kwa sababu ya matukio hayo ya ghafula.
Fikiria mfano mwingine: Biblia inatutia moyo tuwe wakarimu inaposema hivi: “Tupa chakula chako usoni pa maji; maana utakiona baada ya siku nyingi. Uwagawie sehemu watu saba, hata wanane; maana hujui baa gani litakalokuwa juu ya nchi.” (Mhubiri 11:1, 2, italiki ni zetu.) Mara nyingi, misiba hutukia ghafula na watu hawawezi kujua ni lini itakapotokea. Kwa hiyo, profesa wa hesabu Underwood Dudley anaandika hivi kuhusu wabashiri wanaotumia namba: “Wanapuuza kabisa uwezekano wa mambo kutukia ghafula. Mambo yenye kustaajabisha yanaweza kutukia ghafula tu bila mpango wowote.”
Ni kweli kwamba huenda wabashiri hao wakatabiri mambo fulani na yakatokea. Kwa nini? Nyakati nyingine, mambo hayo yanaweza kutukia kwa usahihi bila kutarajiwa. Nyakati nyingine, wabashiri hao wanaweza kutabiri mambo mengi ambayo yanaweza kuhusiana na matukio kadhaa. Lakini kuna jambo jingine zito sana ambalo linahitaji kufikiriwa.
Je, Ni Namna Fulani ya Uaguzi?
Biblia haitaji moja kwa moja ubashiri wa kutumia namba. Lakini inamtaja Hamani, Mwamaleki ambaye alipanga njama ya kuwaangamiza Wayahudi walioishi Uajemi katika karne ya tano K.W.K. Biblia yasema hivi: “Hamani aliagiza kura (yaani Purimu) ifanywe kupata siku na mwezi ambapo angetekeleza njama zake. Basi, kura ikaangukia siku ya kumi na nne ya mwezi wa kumi na mbili uitwao Adari.”—Esta 3:7, Biblia Habari Njema, italiki ni zetu.
Katika nyakati za kale, kupiga kura kulikuwa njia halali ya kukomesha ubishi.a (Mithali 18:18) Lakini Hamani alitumia kura kufanya uaguzi—zoea ambalo linashutumiwa na Biblia. Andiko la Kumbukumbu la Torati 18:10-12, BHN, lasema kwamba Mungu anamchukia kabisa ‘mtu apigaye ramli, mwaguzi, mpiga bao, mchawi, mlozi, mwenye kutaka kauli kwa mizimu na pepo. Yeyote atendaye mambo haya ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu.’
Biblia inaonyesha kwamba uaguzi na nguvu za kiajabu zinahusiana na kuwasiliana na roho waovu. Roho waovu wanaweza kutumia matukio fulani ili kutimiza makusudi yao. Lolote liwalo, jambo moja ni hakika: Mungu anashutumu zoea la kuwasiliana na roho waovu, na kufanya hivyo kunaweza kumfanya mtu awe mtumwa wa roho waovu.—1 Samweli 15:23; Waefeso 6:12.
Kubashiri kwa kutumia namba hakupatani kabisa na sayansi, wala si jambo la kiakili. Na jambo baya zaidi ni kwamba ubashiri huo ni namna fulani ya uaguzi na hivyo ni kinyume cha mafundisho ya Biblia. Kwa hiyo, kubashiri kwa kutumia namba si njia inayofaa ya kupangia maisha yako au miradi yako.
-
-
Mwongozo Unaotegemeka kwa Ajili ya Wakati UjaoAmkeni!—2002 | Septemba 8
-
-
Mwongozo Unaotegemeka kwa Ajili ya Wakati Ujao
JE, KUTOTEGEMEKA kwa ubashiri wa kutumia namba na aina nyinginezo za uaguzi kunamaanisha kwamba hatuwezi kamwe kujua mambo ya wakati ujao? La hasha!
Wanadamu hawawezi kujua mambo ya wakati ujao kupitia namba. Lakini “Mungu aliye hai,” ambaye anatangaza “mwisho tangu mwanzo” amewajulisha mambo ya wakati ujao. Naye huwajulisha kupitia Neno lake, Biblia. (1 Timotheo 4:10; Isaya 46:10) Isitoshe, neno la Mungu aliye hai ‘linaweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo’ na hivyo kukusaidia kujua nia yako na mambo yanayoweza kukufanya ufanikiwe, lakini neno la wabashiri wanaotumia namba haliwezi kufanya hivyo.—Waebrania 4:12.
Muumba wetu, ambaye ni Mtungaji wa Biblia, ndiye tu anayeweza kutabiri kwa usahihi mambo ya wakati ujao. Mungu ana nguvu zisizo na kifani, naye hutumainika sikuzote. Yehova Mungu alisema hivi: “Nimenena, nami nitafanya.” (Isaya 46:11) Baada ya kuwaongoza Waisraeli kuingia Nchi ya Ahadi, Yoshua alisema hivi kwa uhakika: “Halikuanguka neno lo lote katika jambo lo lote lililokuwa ni jema ambalo BWANA alikuwa amelinena katika habari ya nyumba ya Israeli; yalitimia mambo yote.”—Yoshua 21:45; 23:14.
Biblia ina unabii mwingi ambao haujatimizwa. Baadhi ya unabii huo unatabiri kwamba uovu utaondolewa kabisa ili dunia iwe paradiso. (Zaburi 37:10, 11; Mithali 2:21, 22) Je, unavutiwa na wakati ujao wa aina hiyo? Je, unaamini kwamba Muumba wetu ana hekima na nguvu za kuboresha hali duniani? Ikiwa ndivyo, utafurahia kujua yale ambayo Biblia inasema kuhusu hali ya wakati ujao ya dunia.a
Kwa hiyo, badala ya kutafuta habari zako za wakati ujao katika namba, tumia wakati wako kwa hekima sasa kwa kujitahidi kupata ujuzi sahihi wa Biblia na unabii uliomo.
-