-
KusababuFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 48
Kusababu
TUNAFURAHIA jinsi ambavyo Neno la Mungu limebadili maisha yetu, na tunataka wengine pia wafaidike. Na zaidi, tunatambua kwamba wakati ujao wa watu unategemea jinsi wanavyoitikia habari njema. (Mt. 7:13, 14; Yn. 12:48) Tunatamani sana wakubali kweli. Lakini mbali na kuwa na usadikisho thabiti na bidii, tunahitaji vilevile kutumia busara ili tuweze kuwasaidia vizuri.
Kwa kawaida ukifichua kwa madharau fundisho fulani la uwongo ambalo mtu anapenda sana, mtu huyo hatakubali kweli hata umsomee Maandiko mangapi. Kwa mfano, ukishutumu tu sherehe zinazopendwa kwamba ni za kipagani, huenda watu wasibadili maoni yao kuzihusu. Kwa kawaida unaweza kufanikiwa ukisababu naye. Kusababu kunahusisha nini?
Maandiko yanatuambia kwamba ‘hekima ya kutoka juu ni yenye kufanya amani, yenye kukubali sababu.’ (Yak. 3:17) Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “yenye kukubali sababu” hasa linamaanisha “kukubali maoni ya wengine.” Tafsiri nyingine zinalitafsiri kuwa “upole,” “-enye kufikiria wengine,” au “uvumilivu.” Ona kwamba kusababu kunahusiana na hali ya kufanya amani. Tito 3:2 linataja kukubali sababu pamoja na upole na kuitofautisha na sifa ya kupenda ugomvi. Wafilipi 4:5 linatuhimiza tuwe watu wanaojulikana kwa sifa ya “kukubali sababu.” Mtu anayekubali sababu anafikiria malezi, hali, na hisia za wale anaozungumza nao. Yuko tayari kubadilikana iwapo inafaa. Kushughulika na wengine kwa njia hiyo hufanya wafungue akili zao na mioyo yao ili wasikilize tunaposababu nao juu ya Maandiko.
Uanzie Wapi? Mwanahistoria Luka anaripoti kwamba mtume Paulo alipokuwa Thesalonike, alitumia Maandiko, “akieleza na kuthibitisha kwa marejezo kwamba ilikuwa lazima Kristo kuteseka na kufufuliwa kutoka kwa wafu.” (Mdo. 17:2, 3) Ona kwamba Paulo alifanya hivyo katika sinagogi la Wayahudi. Wasikilizaji waliheshimu Maandiko ya Kiebrania. Ilifaa kuanza mazungumzo kwa jambo walilokubali.
Paulo alipozungumza na Wagiriki katika Areopago huko Athene, yeye hakuanza kwa kunukuu Maandiko. Badala yake, alianza kuzungumzia mambo ambayo walijua na kukubali, na alitumia mambo hayo kuwaongoza kumfikiria Muumba na makusudi Yake.—Mdo. 17:22-31.
-