Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jitoe Mwenyewe kwa Usomaji
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Mei 15
    • Kujifunza Masomo Yenye Thamani

      14. Waamuzi sura ya 9 yaweza kutumiwaje kufundisha mtoto uhitaji wa kuwa mnyenyekevu?

      14 Kwa kusoma Neno la Mungu, twaweza kujifunza masomo mengi. Kwa kielelezo, labda unataka kukazia watoto wako uhitaji wa kuwa wanyenyekevu. Inapasa kuwa rahisi kupiga picha akilini na kuelewa kile kilichosemwa katika unabii wa Yothamu mwana wa Gideoni. Anza kusoma kwenye Waamuzi 9:8. “Siku moja,” akasema Yothamu, “miti ilitoka ili kuutia mmoja mafuta uwe mfalme juu yao.” Mzeituni, mtini, na mzabibu ikakataa kutawala. Lakini mti wa miiba wa hali ya chini ulifurahi kuwa mtawala. Baada ya kuwasomea watoto wako simulizi hilo kwa sauti kubwa, unaweza kueleza kwamba mimea yenye thamani iliwakilisha watu wenye ustahiki ambao hawakutafuta umaliki juu ya Waisraeli wenzao. Mti wa miiba, ambao ulifaa kutumiwa kama kuni tu, uliwakilisha utawala wa Abimeleki mwenye kiburi, muuaji-kimakusudi aliyetaka kudhibiti wengine lakini aliyekufa kwa utimizo wa unabii wa Yothamu. (Waamuzi, sura 9) Ni mtoto yupi angetaka kukua na kuwa kama mti wa miiba?

      15. Umuhimu wa uaminifu-mshikamanifu wakaziwaje katika kitabu cha Ruthu?

      15 Umuhimu wa uaminifu-mshikamanifu wadhihirishwa katika kitabu cha Biblia cha Ruthu. Tuseme washiriki wa familia yako wanasoma kwa zamu simulizi hilo kwa sauti kubwa na kujaribu kuelewa linalosema. Mwaona Ruthu Mmoabi akiwa safarini kwenda Bethlehemu akiwa pamoja na mama-mkwe wake aliye mjane, Naomi, nanyi mwasikia Ruthu akisema: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.” (Ruthu 1:16) Ruthu mwenye bidii aonekana akiokota masazo nyuma ya wavunaji katika shamba la Boazi. Mwamsikia Boazi akimpongeza, akisema: “Mji wote pia wa watu wangu wanakujua ya kwamba u mwanamke mwema.” (Ruthu 3:11) Upesi, Boazi amwoa Ruthu. Kwa kupatana na mpango wa ndoa ya ndugu-mkwe, kupitia Boazi Ruthu amzaa mwana “[kwa] Naomi.” Ruthu awa mzazi wa kale wa Daudi na hatimaye wa Yesu Kristo. Kwa hiyo yeye alipokea “thawabu kamili.” Na zaidi, wale wanaosoma hilo simulizi la Kimaandiko hujifunza somo muhimu: Uwe mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova, na utabarikiwa sana.—Ruthu 2:12; 4:17-22; Mithali 10:22; Mathayo 1:1, 5, 6.

      16. Wale Waebrania watatu walipitia mtihani gani, na simulizi hilo laweza kutusaidiaje?

      16 Simulizi la Waebrania walioitwa Shadraka, Meshaki, na Abednego laweza kutusaidia kuwa waaminifu kwa Mungu katika hali zenye kujaribu. Piga picha akilini tukio hilo wakati Danieli sura ya 3, inaposomwa kwa sauti kubwa. Sanamu kubwa sana ya dhahabu yasimama katika uwanda wa Dura, ambako maofisa Wababilonia walikuwa wamekusanywa. Kwa mlio wa ala za muziki, wao waanguka na kuabudu sanamu ambayo Mfalme Nebukadreza alikuwa amesimamisha. Wote ila Shadraka, Meshaki, na Abednego wafanya hivyo. Kwa staha, lakini kwa uthabiti, wao wamwambia mfalme kwamba hawatatumikia miungu yake na kuabudu ile sanamu ya dhahabu. Waebrania hao wachanga watupwa ndani ya ile tanuri iliyopashwa moto kupita kiasi. Lakini ni nini ambalo latendeka? Akitazama ndani, mfalme aona wanaume wanne wenye nguvu, mmoja wao akiwa “mfano wa mwana wa miungu.” (Danieli 3:25) Wale Waebrania watatu waondolewa kutoka ndani ya tanuri, naye Nebukadreza abariki Mungu wao. Imethawabisha kupiga picha akilini simulizi hilo. Nayo yaandaa somo lililoje kuhusu uaminifu kwa Yehova chini ya jaribu!

      Nufaikeni Kutokana na Kusoma Biblia Mkiwa Familia

      17. Taja kifupi baadhi ya mambo yenye manufaa ambayo familia yako yaweza kujifunza kwa kusoma Biblia pamoja.

      17 Familia yako yaweza kupata manufaa nyingi ikiwa mnatumia wakati kwa ukawaida kusoma Biblia pamoja. Ukianza na Mwanzo, mwaweza kushuhudia uumbaji na kuchungulia makao ya mwanadamu ya Paradiso ya awali. Mnaweza kushiriki mambo waliyoona wazee wa ukoo waaminifu na familia zao na kufuata Waisraeli wavukapo Bahari Nyekundu ikiwa imekauka. Mwaweza kuona kijana mchungaji Daudi akilishinda jitu Mfilisti Goliathi. Familia yako yaweza kuona ujenzi wa hekalu la Yehova katika Yerusalemu, yaweza kuona likifanywa ukiwa na majeshi ya Babiloni, na kuona likijengwa upya chini ya Gavana Zerubabeli. Pamoja na wachungaji wanyenyekevu karibu na Bethlehemu, mwaweza kusikia tangazo la kimalaika la kuzaliwa kwa Yesu. Mwaweza kupata mambo madogo-madogo kuhusu ubatizo na huduma ya Yesu, kumwona akitoa uhai wake wa kibinadamu ukiwa fidia, na kushiriki shangwe ya kufufuliwa kwake. Kisha mwaweza kusafiri pamoja na mtume Paulo na kutazama kuanzishwa kwa makutaniko huku Ukristo ukienea. Kisha, katika kitabu cha Ufunuo, familia yako yaweza kufurahia ono tukufu la mtume Yohana la wakati ujao, kutia ndani Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo.

      18, 19. Ni madokezo gani yanayotolewa kuhusu usomaji wa Biblia wa familia?

      18 Ikiwa mnasoma Biblia kwa sauti kubwa mkiwa familia, mwisome kwa uwazi na kwa idili. Mnaposoma sehemu fulani za Maandiko, mshiriki mmoja wa familia—labda baba—huenda akasoma maneno ya usimulizi. Wengine wenu mwaweza kuchukua sehemu za wahusika wa Biblia, mkisoma sehemu zenu kwa hisia zifaazo.

      19 Mnaposhiriki katika usomaji wa Biblia mkiwa familia, uwezo wenu wa kusoma waweza kuboreka. Yaelekea, ujuzi wenu juu ya Mungu utaongezeka, na hilo lapaswa kuwavuta karibu naye zaidi. Asafu aliimba: “Nami kumkaribia Mungu ni kwema kwangu; nimefanya kimbilio kwa Bwana MUNGU, niyahubiri matendo yako yote.” (Zaburi 73:28) Hili litasaidia familia yako kuwa kama Musa, ambaye “alistahimili kama amwonaye yeye asiyeonekana,” yaani, Yehova Mungu.—Waebrania 11:27.

  • Soma Neno la Mungu na Umtumikie Katika Kweli
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Mei 15
    • 3. Ni zipi baadhi ya manufaa zipatikanazo kutokana na usomaji wa Biblia?

      3 Familia za Kikristo zisomapo Biblia pamoja, yaelekea zitapata manufaa zenye kudumu. Hizo huja kujua sheria za Mungu na kujifunza kweli kuhusu mafundisho, mambo ya kiunabii, na mambo mengineyo. Baada ya sehemu ya Biblia kusomwa, kichwa cha familia aweza kuuliza: Hili lapasa kutuathirije? Ni katika njia gani hili lahusika na mafundisho mengine ya Biblia? Tunaweza kutumiaje mambo hayo katika kuhubiri habari njema? Familia hupata ufahamu wa ndani inaposoma Biblia ikiwa inafanya utafiti kwa kutumia Watch Tower Publications Index au faharisi nyinginezo. Mabuku mawili ya Insight on the Scriptures yaweza kurejezewa kwa manufaa.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki