-
Dhabihu Zilizompendeza MunguMnara wa Mlinzi—2000 | Agosti 15
-
-
Dhabihu Zilizompendeza Mungu
“Kila kuhani wa cheo cha juu huwekwa rasmi ili kuzitoa zawadi na dhabihu pia.”—WAEBRANIA 8:3.
1. Kwa nini watu huona uhitaji wa kumwendea Mungu?
“KUTOA dhabihu huonekana kuwa jambo la ‘asili’ kwa mwanadamu kama vile kusali; anayetoa dhabihu huonyesha jinsi ahisivyo juu yake mwenyewe, ilhali yule anayesali huonyesha jinsi ahisivyo juu ya Mungu,” aandika mwanahistoria wa Biblia Alfred Edersheim. Tangu wakati ambapo dhambi iliingia ulimwenguni, imesababisha hisia zenye huzuni za hatia, kutenganishwa na Mungu, na kukosa tumaini. Kitulizo kinahitajika kutokana na hisia hizo. Ni rahisi kuelewa kwamba watu wanapojikuta katika hali kama hiyo yenye kukatisha tamaa, wao huona uhitaji wa kumwendea Mungu ili wapate msaada.—Waroma 5:12.
2. Ni habari gani za mapema zilizoandikwa katika Biblia kuhusu matoleo kwa Mungu?
2 Habari za kwanza zilizoandikwa katika Biblia juu ya matoleo kwa Mungu zahusu Kaini na Abeli. Twasoma: “Ikawa hatimaye Kaini akaleta mazao ya ardhi, sadaka kwa BWANA. Habili naye akaleta wazao wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizonona za wanyama.” (Mwanzo 4:3, 4) Halafu, twaona kwamba Noa, ambaye alihifadhiwa na Mungu katika lile Furiko kubwa ambalo liliharibu kizazi kiovu cha wakati wake, alichochewa ‘kumtolea Yehova sadaka za kuteketezwa [“kuchomwa,” NW] juu ya madhabahu.’ (Mwanzo 8:20) Mara kadhaa, Abrahamu, mtumishi na rafiki mwaminifu wa Mungu, akichochewa na ahadi na baraka za Mungu ‘alijenga madhabahu na kuliitia jina la BWANA.’ (Mwanzo 12:8; 13:3, 4, 18) Baadaye, Abrahamu alikabili jaribu kubwa zaidi la imani yake alipoambiwa na Yehova amtoe mwana wake Isaka akiwa toleo la kuchomwa. (Mwanzo 22:1-14) Masimulizi hayo, yajapokuwa mafupi, yanatoa habari nyingi sana kuhusu dhabihu, kama tutakavyoona.
3. Dhabihu hutimiza fungu gani katika ibada?
3 Kutokana na masimulizi hayo na masimulizi mengine ya Biblia, ni wazi kwamba kutoa aina fulani ya dhabihu kulikuwa sehemu muhimu ya ibada muda mrefu kabla Yehova hajatoa sheria hususa kuhusu dhabihu. Kulingana na hayo, kitabu kimoja chafafanua “dhabihu” kuwa “sherehe ya kidini ambamo kitu fulani hutolewa kwa mungu fulani ili kuanzisha, kudumisha, au kurudisha uhusiano ufaao kati ya mtu na kile akionacho kuwa kitakatifu.” Lakini jambo hilo lazusha maswali fulani muhimu ambayo yafaa tuyachunguze kwa makini, kama vile: Kwa nini dhabihu inahitajiwa katika ibada? Mungu hukubali dhabihu za aina gani? Na dhabihu za kale zamaanisha nini kwetu leo?
Kwa Nini Dhabihu Inahitajiwa?
4. Matokeo yalikuwa nini kwa Adamu na Hawa walipofanya dhambi?
4 Adamu alifanya dhambi kimakusudi. Alikosa kutii kimakusudi kwa kuchukua na kula tunda kutoka kwa mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Adhabu ya tendo hilo la kutotii ilikuwa kifo, kama vile Mungu alivyokuwa amesema wazi: “Siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Hatimaye, Adamu na Hawa wakapata mshahara wa dhambi—wakafa.—Mwanzo 3:19; 5:3-5.
5. Kwa nini Yehova alichukua hatua ya kwanza kwa niaba ya uzao wa Adamu, Naye aliwafanyia nini?
5 Basi, namna gani uzao wa Adamu? Kwa kuwa walirithi dhambi na kutokamilika kutoka kwa Adamu, wao vilevile wametenganishwa na Mungu, hawana tumaini, nao hufa tu kama wanadamu wa kwanza wawili. (Waroma 5:14) Hata hivyo, Yehova si Mungu wa haki na uwezo tu bali pia ni Mungu wa upendo, sifa yake kuu. (1 Yohana 4:8, 16) Kwa hiyo, yeye huchukua hatua ya kwanza kuleta maelewano. Baada ya kusema kwamba “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” Biblia yaendelea kusema, “lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uhai udumuo milele kwa njia ya Kristo Yesu Bwana wetu.”—Waroma 6:23.
6. Mapenzi ya Yehova ni nini kuhusiana na madhara yaliyotokana na dhambi ya Adamu?
6 Hatimaye, ili kutoa uhakikisho kuhusu zawadi hiyo, Yehova Mungu alitoa kitu ambacho kingefunika kile kilichopotea kutokana na dhambi ya Adamu. Katika Kiebrania, yaelekea neno ka·pharʹ mwanzoni lilimaanisha “-funika” au labda “-futa,” nalo pia hutafsiriwa “kufunika.”a Yaani, Yehova aliandaa njia ifaayo ya kufunika dhambi iliyorithiwa kutoka kwa Adamu na kufuta kabisa madhara yaliyotokana nayo ili wale wanaostahili kupata zawadi hiyo waweze kukombolewa kutokana na hatia ya dhambi na kifo.—Waroma 8:21.
7. (a) Hukumu ya Mungu dhidi ya Shetani ilitoa tumaini gani? (b) Ni bei gani ambayo ni lazima ilipwe ili wanadamu wakombolewe kutoka katika dhambi na kifo?
7 Tumaini la kuwekwa huru na utumwa wa dhambi na kifo lilidokezwa mara baada ya wanadamu wa kwanza wawili kufanya dhambi. Akimhukumu Shetani aliyewakilishwa na nyoka, Yehova alisema: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake [“mbegu yako na mbegu yake,” NW]; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwanzo 3:15) Taarifa hiyo ya unabii iliwatolea tumaini wote ambao wangekuwa na imani katika ahadi hiyo. Hata hivyo, bei fulani yapasa kulipwa ili ukombozi huo upatikane. Mbegu iliyoahidiwa haingekuja tu na kumharibu Shetani; lazima Mbegu hiyo ipondwe kisigino, yaani, ife, japo si milele.
8. (a) Kaini alivunjaje matumaini? (b) Kwa nini dhabihu ya Abeli ilikubalika machoni pa Mungu?
8 Yaelekea Adamu na Hawa walitafakari sana juu ya utambulisho wa Mbegu iliyoahidiwa. Hawa alipomzaa Kaini, mwana wake wa kwanza, alitangaza hivi: “Nimepata mtoto mwanamume kwa BWANA.” (Mwanzo 4:1) Je, alikuwa akifikiri kwamba labda mwana wake angekuwa Mbegu hiyo? Iwapo alifikiri hivyo au la, Kaini alivunja matumaini sana na dhabihu yake. Kwa upande mwingine, Abeli ndugu yake alionyesha imani katika ahadi ya Mungu, akachochewa kuwadhabihu wazao wa kwanza wa wanyama wake kwa Yehova. Twasoma hivi: “Kwa imani Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko Kaini, imani ambayo kupitia hiyo alitolewa ushahidi kwamba yeye alikuwa mwadilifu.”—Waebrania 11:4.
9. (a) Abeli aliweka imani katika nini, naye aliionyeshaje? (b) Toleo la Abeli lilitimiza nini?
9 Abeli hakuwa na imani tu kwamba kuna Mungu, imani ambayo huenda Kaini pia alidhihirisha. Abeli alikuwa na imani katika ahadi ya Mungu kuhusu Mbegu fulani ambayo ingewaletea wanadamu waaminifu wokovu. Hakujulishwa jambo hilo lingetimizwaje, lakini ahadi ya Mungu ilimfahamisha Abeli kuwa mtu fulani alipaswa kupondwa kisigino. Naam, yaonekana alifikia mkataa kwamba damu ilipasa kumwagwa—maana hasa ya dhabihu. Abeli alimtolea yule aliye Chanzo cha uhai zawadi iliyohusisha uhai na damu, yaelekea ikiwa wonyesho wa tamaa yake kubwa na matazamio ya kuona kutimizwa kwa ahadi ya Yehova. Wonyesho huo wa imani ndio uliofanya Yehova apendezwe na dhabihu ya Abeli, na kwa kadiri ndogo, ukaonyesha maana halisi ya dhabihu—njia ambayo wanadamu wenye dhambi wanaweza kutumia ili kumkaribia Mungu na kupata kibali chake.—Mwanzo 4:4; Waebrania 11:1, 6.
10. Yehova alidhihirishaje maana ya dhabihu kwa kumwomba Abrahamu amtoe Isaka akiwa dhabihu?
10 Yehova alijulisha wazi, kwa njia yenye kutokeza, maana hasa ya dhabihu alipomwamuru Abrahamu amtoe mwana wake Isaka akiwa toleo la kuchomwa. Ingawa dhabihu hiyo haikutolewa kihalisi, ilifananisha jambo ambalo Yehova angefanya hatimaye—kumtoa Mwana wake mzaliwa-pekee akiwa dhabihu kubwa zaidi iliyopata kutolewa ili kutimiza mapenzi Yake kwa wanadamu. (Yohana 3:16) Kupitia dhabihu na matoleo ya Sheria ya Kimusa, Yehova alitoa vigezo vya unabii ili kuwafundisha wachaguliwa wake yale wapaswayo kufanya ili wasamehewe dhambi zao na kuimarisha tumaini lao la wokovu. Tunaweza kujifunza nini kutokana na hayo?
Dhabihu Zinazokubalika kwa Yehova
11. Kuhani wa cheo cha juu wa Israeli alitoa aina gani mbili za matoleo, na kwa makusudi gani?
11 “Kila kuhani wa cheo cha juu huwekwa rasmi ili kutoa zawadi na dhabihu pia,” asema mtume Paulo. (Waebrania 8:3) Ona kwamba Paulo anatenganisha matoleo ya kuhani wa cheo cha juu wa Israeli la kale katika sehemu mbili, yaani, “zawadi” na “dhabihu” au “dhabihu kwa ajili ya dhambi.” (Waebrania 5:1) Kwa ujumla, watu hutoa zawadi ili kuonyesha upendo na shukrani, na vilevile kusitawisha urafiki, au kupata kibali. (Mwanzo 32:20; Mithali 18:16) Vivyo hivyo, matoleo mengi ambayo Sheria iliagiza yatolewe yanaweza kuonwa kuwa “zawadi” inayotolewa kwa Mungu ili kupata kibali chake.b Kukiuka Sheria kulihitaji malipo, na ili kutoa malipo hayo, “dhabihu kwa ajili ya dhambi” zilitolewa. Vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, hasa Kutoka, Mambo ya Walawi, na Hesabu, vina habari nyingi sana kuhusu aina mbalimbali za dhabihu na matoleo. Ingawa inaweza kuwa vigumu sana kwetu kufahamu na kukumbuka habari hizo zote, inafaa kuchunguza mambo fulani muhimu kuhusu aina mbalimbali za dhabihu.
12. Ni wapi katika Biblia tuwezapo kupata muhtasari wa dhabihu, au matoleo, katika Sheria?
12 Twaweza kuona kwamba katika kitabu cha Mambo ya Walawi sura ya 1 hadi ya 7, aina tano kuu za matoleo—toleo la kuchomwa, toleo la nafaka, dhabihu ya ushirika, toleo la dhambi, na toleo la hatia—zimeelezwa kila moja peke yake, ingawa kwa kweli baadhi ya matoleo hayo yalitolewa pamoja. Twaona pia kwamba matoleo hayo yanaelezwa mara mbili katika sura hizo, kwa malengo tofauti: mara ya kwanza katika Mambo ya Walawi 1:2 hadi 6:7, panapoeleza kinaganaga kile kilichopasa kutolewa kwenye madhabahu, na mara ya pili, katika Mambo ya Walawi 6:8 hadi 7:36, panapoonyesha sehemu zilizotengwa kwa ajili ya makuhani na zile zilizohifadhiwa kwa ajili ya mtoaji. Kisha katika Hesabu sura ya 28 na 29, twaona kile kiwezacho kuonwa kuwa ratiba kamili, inayoeleza ni nini ambacho kilihitaji kutolewa kila siku, kila juma, kila mwezi, na kwenye misherehekeo ya kila mwaka.
13. Fafanua matoleo yaliyotolewa kwa hiari yakiwa zawadi kwa Mungu.
13 Matoleo ya kuchomwa, matoleo ya nafaka, na matoleo ya ushirika ni kati ya matoleo yaliyotolewa kwa hiari yakiwa zawadi au njia ya kumkaribia Mungu ili kupata kibali chake. Wasomi fulani wanaonelea kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa “toleo la kuchomwa” lamaanisha “toleo la kupaa” au “toleo lenye kupaa.” Hiyo ni tafsiri ifaayo kwa sababu toleo la kuchomwa lilipotolewa, mnyama aliyechinjwa alichomwa kwenye madhabahu na harufu tamu, au ya kuburudisha, ikapaa kuelekea mbinguni kwa Mungu. Jambo lililofanya toleo la kuchomwa liwe tofauti ni kwamba baada ya damu yake kunyunyizwa kuzunguka madhabahu, sehemu zote za mnyama huyu zilitolewa kwa Mungu. Makuhani ‘waliziteketeza zote juu ya madhabahu, ili ziwe sadaka ya kuteketezwa [“toleo la kuchomwa,” NW], dhabihu ya kusongezwa kwa njia ya moto, ya harufu ya kupendeza [“kuburudisha,” NW] kwa BWANA.’—Mambo ya Walawi 1:3, 4, 9; Mwanzo 8:21.
14. Toleo la nafaka lilitolewaje?
14 Toleo la nafaka linafafanuliwa kwenye kitabu cha Mambo ya Walawi sura ya 2. Lilikuwa toleo la hiari la unga mwembamba, ambao kwa kawaida ulitiwa mafuta yenye ubani. “[Kuhani] atatwaa konzi moja katika huo unga mwembamba, na katika mafuta yake, na huo ubani wote; kisha kuhani atauteketeza kuwa ndio ukumbusho wake juu ya madhabahu, ni kafara ya kusongezwa kwa njia ya moto, ya harufu ya kupendeza [“kuburudisha,” NW] kwa BWANA.” (Mambo ya Walawi 2:2) Ubani ulikuwa sehemu mojawapo ya uvumba mtakatifu uliochomwa kwenye madhabahu ya uvumba katika tabenakulo na hekalu. (Kutoka 30:34-36) Mfalme Daudi alifikiria hilo aliposema: “Sala yangu ipae mbele zako kama uvumba, kuinuliwa mikono yangu kama dhabihu ya jioni.”—Zaburi 141:2.
15. Dhabihu ya ushirika ilitolewa kwa kusudi gani?
15 Toleo jingine la hiari lilikuwa dhabihu ya ushirika, ambayo yafafanuliwa katika kitabu cha Mambo ya Walawi sura ya 3. Dhabihu ya ushirika yaweza pia kutafsiriwa kuwa “dhabihu ya matoleo ya amani.” Katika Kiebrania, neno “amani” lamaanisha mengi zaidi ya kutokuwa na vita au machafuko. “Katika Biblia, lamaanisha hivyo, na pia lamaanisha hali au uhusiano wenye amani pamoja na Mungu, ufanisi, shangwe, na furaha,” chasema kitabu Studies in the Mosaic Institutions. Hivyo, dhabihu za ushirika zilitolewa si kwa ajili ya kupata amani pamoja na Mungu, kana kwamba kumtuliza, bali ili kushukuru au kusherehekea kwa sababu ya hali nzuri ya amani pamoja na Mungu ambayo hufurahiwa na wale wanaokubaliwa naye. Makuhani na mtoaji walikula dhabihu baada ya kumtolea Yehova damu na mafuta. (Mambo ya Walawi 3:17; 7:16-21; 19:5-8) Katika njia ya mfano na yenye kupendeza, mtoaji, makuhani, na Yehova Mungu walikuwa kana kwamba wanakula pamoja, hilo likionyesha uhusiano wenye amani uliokuwepo miongoni mwao.
16. (a) Kusudi la toleo la dhambi na toleo la hatia lilikuwa nini? (b) Matoleo hayo yalitofautianaje na toleo la kuchomwa?
16 Dhabihu zilizotolewa ili kutafuta msamaha wa dhambi au kufunika ukiukaji wa Sheria zilitia ndani toleo la dhambi na toleo la hatia. Ingawa dhabihu hizi zilichomwa kwenye madhabahu, zilikuwa tofauti na toleo la kuchomwa kwa kuwa mafuta na sehemu fulani za mnyama ndizo zilizotolewa kwa Mungu, bali si mnyama mzima. Mabaki ya mnyama huyo yalitupwa nje ya kambi au wakati mwingine yaliliwa na makuhani. Tofauti hiyo ni muhimu. Toleo la kuchomwa lilikuwa zawadi kwa Mungu ili kufanya iwezekane kumkaribia, hivyo toleo lote lilitolewa kwa Mungu peke yake. Jambo la kutokeza ni kwamba toleo la dhambi au toleo la hatia lilitangulia toleo la kuchomwa, ikidokeza kwamba msamaha wa dhambi ulihitajika ili zawadi ya mtenda-dhambi ikubalike kwa Mungu.—Mambo ya Walawi 8:14, 18; 9:2, 3; 16:3, 5.
17, 18. Toleo la dhambi liliandaliwa kwa sababu gani, na ni kwa kusudi gani matoleo ya hatia yalitolewa?
17 Toleo la dhambi lilikubalika tu kwa ajili ya dhambi isiyo ya kukusudia dhidi ya Sheria, dhambi iliyofanywa kwa sababu ya udhaifu wa mwili. “Kama mtu ye yote akifanya dhambi pasipo kukusudia, katika neno lolote ambalo BWANA amelizuilia lisifanywe,” ndipo mtenda-dhambi angetoa toleo la dhambi kulingana na hadhi, au cheo chake katika jumuiya. (Mambo ya Walawi 4:2, 3, 22, 27) Kwa upande mwingine, watenda-dhambi wasiotubu walikatiliwa mbali; hakukuwa na dhabihu zozote kwa ajili yao.—Kutoka 21:12-15; Mambo ya Walawi 17:10; 20:2, 6, 10; Hesabu 15:30; Waebrania 2:2.
18 Maana na kusudi la toleo la hatia zafafanuliwa katika kitabu cha Mambo ya Walawi sura ya 5 na 6. Huenda mtu akawa alifanya dhambi bila kukusudia. Hata hivyo, huenda ikawa dhambi yake ilimfanya awe na hatia ya kuvunja haki za wanadamu wenzake au za Yehova Mungu, kosa lililopasa kulipizwa au kusahihishwa. Aina kadhaa za dhambi zinatajwa. Baadhi ya dhambi hizo zilikuwa za faragha (5:2-6), nyingine zilikuwa dhambi dhidi ya “mambo matakatifu ya BWANA” (5:14-16), na nyingine, japo kwa kadiri fulani zilikuwa za kukusudia, zilikuwa dhambi zilizotokana na tamaa mbaya au udhaifu wa mwili (6:1-3). Mbali na kutubu dhambi hizo, mkosaji alitakiwa kutoa fidia ikihitajika kisha kutoa toleo la hatia kwa Yehova.—Mambo ya Walawi 6:4-7.
Kuja kwa Kitu Bora
19. Kwa nini Waisraeli walikosa kibali cha Mungu wajapokuwa na Sheria na dhabihu zake?
19 Waisraeli walipewa Sheria ya Kimusa, pamoja na dhabihu na matoleo yake mengi, ili waweze kumkaribia Mungu kusudi wapate na kudumisha kibali na baraka zake hadi Mbegu iliyoahidiwa ifike. Mtume Paulo, Myahudi kwa kuzaliwa, alieleza jambo hilo hivi: “Sheria imekuwa mfunzi wetu ikiongoza kwa Kristo, ili tupate kutangazwa kuwa waadilifu kwa sababu ya imani.” (Wagalatia 3:24) Kwa kusikitisha, Israeli likiwa taifa lilikataa kufunzwa, likatumia vibaya pendeleo hilo. Kwa hiyo, dhabihu zao nyingi zikamchukiza Yehova, aliyesema: “Nimejaa mafuta ya kafara za kondoo waume, na mafuta ya wanyama walionona; nami siifurahii damu ya ng’ombe wala ya wana-kondoo wala ya mbuzi waume.”—Isaya 1:11.
20. Ni nini kilichotukia mwaka wa 70 W.K. kuhusiana na Sheria na dhabihu zake?
20 Mfumo wa mambo wa Wayahudi, pamoja na hekalu lake na ukuhani, ulikoma mwaka wa 70 W.K. Baada ya hilo, haingewezekana kutoa dhabihu kulingana na matakwa ya Sheria. Je, hilo lamaanisha kwamba dhabihu, zikiwa sehemu muhimu ya Sheria, hazina maana yoyote kwa waabudu wa Yehova leo? Tutachunguza jambo hilo katika makala yafuatayo.
[Maelezo ya Chini]
a Kichapo Insight on the Scriptures, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., chaeleza: “Kama litumiwavyo katika Biblia, neno ‘ufuniko’ hasa lamaanisha ‘-funika’ au ‘-badilishana,’ nacho kile kinachotolewa ili kubadilishana na kingine, au kikiwa ‘kifuniko’ cha kingine, lazima kilingane na kinachofunikwa. . . . Ili kufunika ifaavyo kile kilichopotezwa na Adamu, toleo la dhambi lenye thamani inayolingana na uhai mkamilifu wa kibinadamu lingetolewa.”
b Neno la Kiebrania ambalo mara nyingi hutafsiriwa “toleo” ni qor·banʹ. Alipokuwa akiandika juu ya shutumu la Yesu dhidi ya mazoea fulani mabaya ya waandishi na Mafarisayo, Marko alieleza kwamba “korbani” lamaanisha “zawadi iliyowekwa wakfu kwa Mungu.”—Marko 7:11.
-
-
Dhabihu za Sifa Zinazompendeza YehovaMnara wa Mlinzi—2000 | Agosti 15
-
-
Dhabihu za Sifa Zinazompendeza Yehova
‘Toeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu.’—WAROMA 12:1.
1. Biblia inasema nini kuhusu manufaa ya kadiri fulani ya dhabihu zilizotolewa chini ya Sheria ya Kimusa?
“KWA kuwa Sheria ina kivuli cha mambo mema yatakayokuja, lakini si kitu chenyewe hasa cha hayo mambo, watu hawawezi kamwe kwa dhabihu zilezile kutoka mwaka hadi mwaka ambazo wao huzitoa kwa kuendelea kuwafanya wakamilifu wale wakaribiao.” (Waebrania 10:1) Hivyo, kwa taarifa moja yenye kutokeza, mtume Paulo athibitisha kwamba dhabihu zote zilizotolewa chini ya Sheria ya Kimusa hazikuwa na manufaa ya kudumu kuhusiana na wokovu wa mwanadamu.—Wakolosai 2:16, 17.
2. Kwa nini si kazi bure kujaribu kuelewa habari zote katika Biblia kuhusu matoleo na dhabihu za Sheria?
2 Je, hilo lamaanisha kwamba habari iliyomo katika vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia kuhusu matoleo na dhabihu haina manufaa yoyote kwa Wakristo leo? Ni kweli kwamba hivi karibuni, kwa muda uzidio kidogo mwaka mmoja hivi, watu ambao wamejiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walisoma vitabu vitano vya kwanza vya Biblia. Wengine wamejitahidi sana kusoma na kuelewa habari zote. Je, jitihada zao zote zimekuwa za bure? Sivyo kabisa, kwa kuwa “mambo yote yaliyoandikwa wakati wa mbele yaliandikwa kwa kufunzwa kwetu, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Waroma 15:4) Basi, swali ni, Tunapata ‘mafunzo’ na “faraja” gani kutokana na habari katika Sheria zinazohusu matoleo na dhabihu?
Kwa Kufunzwa Kwetu na Faraja
3. Tuna uhitaji gani wa msingi?
3 Ingawa hatuhitajiki kutoa dhabihu halisi kulingana na matakwa ya Sheria, bado tunahitaji sana yale ambayo kwa kadiri fulani dhabihu zilitimizia Waisraeli, yaani kusamehewa dhambi zetu na kufurahia kibali cha Mungu. Tunaweza kupataje manufaa hizo ilhali hatutoi dhabihu halisi? Baada ya kuonyesha upungufu wa dhabihu za wanyama, Paulo atangaza: “Wakati [Yesu] ajapo katika ulimwengu asema: ‘Dhabihu na toleo hukutaka, bali ulinitayarishia mwili. Hukukubalia matoleo mazima ya kuchomwa na toleo la dhambi.’ Ndipo nikasema, ‘Tazama! Nimekuja (katika kikuto cha kitabu imeandikwa juu yangu) ili kufanya mapenzi yako, Ee Mungu.’”—Waebrania 10:5-7.
4. Paulo anatumiaje Zaburi 40:6-8 kumhusu Yesu Kristo?
4 Akinukuu Zaburi 40:6-8, Paulo aonyesha kwamba Yesu hakuja kuendeleza “dhabihu na toleo,” “matoleo mazima ya kuchomwa na toleo la dhambi,” ambazo kufikia wakati ambapo Paulo aliandika, Mungu hakuwa akipendezwa nazo. Badala yake, Yesu alikuja na mwili uliotayarishwa na Baba yake wa mbinguni, mwili ambao ulilingana kabisa na ule ambao Mungu alitayarisha Alipomwumba Adamu. (Mwanzo 2:7; Luka 1:35; 1 Wakorintho 15:22, 45) Akiwa Mwana mkamilifu wa Mungu, Yesu alikuwa ndiye “mbegu” ya mwanamke, kama ilivyotabiriwa kwenye Mwanzo 3:15. Angechukua hatua za ‘kumponda Shetani kichwa,’ ingawa Yesu mwenyewe ‘angepondwa kisigino.’ Kwa njia hiyo, Yesu akawa njia iliyoandaliwa na Yehova kwa ajili ya wokovu wa wanadamu ambao umekuwa ukitazamiwa na watu wa imani tangu wakati wa Abeli.
5, 6. Wakristo wanaweza kumkaribia Mungu kupitia njia gani bora zaidi?
5 Akizungumzia fungu hilo la pekee ambalo Yesu alitimiza, Paulo asema: “Yeye ambaye hakujua dhambi [Mungu] alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili sisi tupate kuwa uadilifu wa Mungu kupitia yeye.” (2 Wakorintho 5:21) Usemi ‘alifanywa kuwa dhambi’ waweza pia kutafsiriwa ‘alifanywa kuwa toleo la dhambi.’ Mtume Yohana asema: “Yeye ni dhabihu yenye kufunika kwa ajili ya dhambi zetu, lakini si kwa ajili ya zetu tu bali pia kwa ajili ya zile za ulimwengu wote.” (1 Yohana 2:2) Hivyo, ingawa Waisraeli walikuwa na njia ya muda ya kumkaribia Mungu kupitia dhabihu zao, Wakristo wana msingi bora zaidi wa kumkaribia Mungu—dhabihu ya Yesu Kristo. (Yohana 14:6; 1 Petro 3:18) Tukidhihirisha imani katika dhabihu ya fidia iliyoandaliwa na Mungu na kumtii Yeye, tunaweza pia kusamehewa dhambi zetu na kufurahia kibali na baraka za Mungu. (Yohana 3:17, 18) Je, hilo si jambo lenye kufariji? Tunaweza kudhihirishaje kwamba tuna imani katika dhabihu ya fidia?
6 Baada ya kueleza kwamba Wakristo wana msingi bora zaidi wa kumkaribia Mungu, mtume Paulo ataja, kama tusomavyo kwenye Waebrania 10:22-25, njia tatu ambazo tunaweza kutumia kudhihirisha imani yetu na uthamini wetu kwa uandalizi wa Mungu wenye upendo. Hata ingawa shauri la Paulo lilikusudiwa wale walio na “njia ya kuingia katika mahali patakatifu”—yaani, Wakristo watiwa-mafuta wenye mwito wa mbinguni—kwa hakika wanadamu wote wanahitaji kuzingatia maneno ya Paulo yaliyopuliziwa ikiwa wanataka kunufaika na dhabihu ya Yesu yenye kufunika.—Waebrania 10:19.
Toa Dhabihu Safi na Zisizo na Unajisi
7. (a) Andiko la Waebrania 10:22 ladhihirishaje kile kilichofanywa wakati wa dhabihu? (b) Ni nini kilichopasa kufanywa ili kuhakikisha kwamba dhabihu ilikuwa yenye kukubalika kwa Mungu?
7 Kwanza, Paulo awahimiza Wakristo hivi: “Acheni tukaribie tukiwa na mioyo ya kweli katika uhakikisho kamili wa imani, mioyo yetu ikiisha kunyunyiziwa kutoka kwenye dhamiri mbovu na miili yetu kuoshwa kwa maji safi.” (Waebrania 10:22) Maneno yanayotumiwa hapa yanaonyesha wazi yale yaliyofanywa wakati wa dhabihu halisi chini ya Sheria. Jambo hilo lafaa kwa sababu ili dhabihu ikubalike, ilipaswa kutolewa kwa sababu ifaayo na ilipaswa iwe safi, isiyo na unajisi. Mnyama aliyetolewa dhabihu alichaguliwa kutoka katika kundi la ng’ombe au la kondoo, yaani, katika wanyama safi, na alikuwa “mkamilifu,” bila kasoro yoyote. Ikiwa dhabihu ya ndege ingetolewa, ingepasa kuwa ya njiwa-tetere au ya makinda wa njiwa. Iwapo matakwa hayo yangetimizwa, ‘dhabihu ingekubaliwa kwa ajili yake, ili kufanya upatanisho kwa ajili yake.’ (Mambo ya Walawi 1:2-4, 10, 14; 22:19-25) Toleo la nafaka halikuwa na chachu yoyote, ambayo yafananisha uchafu; wala halikuwa na asali, yamkini ikimaanisha shira ya matunda, iwezayo kuchachisha. Dhabihu za wanyama au za nafaka zilipotolewa kwenye madhabahu ziliongezwa chumvi, ambayo ni kihifadhi.—Mambo ya Walawi 2:11-13.
8. (a) Mtu anayetoa toleo alihitajika kufanya nini? (b) Tunaweza kuhakikishaje kwamba ibada yetu yakubalika kwa Yehova?
8 Namna gani mtu aliyetoa toleo? Sheria ilisema kwamba yeyote aliyekuja mbele za Yehova alipaswa kuwa safi, asiye na unajisi. Ilimbidi mtu aliyekuwa najisi kwa sababu yoyote ile atoe kwanza toleo la dhambi au la hatia kusudi arudishe msimamo safi mbele za Yehova ili toleo lake la kuchomwa au dhabihu ya ushirika iweze kukubaliwa Naye. (Mambo ya Walawi 5:1-6, 15, 17) Kwa hiyo, je, sisi huthamini umuhimu wa kudumisha msimamo safi mbele za Yehova siku zote? Tukitaka ibada yetu ikubaliwe na Mungu, yatupasa kuchukua hatua upesi kurekebisha ukiukaji wowote wa sheria za Mungu. Yatupasa kuwa wepesi wa kujinufaisha na njia ya kutoa msaada ambayo Mungu ameandaa—“wanaume wazee wa kutaniko” na “dhabihu yenye kufunika kwa ajili ya dhambi zetu,” Yesu Kristo.—Yakobo 5:14; 1 Yohana 2:1, 2.
9. Kuna tofauti gani kuu kati ya dhabihu zilizotolewa kwa Yehova na zile zilizotolewa kwa miungu isiyo ya kweli?
9 Kukaziwa kwa uhitaji wa kutokuwa na unajisi wa aina yoyote ndiko hasa kulikotofautisha dhabihu zilizotolewa kwa Yehova na zile ambazo watu wa mataifa yaliyozunguka Israeli walitolea miungu isiyo ya kweli. Kitabu kimoja cha marejeo chasema hivi kinapoeleza sehemu hii ya pekee ya dhabihu katika Sheria ya Kimusa: “Kuhusu dhabihu katika Sheria ya Kimusa, tunaweza kuona kwamba hakuna jambo linalohusiana na uaguzi au ubashiri; hakuna msisimuko mkubwa wa kidini, kujikatakata, au ukahaba mtakatifu, sherehe zenye ashiki za mambo ya kiuzazi hazikuruhusiwa kabisa; hakuna dhabihu za kibinadamu; hakuna dhabihu kwa ajili ya wafu.” Mambo hayo yote yakazia jambo moja: Yehova ni mtakatifu, naye haruhusu wala hakubali dhambi au uchafu wa aina yoyote. (Habakuki 1:13) Ni lazima ibada na dhabihu tunazomtolea ziwe safi na zisizo na unajisi—kimwili, kiadili, na kiroho.—Mambo ya Walawi 19:2; 1 Petro 1:14-16.
10. Kulingana na ushauri wa Paulo kwenye Waroma 12:1, 2, twapaswa kuchunguza nini juu yetu wenyewe?
10 Kwa kuzingatia hayo, inatupasa kuchunguza sehemu zote za maisha yetu ili tuhakikishe kwamba utumishi wetu unakubalika kwa Yehova. Haitupasi kamwe kufikiri kwamba haidhuru yale tufanyayo katika maisha yetu ya faragha maadamu tu tunashiriki kwa kadiri fulani katika mikutano ya Kikristo na katika huduma. Pia haitupasi kuona kwamba kushiriki katika utendaji wa Kikristo kwa njia fulani hutuondolea uhitaji wa kufuata sheria za Mungu katika sehemu nyingine za maisha yetu. (Waroma 2:21, 22) Hatuwezi kutarajia kubarikiwa na kukubaliwa na Mungu ikiwa tutaruhusu chochote kichafu au chenye unajisi machoni pake kichafue mawazo yetu au matendo yetu. Kumbuka maneno ya Paulo: “Nawasihi sana nyinyi kwa huruma za Mungu, akina ndugu, mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri kuzuri. Na komeni kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe umbo kwa kufanya upya akili yenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—Waroma 12:1, 2.
Toa Dhabihu za Sifa kwa Moyo Wote
11. Usemi “tangazo la hadharani,” unaotajwa kwenye Waebrania 10:23, watia ndani nini?
11 Kisha Paulo akazia sehemu muhimu ya ibada ya kweli, awaandikiapo Waebrania: “Acheni tushike sana tangazo la hadharani la tumaini letu bila kuyumbayumba, kwa maana yeye ni mwaminifu aliyeahidi.” (Waebrania 10:23) Usemi “tangazo la hadharani” kihalisi wamaanisha “ungamo” na Paulo pia ataja “dhabihu ya sifa.” (Waebrania 13:15) Hilo latukumbusha aina ya dhabihu ambayo watu kama Abeli, Noa, na Abrahamu walitoa.
12, 13. Mwisraeli alikiri nini alipotoa dhabihu ya kuchomwa, nasi tunaweza kufanya nini ili kuonyesha roho kama hiyo?
12 Mwisraeli alipotoa dhabihu ya kuchomwa, aliitoa “kwa hiari yake mwenyewe mbele za Yehova.” (Mambo ya Walawi 1:3, NW) Kupitia dhabihu hiyo, alitangaza hadharani, au akakiri kwa hiari, baraka nyingi na fadhili-upendo za Yehova kuelekea watu wake. Kumbuka kwamba jambo lililofanya dhabihu ya kuchomwa iwe ya pekee ni kwamba toleo lote lilichomwa kwenye madhabahu—ufananisho ufaao wa kujitoa kabisa na kujiweka wakfu. Vivyo hivyo, sisi hudhihirisha imani yetu katika dhabihu ya fidia na shukrani zetu kwa uandalizi huo tunapomtolea Yehova kwa hiari na kwa moyo wote “dhabihu [yetu] ya sifa, yaani, tunda la midomo.”
13 Ingawa Wakristo hawatoi dhabihu halisi za wanyama au mboga, wana wajibu wa kutoa ushahidi juu ya habari njema za Ufalme na kufanya wanafunzi wa Yesu Kristo. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Je, wewe hutumia vyema fursa za kutangaza hadharani habari njema za Ufalme wa Mungu ili watu wengi zaidi wapate kujua mambo mazuri ambayo Mungu atawafanyia wanadamu watiifu? Je, unatumia wakati wako na nguvu zako kwa hiari katika kufundisha watu wenye kupendezwa na kuwasaidia wawe wanafunzi wa Yesu Kristo? Kushiriki kwetu kwa bidii katika huduma, kama harufu yenye kuburudisha ya toleo la kuchomwa, kunampendeza Mungu sana.—1 Wakorintho 15:58.
Furahia Ushirika Pamoja na Mungu na Wanadamu
14. Maneno ya Paulo kwenye Waebrania 10:24, 25 yanalinganaje na kusudi la toleo la ushirika?
14 Hatimaye, Paulo avuta fikira kwenye uhusiano wetu na Wakristo wenzetu tunapomwabudu Mungu. “Acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali kutiana moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri mwonavyo siku ikikaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Semi “kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora,” “kukusanyika pamoja sisi wenyewe,” na “kutiana moyo,” zote zatukumbusha kile ambacho toleo la ushirika katika Israeli lilitimizia watu wa Mungu.
15. Twaona ulinganifu gani kati ya dhabihu ya ushirika na mikutano ya Kikristo?
15 Mara kwa mara, usemi “matoleo ya ushirika” hutafsiriwa kuwa “matoleo ya amani.” Hapa neno la Kiebrania linalotafsiriwa “amani” lipo katika wingi, labda likimaanisha kwamba kushiriki katika dhabihu kama hizo hutokeza amani pamoja na Mungu na amani pamoja na waamini wenzetu. Kuhusu dhabihu ya ushirika, msomi mmoja asema: “Kwa kweli hicho kilikuwa kipindi cha ushirika wenye furaha pamoja na Mungu wa Agano, ambamo Alijishusha kuwa Mgeni wa Israeli kwenye chakula cha kidhabihu, huku sikuzote Akiwa Mkaribishaji wao.” Jambo hilo latukumbusha ahadi ya Yesu: “Palipo na wawili au watatu wakiwa wamekusanyika pamoja katika jina langu, hapo mimi nipo katikati yao.” (Mathayo 18:20) Kila tuhudhuriapo mkutano wa Kikristo, sisi hunufaishwa na ushirika wenye kujenga, mafundisho yenye kutia moyo, na kule kujua kwamba Bwana wetu Yesu Kristo yuko pamoja nasi. Hayo hufanya mikutano ya Kikristo iwe yenye kufurahisha na kujenga imani kikweli.
16. Kwa kuzingatia dhabihu ya ushirika, ni nini kifanyacho mikutano ya Kikristo iwe hasa pindi yenye shangwe?
16 Katika dhabihu ya ushirika, mafuta yote—yaliyo kwenye matumbo, figo, na sehemu za ini, na viuno, na vilevile mkia wenye mafuta wa kondoo—yalitolewa kwa Yehova kwa kuchomwa, yakateketezwa kwenye madhabahu ili kufukiza moshi. (Mambo ya Walawi 3:3-16) Mafuta yalionwa kuwa sehemu ya mnyama yenye lishe zaidi na nzuri zaidi. Kuyatoa kwenye madhabahu kulifananisha kumtolea Yehova kilicho bora. Kile ambacho hufanya mikutano ya Kikristo iwe hasa yenye kufurahisha ni kwamba sisi hufundishwa na pia humsifu Yehova. Tunafanya hivyo kwa kushiriki—kadiri tuwezavyo na kwa kiasi—katika kuimba kwa moyo wote, kusikiliza kwa makini, na kutoa maelezo inapowezekana. “Haleluya” akatamka mtunga-zaburi. “Mwimbieni BWANA wimbo mpya, sifa zake katika kusanyiko la watauwa.”—Zaburi 149:1.
Baraka Nyingi Kutoka kwa Yehova Zatungojea
17, 18. (a) Solomoni alitoa dhabihu gani kubwa kwenye mzinduo wa hekalu huko Yerusalemu? (b) Watu walipata baraka gani kutokana na sherehe kwenye mzinduo wa hekalu?
17 Kwenye mzinduo wa hekalu huko Yerusalemu, mwezi wa saba wa mwaka wa 1026 K.W.K., Mfalme Solomoni alitoa “dhabihu kubwa mbele za Yehova,” iliyotia ndani “dhabihu za kuchomwa na toleo la nafaka na vipande vya mafuta vya dhabihu za ushirika.” Mbali na matoleo ya nafaka, jumla ya ng’ombe 22,000 na kondoo 120,000 walitolewa dhabihu wakati huo.—1 Wafalme 8:62-65, NW.
18 Je, unaweza kuwazia gharama na kazi iliyofanywa katika sherehe kubwa hivyo? Hata hivyo, ni wazi kwamba baraka ambazo Waisraeli walipata zilikuwa nyingi sana kushinda gharama waliyopata. Mwishoni kwa sherehe hizo, Solomoni “akaagana na watu, nao wakambarikia mfalme, wakaenda hemani kwao, wakifurahi na kuchangamka moyoni kwa wema wote BWANA aliomfanyia Daudi mtumishi wake, na Israeli watu wake.” (1 Wafalme 8:66) Kwa kweli, kama Solomoni alivyosema, “baraka ya BWANA hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.”—Mithali 10:22.
19. Tunaweza kufanya nini ili kupata baraka nyingi za Yehova sasa na milele?
19 Tunaishi wakati ambapo mahali pa “kivuli cha mambo mema yatakayokuja” pamechukuliwa na “kitu chenyewe hasa cha hayo mambo.” (Waebrania 10:1) Akiwa Kuhani mkubwa halisi wa Cheo cha Juu, Yesu Kristo tayari ameingia mbinguni kwenyewe na kuwasilisha manufaa ya damu yake mwenyewe ili kufunika dhambi za wote wanaodhihirisha imani katika dhabihu yake. (Waebrania 9:10, 11, 24-26) Kwa msingi wa dhabihu hiyo kubwa na kwa kumtolea Mungu kwa moyo wote dhabihu za sifa ambazo ni safi na zisizo na unajisi, sisi pia tunaweza kuendelea ‘kufurahi na kuchangamka moyoni,’ tukitazamia baraka nyingi kutoka kwa Yehova.—Malaki 3:10.
-