-
Furahia Neno la MunguFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Soma Biblia Kila Siku
Mtunga-zaburi alisema hivi kuhusu mtu anayesoma Neno la Mungu kila siku: “Kila alitendalo litafanikiwa.” (Zab. 1:3) Ndiyo, japo hatujakamilika, japo tunaishi katika mfumo mwovu wa mambo wa Shetani, na japo jitihada za Ibilisi za kutuangamiza, kusoma na kuyatumia kwa ukawaida yaliyomo katika Neno la Mungu kutafanya tufanikiwe katika mambo yote yanayohusu uhusiano wetu na Yehova.
Kwa sababu tumekazwa sana na mfumo huu, tunaweza kuimarishwa tukichukua hata dakika chache muhimu kila siku kujifunza mawazo ya Muumba. Wengine ambao walifungwa gerezani kwa sababu ya imani yao waliweza kupata tu mstari mmoja-mmoja wa Biblia ulionukuliwa katika magazeti ya habari. Walikata manukuu hayo, wakayashika akilini, na kuyatafakari. Yehova alibariki jitihada zao kwa sababu walifanya kadiri hali zao zilivyoruhusu ili kujua Neno la Mungu. (Mt. 5:3) Lakini, wengi wetu wana uhuru mkubwa zaidi. Tusifikirie kwamba tutatimiza maajabu kwa kusoma haraka-haraka mstari fulani wa Biblia mara moja kwa siku. Lakini tutabarikiwa tukirekebisha hali yetu ili jambo la kwanza liwe ni kusoma sehemu fulani ya Biblia kila siku, kuitafakari, na kuitumia maishani.
Hata mipango bora inaweza kuvurugika. Mipango yetu inapovurugwa, tutangulize mambo muhimu zaidi. Kwa mfano, hatuwezi kukataa kimakusudi kunywa maji kwa siku moja au mbili. Basi hata hali gani itukie katika maisha yetu ya kila siku, na tuchukue muda fulani wa kujiburudisha kwa maji ya kweli.—Mdo. 17:11.
-