-
Yehova Hatasahau Kazi Yenu Enyi Vijana!Mnara wa Mlinzi—2003 | Aprili 15
-
-
5. (a) Mojawapo ya njia bora zaidi za kuonyesha kwamba moyo wako ni kamili kwa Yehova ni ipi? (b) Kwa nini huenda ikaonekana kuwa vigumu kuwaeleza wengine kuhusu imani yako?
5 Njia moja bora zaidi ya kuonyesha kwamba moyo wako ni kamili kwa Yehova ni kuwaeleza wengine juu yake. Je, umewahi kupata nafasi ya kuwaeleza baadhi ya wanafunzi wenzako kuhusu imani yako? Huenda mwanzoni jambo hilo likaonekana kuwa gumu na pengine ukaogopa kidogo. Huenda ukajiuliza, ‘Vipi wakinicheka au wakiona kwamba dini yangu ni ya kiajabu-ajabu?’ Yesu alisema kwamba si kila mtu atakayesikiliza ujumbe wa Ufalme. (Yohana 15:20) Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba utadhihakiwa na kukataliwa daima. Kinyume cha hilo, vijana wengi Mashahidi wamesikilizwa, na hata wameheshimiwa na wanafunzi wenzao kwa sababu wanaishi kupatana na imani yao.
“Yehova Atakusaidia”
6, 7. (a) Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 17 aliwezaje kuwatolea wanafunzi wenzake ushahidi? (b) Umejifunza nini kutokana na kisa cha Jennifer?
6 Lakini unawezaje kupata ujasiri wa kuzungumza kuhusu imani yako? Mbona usiazimie kusema waziwazi watu wanapokuuliza kuhusu dini yako? Fikiria kisa cha Jennifer mwenye umri wa miaka 17. Anasema hivi: “Tulikuwa tukila chakula cha mchana shuleni. Wasichana walioketi karibu nami walikuwa wakizungumza juu ya dini na mmoja wao akaniuliza mimi ni mfuasi wa dini gani.” Je, Jennifer aliogopa alipojibu? Anasema: “Bila shaka niliogopa kwa sababu sikujua watasema nini.” Kwa hiyo Jennifer alifanya nini? Anaendelea: “Niliwaambia wasichana hao kwamba mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwanza walishangaa. Yaelekea, walifikiri kwamba Mashahidi wa Yehova si watu wa kawaida. Hilo lilifanya waniulize maswali, nami niliweza kusahihisha maoni fulani yasiyofaa waliyokuwa nayo. Hata baada ya siku hiyo, baadhi ya wasichana walinijia mara kwa mara ili kuuliza maswali.”
7 Je, Jennifer alighairi kwamba alizungumza kuhusu imani yake? Hata kidogo! Anasema: “Nilifurahi sana baada ya kipindi hicho cha mapumziko ya mchana. Sasa wasichana hao wanaelewa imani ya Mashahidi wa Yehova vizuri zaidi.” Jennifer anatoa ushauri huu: “Ukiona ni vigumu kuwatolea wanafunzi wenzako au walimu ushahidi toa sala fupi. Yehova atakusaidia. Utafurahi kwamba ulitumia vizuri nafasi hiyo kutoa ushahidi.”—1 Petro 3:15.
8. (a) Sala ilimsaidiaje Nehemia alipokabili hali isiyotazamiwa? (b) Huenda ukahitaji kutoa sala fupi ya moyoni kwa Yehova unapokabili hali zipi shuleni?
8 Ona kwamba Jennifer anapendekeza ‘utoe sala fupi’ kwa Yehova unapopata nafasi ya kutoa ushahidi kuhusu imani yako. Hivyo ndivyo Nehemia, mnyweshaji wa Mfalme Artashasta wa Uajemi, alivyofanya alipokabili hali isiyotazamiwa. Nehemia alionekana kuwa mwenye huzuni kwa sababu alikuwa ameelezwa juu ya hali mbaya ya Wayahudi na kwamba ukuta na malango ya Yerusalemu yalikuwa yameharibika. Mfalme aliona kwamba Nehemia alikuwa na wasiwasi, basi akamwuliza alikuwa na tatizo gani. Kabla ya kumjibu, Nehemia alisali ili kupata mwongozo. Kisha kwa ujasiri akaomba ruhusa ya kurudi Yerusalemu akasaidie kujenga upya jiji lililobomoka. Artashasta alikubali ombi lake. (Nehemia 2:1-8) Unajifunza nini kutokana na hilo? Ukiwa na wasiwasi unapopata nafasi ya kutoa ushahidi kuhusu imani yako, usikose kutoa sala ya moyoni. Petro aliandika hivi: ‘Mtupieni Yehova hangaiko lenu lote, kwa sababu yeye huwajali nyinyi.’—1 Petro 5:7; Zaburi 55:22.
“Tayari Kujitetea”
9. Leah mwenye umri wa miaka 13 aliwezaje kuwaachia wanafunzi wenzake nakala 23 za kitabu Vijana Huuliza?
9 Fikiria kisa kingine. Leah, mwenye umri wa miaka 13, alikuwa akisoma kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazia wakati wa mapumziko ya mchana shuleni. Anasema: “Wanafunzi wengine walikuwa wakinitazama, punde si punde wanafunzi wengi walisimama nyuma yangu na kutazama. Kisha wakaanza kuuliza maswali kuhusu kitabu hicho.” Wasichana wanne walimwomba Leah kitabu Vijana Huuliza siku hiyo. Muda mfupi baada ya hapo wasichana hao walisoma vitabu hivyo pamoja na wengine, kisha hao pia wakataka nakala zao. Leah aliwaachia wanafunzi wenzake na marafiki wake nakala 23 za kitabu Vijana Huuliza katika majuma machache yaliyofuata. Je, ilikuwa rahisi kwa Leah kutoa ushahidi hapo mwanzoni wengine walipomwuliza juu ya kitabu alichokuwa akisoma? Sivyo! Anasema hivi: “Mwanzoni, nilikuwa na wasiwasi. Hata hivyo, nilisali, na nilijua kwamba Yehova alikuwa pamoja nami.”
10, 11. Msichana mdogo Mwisraeli aliwezaje kumsaidia mkuu wa jeshi la Siria ajifunze kumhusu Yehova, na mtu huyo alifanya mabadiliko gani baadaye?
10 Huenda kisa cha Leah kikakukumbusha hali iliyompata msichana mdogo Mwisraeli aliyepelekwa utekwani huko Siria. Mkuu wa jeshi la Siria, Naamani, alikuwa mwenye ukoma. Inawezekana kwamba mke wake ndiye aliyeanzisha mazungumzo yaliyomsukuma huyo msichana mdogo kumweleza imani yake. Alisema: “Laiti bwana wangu angekuwa pamoja na yule nabii aliyeko Samaria! Maana angemponya ukoma wake.”—2 Wafalme 5:1-3.
11 Kwa sababu ya ujasiri wa msichana huyo mdogo, Naamani alipata kujua kwamba “hakuna Mungu duniani mwote, ila katika Israeli.” Hata aliazimia kwamba ‘hangetoa tena sadaka ya kuteketezwa wala dhabihu kwa miungu mingine, ila kwa BWANA.’ (2 Wafalme 5:15, 17) Bila shaka Yehova alibariki tendo la ujasiri la msichana huyo mdogo. Anaweza, na anataka kuwabariki vijana leo pia. Leah amepata baraka kama hizo. Baada ya muda mfupi, baadhi ya wanafunzi wenzake walimwendea na kumwambia kwamba kitabu Vijana Huuliza kimewasaidia kufanya mabadiliko katika mwenendo wao. Leah anasema, “Nilifurahi kwa sababu nilijua kwamba nilikuwa nikiwasaidia wengine wajifunze kumhusu Yehova na kufanya mabadiliko maishani.”
12. Unawezaje kuimarishwa kutetea imani yako?
12 Wewe pia unaweza kupata matokeo mazuri kama Jennifer na Leah. Fuata ushauri wa Petro, aliyeandika kwamba sikuzote Mkristo anapaswa kuwa ‘tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hudai kwake sababu ya tumaini lililo katika yeye, akifanya hivyo kwa tabia-pole na staha yenye kina kirefu.’ (1 Petro 3:15) Unawezaje kufuata ushauri huo? Iga mfano wa Wakristo wa karne ya kwanza waliomwomba Yehova awasaidie kuhubiri “kwa ujasiri wote.” (Matendo 4:29) Kisha uwe na ujasiri unapozungumza na wengine juu ya imani yako. Huenda ukapata matokeo mazuri kuliko ulivyotazamia. Isitoshe, utaufurahisha moyo wa Yehova.
Video na Miradi Hususa
13. Vijana fulani wametumia nafasi zipi ili kutoa ushahidi? (Ona masanduku kwenye ukurasa wa 20 na 21.)
13 Vijana wengi wamewaeleza wanafunzi wenzao au walimu imani yao kwa kutumia video. Nyakati nyingine, wamepata nafasi ya kumsifu Yehova kupitia miradi mbalimbali ya shule. Kwa mfano, wavulana wawili wenye umri wa miaka 15, ambao ni Mashahidi wa Yehova, waliambiwa waandike ripoti katika somo lao la historia kuhusu mojawapo ya dini za ulimwengu. Wavulana hao walishirikiana kuandika ripoti kuwahusu Mashahidi wa Yehova wakitumia habari iliyo katika kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu.b Pia, walipaswa kutoa hotuba ya dakika tano. Baadaye, mwalimu na wanafunzi walikuwa na maswali mengi sana hivi kwamba wavulana hao waliendelea na mazungumzo darasani kwa dakika nyingine 20. Kwa majuma kadhaa baadaye, wanafunzi waliendelea kuuliza maswali kuwahusu Mashahidi wa Yehova!
14, 15. (a) Kwa nini kuwaogopa wanadamu ni mtego? (b) Kwa nini unapaswa kuwaelezea wengine imani yako bila woga?
14 Kama inavyoonyeshwa na visa hivyo, unaweza kupata baraka nyingi kwa kuwaeleza wengine juu ya imani yako ukiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Usipoteze pendeleo na shangwe ya kuwasaidia wengine wamjue Yehova kwa sababu ya kuwaogopa wanadamu. Biblia inasema: “Kuwaogopa wanadamu huleta mtego; bali amtumainiye BWANA atakuwa salama.”—Mithali 29:25.
15 Kumbuka kwamba ukiwa kijana Mkristo, una kitu fulani ambacho vijana wenzako wanahitaji sana, yaani, maisha bora sasa na ahadi ya kuishi milele wakati ujao. (1 Timotheo 4:8) Ijapokuwa huenda ukafikiri kwamba watu hawapendezwi na dini nchini Marekani, jambo la kupendeza ni kwamba kura ya maoni ilionyesha kuwa nusu ya vijana nchini humo wanapendezwa sana na dini, na theluthi moja wanasema kwamba dini ni ‘muhimu sana maishani mwao.’ Yaelekea ndivyo ilivyo katika sehemu nyinginezo ulimwenguni. Kwa hiyo huenda wanafunzi wenzako wakafurahia kusikiliza mambo unayowaeleza kuhusu Biblia.
-
-
Yehova Hatasahau Kazi Yenu Enyi Vijana!Mnara wa Mlinzi—2003 | Aprili 15
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]
Hali Fulani Ambazo Wengine Wametumia Kueleza Imani Yao
Wanapopewa mgawo wa kutayarisha ripoti au kufanya mradi fulani shuleni, wengine wamechagua habari itakayowapatia nafasi ya kutoa ushahidi
Vijana kadhaa wamempa mwalimu wao video, kitabu, au gazeti linalohusu habari ambayo itazungumziwa darasani
Vijana fulani waliokuwa wakisoma Biblia au kitabu ambacho kinazungumzia Biblia wakati wa mapumziko, wamefikiwa na vijana wengine na kuulizwa maswali
-