Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Uendako Nitaenda”
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Julai 1
    • “Uendako Nitaenda”

      RUTHU alitembea pamoja na Naomi kwenye barabara iliyopita katika nyanda ndefu za Moabu. Walikuwa peke yao, watu wawili wadogo katika eneo kubwa na lisilo watu. Wazia Ruthu akitambua kwamba ni jioni, kisha anamtazama mama mkwe wake na kuwaza ikiwa ni wakati wa kutafuta mahali pa kupumzika usiku. Alimpenda sana Naomi na alikuwa tayari kufanya lolote ili kumtunza.

      Wote wawili walikuwa na huzuni nyingi. Tayari Naomi alikuwa mjane kwa miaka kadhaa, lakini sasa alikuwa akiomboleza misiba mingine, vifo vya wanawe wawili Kilioni, na Maloni. Ruthu pia alikuwa akiomboleza. Maloni alikuwa mume wake. Ruthu na Naomi walikuwa wanaelekea Bethlehemu, mji ulio huko Israeli. Hata hivyo safari zao zilitofautiana kwa njia fulani. Naomi alikuwa akirudi nyumbani. Ruthu alikuwa akienda mahali asipopajua, huku akiacha watu wake wa ukoo, nchi yake, na tamaduni zake, kutia ndani miungu ya nchi hiyo.​—Ruthu 1:3-6.

  • “Uendako Nitaenda”
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Julai 1
    • Kwa upande mwingine, Naomi alitamani sana kupata habari kutoka nyumbani kwao. Siku moja alisikia, labda kupitia mfanyabiashara msafiri, kwamba janga la njaa lilikuwa limekwisha huko Israeli. Yehova alikuwa amewakumbuka watu wake. Sasa mji wa Bethlehemu ulikuwa na maana yake kamili, yaani, “Nyumba ya Mkate.” Naomi akaamua kurudi nyumbani.​—Ruthu 1:6.

      Sasa Ruthu na Orpa wangefanya nini? (Ruthu 1:7) Walikuwa wamesitawisha uhusiano wa karibu na Naomi kutokana na mambo yaliyowapata. Inaonekana, hasa Ruthu, alivutiwa na fadhili za Naomi na imani yake imara kwa Yehova. Wajane wote watatu waliondoka kuelekea Yuda pamoja.

      Simulizi la Ruthu linatukumbusha kwamba misiba huwapata watu wote, wazuri na wabaya. (Mhubiri 9:2, 11) Pia, linatukumbusha kwamba tunapokabiliana na misiba mikubwa, ni jambo la hekima kutafuta faraja na kitulizo kutoka kwa watu wengine, hasa wale ambao wanatafuta kimbilio katika Yehova, Mungu ambaye Naomi alimwabudu.​—Methali 17:17.

      Upendo Mshikamanifu wa Ruthu

      Wajane hao watatu walipokuwa wakiendelea na safari yao, jambo lingine lilianza kumhangaisha Naomi. Aliwafikiria wanawake hao wawili waliokuwa wakiandamana naye na kuhusu upendo waliokuwa wamemwonyesha yeye na wanawe. Hakutaka kuwaongezea mizigo mingine. Ikiwa wangeacha nchi yao na kumfuata, angewasaidiaje huko Bethlehemu?

      Mwishowe, Naomi akawaambia hivi: “Nendeni, rudini, kila mmoja nyumbani kwa mama yake. Yehova na awaonyeshe fadhili zenye upendo, kama vile tu mlivyowaonyesha wanaume hawa ambao sasa wamekufa na mimi pia.” Pia, alionyesha kwamba alitumaini kuwa Yehova angewabariki kwa kuwapa waume wengine na waanze maisha mapya. “Kisha akawabusu,” simulizi hilo linasema, “nao wakaanza kupaaza sauti zao na kulia.” Ni rahisi kuelewa kwa nini Ruthu na Orpa walikuwa na uhusiano wa karibu na mwanamke huyo mwenye fadhili na asiye na ubinafsi. Wote wawili waliendelea kusisitiza hivi: “Hapana, bali tutarudi pamoja nawe kwa watu wako.”​—⁠Ruthu 1:​8-10.

      Hata hivyo, Naomi hakushawishiwa kwa urahisi. Aliwasadikisha kwamba hangeweza kuwasaidia huko Israeli, kwa sababu hakuwa na mume wa kumwandalia, wala wana ambao wangewaoa, wala tumaini lolote. Aliwaambia kwamba alikuwa na uchungu mwingi kwa sababu hakuwa na uwezo wa kuwaandalia.​—Ruthu 1:11-13.

      Orpa alielewa kabisa maneno ya Naomi. Huko Moabu alikuwa na mama, watu wa familia, na makao. Lilikuwa jambo linalopatana na akili kubaki Moabu. Hivyo, shingo upande alimbusu Naomi, akamwambia kwaheri na kuondoka.​—Ruthu 1:14.

      Namna gani Ruthu? Maneno ya Naomi yalimhusu pia. Hata hivyo, tunasoma hivi: “Bali Ruthu akashikamana naye.” Labda Naomi alikuwa ameanza kutembea tena barabarani lakini akatambua kwamba Ruthu alikuwa akimfuata. Akamwambia hivi: “Tazama! Shemeji yako amerudi kwa watu wake na kwa miungu yake. Rudi pamoja naye.” (Ruthu 1:15) Maneno ya Naomi yanatufunulia jambo fulani muhimu. Orpa hakuwa tu amerudi kwa watu wake, bali pia kwa “miungu yake.” Alikuwa tayari kuendelea kumwabudu Kemoshi na miungu mingine ya uwongo. Je, Ruthu alihisi hivyo pia?

      Huku akimtazama Naomi wakiwa kwenye barabara hiyo isiyo na watu, Ruthu alikuwa na uhakika na utulivu moyoni. Moyo wake ulikuwa na upendo mwingi kumwelekea Naomi, na Mungu ambaye Naomi aliabudu. Hivyo akasema: “Usiniombe nikuache, nigeuke nisifuatane nawe; kwa maana uendako nitaenda, na mahali utakapokaa usiku kucha nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu. Pale utakapokufa nitakufa nami, na hapo ndipo nitakapozikwa. Yehova na anitende hivyo na kuzidi ikiwa chochote isipokuwa kifo kitatutenganisha mimi na wewe.”​—⁠Ruthu 1:16, 17.

      Maneno ya Ruthu yalikuwa ya pekee sana, hivi kwamba bado yanakumbukwa hata baada ya miaka elfu tatu kupita. Maneno yake yanafafanua vizuri sifa yenye thamani, yaani, upendo mshikamanifu. Ruthu alikuwa na upendo wenye nguvu na wenye ushikamanifu sana hivi kwamba alikuwa tayari kushikamana na Naomi na kwenda popote pale pamoja naye. Wangetenganishwa tu na kifo. Watu wa Naomi wangekuwa watu wake, kwa kuwa Ruthu alikuwa tayari kuacha kila kitu alichokijua huko Moabu, hata miungu ya Wamoabu. Tofauti na Orpa, Ruthu alisema kwa moyo wote kwamba alitaka Mungu wa Naomi, Yehova, awe Mungu wake pia.b

      Basi, wakaendelea na safari wakiwa wawili tu, kwenye barabara ndefu ya kwenda Bethlehemu. Kulingana na mkadiriaji mmoja, huenda safari hiyo ilichukua juma moja. Bila shaka, ingawa walikuwa na huzuni kila mmoja wao alifarijiwa na mwenzake kwa kiasi fulani.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki