Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Tufuate Imani Bila Kufikiri?
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Aprili 1
    • Je, Tufuate Imani Bila Kufikiri?

      Mkuu wa kitivo cha theolojia katika chuo fulani huko Marekani aliandika: “Kuna watu wengi wanaodai kuwa na imani katika dini, wanaojiunga na dini hasa ili waepuke kutumia nguvu zao za kufikiri.” Kisha aongezea kusema: “Wanataka tu kuamini kila jambo bila kutaka uthibitisho.”

      HILI ladokeza kwamba watu wengi wanaodai kwamba wanaamini mafundisho ya dini hawafikirii ni kwa nini wana imani hiyo au kama imani yao ina msingi mzuri. Si ajabu kwamba wengi hawapendi kuzungumza kuhusu dini.

      Inasikitisha kwamba, mazoea kama yale ya kutumia mifano ya kidini na sala zinazokaririwa hufanya watu wasifikiri kwa njia ifaayo. Mazoea hayo, pamoja na majengo yenye kuvutia, madirisha ya vioo yenye rangi mbalimbali, na miziki yenye kusisimua, ndiyo mambo tu yapatikanayo katika dini nyingi. Ijapokuwa makanisa mengi yanadai kwamba imani yao ina msingi wa Biblia, ujumbe wao unaosema ‘amini katika Yesu nawe utaokolewa’ hauwachochei watu kujifunza Biblia kwa bidii. Wengine huhubiri gospeli ya kijamii au ya kisiasa. Matokeo yamekuwa nini?

      Mwandishi fulani wa dini alisema hivi kuhusu hali za kule Amerika Kaskazini: “Ukristo unaelekea kuwa wa kijuu-juu tu, na waumini hawafunzwi vizuri ile imani.” Msimamizi mmoja wa kura ya maoni alieleza kuwa Marekani ni “taifa la watu wasio na elimu ya Biblia.” Kwa hakika, maoni hayo yahusu pia nchi nyinginezo zinazodai kuwa za Kikristo. Pia dini nyingi zisizo za Kikristo haziwasaidii watu kufikiri badala yake zinatilia mkazo kukariri nyimbo, sala za kidesturi, na kutafakari kwa namna mbalimbali kunakohusisha mafumbo badala ya kufikiri kwa njia ifaayo.

      Hata hivyo, watu haohao wasiojali usahihi au ukweli wa imani yao ya kidini, mara nyingi hufikiria mambo mengine kwa makini sana katika maisha yao ya kila siku. Je, si jambo la kusikitisha kwamba mtu anayefanya utafiti mwingi ili anunue tu gari ambalo hatimaye litaharibika na kutupwa aweza kusema hivi kuhusu dini, ‘Ikiwa iliwaridhisha wazazi wangu, itaniridhisha pia.’

      Ikiwa kwa kweli twataka kumpendeza Mungu, je, hatupaswi kufikiria kwa uzito usahihi wa yale tunayoamini kumhusu? Mtume Paulo alizungumza kuhusu watu fulani wa kidini wa siku zake ambao walikuwa na “bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Watu kama hao waweza kufananishwa na mpaka-rangi anayeajiriwa apake nyumba rangi lakini anatumia rangi zisizofaa kwa sababu hakusikiliza maagizo ya mwajiri wake. Huenda mpaka-rangi akapendezwa na kazi yake, lakini je, itakubaliwa na mwenye nyumba?

      Ni nini kinachokubaliwa na Mungu kuhusiana na ibada ya kweli? Biblia yajibu: “Hili ni bora na lenye kukubalika machoni pa Mwokozi wetu, Mungu, ambaye mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:3, 4) Huenda wengine wakahisi kwamba haiwezekani kupata ujuzi wa aina hiyo miongoni mwa dini nyingi za siku hizi. Lakini fikiria—ikiwa ni mapenzi ya Mungu kwamba watu waje kwenye ujuzi sahihi wa kweli, je, angeweza kuuficha isivyo haki kutoka kwao? Sivyo kwa kuwa Biblia, inasema: “Ukimtafuta [Mungu], ataonekana nawe.”—1 Mambo ya Nyakati 28:9.

      Mungu anawezaje kupatikana kwa wale wanaomtafuta kwa unyofu? Makala ifuatayo itajibu swali hilo.

  • Mtafute Mungu kwa Moyo na Akili
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Aprili 1
    • Mtafute Mungu kwa Moyo na Akili

      Ukristo wa kweli huwatia watu moyo watumie akili na kuchochewa na mioyo yao ili kujenga imani inayompendeza Mungu.

      KWA hakika mwanzilishi wa Ukristo, Yesu Kristo, alifunza kwamba ni lazima tumpende Mungu kwa ‘akili yote,’ au uwezo wetu wa kufikiri, na pia kwa ‘moyo wote’ na ‘nafsi yote.’ (Mathayo 22:37) Naam, uwezo wetu wa kufikiri una sehemu muhimu katika ibada yetu.

      Mara nyingi Yesu alisema hivi alipowakaribisha wasikilizaji wake wafikirie mafundisho yake: “Nyinyi mwafikiri nini?” (Mathayo 17:25; 18:12; 21:28; 22:42) Katika njia hiyohiyo, mtume Petro aliwaandikia waamini wenzake ili ‘aamshe uwezo wao mwangavu wa kufikiri.’ (2 Petro 3:1) Mtume Paulo, mishonari wa mapema aliyesafiri sana, aliwasihi Wakristo wenzake watumie ‘nguvu zao za kufikiri’ na “kujithibitishia [wenyewe] mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na matakatifu.” (Waroma 12:1, 2) Kwa kuchunguza tu kwa makini mambo wanayoamini, Wakristo wanaweza kujenga imani inayompendeza Mungu na inayowawezesha kukabiliana na majaribu yanayotokea maishani.—Waebrania 11:1, 6.

      Ili kuwasaidia wengine wajenge imani kama hiyo, Wakristo waeneza-evanjeli wa mapema ‘walijadiliana nao kwa kutoa sababu kutokana na Maandiko, wakieleza na kuthibitisha kwa marejezo’ mambo waliyofundisha. (Matendo 17:1-3) Mtazamo wa aina hiyo unaopatana na kufikiri kuzuri ulikuwa na matokeo mazuri kwa watu wenye mioyo minyofu. Kwa mfano, watu katika jiji la Beroya la Makedonia“walipokea neno [la Mungu] kwa hamu ya akili iliyo kubwa zaidi sana, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku juu ya kama mambo hayo [waliyoelezwa na Paulo na wenzake] yalikuwa hivyo.” (Matendo 17:11) Inafaa tukumbuke mambo mawili hapa. Kwanza, Waberoya walikuwa na hamu ya kusikia Neno la Mungu; pili, hawakuamini tu bila kufikiri kwamba yale waliyosikia yalikuwa kweli bali walihakikisha mambo hayo kwa kutumia Maandiko. Kwa sababu hiyo mishonari Mkristo Luka aliwapongeza Waberoya kwa heshima na kuwaita “wenye uelekevu bora.” Je, unaonyesha uelekevu wa namna hiyo unaposhughulikia mambo ya kiroho?

      Akili na Moyo Hushirikiana

      Kama ilivyotangulia kutajwa, ibada ya kweli huhusisha akili na moyo. (Marko 12:30) Fikiria ule mfano wa yule mpaka-rangi katika makala iliyotangulia ambaye alipaka nyumba rangi akitumia rangi zisizofaa. Kama angesikiliza kwa makini maagizo aliyopewa na mwajiri wake, angefanya kazi hiyo kwa moyo wote akiwa na uhakika kwamba ingekubaliwa na mwenye nyumba. Ndivyo ilivyo na ibada yetu.

      Yesu alisema, ‘waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli.’ (Yohana 4:23) Kwa sababu hiyo mtume Paulo aliandika hivi: “Hiyo ndiyo sababu pia sisi . . . hatujaacha kusali kwa ajili yenu na kuomba ili nyinyi mpate kujazwa ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na ufahamivu wa kiroho, kusudi mtembee kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye.” (Wakolosai 1:9, 10) ‘Ujuzi huo sahihi’ huwawezesha watu wanyofu kuabudu kwa moyo na nafsi yote wakiwa na uhakika kamili kwa sababu ‘wanaabudu kile wajuacho.’—Yohana 4:22.

      Kwa sababu hizo, Mashahidi wa Yehova hawabatizi vitoto au watu wanaoanza tu kujifunza ambao hawajajifunza Maandiko kwa makini. Yesu aliwaagiza wafuasi wake hivi: “Mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Ni baada tu ya kupata ujuzi sahihi wa mapenzi ya Mungu ndipo wanafunzi wanyofu wa Biblia wanaweza kuamua kuhusu jinsi ya kuabudu wakitegemea ujuzi huo. Je, unajitahidi kupata ujuzi huo sahihi?

      Kuelewa ile Sala ya Bwana

      Ili kuona tofauti iliyopo kati ya ujuzi sahihi wa Biblia na kuelewa kijuu-juu tu yale Biblia inayosema, tutachunguza ile sala iitwayo kwa kawaida Baba Yetu, au Sala ya Bwana, inayopatikana katika andiko la Mathayo 6:9-13.

      Sala ya Yesu ya kielelezo hukaririwa kanisani kwa ukawaida na mamilioni ya watu. Lakini ni wangapi ambao wamefundishwa hasa maana ya maneno ya utangulizi ya sala hiyo yanayozungumzia jina la Mungu na Ufalme wake? Mambo hayo ni muhimu sana hivi kwamba Yesu aliyatanguliza katika sala yake.

      Inaanza hivi: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe,” au litukuzwe. Ona kwamba Yesu alisema tuombe jina la Mungu litakaswe. Kwa wengi, maneno hayo hutokeza maswali mawili. Kwanza, jina la Mungu ni nani? Na la pili, kwa nini lahitaji kutakaswa?

      Jibu kwa swali la kwanza laweza kupatikana katika Biblia zaidi ya mara 7,000 katika lugha za awali za Biblia. Mojawapo ni katika Zaburi 83:18: “Wajue ya kuwa Wewe uitwaye jina lako Yehova, ndiwe peke yako uliye juu, juu ya nchi yote.” Kuhusu jina la Mungu, Yehova, andiko la Kutoka 3:15 husema: “Hili ndilo jina langu hata milele, nalo ni kumbukumbu langu hata vizazi vyote.”a Lakini kwa nini jina la Mungu lililo safi na takatifu sana lahitaji kutakaswa? Kwa sababu tangu mwanzo wa historia ya binadamu jina hilo limesutwa na kushushiwa heshima.

      Adamu na Hawa wakiwa Edeni, waliambiwa na Mungu kwamba wangekufa kama wangekula tunda lililokatazwa. (Mwanzo 2:17) Kwa ushupavu, Shetani akampinga Mungu kwa kumwambia Hawa: “Hakika hamtakufa.” Kwa hiyo Shetani akamlaumu Mungu kuwa mwongo. Zaidi ya hayo, aliongezea suto kwa jina la Mungu kwa kumwambia Hawa kwamba Mungu alikuwa amemficha isivyo haki ujuzi fulani wa maana. “Kwa maana Mungu anajua kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” Ni uchongezi ulioje!—Mwanzo 3:4, 5.

      Adamu na Hawa wakajiunga na Shetani kwa kula tunda lililokatazwa. Tangu wakati huo, wanadamu wengi kwa kujua au kwa kutojua, wameendelea kulisuta jina la Mungu kwa kukataa viwango vya Mungu vya uadilifu. (1 Yohana 5:19) Bado watu wanamchongea Mungu kwa kumlaumu wanapoteseka hata kama huenda wakati mwingine ni kwa sababu ya njia zao mbaya. Andiko la Mithali 19:3 husema: “Upumbavu wa mtu hupotosha njia yake; na moyo wake hununa juu ya BWANA.” Je, umeelewa ni kwa nini Yesu, aliyempenda Baba yake kikweli alisali kwamba jina Lake litakaswe?

      “Acha Ufalme Wako Uje”

      Baada ya kusali kwamba jina la Mungu litakaswe, Yesu alisema: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:10) Kuhusiana na kifungu hicho, twaweza kuuliza: ‘Ufalme wa Mungu ni nini? Na kuja kwake kunahusianaje na kufanywa kwa mapenzi ya Mungu duniani?’

      Katika Biblia, neno “ufalme” hasa linamaanisha “utawala wa mfalme.” Bila shaka basi, Ufalme wa Mungu unarejelea utawala, au serikali, ya Mungu, ikiwa na mfalme aliyemchagua. Mfalme huyo si mwingine ila Yesu Kristo aliyefufuliwa—aliye “Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana.” (Ufunuo 19:16; Danieli 7:13, 14) Kuhusiana na Ufalme wa Kimesiya wa Mungu mikononi mwa Yesu Kristo, nabii Danieli aliandika: “Na katika siku za wafalme hao [serikali za wanadamu zinazotawala sasa] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.

      Naam, Ufalme wa Mungu utadhibiti dunia yote, na kuiondolea mbali uovu wote na utatawala “milele na milele.” Kwa njia hii, Ufalme wa Mungu ndiyo njia ambayo Yehova anatumia kulitakasa jina lake, akiliondolea lawama yote ya Shetani na wanadamu waovu.—Ezekieli 36:23.

      Ufalme wa Mungu una raia kama vile serikali nyinginezo. Raia hao ni nani? Biblia yajibu: “Wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:11) Kuhusiana na hilo, Yesu pia alisema hivi: “Wenye furaha ni wenye tabia-pole, kwa kuwa wao watairithi dunia.” Bila shaka, hao wana ujuzi sahihi kuhusu Mungu, ambao ni takwa la uhai.—Mathayo 5:5; Yohana 17:3.

      Je, unaweza kuwazia dunia nzima iliyojaa wanadamu wenye tabia-pole wanaompenda Mungu na wanaopendana kikweli? (1 Yohana 4:7, 8) Hivyo ndivyo Yesu alivyoomba aliposema: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” Je, unaelewa ni kwa nini Yesu aliwafunza wafuasi wake wasali hivyo? Na zaidi ya hilo, je, unaona jinsi utimizo wa sala hiyo huenda ukakuathiri?

      Mamilioni Sasa Wanafikiri Kulingana na Maandiko

      Yesu alitabiri kuhusu kampeni ya ulimwenguni pote ya elimu ya kiroho ambayo ingetangaza Ufalme wa Mungu unaokaribia. Yeye alisema: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho [wa ulimwengu, au mfumo uliopo] utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

      Duniani pote Mashahidi wa Yehova wapatao 6,000,000 wanawahubiria majirani wao habari hizo njema. Wanakualika ujifunze zaidi kuhusu Mungu na Ufalme wake kwa “kuyachunguza Maandiko kwa uangalifu,” ukitumia uwezo wako wa kufikiri. Ukifanya hivyo imani yako itaimarishwa nawe utafurahi kufikiria tumaini la uhai katika dunia paradiso, itakayojawa “na kumjua BWANA kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:6-9.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki