Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mambo Yanayowahatarisha Wafanyakazi
    Amkeni!—2002 | Februari 22
    • Mambo Yanayowahatarisha Wafanyakazi

      “Idadi ya watu wanaokufa kazini ni kubwa kuliko ile ya watu wanaokufa kwa sababu ya misiba ya barabarani.” Maneno hayo yaliandikwa kwa herufi nzito kwenye mabango yaliyosambazwa na shirika la WorkCover linaloshughulikia usalama kazini huko New South Wales, Australia.

      PASINA SHAKA, mbali na misiba inayosababisha kifo, kuna mambo mengine yanayowahatarisha wafanyakazi. Kila mwaka, mamilioni ya watu hupata majeraha mabaya sana kazini ambayo hata hubadili maisha yao kabisa. Wengine wengi hufa mapema kwa sababu ya kufanya kazi na kemikali hatari au kwa sababu ya mfadhaiko kazini.

      Kwa kuwa majeraha mabaya na vifo vinavyosababishwa na hali za kikazi hutokea katika karibu aina zote za biashara na viwanda, swali hili lafaa: Uko salama kadiri gani kazini? Ni mambo gani yanayoweza kuhatarisha afya na uhai wako kazini?

      Misongo Kazini

      Mara nyingi, wafanyakazi hulazimishwa kufanya kazi nyingi. Neno karoshi linalomaanisha “kifo kinachosababishwa kwa kufanya kazi kupindukia,” lilitumiwa kwa mara ya kwanza huko Japani wakati familia zilizofiwa zilipodai fidia ya bima. Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa huko miaka mingi iliyopita, asilimia 40 ya watu wanaofanya kazi ofisini huko Japani walihofu kwamba watakufa kwa sababu ya kufanya kazi kupindukia. Wakili mmoja anayehusika na madai ya bima alikadiria kwamba ‘kila mwaka, angalau watu 30,000 huko Japani hufa kwa sababu ya kufanya kazi kupindukia.’

      Polisi huko Japani wamedai kwamba matatizo yanayosababishwa na kazi ni kisababishi kikuu cha ongezeko la visa vya kujiua miongoni mwa watu wenye umri wa miaka 50 hadi 59. Kitabu The Violence-Prone Workplace kilisema kuwa mahakama moja ilimhukumu mwajiri fulani kwa kusababisha mwajiriwa wake ajiue kwa sababu ya matatizo mengi kazini.

      Gazeti la The Canberra Times la Australia lilisema kwamba ‘Sasa Wamarekani ndio watu wanaofanya kazi kwa saa nyingi zaidi ulimwenguni, na hivyo wamewapita Wajapani.’ Hivyo, habari zenye vichwa kama “Watu Wafa kwa Kufanya Kazi kwa Saa Nyingi” zinaonyesha jinsi wafanyakazi waliochoka, kama vile madereva wa ambulansi, marubani, wajenzi, wafanyakazi wanaotoa huduma za usafiri, na watu wanaofanya kazi usiku wanavyofia kazini.

      Makampuni yanapobadili utaratibu na kupunguza idadi ya wafanyakazi ili yaendelee kupata faida, waajiriwa hulazimika kufanya kazi nyingi zaidi. Gazeti la British Medical Journal liliripoti kwamba afya ya waajiriwa huathiriwa wakati idadi ya wafanyakazi inapopunguzwa.

      Ujeuri Kazini

      Wafanyakazi wanaofanya kazi kupindukia na waliofadhaika huhatarisha wafanyakazi wenzao. Uchunguzi uliofanywa huko Uingereza ulionyesha kwamba kila siku watu wengi wanaofanyakazi ofisini hukasirishwa na wafanyakazi wenzao na mara nyingi migogoro hiyo husababisha ujeuri.

      Gazeti la Business Week lilisema kwamba “kila juma, wafanyakazi Wamarekani wapatao 15 huuawa kazini.” Gazeti la Harvard Business Review lasema hivi: “Hakuna mkurugenzi yeyote anayependa kuzungumza kuhusu ujeuri kazini. Lakini ukweli ni kwamba kila mwaka mamia ya wafanyakazi huwashambulia au hata kuwaua wafanyakazi wenzao.”

      Kwa upande mwingine, wafanyakazi wengi huvamiwa kazini na wateja wao. Ripoti moja ya elimu ya jinai kutoka Australia inasema kuwa madaktari fulani huhofu sana kushambuliwa hivi kwamba wanaomba wasindikizwe wanapowatembelea wagonjwa nyumbani. Polisi na walimu wamo hatarini pia.

      Ujeuri mwingine unaotokea kazini ni uchokozi. Shirika la Umoja wa Mataifa la Wafanyakazi huufafanua kuwa ujeuri wa kiakili. Namna moja ya ujeuri huo ni kutendewa kikatili.

      Profesa Robert L. Veninga wa Chuo Kikuu cha Minnesota, Marekani, anaripoti kwamba “mfadhaiko na madhara yake huwaathiri wafanyakazi katika karibu sehemu zote za ulimwengu.” Alisema kwamba “Ripoti ya Wafanyakazi Ulimwenguni ya 1993, iliyotolewa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Wafanyakazi, ilisema kuwa tatizo kuu ni kwamba mfadhaiko husababishwa na mazingira magumu ya kikazi, yanayobadilika-badilika, na mara nyingi yasiyopendeza.”

      Hivyo basi, swali lazuka, Waajiri na waajiriwa wanaweza kufanya nini ili kuwe na usalama kazini? Swali hilo litazungumziwa katika makala ifuatayo.

  • Kufanya Mahala Pako pa Kazi Pawe Salama
    Amkeni!—2002 | Februari 22
    • Kufanya Mahala Pako pa Kazi Pawe Salama

      LICHA ya kuwepo kwa sheria zinazohusu afya na usalama wa wafanyakazi, bado watu wengi hufa na kujeruhiwa kazini. Hivyo basi, ni wazi kwamba sheria pekee haziwezi kuleta usalama kazini. Waajiri na waajiriwa wana jukumu la kujilinda na kuwalinda wengine.

      Kwa hiyo, wafanyakazi wote wanapaswa kuchunguza kwa makini mazingira na mazoea yao ya kikazi. Kwa mfano, je, umewahi kuchunguza iwapo mahala pako pa kazi ni salama? Je, wewe hutumia kemikali zenye sumu kazini? Ikiwa ndivyo, je, wewe hujilinda kabisa? Je, wewe hukabili mfadhaiko sikuzote? Je, wewe hukubali kufanya kazi kwa muda mrefu kuliko vile sheria inavyoruhusu au kufanya kazi inayokiuka mipaka iliyowekwa?

      Majibu yako kwa maswali hayo yataonyesha iwapo uko salama kazini.

      Kufahamu Hatari

      Ni hatari kuendelea kujaribu kufanya kazi kupindukia. Baada ya kuchunguza matokeo ya utafiti uliohusu wafanyakazi milioni 3.6 na mahala 37,200 pa kazi, Profesa Lawson Savery wa Chuo Kikuu cha Curtin huko Australia pamoja na mtafiti mmoja, walichapisha uchunguzi wao wenye kichwa “Je, Ni Hatari Kufanya Kazi kwa Muda Mrefu? na Je, Watu Hukubali Kufanya Hivyo kwa Hiari?” Jibu la maswali hayo ni, ndiyo.

      Wafanyakazi waliochoka hufanya makosa mengi na hawawezi kufanya kazi vizuri. Profesa Savery alisema hivi, kama ilivyoripotiwa katika gazeti la The Sun-Herald la Australia: “Makampuni mengi yaliwatia watu moyo kufanya kazi kupindukia na yalitafuta sana wafanyakazi wa aina hiyo na kuwalipa vizuri.” Matokeo ya kufanya kazi kupindukia yaweza kudhuru sana. Jambo hilo linaonekana sana katika biashara ya usafiri. Madereva hutiwa moyo au hata hulazimishwa kuendesha magari kwa muda mrefu bila kupumzika—jambo ambalo ni kinyume cha sheria katika nchi fulani.

      Mazoea mabaya ya kazi, ambayo yanaweza kutia ndani ukosefu wa utaratibu na usafi, hutokeza hatari nyingine. Majeraha au hata vifo husababishwa mara nyingi kwa kuacha vifaa ovyoovyo sakafuni au nyaya za stima zikiwa hazijafunikwa. Ni hatari pia kupuuza kanuni za usalama unapotumia vifaa na mashine za stima. Jambo jingine linalosababisha watu waumie na kufa, ni kutosafisha sehemu zilizomwagikiwa na umajimaji—hasa umajimaji wenye sumu. Wafanyakazi wengi wamejeruhiwa kwa kuteleza kwenye sakafu zenye maji au mafuta. Hivyo, hatua ya kwanza ya kuwa mfanyakazi bora ni kudumisha mahala pa kazi pakiwa safi na penye utaratibu.

      Hata hivyo, watu wengi huwa na mwelekeo wa kupuuza kanuni za usalama. Jarida la Monthly Labor Review lilisema hivi: “Watu wanapokuwa na kazi nyingi huenda wakafikiri kwamba wanaweza kumaliza kazi haraka kwa kuacha kufuata utaratibu wa kawaida wa kufanya kazi.” Hivyo, huenda wengine wakafikiri kwamba kupuuza kanuni fulani kwafaa kwani hawajawahi kamwe kupata matatizo yoyote kwa kuipuuza. Mkurugenzi mmoja wa kiwanda mwenye ujuzi alisema hivi alipozungumzia jambo hilo: “Mojawapo ya mambo mabaya zaidi ambayo mtu anaweza kufanya kazini ni kupuuza tahadhari na asiumie!” Kwa nini? Kwa sababu mtu asipoumia, hiyo itamfanya awe na uhakika kupita kiasi na asiyejali, hivyo atasababisha misiba mingi zaidi.

      Mlipuko uliotokea kwenye kiwanda cha Chernobyl huko Ukrainia mnamo mwaka wa 1986 husemekana kuwa “msiba mbaya zaidi wa nyukilia ulimwenguni.” Msiba huo ulisababishwa na nini? Ripoti moja kuhusu msiba huo inataja visababishi kama vile ‘kutofuata utaratibu mbalimbali’ na “mazoea ya kupuuza tahadhari.”

      Waajiri na waajiriwa wanaweza kushirikiana kutambua hatari zinazoweza kutokea. Mithali moja yenye hekima katika Biblia, husema hivi: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha.” (Mithali 22:3) Naam, mwenye hekima hutambua mambo yanayoweza kusababisha hatari na kutafuta njia za kujilinda na kuwalinda wengine.

      Waajiri wanapofanya hivyo, wao na vilevile waajiriwa wao hunufaika. Kwa mfano, kampuni moja iliyorekebisha jengo lake la ofisi ili kuepuka magonjwa yanayosababishwa na kemikali zenye sumu kwenye majengo, iligundua kwamba muda si muda ilipata mapato mengi na wafanyakazi wengi walifurahi. Pia, ni wafanyakazi wachache tu waliokosa kufika kazini kwa sababu ya ugonjwa. Kufikiria afya ya wengine kwa njia hiyo hufanya waajiri na waajiriwa wawe na mazingira yenye kupendeza na vilevile hutokeza faida za kiuchumi kama vile mfano huo unavyoonyesha.

      Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, ujeuri umeongezeka kazini. Unaweza kufanya nini ili kujilinda?

      Hatua Unazoweza Kuchukua

      Hata visa vidogo vya uchokozi kazini vimetokeza visa vibaya zaidi vya mnyanyaso. Gazeti la Harvard Business Review linatoa shauri hili: “Unapojaribu kutatua tatizo hilo la ujeuri kazini, fahamu kwamba mara nyingi watu wanaofanya matendo madogo ya ujeuri hufanya matendo makubwa zaidi kama hayo baadaye.”

      Huenda mwanamke asinuie kuwavutia wafanyakazi wengine. Lakini iwapo mwenendo, usemi, na mavazi yake si ya kiasi, wengine wanaweza kufikiri kwamba ana maadili mabaya. Katika siku za karibuni, mwenendo ambao haukukusudiwa kuvutia kingono, nyakati nyingine umetokeza matatizo makubwa kama vile, kufuatwa-fuatwa, kubakwa, au hata kuuawa. Basi fikiria jinsi mavazi na mwenendo wako unavyowaathiri wengine. Tii shauri hili la Biblia: ‘Jirembeni katika mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili.’—1 Timotheo 2:9.

      Gazeti la Monthly Labor Review lilionyesha hali nyingine inayoweza kusababisha hatari, liliposema hivi: “Kuna mahangaiko kuhusu watu wanaofanya kazi peke yao usiku katika maeneo yasiyokuwa na watu.” Hivyo, fikiria hili: Je, ni jambo la hekima ujihatarishe kwa kufanya kazi ukiwa peke yako, hasa usiku sana? Je, kuna faida kujihatarisha ili kupata pesa?

      Ni muhimu pia kufikiria jinsi tunavyotenda wakati tunapokabili tabia zenye kuudhi na za ukatili za wafanyakazi wenzetu waliofadhaika. Ni jambo gani linaloweza kufanywa ili kutuliza hali inayoweza kusababisha hatari? Mithali moja ya Biblia yashauri hivi: “Jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.” (Mithali 15:1) Naam, ukiwa mwenye fadhili na mwenye heshima, utakomesha hali ya kutoelewana na kuepuka mgogoro.

      Katika ulimwengu huu wenye misongo mingi, watu wengi hutenda mambo ya kuudhi na ya kikatili. Ingawa huenda tukadhania kwamba mtu fulani anataka kutuudhi, labda anafanya hivyo tu kwa sababu amefadhaika kwa muda mrefu. Huenda ikawa tumejikuta tu mahala pabaya wakati usiofaa. Basi, jinsi tunavyotenda katika hali hiyo ni muhimu. Matendo yetu yaweza kutuliza au kuzidisha mgogoro.

      Hata hivyo, huenda maoni yakatofautiana. Kitabu Resolving Conflicts at Work chataja jambo hili: ‘Mara nyingi tunapohusika katika mgogoro, hatusemi wazi jinsi tunavyohisi.’ Sababu yaweza kuwa nini? Kitabu hicho kiliendelea kusema hivi: “Migogoro inaweza kutuchanganya na kutuvuruga sana, hivi kwamba tunafikiri kwamba suluhisho ni vita tu.”

      Basi suluhisho ni nini? SIKILIZA! Kitabu kilichonukuliwa kwenye ukurasa uliotangulia chasema hivi: ‘Tukiwasikiliza kabisa watu tunaohitilafiana nao, twaweza kutulia, kuacha mgogoro, na kutafuta masuluhisho.’ Hilo ni shauri zuri la kuzuia kutoelewana kusisitawi na kusababisha mapambano.

      Hivyo basi, tumia busara ili uwe salama. Hiyo yatia ndani kujitahidi kutii kanuni za usalama zilizowekwa. Jambo hilo laweza kusaidia sana kufanya mahala pako pa kazi pawe salama.

      Pia, mtazamo wetu juu ya maisha, kazi, na wasaa wa kustarehe unaweza kuathiri uchaguzi wetu wa kazi na maoni yetu kuhusu usalama. Makala ifuatayo inaweza kutusaidia kufanya uchaguzi unaofaa kuhusiana na hilo.

      [Picha katika ukurasa wa 5]

      Safisha kabisa sehemu zilizomwagikiwa mafuta

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Jawabu la upole laweza kukomesha hali ya kutoelewana

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki