Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Ninyi Ni Rafiki Zangu”
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Oktoba 15
    • Tunaweza Kupata Wapi Marafiki Wazuri?

      19, 20. Tunaweza kupata nini katika kutaniko, na tutachunguza nini katika habari inayofuata?

      19 Yesu anaendelea kututunza si kupitia tu usimamizi wa wachungaji wenye upendo, bali pia kupitia mama, ndugu, na dada wa kiroho katika kutaniko. (Soma Marko 10:29, 30.) Ulipoanza kwa mara ya kwanza kushirikiana na tengenezo la Yehova, watu wako wa ukoo waliitikia jinsi gani? Labda, walikuunga mkono katika jitihada zako za kumkaribia Mungu na Kristo. Lakini Yesu alionya kwamba wakati fulani “adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani kwake mwenyewe.” (Mt. 10:36) Inafariji kama nini kujua kwamba katika kutaniko, tunaweza kupata wale ambao watashikamana nasi kwa ukaribu kuliko ndugu zetu wa kimwili!—Met. 18:24.

      20 Kama inavyoonyeshwa na salamu za Paulo mwenyewe mwishoni mwa barua yake kwa kutaniko la Roma, alianzisha urafiki wa karibu sana na watu wengi. (Rom. 16:8-16) Mtume Yohana alimalizia barua yake ya tatu kwa maneno haya: “Wape rafiki salamu zangu kwa jina.” (3 Yoh. 14) Ni wazi kwamba yeye pia alianzisha urafiki wa kudumu na watu wengi.

  • Kudumisha Urafiki Katika Ulimwengu Usio na Upendo
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Oktoba 15
    • Kudumisha Urafiki Katika Ulimwengu Usio na Upendo

      “Mambo haya ninawaamuru ninyi, kwamba mpendane.”—YOH. 15:17.

      1. Kwa nini Wakristo wa karne ya kwanza walihitaji kuendelea kuwa marafiki wa karibu?

      KATIKA usiku wake wa mwisho duniani, Yesu aliwatia moyo wanafunzi wake washikamanifu waendelee kuwa marafiki. Mapema jioni hiyo, alisema kwamba upendo ambao wangeonyeshana ungewatambulisha kuwa wafuasi wake. (Yoh. 13:35) Mitume walihitaji kuendelea kuwa marafiki wa karibu ikiwa wangevumilia majaribu ambayo yalikuwa mbele yao na kutimiza kazi ambayo Yesu angewakabidhi baada ya muda mfupi. Kwa kweli, Wakristo wa karne ya kwanza walijulikana kwa sababu ya ujitoaji wao wa moyo wote kwa Mungu na kwa waamini wenzao.

      2. (a) Tumeazimia kufanya nini, na kwa nini? (b) Tutachunguza maswali gani?

      2 Leo, inafurahisha kama nini kushirikiana na tengenezo la ulimwenguni pote ambalo washiriki wake wanafuata kielelezo kilichowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza! Tumeazimia kutii amri ya Yesu ya kuonyeshana upendo wa kweli. Hata hivyo, katika siku hizi za mwisho, watu kwa ujumla si washikamanifu na hawaonyeshi upendo wa asili. (2 Tim. 3:1-3) Mara nyingi urafiki wao ni wa kijuu-juu tu na wa kichoyo. Ili tuendelee kutambuliwa kuwa Wakristo wa kweli, ni lazima tuepuke mitazamo kama hiyo. Acheni basi tuchunguze maswali yafuatayo: Ni nini msingi wa urafiki mzuri? Tunaweza kupata jinsi gani marafiki wazuri? Ni wakati gani tunapohitaji kukomesha urafiki? Na tunaweza kudumisha jinsi gani urafiki wenye kujenga?

      Ni Nini Msingi wa Urafiki Mzuri?

      3, 4. Ni nini msingi wa urafiki wenye nguvu zaidi, na kwa nini?

      3 Urafiki wenye nguvu zaidi unajengwa juu ya msingi wa upendo kwa Yehova. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Mtu akiweza kumshinda nguvu mmoja aliye peke yake, wawili wakiwa pamoja wataweza kusimama dhidi yake. Nayo kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.” (Mhu. 4:12) Yehova anapokuwa uzi wa tatu katika urafiki, urafiki huo utadumu.

      4 Ni kweli kwamba wale wasiompenda Yehova wanaweza pia kuanzisha urafiki mzuri. Lakini watu wanapokuwa marafiki kwa sababu wote wawili wanampenda Mungu, urafiki wao utakuwa imara kabisa. Wanapokosa kuelewana, marafiki wa kweli wanatendeana kwa njia ambayo inampendeza Yehova. Ikiwa wapinzani wa Mungu wanajaribu kusababisha migawanyiko, maadui hao wanagundua kwamba urafiki kati ya Wakristo wa kweli hauwezi kuvunjwa. Katika historia yote, watumishi wa Yehova wamethibitisha kwamba wako tayari kufa badala ya kuwasaliti waabudu wenzao.—Soma 1 Yohana 3:16.

      5. Kwa nini urafiki kati ya Ruthu na Naomi ulikuwa wenye kudumu?

      5 Bila shaka, tunaweza kufurahia urafiki ulio mzuri zaidi pamoja tu na wale ambao wanampenda Yehova. Fikiria mfano wa Ruthu na Naomi. Wanawake hao walijenga urafiki ambao ni kati ya urafiki wenye kuvutia zaidi katika Biblia. Kwa nini urafiki wao ulikuwa wenye nguvu na wenye kudumu? Ruthu alifunua sababu alipomwambia Naomi hivi: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu. . . . Yehova na anitende hivyo na kuzidi ikiwa chochote isipokuwa kifo kitatutenganisha mimi na wewe.” (Rut. 1:16, 17) Ni wazi kwamba Ruthu na Naomi wote wawili walimpenda sana Mungu, na waliacha upendo huo uongoze jinsi walivyotendeana. Kwa sababu hiyo, wanawake hao wawili walibarikiwa na Yehova.

      Jinsi ya Kupata Marafiki Wazuri

      6-8. (a) Urafiki wenye kudumu unategemea nini? (b) Unaweza kuchukua jinsi gani hatua ya kwanza ili upate marafiki?

      6 Mfano wa Ruthu na Naomi unaonyesha kwamba urafiki mzuri haujitokezi wenyewe tu. Msingi wa kweli wa urafiki ni kwamba marafiki wote wawili wanapaswa kumpenda Yehova. Lakini ni lazima tujitahidi sana na kujidhabihu ili tuwe na urafiki wenye kudumu. Hata ndugu na dada wa kimwili wanaomwabudu Yehova katika familia za Kikristo wanahitaji kujitahidi sana ili kuwa marafiki wa karibu. Hivyo basi, unaweza kuanzisha jinsi gani urafiki mzuri?

      7 Chukua hatua ya kwanza. Mtume Paulo aliwatia moyo marafiki wake katika kutaniko la Roma ‘wafuate mwendo wa ukaribishaji-wageni.’ (Rom. 12:13) Kufuata kihalisi njia fulani kunatia ndani kupiga hatua mbalimbali, moja baada ya nyingine. Vivyo hivyo, kuwa mkaribishaji-wageni kunatia ndani kuchukua hatua fulani ndogo-ndogo, kwa ukawaida. Hakuna mtu mwingine anayeweza kufuata njia au mwendo wa ukaribishaji-wageni kwa niaba yako. (Soma Methali 3:27.) Njia moja ya kuwa mkaribishaji-wageni ni kuwaalika watu mbalimbali katika kutaniko ili wale chakula chepesi pamoja nawe. Je, unaweza kufanya ukaribishaji-wageni uwe zoea lako kwa kuwaalika washiriki wa kutaniko lenu?

      8 Njia nyingine ambayo unaweza kutumia ili kupata marafiki ni kuwaalika watu mbalimbali washiriki pamoja nawe katika kazi ya kuhubiri. Unaposimama kwenye mlango wa mwenye nyumba na kumsikia yule ambaye unahubiri naye akizungumza kutoka moyoni kuhusu upendo wake kwa Yehova, utachochewa kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na mtu huyo.

      9, 10. Paulo alituwekea mfano gani, na tunaweza kumwiga namna gani?

      9 Panuka katika upendo wako. (Soma 2 Wakorintho 6:12, 13.) Je, umewahi kuhisi kwamba hakuna mtu yeyote katika kutaniko lenu anayeweza kuwa rafiki yako? Ikiwa ndivyo, je, inaweza kuwa kwamba una matakwa makali kuhusu ni nani anayeweza kuwa rafiki yako? Mtume Paulo aliweka mfano mzuri wa kupanuka katika upendo. Pindi moja, hangewazia kamwe kuwa na urafiki wa karibu na watu wasio Wayahudi. Hata hivyo, alikuja kuwa “mtume kwa mataifa.”—Rom. 11:13.

      10 Zaidi ya hayo, Paulo hakuanzisha urafiki na watu wa umri wake tu. Kwa mfano, yeye na Timotheo walikuja kuwa marafiki wa karibu ingawa walikuwa na umri na malezi tofauti. Leo, vijana wengi wanathamini sana kuanzisha urafiki na washiriki wenye umri mkubwa kutanikoni. Vanessa, mwenye umri wa miaka 20 na kitu, anasema hivi: “Nina rafiki mpendwa sana ambaye ana umri wa miaka zaidi ya 50. Ninaweza kumweleza kila jambo ambalo ninaweza kumweleza rafiki wa umri wangu. Ananijali sana.” Walianzisha urafiki huo jinsi gani? Vanessa anasema: “Nilijitahidi sana kuanzisha urafiki huo, sikungoja urafiki huo ujianzishe tu.” Je, uko tayari kuanzisha urafiki pamoja na watu wasio wa umri wako? Bila shaka, Yehova atakuthawabisha kwa sababu ya jitihada zako.

      11. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yonathani na Daudi?

      11 Uwe mshikamanifu. Sulemani aliandika hivi: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Met. 17:17) Alipokuwa akiandika maneno hayo, huenda Sulemani alikuwa akifikiria urafiki ambao baba yake, Daudi, alikuwa nao pamoja na Yonathani. (1 Sam. 18:1) Mfalme Sauli alitaka mwana wake Yonathani awe mrithi wa kiti cha ufalme wa Israeli. Lakini Yonathani alikubali uhakika wa kwamba Yehova alimchagua Daudi kwa ajili ya pendeleo hilo. Tofauti na Sauli, Yonathani hakumwonea wivu Daudi. Hakuchukizwa na pongezi ambazo Daudi alipewa, wala hakuamini uchongezi ambao Sauli alieneza kumhusu Daudi. (1 Sam. 20:24-34) Je, sisi ni kama Yonathani? Marafiki wetu wanapopata mapendeleo, je, tunafurahi pamoja nao? Wanapopatwa na matatizo, je, tunawafariji na kuwategemeza? Tukisikia porojo zenye kuumiza zikienezwa kumhusu rafiki yetu, je, tunafanya haraka kuziamini? Au, kama Yonathani, tunamtetea rafiki yetu kwa ushikamanifu?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki