-
Ninawezaje Kujilinda na Washambuliaji wa Kingono?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
-
-
Kupambana na Hisia za Hatia
Mpaka sasa Annette anapambana na hisia za hatia kuhusu mambo yaliyompata. “Najiona kuwa adui yangu mwenyewe,” anasema. “Naufikiria usiku huo tena na tena. Nahisi nilipaswa kujaribu zaidi kumzuia mtu huyo. Ukweli ni kwamba, baada ya kudungwa kisu, niliogopa sana. Sikuweza kufanya lolote, lakini nahisi kwamba nilipaswa kufanya jambo fulani.”
Natalie pia anapambana na hisia za hatia. Anasema: “Sikupaswa kumwamini mtu yeyote. Wazazi wetu walituamuru mimi na dada yangu tuwe tukicheza pamoja, lakini sikutii. Kwa hiyo, nahisi kwamba nilimpa jirani yangu nafasi ya kuniumiza. Mambo yaliyonipata yaliumiza familia yetu, nami najilaumu kwa kuwasababishia uchungu mwingi. Hilo linaniumiza hata zaidi.”
Unaweza kupambana jinsi gani na hatia ikiwa hisia zako ni kama za Annette au Natalie? Kwanza, kumbuka kwamba ikiwa ulilalwa kinguvu, hukutaka kufanya hivyo. Watu fulani hupunguza uzito wa kosa hilo kwa kusema kwamba ni kawaida kwa wanaume kufanya hivyo na kwamba wanaolalwa kinguvu ndio wenye kulaumiwa. Hata hivyo, hakuna mtu anayepaswa kulalwa kinguvu. Ikiwa ulitendewa uovu huo, huwezi kulaumiwa!
Ni kweli kwamba ni rahisi kusoma taarifa inayosema “huwezi kulaumiwa,” lakini si rahisi kuiamini. Wengine hawasemi kuhusu mambo yaliyotokea nao wanaumia kutokana na hisia za hatia, na hisia nyingine mbaya. Hata hivyo, kukaa kimya kunamsaidia nani—wewe au mshambuliaji wako? Unahitaji kuchukua hatua nyingine.
Sema Yaliyokupata
Biblia inasema kwamba Ayubu, yule mwanamume mwadilifu, akiwa amechanganyikiwa sana alisema: “Nitaonyesha hangaiko langu kujihusu mwenyewe. Nitasema kwa uchungu wa nafsi yangu!” (Ayubu 10:1) Utafaidika kwa kufanya hivyo pia. Kuzungumza na mtu ambaye unamtumaini kuhusu mambo yaliyokupata kunaweza kukusaidia kupambana na hali hiyo na kupata kitulizo kutokana na hisia zako zenye kuumiza.
Ikiwa wewe ni Mkristo, ni muhimu kuzungumza na mzee wa kutaniko kuhusu mambo yaliyokupata. Maneno yenye kufariji ya mchungaji mwenye upendo yatakuhakikishia kwamba kwa kulalwa kinguvu hutaonwa kuwa mchafu kutokana na dhambi ya mtu mwingine. Hivyo ndivyo Annette alivyotambua. Anasema: “Nilizungumza na rafiki yangu wa karibu, naye akanihimiza nizungumze na wazee wawili Wakristo katika kutaniko letu. Nafurahi nilifanya hivyo. Walizungumza nami mara kadhaa na kuniambia kwamba yaliyotokea hayakuwa makosa yangu. Sikufanya kosa lolote.”
Kuzungumza kuhusu mambo yaliyotokea na kueleza hisia zako kunaweza kukusaidia usilemewe na hasira na kinyongo. (Zaburi 37:8) Huenda pia kukakusaidia kupata kitulizo, labda kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi. Natalie aliona ukweli wa maneno hayo baada ya kuwaambia wazazi wake kuhusu jinsi alivyotendewa vibaya. Anasema: “Walinisaidia. Walinitia moyo kuzungumza, na hilo likanisaidia kutohuzunika sana na kuwa na hasira nyingi.” Pia, Natalie alipata faraja kwa kusali. Anasema: “Kuzungumza na Mungu kulinisaidia hasa nyakati ambazo niliona kwamba siwezi kuzungumza na mwanadamu. Ninaweza kuzungumza kwa uhuru ninaposali. Kufanya hivyo kunanipa amani ya kweli na utulivu.”e
Huenda wewe pia ukatambua kwamba kuna ‘wakati wa kupona.’ (Mhubiri 3:3) Tegemea marafiki wanaoweza kukusaidia ambao ni kama wazee Wakristo wanaofafanuliwa kuwa sawa na “mahali pa kujificha kutokana na upepo na mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua.” (Isaya 32:2) Jitunze kimwili na kihisia. Pumzika vya kutosha. Na zaidi ya yote, mtegemee Mungu wa faraja yote, Yehova, ambaye karibuni ataleta ulimwengu mpya ambamo “watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia.”—Zaburi 37:9.
-
-
Ninawezaje Kujilinda na Washambuliaji wa Kingono?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
-
-
e Nyakati nyingine watu ambao wametendewa vibaya wanashuka moyo sana. Katika hali kama hizo, huenda ikafaa kumwona daktari. Pata habari zaidi kuhusu jinsi ya kukabiliana na hisia zenye kuumiza katika Sura ya 13 na 14 ya kitabu hiki.
-