-
Rumania2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kwa kuwa habari njema ilikuwa ikienea sana, Jacob B. Sima, Mwanafunzi wa Biblia mwenye asili ya Kirumania, alitumwa Rumania kusaidia kupanga kazi ya kuhubiri na kuiandikisha kisheria. Punde baada ya kufika Cluj-Napoca mnamo mwaka wa 1920, Ndugu Sima alifanya mkutano na Károly Szabó, na baadaye József Kiss. Hangaiko lao kuu lilikuwa kupata nyumba inayofaa jijini Cluj-Napoca ambayo ingetumiwa kama ofisi ya tawi. Hata hivyo, kwa sababu ya upungufu wa nyumba, ndugu hao waliamua kufungua ofisi nyumbani kwa ndugu fulani. Kwa hiyo, ofisi ya tawi ya kwanza ilifunguliwa Aprili 1920 na shirika la kisheria la Mashahidi wa Yehova likaandikishwa.
-
-
Rumania2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 77]
Ujenzi wa ofisi mpya jijini Cluj-Napoca, mwaka wa 1924
-
-
Rumania2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kwa kuwa gharama ya uchapaji katika viwanda vya kibiashara ilizidi kupanda, ndugu kwenye ofisi ya tawi walitafuta njia nyingine za kuchapa. Wakati huohuo, kiwanda cha uchapaji ambacho ndugu walikuwa wakitumia kwenye Barabara ya Regina Maria, Na. 36, huko Cluj-Napoca, kilikuwa kikiuzwa. Baada ya kupata kibali kutoka makao makuu, ofisi ya tawi ilinunua kiwanda hicho kilichokuwa kwenye kiwanja chenye jengo moja lenye orofa nne na lingine lenye orofa mbili.
Marekebisho ya majengo hayo yalianza mnamo Machi 1924, na ndugu kutoka sehemu za mbali kama vile Baia-Mare, Bistriţa, na Rodna walijitolea kufanya kazi. Ili kutoa michango kwa ajili ya mradi huo, ndugu kadhaa waliuza baadhi ya vitu vyao, na wengine walichanga chakula na vifaa vya ujenzi. Walisafirisha vifaa vingi kwa kutumia mifuko ya pekee inayoitwa desagi, iliyobebwa kwa mikanda begani au na farasi.
Ili kuboresha uchapaji, ofisi ya tawi ilinunua mashine tatu za kupanga herufi, mashine tatu za kuchapa, mashine ya kukunja karatasi, mashine ya kupamba kwa dhahabu, na vifaa vingine. Kwa hiyo, vitabu vilivyochapwa katika kiwanda hicho vilikuwa bora kuliko vitabu vyote nchini Rumania.
Kulikuwa na Wanabetheli 8 na mmoja wao aliwasimamia watu 40 wasiokuwa Mashahidi ambao waliajiriwa kufanya kazi kwa zamu tatu katika kiwanda hicho. Ripoti ya mwaka wa kwanza wa uchapaji, yaani mwaka wa 1924, inaonyesha kwamba walifanya kazi kwa bidii. Magazeti 175,000, vitabu 226,075, na vijitabu 100,000, vilichapwa katika Kirumania na Kihungaria! Kitabu The Harp of God kilichapwa, na pia The Divine Plan of the Ages ambacho ni cha kwanza kati ya vitabu saba vya Studies in the Scriptures.
Baada ya matayarisho ya miaka miwili, ofisi ya tawi ilichapa pia katika Kirumania kitabu (Scenario of the Photo-Drama of Creation) kinachotegemea hotuba kuhusu uumbaji (“Photo-Drama of Creation”). Hotuba hiyo ina sinema na picha zenye rangi zilizoambatanishwa na sauti. Wahudhuriaji walionyeshwa matukio kuanzia uumbaji wa dunia hadi mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Kitabu hicho, hakikuvutia sana kama ile hotuba, lakini kilikuwa na picha 400, na masomo mafupi kuhusu mafundisho ya Biblia, historia, na sayansi, yaliyowachochea wasomaji wengi waichunguze Biblia zaidi.
-