-
“Uendako Nitaenda”Mnara wa Mlinzi—2012 | Julai 1
-
-
Wanawake hao walipoendelea na maisha huko Bethlehemu, Ruthu alianza kufikiria jinsi ambavyo angetimiza mahitaji yake na ya Naomi pia. Alijifunza kwamba Sheria ambayo Yehova alikuwa amewapa watu wake huko Israeli ilitia ndani mpango wenye upendo kwa ajili ya maskini. Waliruhusiwa kwenda mashambani wakati wa mavuno na kuwafuata wavunaji, huku wakikusanya masalio yaliyobaki na vilevile kuvuna nafaka iliyokua kwenye ukingo wa mashamba.c—Mambo ya Walawi 19:9, 10; Kumbukumbu la Torati 24:19-21.
Ulikuwa wakati wa kuvuna shayiri, inaelekea ulikuwa mwezi wa Aprili kulingana na kalenda ya kisasa, na Ruthu alienda mashambani ili kuona kama kuna mtu ambaye angemruhusu akusanye masalio nyuma ya wavunaji. Aliingia katika shamba la mwanamume aliyeitwa Boazi, tajiri aliyekuwa na mashamba na ambaye alikuwa mtu wa ukoo wa Elimeleki, mume wa Naomi aliyekuwa amekufa. Ingawa Sheria ilimruhusu kukusanya masalio, hakuona kwamba ilikuwa haki yake, alimwomba ruhusa mwanamume aliyewasimamia wavunaji ili aanze kazi ya kukusanya. Alimruhusu, na Ruthu akaanza kazi.—Ruthu 1:22–2:3, 7.
Wazia Ruthu akiwafuata wavunaji. Wavunaji hao walipokuwa wakikata shayiri wakitumia miundu yao, aliinama ili aokote masuke yaliyoanguka au waliyobakisha, akayakusanya katika miganda, na kuibeba mpaka mahali ambapo angeipiga-piga na kupata nafaka baadaye. Ilikuwa kazi ya polepole, yenye kuchosha, na ilikuwa ngumu zaidi kadiri jua lilivyozidi kuwa kali. Hata hivyo, Ruthu aliendelea, akisimama kidogo tu ili kupangusa jasho kwenye paji la uso wake na kula chakula chepesi cha mchana katika “nyumba”—inaelekea ni kibanda kilichotengenezwa ili kuwapa wafanyakazi kivuli.
Inaelekea Ruthu hakutazamia mtu yeyote amtambue, lakini kuna mtu aliyemtambua. Boazi alimwona na kumwuliza msimamizi fulani kijana kuhusu mwanamke huyo. Boazi, mwanamume mwenye imani thabiti, aliwasalimu wafanyakazi wake—huenda wengine walikuwa vibarua wa siku moja au hata watu wa mataifa ya kigeni—akiwaambia “Yehova na awe pamoja nanyi.” Nao wakaitikia kwa maneno kama hayo. Mwanamume huyo mwenye umri mkubwa aliyempenda Yehova alimtendea Ruthu kama bintiye.—Ruthu 2:4-7.
Huku akimwita “binti yangu,” Boazi alimshauri Ruthu aendelee kurudi kwenye mashamba yake ili akusanye masalio na kwamba afanye kazi karibu na wanawake vijana wa nyumba yake ili asisumbuliwe na wafanyakazi wa kiume. Alihakikisha kwamba alipata chakula cha mchana. Zaidi ya hayo, alitafuta nafasi ya kumpongeza na kumtia moyo. Jinsi gani?—Ruthu 2:8, 9, 14.
Ruthu alipomwuliza Boazi kwa nini alimtendea kwa fadhili hivyo, Boazi alimwambia alikuwa amesikia yote aliyokuwa amemfanyia Naomi, mama-mkwe wake. Inaelekea kwamba Naomi alikuwa amemsifu Ruthu aliyempenda mbele ya wanawake wa Bethlehemu, na habari hiyo ilikuwa imemfikia Boazi. Pia, alijua kwamba Ruthu alikuwa ameanza kumwabudu Yehova kwa kuwa alisema: “Yehova na akupe thawabu kwa sababu ya jinsi unavyotenda, na upate malipo kamili kutoka kwa Yehova Mungu wa Israeli, ambaye umekuja kutafuta kimbilio chini ya mabawa yake.”—Ruthu 2:12.
Maneno hayo yalimtia moyo sana Ruthu! Kwa kweli, alikuwa ameamua kutafuta kimbilio chini ya mabawa ya Yehova Mungu, kama ndege mdogo anavyojificha kando ya mama yake. Alimshukuru Boazi kwa kumtia moyo. Na akaendelea kufanya kazi mpaka jioni.—Ruthu 2:13, 17.
Leo, sote tunaweza kuiga jinsi Ruthu alivyotenda kwa imani kwa sababu tunapambana na hali ngumu za kiuchumi. Hakutazamia kwamba watu wengine walipaswa kumtendea kwa fadhili, hivyo alithamini kila jambo alilofanyiwa. Hakuaibika kufanya kazi ngumu kwa saa nyingi ili kumwandalia mtu aliyempenda, ingawa ilikuwa kazi ya hali ya chini. Alikubali kwa furaha na akafuata mashauri yenye hekima kuhusu jinsi angefanya kazi akiwa salama na kushirikiana na watu wazuri. Jambo la maana zaidi ni kwamba hakusahau kamwe mahali ambapo angepata kimbilio la kweli, yaani, kwa Baba yake aliyemlinda, Yehova Mungu.
-
-
“Uendako Nitaenda”Mnara wa Mlinzi—2012 | Julai 1
-
-
c Ilikuwa sheria ya pekee sana, bila shaka, ilikuwa tofauti na mpango wowote ambao Ruthu alijua katika nchi yao. Zamani, katika Mashariki ya Karibu, wajane walitendewa vibaya. Kitabu kimoja cha marejezo kinasema hivi: “Baada ya kufiwa na mumewe, kwa kawaida mjane angetegemea wanawe ili kupata mahitaji; kama hakuwa na wana, huenda angejiuza awe mtumwa, angefanya ukahaba, au afe.”
-