-
Rwanda2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
KISA CHA JEAN NA CHANTAL
Jean de Dieu (John) Mugabo, ndugu mchangamfu na mwenye kujali, alianza kujifunza na Mashahidi wa Yehova mnamo 1982. Kabla ya kubatizwa katika mwaka wa 1984, alikuwa tayari amefungwa gerezani mara tatu kwa sababu ya msimamo wake kama Shahidi wa Yehova. Mke wake, Chantal, alibatizwa pia mwaka wa 1984, na wakafunga ndoa mwaka wa 1987. Mauaji ya jamii nzima-nzima yalipoanza, walikuwa na watoto watatu, wote wasichana. John na Chantal waliishi na kitinda-mimba wao mwenye umri wa miezi sita huku wale watoto wengine wakiishi na wazazi wa Chantal katika eneo lingine.
Siku ya kwanza ya mauaji, Aprili 7, 1994, askari na wapiganaji wa Interahamwe walianza kuvamia nyumba zote za Watutsi. John alikamatwa na kupigwa kwa marungu; lakini akafanikiwa kutoroka na kukimbilia Jumba la Ufalme lililo karibu akiwa pamoja na ndugu mwingine. Chantal naye, bila kujua kilichompata mumewe, alijaribu kuondoka mjini pamoja na mtoto wao mdogo ili kwenda kuungana na watoto wao wengine.
John asimulia mambo yaliyompata: “Jumba la Ufalme lilikuwa na dohani kubwa kwa maana jengo hilo lilikuwa duka la kuokea mikate hapo awali. Kwa juma moja, tulijificha katika Jumba la Ufalme lenyewe, na dada mmoja Mhutu alituletea chakula ilipokuwa salama kufanya hivyo. Baadaye, tulijificha kwenye paa, kati ya mabati na dari, ambapo kulikuwa na joto sana jua lilipowaka. Tulitaka sana kupata mahali pazuri zaidi pa kujificha, kwa hiyo tulibomoa sehemu fulani ya dohani hilo la matofali, tukaingia na kukaa huko kwa zaidi ya mwezi mmoja tukiwa tumechutama.
“Karibu na hapo, wapiganaji wa Interahamwe walikuwa wameweka kizuizi cha barabarani na mara nyingi waliingia ndani ya Jumba la Ufalme kuzungumza au kujikinga mvua. Tungewasikia wakiongea. Dada huyo aliendelea kutuletea chakula ilipowezekana. Wakati mwingine, nilihisi sitaweza kuvumilia tena, lakini tuliendelea kumwomba Yehova atusaidie kustahimili. Mwishowe, mnamo Mei 16, dada huyo alitujulisha kwamba wanajeshi wa Rwandan Patriotic Front wamechukua udhibiti wa eneo hilo la mji, na hivyo hakuna haja ya kujificha tena.”
Naye Chantal, mke wa John, alipatwa na nini? Anaeleza: “Nilifaulu kutoroka kutoka nyumbani pamoja na mtoto wetu mnamo Aprili 8. Nilikutana na Immaculée, ambaye kitambulisho chake kilionyesha kwamba yeye ni Mhutu, na Suzanne, ambaye ni Mtutsi. Tulitaka kufika Bugesera, mji ulio umbali wa kilomita 50, ambapo wazazi wangu waliishi pamoja na watoto wetu. Kwa kuwa tulisikia kwamba kuna vizuizi katika barabara zote za kuelekea nje ya mji, tuliamua kwenda kwenye kijiji kilicho karibu na mji wa Kigali, ambako Immaculée alikuwa na mtu wa ukoo aliyeitwa Gahizi, na ambaye pia alikuwa Shahidi wa Yehova. Gahizi, aliyekuwa Mhutu, alitukaribisha na licha ya vitisho kutoka kwa majirani, alifanya yote aliyoweza ili kutusaidia. Askari wa serikali na wapiganaji wa Interahamwe waliposikia kwamba Gahizi alikuwa anawalinda Watutsi, walimpiga risasi.
“Baada ya kumwua Gahizi, askari hao walitupeleka mtoni ili kutuua. Tukiwa na hofu nyingi, tulisubiri kuuawa. Ghafula, kukazuka bishano kali kati ya askari hao, na mmoja wao akasema: ‘Usiue wanawake. Tukiwaua, tutapatwa na mkosi. Huu ni wakati wa kuua wanaume tu.’ Baada ya hapo, André Twahirwa, mmoja wa ndugu waliokuwa wakitufuata na ambaye alikuwa amebatizwa juma lililotangulia, akatupeleka kwake nyumbani licha ya kukatazwa na majirani. Siku iliyofuata, akaandamana nasi hadi Kigali, ambapo alinuia kututafutia mahali salama pa kukaa. Alitusaidia kupita vizuizi kadhaa vya barabarani vilivyokuwa hatari sana. Immaculée alibeba mtoto wangu ili tukikamatwa, aweze kumwokoa. Mimi na Suzanne tulipasua vitambulisho vyetu ili tusigunduliwe.
“Katika kizuizi kimoja, Interahamwe walimgonga Immaculée na kusema, ‘Mbona unasafiri na Watutsi hawa?’ Mimi na Suzanne tulizuiwa tusipite. Hivyo Immaculée na André walitangulia hadi nyumbani kwa Ndugu Rwakabubu. André na ndugu wengine wawili, Simon na Mathias, walihatarisha uhai wao sana ili kutusaidia kupita kizuizi hicho cha mwisho na kunipeleka kwa Ndugu Rwakabubu, naye Suzanne akaenda kwa mmoja wa watu wake wa ukoo.
“Hata hivyo, ilikuwa hatari sana kwangu kuendelea kuishi kwa Ndugu Rwakabubu, hivyo, kwa shida nyingi, ndugu walinisaidia kwenda kwenye Jumba la Ufalme ambapo Mashahidi wengine walifichwa. Kufikia wakati huo, ndugu na dada kumi ambao ni Watutsi walikuwa wamejificha humo. Immaculée alikataa kuniacha. Alisema, ‘Wakikuua nami ninusurike, nitamwokoa mtoto wako.’”c
Wakati huo, Védaste Bimenyimana, ndugu aliyeishi karibu na ambaye alikuwa na mke Mtutsi, alikuwa tu amefaulu kupeleka familia yake mahali salama. Baadaye, akarudi kwenye Jumba la Ufalme kuwasaidia ndugu kukimbilia mahali salama. Inapendeza kwamba wote waliokoka.
Baada ya mauaji, John na Chantal walipata habari kwamba wazazi wao kutia ndani binti zao wawili wenye umri wa miaka miwili na mitano, ambao waliishi pamoja na wazazi hao, walikuwa wameuawa pamoja na watu wengine 100 wa ukoo. Walihisije baada ya kufiwa na watu wengi hivyo? “Mwanzoni, haikuwa rahisi kuvumilia,” asema Chantal. “Tulihisi tumekufa ganzi. Hakuna aliyewazia kwamba watu wengi hivyo wangekufa. Tuliacha yote mikononi mwa Yehova, tukiwa na tumaini la kuwaona watoto wetu tena wakati wa ufufuo.”
-
-
Rwanda2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 214]
Kuanzia kushoto kuelekea kulia: (nyuma) André Twahirwa, Jean de Dieu, Immaculée, Chantal (na mtoto), Suzanne; (mbele) watoto wa Mugabo: Jean-Luc na Agapé
-