Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jitoe Mwenyewe kwa Usomaji
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Mei 15
    • Jitoe Mwenyewe kwa Usomaji

      “Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha.”—1 TIMOTHEO 4:13.

      1. Tunaweza kupataje manufaa kutokana na kusoma Biblia?

      YEHOVA MUNGU amewapa wanadamu uwezo wa ajabu wa kujifunza kusoma na kuandika. Pia ameandaa Neno lake, Biblia, ili tuweze kufundishwa vizuri. (Isaya 30:20, 21) Kitamathali, kurasa zayo hutusaidia “kutembea” pamoja na wazee wa ukoo wenye kumhofu Mungu kama Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Twaweza “kuona” wanawake wa kimungu kama Sara, Rebeka, na Ruthu Mmoabi aliyekuwa mwaminifu-mshikamanifu. Ndiyo, nasi twaweza “kusikia” Yesu Kristo akitoa Mahubiri ya Mlimani. Twaweza kupata raha hiyo yote na mafundisho matukufu kutoka kwa Maandiko Matakatifu ikiwa sisi ni wasomaji wazuri.

      2. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu na mitume wake waliweza kusoma vizuri?

      2 Bila shaka, mtu mkamilifu Yesu Kristo alikuwa na uwezo bora wa kusoma, na hakika yeye alijua Maandiko ya Kiebrania vizuri sana. Basi, aliposhawishiwa na Ibilisi, Yesu aliyarejezea kwa kurudia-rudia akisema, “Imeandikwa.” (Mathayo 4:4, 7, 10) Pindi moja katika sinagogi huko Nazareti, yeye alisoma mbele ya watu wote na kuhusisha sehemu ya unabii wa Isaya kwake mwenyewe. (Luka 4:16-21) Vipi juu ya mitume wa Yesu? Katika maandishi yao, mara nyingi walinukuu Maandiko ya Kiebrania. Ingawa watawala wa Wayahudi waliwaona Petro na Yohana kuwa wasio na elimu na watu wa kawaida tu kwa sababu hawakuelimishwa katika shule za Kiebrania za masomo ya juu, barua zao zilizopuliziwa kimungu kwa wazi zilithibitisha kwamba wao waliweza kusoma na kuandika vema. (Matendo 4:13) Lakini, je, kweli uwezo wa kusoma ni muhimu?

      “Mwenye Furaha Ni Yeye Asomaye kwa Sauti Kubwa”

      3. Kwa nini ni muhimu sana kusoma Maandiko na vichapo vya Kikristo?

      3 Kutwaa na kutumia ujuzi sahihi wa Maandiko kwaweza kutokeza uhai wa milele. (Yohana 17:3) Basi Mashahidi wa Yehova hutambua kwamba ni muhimu sana kusoma na kujifunza Maandiko Matakatifu na vichapo vya Kikristo vinavyoandaliwa na Mungu kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili ya Wakristo watiwa-mafuta. (Mathayo 24:45-47) Kwa hakika, kwa kutumia vichapo vya Watch Tower vilivyotayarishwa kipekee, maelfu ya watu wamefundishwa kusoma na hivyo kupokea ujuzi wa Neno la Mungu wenye kuleta uhai.

      4. (a) Kwa nini kusoma, kujifunza, na kutumia Neno la Mungu hutokeza furaha? (b) Kwa habari ya usomaji, Paulo alimwambia Timotheo nini?

      4 Furaha hutokana na kusoma, kujifunza, na kutumia Neno la Mungu. Ndivyo ilivyo kwa sababu kwa kufanya hivyo sisi humfurahisha na kumheshimu Mungu, hupokea baraka yake, na kupata shangwe. Yehova hutaka watumishi wake wawe na furaha. Hivyo, yeye aliwaamuru makuhani wasome Sheria yake kwa watu wa Israeli la kale. (Kumbukumbu la Torati 31:9-12) Mnakili Ezra na wengine waliposoma Sheria mbele ya watu waliokusanyika Yerusalemu, maana yayo ilidhihirishwa, na tokeo likawa “furaha nyingi.” (Nehemia 8:6-8, 12) Mtume Mkristo, Paulo, baadaye alimwambia mfanyakazi mwenzake Timotheo: “Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha.” (1 Timotheo 4:13) Tafsiri nyingine husema: “Jitoe mwenyewe kwa usomaji wa Maandiko mbele ya watu wote.”—New International Version.

      5. Ufunuo 1:3 huunganishaje furaha pamoja na usomaji?

      5 Jambo la kwamba furaha yetu hutegemea kusoma na kutumia Neno la Mungu ladhihirishwa kwenye Ufunuo 1:3. Hapo twaambiwa hivi: “Heri asomaye [“Mwenye furaha ni yeye asomaye kwa sauti kubwa,” NW] na wao wayasikiao maneno ya unabii huu, na kuyashika yaliyoandikwa humo; kwa maana wakati u karibu.” Ndiyo, twahitaji kusoma kwa sauti kubwa na kusikia maneno ya Mungu ya kiunabii katika Ufunuo na katika Maandiko yote. Mtu ambaye kwa kweli ni mwenye furaha ni yule ambaye “sheria ya BWANA ndiyo impendezayo, na sheria yake huitafakari mchana na usiku.” Tokeo ni nini? “Kila alitendalo litafanikiwa.” (Zaburi 1:1-3) Basi, kwa sababu nzuri, tengenezo la Yehova huhimiza kila mmoja wetu kusoma na kujifunza Neno lake akiwa peke yake, wakiwa familia, na pamoja na marafiki.

      Fikiri kwa Bidii na Utafakari

      6. Yoshua aliagizwa asome nini, na kufanya hivyo kulikuwaje na manufaa?

      6 Unaweza kufaidikaje zaidi na usomaji wako wa Neno la Mungu na vichapo vya Kikristo? Yaelekea utapata kuwa ni jambo lenye manufaa kufanya yale aliyofanya Yoshua, kiongozi wa Israeli la kale aliyemhofu Mungu. Yeye aliamriwa: “Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari [“uyasome kwa sauti ya chini,” NW] maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana.” (Yoshua 1:8) ‘Kusoma kwa sauti ya chini’ kwamaanisha kujisemea mwenyewe maneno kwa sauti ya chini. Huko ni msaada wa kukumbuka, kwa kuwa kunakazia habari akilini. Yoshua alipaswa kusoma Sheria ya Mungu “mchana na usiku,” au kwa ukawaida. Kulikuwa ndiko njia ya kufanikiwa na kutenda kwa hekima katika kutekeleza madaraka aliyopewa na Mungu. Kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida hivyo kwaweza kukusaidia kwa njia iyo hiyo.

      7. Kwa nini hatupaswi kukazia akili kusoma kwa kasi tusomapo Neno la Mungu?

      7 Usikazie akili kusoma kwa kasi unaposoma Neno la Mungu. Ikiwa ulipanga kutumia wakati fulani kusoma Biblia au kichapo fulani cha Kikristo, soma kwa mwendo wa pole. Hili ni la maana sana unapojifunza ukiwa na lengo la kukumbuka mambo makuu. Unaposoma, fikiri kwa bidii. Changanua taarifa za mwandikaji wa Biblia. Jiulize, ‘Anakazia nini? Naweza kutumiaje habari hii?’

      8. Kwa nini kuna manufaa kutafakari tunaposoma Maandiko?

      8 Chukua wakati wa kutafakari unaposoma Maandiko Matakatifu. Kufanya hivyo kutakusaidia kukumbuka masimulizi ya Biblia na kutumia kanuni za Kimaandiko. Kutafakari Neno la Mungu na kwa kufanya hivyo ukikazia mambo makuu akilini pia kutakusaidia kusema kutoka moyoni, ukiwapa wauliza-maswali wanyoofu majibu sahihi badala ya kusema jambo ambalo huenda ukaghairi baadaye. Mithali moja iliyopuliziwa kimungu husema: “Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu.”—Mithali 15:28.

      Shirikisha Mambo Mapya na Yale ya Zamani

      9, 10. Usomaji wako wa Biblia waweza kuboreshwaje kwa kushirikisha mambo mapya ya Kimaandiko pamoja na yale ambayo tayari unayajua?

      9 Wakristo walio wengi ni lazima wakiri kwamba pindi moja walijua machache juu ya Mungu, Neno lake, na makusudi yake. Hata hivyo, leo wahudumu hao Wakristo, kuanzia uumbaji wa mwanadamu na kutumbukia kwake katika dhambi, waweza kueleza kusudi la dhabihu ya Kristo, waweza kueleza uharibifu wa mfumo huu mwovu wa mambo, nao waweza kuonyesha jinsi wanadamu watiifu watakavyobarikiwa kwa uhai wa milele katika dunia iliyo paradiso. Hilo lawezekana hasa kwa sababu watumishi hao wa Yehova wametwaa “ujuzi wenyewe wa Mungu” kwa kujifunza Biblia na vichapo vya Kikristo. (Mithali 2:1-5, NW) Polepole wao wameshirikisha mambo mapya waliyojifunza pamoja na ya zamani ambayo tayari walikuwa wameyaelewa.

      10 Kushirikisha mambo mapya ya Kimaandiko pamoja na yale ambayo tayari unayajua ni kwenye manufaa nako huthawabisha. (Isaya 48:17) Wakati sheria za Biblia, kanuni, au hata mawazo fulani yasiyo wazi sana yanapotokezwa, uyashirikishe pamoja na yale ambayo tayari unayajua. Patanisha habari hiyo na yale ambayo tayari umejifunza kuhusu “kielelezo cha maneno yenye uzima.” (2 Timotheo 1:13) Tafuta habari ambayo inaweza kukusaidia kuimarisha uhusiano wako na Mungu, kuboresha utu wako wa Kikristo, au kukusaidia kushiriki kweli za Biblia na wengine.

      11. Unaweza kufanya nini unaposoma jambo ambalo Biblia husema juu ya mwenendo? Toa kielezi.

      11 Unaposoma jambo fulani ambalo Biblia husema juu ya mwenendo, jaribu kufahamu kanuni ihusikayo. Litafakari, na uamue lile ungefanya chini ya hali kama hizo. Mwana wa Yakobo, Yosefu, sikuzote alikataa kujiingiza katika ukosefu wa adili pamoja na mke wa Potifa, akiuliza: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?” (Mwanzo 39:7-9) Katika simulizi hili lenye kugusa moyo, unapata kanuni ya msingi—ukosefu wa adili ni dhambi dhidi ya Mungu. Unaweza kushirikisha kanuni hii akilini pamoja na taarifa nyinginezo zilizomo katika Neno la Mungu, nawe unaweza kuikumbuka na kunufaika nayo ukishawishiwa kujiingiza katika kosa kama hilo.—1 Wakorintho 6:9-11.

      Piga Picha Akilini Matukio ya Kimaandiko

      12. Kwa nini upige picha akilini masimulizi ya Biblia unapoyasoma?

      12 Ili kukazia mambo akilini mwako unaposoma, piga picha akilini kile kinachotukia. Ona akilini mandhari, makao, na watu. Sikia sauti zao. Nusa mkate unaookwa katika tanuu. Wazia mandhari hizo tena. Ndipo usomaji wako utakapokuwa ono lenye kugusa moyo, kwa kuwa unaweza kuona jiji fulani la kale, kukwea mlima wenye kimo cha juu, kustaajabia maajabu ya uumbaji, au kushirikiana na wanaume na wanawake wenye imani kubwa.

      13. Unaweza kufafanuaje yale yaliyorekodiwa kwenye Waamuzi 7:19-22?

      13 Tuseme unasoma Waamuzi 7:19-22. Piga picha akilini kile kinachotukia. Mwamuzi Gideoni na wanaume mashujaa mia tatu wa Israeli wametwaa mahali pao ukingoni mwa kambi ya Wamidiani. Ni karibu saa nne za usiku, mwanzo wa “zamu ya kati.” Walinzi wa Wamidiani walikuwa wameanza tu kushika zamu, nalo giza lafunika kambi ya maadui wa Israeli wanaolala usingizi. Tazama! Gideoni na wanaume wake wana mabaragumu. Wao wana mitungi mikubwa inayofunika mienge wanayobeba katika mikono yao ya kushoto. Kwa ghafula, vikosi vitatu vya watu mia moja kila kimoja vyapiga mabaragumu, vyavunja mitungi, vyainua mienge juu, na kusema kwa sauti kuu: “Upanga wa BWANA na wa Gideoni.” Unatazama kambi. Wamidiani wote watoroka na kuanza kupiga makelele! Wale mia tatu waendeleapo kupiga mabaragumu yao, Mungu afanya panga za Wamidiani ziwe dhidi yao wenyewe kwa wenyewe. Wamidiani wametoroka, na Yehova amepatia Israeli ushindi.

      Kujifunza Masomo Yenye Thamani

      14. Waamuzi sura ya 9 yaweza kutumiwaje kufundisha mtoto uhitaji wa kuwa mnyenyekevu?

      14 Kwa kusoma Neno la Mungu, twaweza kujifunza masomo mengi. Kwa kielelezo, labda unataka kukazia watoto wako uhitaji wa kuwa wanyenyekevu. Inapasa kuwa rahisi kupiga picha akilini na kuelewa kile kilichosemwa katika unabii wa Yothamu mwana wa Gideoni. Anza kusoma kwenye Waamuzi 9:8. “Siku moja,” akasema Yothamu, “miti ilitoka ili kuutia mmoja mafuta uwe mfalme juu yao.” Mzeituni, mtini, na mzabibu ikakataa kutawala. Lakini mti wa miiba wa hali ya chini ulifurahi kuwa mtawala. Baada ya kuwasomea watoto wako simulizi hilo kwa sauti kubwa, unaweza kueleza kwamba mimea yenye thamani iliwakilisha watu wenye ustahiki ambao hawakutafuta umaliki juu ya Waisraeli wenzao. Mti wa miiba, ambao ulifaa kutumiwa kama kuni tu, uliwakilisha utawala wa Abimeleki mwenye kiburi, muuaji-kimakusudi aliyetaka kudhibiti wengine lakini aliyekufa kwa utimizo wa unabii wa Yothamu. (Waamuzi, sura 9) Ni mtoto yupi angetaka kukua na kuwa kama mti wa miiba?

      15. Umuhimu wa uaminifu-mshikamanifu wakaziwaje katika kitabu cha Ruthu?

      15 Umuhimu wa uaminifu-mshikamanifu wadhihirishwa katika kitabu cha Biblia cha Ruthu. Tuseme washiriki wa familia yako wanasoma kwa zamu simulizi hilo kwa sauti kubwa na kujaribu kuelewa linalosema. Mwaona Ruthu Mmoabi akiwa safarini kwenda Bethlehemu akiwa pamoja na mama-mkwe wake aliye mjane, Naomi, nanyi mwasikia Ruthu akisema: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.” (Ruthu 1:16) Ruthu mwenye bidii aonekana akiokota masazo nyuma ya wavunaji katika shamba la Boazi. Mwamsikia Boazi akimpongeza, akisema: “Mji wote pia wa watu wangu wanakujua ya kwamba u mwanamke mwema.” (Ruthu 3:11) Upesi, Boazi amwoa Ruthu. Kwa kupatana na mpango wa ndoa ya ndugu-mkwe, kupitia Boazi Ruthu amzaa mwana “[kwa] Naomi.” Ruthu awa mzazi wa kale wa Daudi na hatimaye wa Yesu Kristo. Kwa hiyo yeye alipokea “thawabu kamili.” Na zaidi, wale wanaosoma hilo simulizi la Kimaandiko hujifunza somo muhimu: Uwe mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova, na utabarikiwa sana.—Ruthu 2:12; 4:17-22; Mithali 10:22; Mathayo 1:1, 5, 6.

      16. Wale Waebrania watatu walipitia mtihani gani, na simulizi hilo laweza kutusaidiaje?

      16 Simulizi la Waebrania walioitwa Shadraka, Meshaki, na Abednego laweza kutusaidia kuwa waaminifu kwa Mungu katika hali zenye kujaribu. Piga picha akilini tukio hilo wakati Danieli sura ya 3, inaposomwa kwa sauti kubwa. Sanamu kubwa sana ya dhahabu yasimama katika uwanda wa Dura, ambako maofisa Wababilonia walikuwa wamekusanywa. Kwa mlio wa ala za muziki, wao waanguka na kuabudu sanamu ambayo Mfalme Nebukadreza alikuwa amesimamisha. Wote ila Shadraka, Meshaki, na Abednego wafanya hivyo. Kwa staha, lakini kwa uthabiti, wao wamwambia mfalme kwamba hawatatumikia miungu yake na kuabudu ile sanamu ya dhahabu. Waebrania hao wachanga watupwa ndani ya ile tanuri iliyopashwa moto kupita kiasi. Lakini ni nini ambalo latendeka? Akitazama ndani, mfalme aona wanaume wanne wenye nguvu, mmoja wao akiwa “mfano wa mwana wa miungu.” (Danieli 3:25) Wale Waebrania watatu waondolewa kutoka ndani ya tanuri, naye Nebukadreza abariki Mungu wao. Imethawabisha kupiga picha akilini simulizi hilo. Nayo yaandaa somo lililoje kuhusu uaminifu kwa Yehova chini ya jaribu!

      Nufaikeni Kutokana na Kusoma Biblia Mkiwa Familia

      17. Taja kifupi baadhi ya mambo yenye manufaa ambayo familia yako yaweza kujifunza kwa kusoma Biblia pamoja.

      17 Familia yako yaweza kupata manufaa nyingi ikiwa mnatumia wakati kwa ukawaida kusoma Biblia pamoja. Ukianza na Mwanzo, mwaweza kushuhudia uumbaji na kuchungulia makao ya mwanadamu ya Paradiso ya awali. Mnaweza kushiriki mambo waliyoona wazee wa ukoo waaminifu na familia zao na kufuata Waisraeli wavukapo Bahari Nyekundu ikiwa imekauka. Mwaweza kuona kijana mchungaji Daudi akilishinda jitu Mfilisti Goliathi. Familia yako yaweza kuona ujenzi wa hekalu la Yehova katika Yerusalemu, yaweza kuona likifanywa ukiwa na majeshi ya Babiloni, na kuona likijengwa upya chini ya Gavana Zerubabeli. Pamoja na wachungaji wanyenyekevu karibu na Bethlehemu, mwaweza kusikia tangazo la kimalaika la kuzaliwa kwa Yesu. Mwaweza kupata mambo madogo-madogo kuhusu ubatizo na huduma ya Yesu, kumwona akitoa uhai wake wa kibinadamu ukiwa fidia, na kushiriki shangwe ya kufufuliwa kwake. Kisha mwaweza kusafiri pamoja na mtume Paulo na kutazama kuanzishwa kwa makutaniko huku Ukristo ukienea. Kisha, katika kitabu cha Ufunuo, familia yako yaweza kufurahia ono tukufu la mtume Yohana la wakati ujao, kutia ndani Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo.

      18, 19. Ni madokezo gani yanayotolewa kuhusu usomaji wa Biblia wa familia?

      18 Ikiwa mnasoma Biblia kwa sauti kubwa mkiwa familia, mwisome kwa uwazi na kwa idili. Mnaposoma sehemu fulani za Maandiko, mshiriki mmoja wa familia—labda baba—huenda akasoma maneno ya usimulizi. Wengine wenu mwaweza kuchukua sehemu za wahusika wa Biblia, mkisoma sehemu zenu kwa hisia zifaazo.

      19 Mnaposhiriki katika usomaji wa Biblia mkiwa familia, uwezo wenu wa kusoma waweza kuboreka. Yaelekea, ujuzi wenu juu ya Mungu utaongezeka, na hilo lapaswa kuwavuta karibu naye zaidi. Asafu aliimba: “Nami kumkaribia Mungu ni kwema kwangu; nimefanya kimbilio kwa Bwana MUNGU, niyahubiri matendo yako yote.” (Zaburi 73:28) Hili litasaidia familia yako kuwa kama Musa, ambaye “alistahimili kama amwonaye yeye asiyeonekana,” yaani, Yehova Mungu.—Waebrania 11:27.

      Kusoma na Huduma ya Kikristo

      20, 21. Utume wetu wa kuhubiri unahusianaje na uwezo wa kusoma?

      20 Tamaa yetu ya kumwabudu “yeye asiyeonekana” yapaswa kutusukuma kufanyia kazi kuwa wasomaji wazuri. Uwezo wa kusoma vizuri hutusaidia kutoa ushahidi kutoka kwa Neno la Mungu. Kwa hakika hutusaidia kuendelea katika kazi ya kuhubiri juu ya Ufalme ambayo Yesu aliagiza wafuasi wake kuihusu aliposema hivi: “Enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8) Kutoa ushahidi ndiyo kazi kuu ya watu wa Yehova, na uwezo wa kusoma hutusaidia kuitimiza.

      21 Jitihada inahitajika ili kuwa msomaji mzuri na mwalimu stadi wa Neno la Mungu. (Waefeso 6:17) Basi, ‘jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, ukitumia kwa halali neno la kweli.’ (2 Timotheo 2:15) Ongeza ujuzi wako wa kweli ya Kimaandiko na uwezo wako ukiwa Shahidi wa Yehova kwa kujitoa mwenyewe kwa usomaji.

  • Soma Neno la Mungu na Umtumikie Katika Kweli
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Mei 15
    • Soma Neno la Mungu na Umtumikie Katika Kweli

      “Ee BWANA, unifundishe njia yako; nitakwenda katika kweli yako.”—ZABURI 86:11.

      1. Toleo la kwanza la gazeti hili lilisema nini hasa kuhusu kweli?

      YEHOVA hutoa nuru na kweli. (Zaburi 43:3) Yeye hutupa pia uwezo wa kusoma Neno lake, Biblia, na kujifunza kweli. Toleo la kwanza la jarida hili—Julai 1879—lilisema: “Kweli, kama ua dogo kati ya mimea mingi sana, imezungukwa na hata karibu kusongwa na usitawi mwingi wa magugu ya makosa. Ili uipate ni lazima uwe macho wakati wote. Ili uone umaridadi wayo ni lazima uondoe magugu ya makosa na michongoma ya ushupavu. Ili uipate ni lazima uiname kuichukua. Usiridhike na ua moja la kweli. Kama ua moja la kweli lingalitosha kusingalikuwa na mengine. Endelea kukusanya, tafuta mengine zaidi.” Kusoma na kujifunza Neno la Mungu hutuwezesha kupata ujuzi sahihi na kutembea katika kweli yake.—Zaburi 86:11.

      2. Matokeo yalikuwa nini Ezra na wengine waliposoma Sheria ya Mungu mbele ya Wayahudi katika Yerusalemu la kale?

      2 Baada ya kuta za Yerusalemu kujengwa upya katika 455 K.W.K., kuhani Ezra na wengine waliwasomea Wayahudi Sheria ya Mungu. Hilo lilifuatwa na Msherehekeo wa Mabanda wenye shangwe, ungamo la dhambi, na kumalizia kwa “agano la hakika.” (Nehemia 8:1–9:38) Twasoma: “Nao wakasoma katika kitabu, katika torati ya Mungu, kwa sauti ya kusikilika; wakaeleza maana yake, hata wakayafahamu yaliyosomwa.” (Nehemia 8:8) Wasomi fulani hudokeza kwamba Wayahudi hawakuelewa Kiebrania vizuri na basi fasiri ilifanywa katika Kiaramu. Lakini hilo andiko halionyeshi kueleweshwa kwa lugha ya Kiebrania. Ezra na wengine walifafanua Sheria ili kwamba watu waweze kushika kanuni zayo na kuzitumia. Vichapo na mikutano ya Kikristo pia ‘hueleza maana’ ya Neno la Mungu. Ndivyo ilivyo na wazee waliowekwa rasmi, ‘wajuao kufundisha.’—1 Timotheo 3:1, 2; 2 Timotheo 2:24.

      Manufaa Zenye Kudumu

      3. Ni zipi baadhi ya manufaa zipatikanazo kutokana na usomaji wa Biblia?

      3 Familia za Kikristo zisomapo Biblia pamoja, yaelekea zitapata manufaa zenye kudumu. Hizo huja kujua sheria za Mungu na kujifunza kweli kuhusu mafundisho, mambo ya kiunabii, na mambo mengineyo. Baada ya sehemu ya Biblia kusomwa, kichwa cha familia aweza kuuliza: Hili lapasa kutuathirije? Ni katika njia gani hili lahusika na mafundisho mengine ya Biblia? Tunaweza kutumiaje mambo hayo katika kuhubiri habari njema? Familia hupata ufahamu wa ndani inaposoma Biblia ikiwa inafanya utafiti kwa kutumia Watch Tower Publications Index au faharisi nyinginezo. Mabuku mawili ya Insight on the Scriptures yaweza kurejezewa kwa manufaa.

      4. Yoshua alipaswa kutumiaje agizo lililorekodiwa kwenye Yoshua 1:8?

      4 Kanuni zitolewazo katika Maandiko zaweza kutuongoza maishani. Na zaidi, kusoma na kujifunza ‘maandiko matakatifu kwaweza kutuhekimisha hata tupate wokovu.’ (2 Timotheo 3:15) Tukiacha Neno la Mungu lituongoze, tutaendelea kutembea katika kweli yake na tamaa zetu zenye uadilifu zitatimizwa. (Zaburi 26:3; 119:130) Hata hivyo, twahitaji kutafuta uelewevu, kama alivyofanya Yoshua, aliyechukua mahali pa Musa. ‘Kitabu cha torati’ hakikupaswa kuondoka kinywani mwake, naye alipaswa kukisoma mchana na usiku. (Yoshua 1:8) Kutoacha ‘kitabu cha torati’ kiondoke kinywani mwake kulimaanisha kwamba Yoshua hakupaswa kuacha kuwaambia wengine mambo yenye kuelimisha ambayo kilisema. Kusoma Sheria mchana na usiku kulimaanisha kwamba Yoshua alipaswa kuitafakari na kujifunza. Mtume Paulo vilevile alimhimiza Timotheo ‘atafakari’ juu ya mwenendo, huduma, na ufundishaji wake. Akiwa mzee Mkristo, Timotheo alihitaji hasa kuwa mwangalifu kwamba maisha yake yalikuwa yenye kielelezo kizuri na kwamba alifundisha kweli ya Kimaandiko.—1 Timotheo 4:15.

      5. Ni nini ambacho kinahitajika ili tupate kweli ya Mungu?

      5 Kweli ya Mungu ni hazina yenye thamani kubwa sana. Kuipata kwahitaji kuchimba, kudumu katika kuchunguza Maandiko. Ni kwa kuwa tu kama watoto wenye kujifunza wa Mfunzi Mtukufu ndipo twapata hekima na kuja kuelewa hofu yenye kicho ya Yehova. (Mithali 1:7; Isaya 30:20, 21) Bila shaka, twapaswa kujithibitishia mambo Kimaandiko. (1 Petro 2:1, 2) Wayahudi katika Beroya “walikuwa waungwana kuliko wale wa Thesalonike, kwa kuwa walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo [yaliyosemwa na Paulo] ndivyo yalivyo.” Waberoya walipongezwa badala ya kushutumiwa kwa kufanya hivyo.—Matendo 17:10, 11.

      6. Kwa nini Yesu alionyesha kwamba hakukuwa na manufaa kwa Wayahudi fulani kuchunguza Maandiko?

      6 Yesu aliwaambia Wayahudi fulani: “Mwayachunguza maandiko, kwa sababu mnadhani kwamba ninyi mna uzima wa milele ndani yake; na hayo ndiyo yanayonishuhudia. Wala hamtaki kuja kwangu mpate kuwa na uzima.” (Yohana 5:39, 40) Wao walichunguza Maandiko wakiwa na lengo zuri—kwamba hayo yaweze kuwaongoza kwenye uhai. Kwa kweli, Maandiko yalikuwa na unabii mbalimbali wa Kimesiya ulioelekeza kwa Yesu kuwa njia ya kupata uhai. Lakini Wayahudi walimkataa. Basi, kuchunguza Maandiko hakukuwaletea manufaa yoyote.

      7. Ni nini ambacho kinahitajika kukua katika kuelewa Biblia, na kwa nini?

      7 Ili kukua katika kuelewa Biblia, twahitaji mwongozo wa roho ya Mungu, au kani yake ya utendaji. “Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu” ili kudhihirisha maana yayo. (1 Wakorintho 2:10, NW) Wakristo katika Thesalonike walipaswa ‘kujaribu mambo yote’ katika unabii wowote ule waliousikia. (1 Wathesalonike 5:20, 21) Paulo alipowaandikia Wathesalonike (karibu 50 W.K.), sehemu ya pekee ya Maandiko ya Kigiriki iliyokuwa tayari imeandikwa ilikuwa Gospeli ya Mathayo. Hivyo, Wathesalonike na Waberoya waliweza kuhakikisha mambo yote, yaelekea kwa kuchunguza fasiri ya Septuagint ya lugha ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania. Wao walihitaji kusoma na kujifunza Maandiko, na ndivyo ilivyo na sisi.

      Muhimu kwa Wote

      8. Kwa nini wazee waliowekwa rasmi wapaswa kufahamu sana ujuzi wa Biblia?

      8 Wazee waliowekwa rasmi wapaswa kufahamu sana ujuzi wa Biblia. Ni lazima ‘wajue kufundisha’ na ‘kulishika lile neno la imani.’ Mwangalizi Timotheo alipaswa ‘kutumia kwa halali neno la kweli.’ (1 Timotheo 3:2; Tito 1:9; 2 Timotheo 2:15) Mama yake, Eunike, na nyanya yake, Loisi, walikuwa wamemfundisha maandiko matakatifu tangu utoto-mchanga, wakimkazia ‘imani isiyo na unafiki,’ ingawa baba yake alikuwa asiyeamini. (2 Timotheo 1:5; 3:15) Baba wenye kuamini wanapaswa kulea watoto wao “katika adabu na maonyo ya Bwana,” na hasa wazee ambao ni akina baba ni lazima wawe na watoto ‘waaminio, wasioshitakiwa kuwa ni wafisadi wala wasiotii.’ (Waefeso 6:4; Tito 1:6) Basi, hata tuwe na hali gani twapaswa kuchukua kwa uzito sana uhitaji wa kusoma, kujifunza, na kutumia Neno la Mungu.

      9. Kwa nini tujifunze Biblia pamoja na Wakristo wenzi?

      9 Pia twapaswa kujifunza Biblia pamoja na waamini wenzetu. Paulo alitaka Wakristo Wathesalonike wajadiliane juu ya shauri lake. (1 Wathesalonike 4:18) Ili kuboresha uelewevu wetu juu ya kweli, hakuna jambo bora kuliko kujiunga na wanafunzi wengine waliojitoa katika kuchunguza Maandiko. Mithali hii ni ya kweli: “Chuma hunoa chuma; ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake.” (Mithali 27:17) Chombo cha chuma huweza kushika kutu kisipotumiwa na kunolewa. Vivyo hivyo, sisi huhitaji kukutana kwa ukawaida na kunoana kwa kushiriki pamoja ujuzi ambao tumepata kutokana na kusoma, kujifunza, na kutafakari Neno la Mungu la kweli. (Waebrania 10:24, 25) Na zaidi, hii ni njia moja ya kuhakikisha kwamba twanufaika na mimweko ya nuru ya kiroho.—Zaburi 97:11; Mithali 4:18.

      10. Yamaanisha nini kuenenda katika kweli?

      10 Tunapojifunza Maandiko, twaweza kwa kufaa kumwomba Mungu kama alivyofanya mtunga-zaburi: “Niletewe nuru yako na kweli yako ziniongoze.” (Zaburi 43:3) Tukitamani kupata kibali cha Mungu, ni lazima tuenende katika kweli yake. (3 Yohana 3, 4) Hili latia ndani kufuata matakwa yake na kumtumikia kwa uaminifu na unyoofu. (Zaburi 25:4, 5; Yohana 4:23, 24) Ni lazima tumtumikie Yehova katika kweli, kama ifunuliwavyo katika Neno lake na kudhihirishwa katika vichapo vya “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45-47) Jambo hilo lataka ujuzi sahihi wa Maandiko. Basi, tunapaswa kusomaje na kujifunza Neno la Mungu? Je, tunapaswa kuanzia Mwanzo sura ya 1, mstari wa 1, na kupitia vitabu vyote 66? Ndiyo, kila Mkristo aliye na Biblia nzima katika lugha yake apaswa kuisoma toka Mwanzo hadi Ufunuo. Na lengo letu katika kusoma Biblia na vichapo vya Kikristo lapaswa kuwa kuongeza ufahamu wetu juu ya kweli nyingi za Kimaandiko ambazo Mungu ameandaa kupitia “mtumwa mwaminifu.”

      Soma Neno la Mungu kwa Sauti Kubwa

      11, 12. Kwa nini kunanufaisha kusoma Biblia kwa sauti kubwa kwenye mikutano?

      11 Twaweza kusoma kwa ukimya tukiwa peke yetu. Hata hivyo, katika nyakati za kale, usomaji wa faragha ulifanywa kwa sauti kubwa. Yule towashi Mwethiopia alipokuwa amepanda gari lake, mweneza-evanjeli Filipo akamsikia akisoma kutoka unabii wa Isaya. (Matendo 8:27-30) Neno la Kiebrania lililotafsiriwa “soma” hasa humaanisha “kuita.” Hivyo wale ambao mwanzoni hawawezi kusoma kwa ukimya na kupata maana ya yale wasomayo waweza kutamka kila neno kwa sauti kubwa. Jambo kuu ni kujifunza kweli kwa kusoma Neno la Mungu lililoandikwa.

      12 Kwanufaisha kusoma Biblia kwa sauti kubwa kwenye mikutano ya Kikristo. Mtume Paulo alimhimiza mfanyakazi mwenzake Timotheo: “Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma [“usomaji mbele ya watu wote,” NW] na kuonya na kufundisha.” (1 Timotheo 4:13, italiki ni zetu.) Paulo aliwaambia Wakolosai hivi: “Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu fanyeni kwamba usomwe katika kanisa la Walaodikia pia; na ule wa Laodikia usomwe na ninyi.” (Wakolosai 4:16) Na Ufunuo 1:3 husema: “Heri asomaye [“Mwenye furaha ni yeye asomaye kwa sauti kubwa,” NW] na wao wayasikiao maneno ya unabii huu, na kuyashika yaliyoandikwa humo; kwa maana wakati u karibu.” Basi, msemaji wa watu wote apaswa kusoma maandiko kutoka Biblia ili kuthibitisha yale anayoliambia kutaniko.

      Kujifunza kwa Kufuata Vichwa

      13. Ni njia ipi iliyo nzuri zaidi ya kujifunza kweli za Biblia, na ni nini ambacho chaweza kutusaidia kupata maandiko?

      13 Kujifunza kwa kufuata vichwa ndiko njia nzuri zaidi ya kujifunza kweli za Kimaandiko. Konkodansi, ambazo zimeorodhesha maneno ya Biblia kialfabeti katika muktadha wao kulingana na kitabu, sura, na mstari, hufanya iwe rahisi kutafuta maandiko yanayohusiana na habari fulani. Na maandiko hayo yaweza kupatanishwa moja na jingine kwa sababu Mtungaji wa Biblia hajipingi. Kwa roho takatifu, yeye aliwapulizia wanaume wapatao 40 kuandika Biblia kwa muda uzidio karne 16, na kujifunza Biblia kwa kufuata vichwa ni njia ya kujifunza kweli ambayo imethibitishwa kwa muda mrefu.

      14. Kwa nini usome Maandiko ya Kiebrania na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pamoja?

      14 Uthamini wetu kwa kweli ya Biblia wapaswa kutuchochea kusoma na kujifunza Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pamoja na Maandiko ya Kiebrania. Hilo litaonyesha jinsi Maandiko ya Kigiriki hupatana na kusudi la Mungu nalo litaangaza nuru katika unabii mbalimbali wa Maandiko ya Kiebrania. (Warumi 16:25-27; Waefeso 3:4-6; Wakolosai 1:26) Yenye msaada sana kwa habari hii ni New World Translation of the Holy Scriptures. Ilitayarishwa na watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu waliotumia ujuzi uliongezeka upatikanao kuhusu maandiko ya awali ya Biblia pamoja na asili yayo na nahau zayo. Vyenye umuhimu pia ni visaidizi vya kujifunza Biblia ambavyo Yehova ameandaa kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.”

      15. Unaweza kuthibitishaje kwamba ni sawa kunukuu hapa na pale katika Biblia?

      15 Huenda wengine wakasema, ‘Vichapo vyenu hufanya maelfu ya manukuu kutoka Biblia, lakini mbona mwayatoa manukuu hayo hapa na pale?’ Kwa kunukuu hapa na pale katika vitabu 66 vya Biblia, vichapo hivyo hutumia mashahidi kadhaa waliopuliziwa ili kuthibitisha ukweli wa fundisho fulani. Yesu mwenyewe alitumia njia hii ya kufunza. Alipotoa Mahubiri ya Mlimani, alifanya manukuu 21 kutoka Maandiko ya Kiebrania. Hotuba hiyo ina manukuu matatu kutoka Kutoka, mawili kutoka Mambo ya Walawi, moja kutoka Hesabu, sita kutoka Kumbukumbu la Torati, moja kutoka Wafalme wa Pili, manne kutoka Zaburi, matatu kutoka Isaya, na moja kutoka Yeremia. Je, kwa kufanya hivyo Yesu alikuwa ‘akijaribu kuthibitisha jambo lolote tu’? La, kwa sababu ‘alifundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi.’ Ndivyo ilivyokuwa kwa sababu Yesu alitegemeza mafundisho yake kwa amri ya Neno la Mungu lililoandikwa. (Mathayo 7:29) Na ndivyo alivyofanya mtume Paulo.

      16. Paulo alifanya manukuu gani ya Kimaandiko kwenye Warumi 15:7-13?

      16 Katika fungu la maandiko lipatikanalo kwenye Warumi 15:7-13, Paulo alinukuu kutoka sehemu tatu za Maandiko ya Kiebrania—Sheria, Manabii, na Zaburi. Yeye alionyesha kwamba Wayahudi na Wasio Wayahudi wangemtukuza Mungu, na hivyo Wakristo walipaswa kuwakaribisha watu wa mataifa yote. Paulo alisema: “Mkaribishane ninyi kwa ninyi, kama naye Kristo alivyotukaribisha, ili Mungu atukuzwe. Kwa maana nasema, ya kwamba Kristo amefanyika mhudumu wa agano la kutahiriwa kwa ajili ya kweli ya Mungu, kusudi azithibitishe ahadi walizopewa baba zetu; tena ili Mataifa wamtukuze Mungu kwa ajili ya rehema zake; kama ilivyoandikwa, [kwenye Zaburi 18:49], Kwa hiyo nitakushukuru kati ya Mataifa, nami nitaliimbia jina lako. Na tena anena [kwenye Kumbukumbu la Torati 32:43], Furahini, Mataifa, pamoja na watu wake. Na tena [kwenye Zaburi 117:1], Enyi Mataifa yote, msifuni Bwana; enyi watu wote, mhimidini. Na tena Isaya [11:1, 10] anena, Litakuwako shina la Yese, naye aondokeaye kuwatawala Mataifa; ndiye Mataifa watakayemtumaini. Basi Mungu wa tumaini na awajaze ninyi furaha yote na amani katika kuamini, mpate kuzidi sana kuwa na tumaini, katika nguvu za Roho Mtakatifu.” Kwa njia hii ya kufuata vichwa, Paulo alionyesha jinsi ya kunukuu maandiko ili kuthibitisha kweli za Biblia.

      17. Ni kwa kupatana na kielelezo gani Wakristo hunukuu hapa na pale katika Biblia nzima?

      17 Barua ya kwanza iliyopuliziwa ya mtume Petro ina manukuu 34 kutoka vitabu kumi katika Sheria, Manabii, na Zaburi. Katika barua yake ya pili, Petro anukuu mara sita kutoka vitabu vitatu. Gospeli ya Mathayo ina manukuu 122 kutoka Mwanzo hadi Malaki. Katika vitabu 27 vya Maandiko ya Kigiriki, kuna manukuu 320 ya moja kwa moja kutoka Mwanzo hadi Malaki na vilevile mamia ya marejezo mengine yanayorejezea Maandiko ya Kiebrania. Kwa kupatana na kielelezo kilichowekwa na Yesu na kufuatwa na mitume wake, Wakristo wa kisasa wajifunzapo kwa kufuata vichwa mbalimbali vya habari ya Kimaandiko, wao hunukuu hapa na pale katika Biblia nzima. Hilo lafaa hasa katika hizi “siku za mwisho,” ambapo karibu Maandiko yote ya Kiebrania na Kigiriki yanatimizwa. (2 Timotheo 3:1) “Mtumwa mwaminifu” hutumia Biblia hivyo katika vichapo vyake, lakini haongezei wala haondoi jambo kwa Neno la Mungu.—Mithali 30:5, 6; Ufunuo 22:18, 19.

      Sikuzote Enenda Katika Kweli

      18. Kwa nini ‘tuenende katika kweli’?

      18 Tusiondoe kamwe chochote kutoka kwa Biblia, kwa kuwa mafundisho yote ya Kikristo katika Neno la Mungu ni “kweli” au ‘kweli ya [“habari njema,” NW].’ Kushikamana na kweli hii—‘kuenenda’ katika hiyo—ni muhimu ili kupata wokovu. (Wagalatia 2:5; 2 Yohana 4; 1 Timotheo 2:3, 4) Kwa kuwa Ukristo ni “njia ya kweli,” kwa kusaidia wengine katika kuendeleza mapendezi yayo, twawa “watenda kazi pamoja na kweli.”—2 Petro 2:2; 3 Yohana 8.

      19. Tunaweza ‘kuenendaje katika kweli’?

      19 Ikiwa ‘tutakwenda katika kweli,’ ni lazima tusome Biblia na kuwa tayari kupata msaada wa kiroho ambao Mungu huandaa kupitia “mtumwa mwaminifu.” (3 Yohana 4) Na tufanye hivyo kwa manufaa yetu wenyewe na ili tuweze kufundisha wengine juu ya Yehova Mungu, Yesu Kristo, na kusudi la kimungu. Na tushukuru kwamba roho ya Yehova hutusaidia kuelewa Neno lake na kufanikiwa katika kumtumikia katika kweli.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki