-
Mgogoro Kati ya Sayansi na DiniAmkeni!—2002 | Juni 8
-
-
Mgogoro Kati ya Sayansi na Dini
“Je, dini ni ugonjwa wa akili ambao unaenea?”—Mwanabiolojia Richard Dawkins.
NYAKATI nyingine, watu huona kwamba dini na sayansi hazipatani kabisa. Wengine huonelea kwamba kuna mgogoro mkubwa sana kati ya mambo hayo mawili hivi kwamba huenda jambo moja litashinda endapo tu jambo lile jingine litatokomea.
Wanasayansi fulani, kama vile mtaalamu wa kemia Peter Atkins, wanaona kwamba “haiwezekani” kupatanisha dini na sayansi. Atkins anasema kwamba kuamini “kuwa kuwapo kwa Mungu kunajibu maswali (yoyote, sembuse maswali yote) ni jambo la upumbavu kabisa.”
Kwa upande mwingine wanadini wanalalamika kwamba sayansi imedhoofisha imani ya watu. Watu hao huamini kwamba sayansi ya kisasa ina udanganyifu; huenda maelezo ya kisayansi yakawa kweli, lakini imani ya wanadini hudhoofishwa wakati maelezo hayo yanapofafanuliwa kimakosa. Kwa mfano, mwanabiolojia William Provine anasema kuwa nadharia ya mageuzi huonyesha kwamba “hakuna msingi thabiti wa maadili; hakuna kusudi muhimu maishani.”
Hata hivyo, sehemu fulani ya mgogoro huo imesababishwa na madai ya uwongo au yasiyoweza kuthibitishwa kutoka pande hizo mbili. Kwa karne nyingi, viongozi wa dini wamefundisha hekaya na mafundisho ya uwongo ambayo hayapatani na ugunduzi wa kisasa wa sayansi wala na Maandiko yaliyoongozwa na Mungu. Kwa mfano, Kanisa Katoliki lilimshutumu Galileo kwa sababu alikata kauli, ya kweli, kwamba dunia inazunguka jua. Maoni ya Galileo hayakupinga Biblia, lakini yalikuwa tofauti na mafundisho ya kanisa ya wakati huo. Kwa upande mwingine, wanasayansi wanakosea wanapofundisha ile nadharia ambayo haijathibitishwa kuwa ya kweli inayosema kwamba uhai ulitokana na kitu kisichokuwa na uhai na si kutoka kwa Mungu. Wao hudhihaki mafundisho ya kidini wakisema kwamba hayapatani na sayansi.
Basi, je, inawezekana kupatanisha sayansi na dini? Naam, inawezekana. Kwa kweli, sayansi iliyothibitishwa kuwa ya kweli na dini ya kweli hukamilishana badala ya kupingana.
-
-
Chanzo cha Ulimwengu na Uhai Ni Nini?Amkeni!—2002 | Juni 8
-
-
Chanzo cha Ulimwengu na Uhai Ni Nini?
‘Sayansi haina nguvu bila dini, dini bila sayansi imepungukiwa.’—Albert Einstein.
HIZI ni siku zenye kustaajabisha sana kuliko wakati mwingine wowote. Ugunduzi mpya huko angani unawalazimu wataalamu wa nyota kubadili maoni yao kuhusu chanzo cha ulimwengu wetu. Watu wengi wanastaajabishwa na ulimwengu na wanauliza maswali ambayo yameulizwa tangu zamani kuhusu kuwapo kwetu ndani yake: Ulimwengu na uhai ulitokeaje, na kwa nini ulitokea?
Hata tukichunguza miili yetu kupatana na uchunguzi uliofanywa hivi karibuni kuhusu chembe za urithi, maswali haya yanazuka: Viumbe wengi tofauti-tofauti waliumbwaje? Ikiwa kuna mtu aliyewaumba, mtu huyo ni nani? Rais mmoja wa Marekani alisema hivi kuhusu namna ambavyo chembe zetu za urithi zimeundwa kwa njia tata sana: ‘Tunajifunza jinsi Mungu alivyoumba viumbe.’ Mmojawapo wa wanasayansi wakuu waliohusika katika uchunguzi huo wa chembe za urithi alisema hivi kwa unyenyekevu: “Tumegundua habari chache kuhusu chembe zetu za urithi ambazo hapo awali ni Mungu tu aliyezijua.” Lakini maswali haya hayajajibiwa—uhai ulitokeaje, na kwa nini ulitokea?
“Madirisha Mawili”
Wanasayansi fulani wanasema kwamba utaratibu unaotumiwa kuendesha ulimwengu unaweza kuelezwa kwa kutumia akili, bila kutumia hekima ya Mungu. Lakini watu wengi, kutia ndani wanasayansi, wana mashaka kuhusu maoni hayo. Wanajaribu kuelewa ukweli wa mambo kwa kuchunguza sayansi na vilevile dini. Wanaonelea kwamba sayansi inaeleza jinsi ambavyo uhai na ulimwengu ulivyotokea, na dini inaeleza kwa nini vitu hivyo vilitokea.
Akizungumzia mbinu hiyo ya kuchunguza pande zote mbili, mwanafizikia Freeman Dyson alisema hivi: “Sayansi na dini ni kama madirisha mawili ambayo watu wanachungulia wanapojaribu kuelewa ule ulimwengu mkubwa huko nje.”
Mwandishi William Rees-Mogg alisema hivi: ‘Sayansi inashughulika na mambo yanayoweza kupimwa, na dini inashughulika na mambo yasiyoweza kupimwa. Sayansi haiwezi kuthibitisha kwamba kuna Mungu wala haiwezi kuthibitisha kwamba hakuna Mungu, sawa na jinsi ambavyo haiwezi kuthibitisha ubora wala ubaya wa maadili au sanaa. Hakuna sababu ya kisayansi ya kumpenda jirani au kuheshimu uhai wa mwanadamu. Ni kosa kubwa sana kusema kwamba ikiwa sayansi haiwezi kuthibitisha jambo fulani basi jambo hilo halipo. Hilo lingemaanisha kuwa karibu mambo yote muhimu maishani hayapo, kama vile Mungu, utu wa mwanadamu, upendo, ushairi, na muziki.’
Mafundisho ya Sayansi
Mara nyingi watu huamini nadharia za wanasayansi bila kuwa na uthibitisho wowote. Kwa mfano, kuhusiana na chanzo cha uhai, watu wengi wanaoamini mageuzi hushikilia maoni ambayo hayajathibitishwa na sayansi. Mambo yaliyothibitishwa huunganishwa na nadharia mbalimbali. Na wanasayansi wanapotumia mamlaka yao kuwalazimisha watu waamini nadharia ya mageuzi bila uthibitisho, wao humaanisha hivi: ‘Kwa kuwa wewe ulitokana na utendaji wa kibiolojia, wa kikemia, au wa kifizikia tu, huna wajibu wowote kuhusu mwenendo wako.’ Mwanabiolojia Richard Dawkins anasema kwamba katika ulimwengu ‘hakuna ubunifu, kusudi, uovu wala wema, hakuna chochote ila kutojali.’
Ili kudumisha maoni yao, wanasayansi fulani hupuuza uchunguzi mwingi ambao umefanywa na wanasayansi wengine wanaopinga mambo ya msingi kuhusu nadharia zao juu ya chanzo cha uhai. Hata mabilioni ya miaka ikipita, imethibitika wazi kwamba haiwezekani kwa molekuli tata kujifanyiza zenyewe kisha zitokeze chembe yenye uhai inayofanya kazi.a Hivyo, nadharia kuhusu chanzo cha uhai zinazopatikana katika vitabu vingi zinapasa kuonwa kuwa za uwongo.
Kuamini kwamba uhai ulijitokeza kunahitaji imani nyingi zaidi kuliko kuamini katika uumbaji. David Block, ambaye ni mtaalamu wa nyota, alisema hivi: ‘Mtu asiyemwamini Muumba anahitaji imani nyingi zaidi kuliko mtu anayemwamini. Mtu anaposema kwamba hakuna Mungu, anatoa taarifa isiyo na msingi wowote—kauli isiyothibitishwa ambayo inategemea imani tu.’
Uvumbuzi wa kisayansi unaweza kuwafanya wanasayansi fulani kuwa na kicho. Albert Einstein alikubali hivi: ‘Si rahisi kumpata mwanasayansi mwenye akili nyingi sana ambaye hana hisia fulani ya kidini. Hisia hiyo ya kidini yaweza kuonekana kwa jinsi anavyostaajabia sana upatano wa mambo ya asili, ambao unaonyesha kwamba ulifanyizwa kwa akili nyingi sana. Matendo ya mwanadamu na uwezo wake wote wa kufikiri ni mdogo sana unapolinganishwa na akili hiyo.’ Hata hivyo, jambo hilo haliwachochei wanasayansi kumwamini Muumba, Mungu mwenye utu.
Mipaka ya Sayansi
Inafaa kuheshimu kwa njia inayofaa maarifa na mafanikio ya sayansi. Hata hivyo, wengi watakubali kwamba ijapokuwa sayansi ni njia ya kupata maarifa, hiyo siyo njia pekee ya kupata maarifa. Kusudi la sayansi ni kueleza matukio ya asili na kusaidia kuonyesha jinsi matukio hayo yanavyotokea.
Sayansi hutuwezesha kuelewa kwa undani ulimwengu wa maumbile, yaani, kila kitu kinachoonekana. Lakini hata uchunguzi wa sayansi uwe wa hali ya juu jinsi gani, hauwezi kamwe kuonyesha kusudi la kuwepo kwa ulimwengu.
Mwandishi Tom Utley anasema hivi: ‘Kuna maswali fulani ambayo wanasayansi hawawezi kamwe kuyajibu. Huenda ikawa mlipuko mkubwa ulitukia miaka bilioni 12 iliyopita na hivyo ulimwengu ukaanza. Lakini kwa nini mlipuko huo ulitukia? Chembe zilizolipuka zilitoka wapi? Ni nini kilichokuwapo kabla ya tukio hilo?’ Utley amalizia hivi: “Inaonekana . . . wazi kwamba sayansi haitaweza kamwe kujibu maswali yote ya wanadamu.”
Badala ya kuthibitisha kwamba hakuna Mungu, maarifa ya sayansi ambayo yamepatikana kupitia uchunguzi kama huo yamethibitisha kwamba ulimwengu tunamoishi ni wa ajabu sana, una utata mwingi, na unatia kicho. Watu wengi wenye akili wanaona kwamba ni jambo linalofaa kukata kauli kuwa kanuni za mambo ya asili, utendaji wa kemikali, DNA, na unamna-namna wa viumbe unaonyesha wazi kwamba kuna Muumba. Hakuna uthibitisho unaopinga kauli hiyo.
“Imani Ni Halisi”
Iwapo kuna Muumba aliyeumba ulimwengu, basi hatuwezi kutazamia kumfahamu au kujua makusudi yake kwa kutumia darubini, hadubini, au vifaa vingine vya kisayansi. Hebu fikiria mfano wa mfinyanzi na chombo cha maua ambacho amefanyiza. Hata ukichunguza chombo hicho kadiri gani, hutaweza kamwe kujua kwa nini kilitengenezwa. Ili kupata jibu, ni lazima tumuulize mfinyanzi.
Mwanabiolojia wa molekuli Francis Collins anaeleza jinsi ambavyo imani na mambo ya kiroho yanavyoweza kujibu maswali yasiyoweza kujibiwa na sayansi: “Siwezi kutazamia dini ieleze muundo wa chembe za urithi za mwanadamu, na vilevile siwezi kutazamia sayansi ifundishe kuhusu mambo ya kiroho yasiyoonekana. Lakini ninaonelea kwamba sayansi haijibu kikamili maswali muhimu, kama vile ‘Ni nini kusudi la uhai?’ au ‘Kwa nini wanadamu wanapenda mambo ya kiroho?’ Mambo mengi ya ushirikina yametokea na kupotea. Imani imedumu, na hilo linaonyesha kwamba imani ni halisi.”
Sababu ya Kutokea kwa Ulimwengu na Uhai
Zaidi ya kuonyesha kusudi la uhai na kwa nini ulimwengu ulitokea, dini ya kweli hutoa pia kanuni za maadili, na vilevile mwongozo maishani. Mwanasayansi Allan Sandage alieleza jambo hilo hivi: “Sihitaji kusoma kitabu cha biolojia ili nijue jinsi ya kuishi.”
Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanahisi kwamba wamegundua namna wanavyoweza kujua jinsi ya kuishi vizuri. Pia, wanahisi kwamba wamepata majibu yenye kuridhisha kwa maswali haya: Kwa nini tuko hai? Na ni nini kitakachotokea wakati ujao? Majibu yapo. Yapo wapi? Katika kitabu kitakatifu na cha kale zaidi ambacho kimesambazwa zaidi ya kitabu kingine chochote, Biblia.
Biblia inatueleza kwamba Mungu aliumba dunia kwa ajili ya wanadamu hasa. Isaya 45:18 inasema hivi kuhusu dunia: “Mungu . . . hakuiumba ukiwa, [lakini] aliiumba ili ikaliwe na watu.” Na aliweka kila kitu ambacho wanadamu wangehitaji duniani, si ili waishi tu bali ili wafurahie maisha kabisa.
Wanadamu waliagizwa watunze dunia, ‘wailime na kuitunza.’ (Mwanzo 2:15) Biblia pia inaeleza kuwa ujuzi na hekima ni zawadi kutoka kwa Mungu na kwamba tunapaswa kuwatendea wengine kwa upendo na haki. (Ayubu 28:20, 25, 27; Danieli 2:20-23) Hivyo, maisha ya wanadamu yanaweza kuwa na kusudi iwapo tu watatambua na kukubali yale ambayo Mungu amekusudia kwa ajili yao.b
Mtu mwenye akili leo anaweza kufanya nini ili kukubali maoni ya kisayansi na vilevile ya kidini? Ni kanuni zipi zinazoweza kumsaidia mtu kufanya hivyo?
[Maelezo ya Chini]
a Ona sura ya 3 yenye kichwa “Uhai Ulianzaje?” katika kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
b Ili kupata habari kamili, ona broshua Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai? Wewe Waweza Kulipataje?, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]
Maoni ya Wanasayansi Fulani
Watu fulani hufikiri kwamba wanasayansi wengi huepuka kuzungumzia mambo ya kiroho na ya kidini kwa sababu wao si wanadini au hawapendi kujihusisha katika mjadala kati ya sayansi na dini. Naam, wanasayansi wengine wana maoni hayo, lakini si wote. Hebu ona maoni yafuatayo ya wanasayansi.
“Ulimwengu ulikuwa na mwanzo fulani lakini wanasayansi hawawezi kueleza kwa nini ulitokea. Mungu ndiye aliyeuumba.” “Mimi huiona Biblia kuwa kitabu cha kweli kutoka kwa Mungu. Bila shaka kuna mtu mwenye akili aliyeanzisha uhai.”—Ken Tanaka, mwanajiolojia wa mambo ya sayari kwenye Taasisi ya Uchunguzi wa Jiolojia ya Marekani.
“Wanadamu ndio wamesababisha tofauti kati ya ujuzi mbalimbali (wa kisayansi na wa kidini). . . . Ujuzi kumhusu Muumba na ujuzi kuhusu uumbaji unahusiana sana.”—Enrique Hernández, mtafiti na profesa kwenye Idara ya Fizikia na Nadharia ya Kemia ya Chuo Kikuu cha Kitaifa cha Mexico.
‘Tunapoendelea kujua zaidi juu ya habari hizi zote [kuhusu chembe za urithi za mwanadamu], tutaona utata uliopo na jinsi zote zinavyohusiana. Itaonyesha kwamba kuna muumba mwenye akili, yaani, nguvu fulani au mtu mwenye akili.’—Duane T. Gish, mtaalamu wa biokemia.
“Sayansi na dini zinapatana. Zote zinatafuta ukweli mmoja. Sayansi inaonyesha kwamba kuna Mungu.”—D.H.R. Barton, profesa wa kemia, Texas.
[Hisani]
NASA/U.S. Geological Survey
Picha: www.comstock.com
NASA and The Hubble Heritage Team (STScI/AURA)
[Picha katika ukurasa wa 5]
Je, uchunguzi wa kisayansi unaweza kutuonyesha kusudi la uhai?
[Hisani]
Courtesy Arecibo Observatory/David Parker/Science Photo Library
[Picha katika ukurasa wa 6]
Nyota kwenye ukurasa wa 2, 3, 5, na juu kwenye ukurasa wa 7: National Optical Astronomy Observatories
-
-
Kupatanisha Sayansi na DiniAmkeni!—2002 | Juni 8
-
-
Kupatanisha Sayansi na Dini
“Siku hizi watu wanaonelea kwamba sayansi na dini zinaweza kupatanishwa.”—Gazeti la The Daily Telegraph la London la Mei 26, 1999.
SAYANSI na dini inayofaa hutafuta ukweli. Uvumbuzi wa sayansi hufunua ulimwengu wenye utaratibu wa hali ya juu, ulimwengu unaoonyesha wazi kwamba ulibuniwa na mtu mwenye akili. Dini ya kweli hufanya uvumbuzi huo uwe na maana kwa kufundisha kwamba Muumba mwenye akili ndiye aliyebuni ulimwengu.
Francis Collins, ambaye ni mwanabiolojia wa molekuli, anasema hivi: ‘Ninaona kwamba uelewevu wangu wa sayansi unaongezwa sana na dini. Ninapogundua jambo fulani kuhusu chembe za urithi za mwanadamu, ninahisi kicho kuhusu utata wa uhai, nami hujiambia hivi, “Lo! Ni Mungu tu aliyejua jambo hilo.” Hisia hiyo ni nzuri ajabu na inanichochea, nayo hunisaidia kumthamini Mungu na kufanya sayansi ipendeze hata zaidi.’
Ni nini kinachoweza kumsaidia mtu kupatanisha sayansi na dini?
Ni Jambo Linaloendelea
Kubali mipaka iliyopo: Yaonekana tutaendelea kujifunza kuhusu ulimwengu, anga, na wakati usio na kikomo. Mwanabiolojia Lewis Thomas alisema hivi: ‘Kujifunza hakutakoma, kwani wanadamu hupenda sana kujua, kupeleleza, kuchunguza na kujaribu kuelewa mambo. Hatutajua kamwe mambo yote. Sifikiri kutakuwa na wakati ambapo kila mtu ataweza kusema kwamba anajua kila kitu. Wanadamu hawataweza kamwe kuelewa mambo hayo.’
Vivyo hivyo, tamaa ya kufahamu kweli ya kidini haina kikomo. Paulo, mmoja wa waandikaji wa Biblia, alisema hivi: “Tunachoona sasa ni kama tu sura hafifu katika kioo . . . Sasa ninajua kiasi fulani tu.”—1 Wakorintho 13:12, Biblia Habari Njema.
Hata hivyo, ujuzi wa kiasi tu kuhusu sayansi na dini hauwezi kutuzuia kukata kauli zinazofaa ambazo zinategemea mambo ya kweli tunayofahamu. Hatuhitaji kujua mengi sana kuhusu chanzo cha jua ili tuwe na uhakika kabisa kwamba litachomoza kesho.
Fikiria ukweli wa mambo: Tunapotafuta majibu, tunahitaji kuongozwa na kanuni sahihi. Tusipoamini tu uthibitisho unaotegemeka kabisa, itakuwa rahisi kupotoshwa tunapotafuta ukweli wa kisayansi na wa kidini. Ni kweli kwamba hakuna mtu yeyote anayeweza kuanza kuchunguza dhana zote na maarifa yote ya kisayansi yanayopatikana katika maktaba kubwa-kubwa za leo. Kwa upande mwingine, Biblia ni kitabu ambacho kina mafundisho ya kiroho kwa ajili yetu na ni rahisi kukichunguza. Habari za Biblia zimethibitishwa kuwa za kweli.a
Hata hivyo, kuhusiana na ujuzi wa aina yoyote ile, mtu anahitaji kujitahidi sana kutofautisha kati ya ukweli wa mambo na mambo ya kukisia, kati ya mambo halisi na ya uwongo—iwe ni katika sayansi au dini. Kama vile Paulo, mwandikaji wa Biblia, alivyoshauri, tunahitaji kukataa “mapinganisho yenye kuitwa ‘ujuzi’ isivyo kweli.” (1 Timotheo 6:20) Ili kupatanisha sayansi na Biblia, ni lazima tuchunguze ukweli wa mambo na kuepuka makisio, na kuchunguza jinsi mambo ya kweli yanavyopatana.
Kwa mfano, tunapoelewa kwamba Biblia hutumia usemi “siku” ili kuwakilisha vipindi mbalimbali vya wakati, basi tunaona kwamba simulizi la Mwanzo kuhusu siku sita za uumbaji halipingani na maelezo ya kisayansi yanayosema kwamba dunia imekuwapo kwa miaka bilioni nne na nusu hivi iliyopita. Kulingana na Biblia, dunia ilikuwapo kwa muda usiojulikana kabla ya siku za uumbaji kuanza. (Ona sanduku “Je, Kila Siku ya Uumbaji Ilikuwa na Saa 24 Tu?”) Hata wanasayansi wakirekebisha maelezo yao na kuonyesha kwamba dunia iliumbwa katika kipindi tofauti na hicho, bado maelezo ya Biblia ni ya kweli. Katika visa vingi kama hivyo, sayansi haipingi Biblia bali inatoa habari nyingi za ziada kuhusu ulimwengu wa sasa na pia ule wa zamani.
Imani, si kuamini mambo bila uthibitisho: Biblia hutupatia ujuzi juu ya Mungu na makusudi yake ambayo hayapatikani mahali pengine popote. Kwa nini tuamini Biblia? Biblia yenyewe inatutia moyo tuichunguze ili tuone ikiwa ni sahihi. Hebu fikiria masimulizi yake ya kweli ya historia, jinsi inavyoweza kutusaidia maishani, unyoofu wa waandikaji wake, na jinsi ilivyoandikwa kwa usahihi. Mtu anapochunguza usahihi wa Biblia, kutia ndani taarifa zake zinazohusu mambo ya sayansi, na hata mamia ya unabii ambao umetimia kabisa zamani na katika wakati huu, anaweza kuiamini kwa uhakika kuwa Neno la Mungu. Kwa kuwa taarifa za Maandiko zimethibitishwa, kuamini Biblia si kuamini mambo bila uthibitisho bali ni kuwa na uhakika kwamba taarifa hizo ni sahihi.
Heshimu sayansi: tambua thamani ya imani ya kidini: Mashahidi wa Yehova wanawaomba watu wanaoweza kukubali maoni mapya, iwe ni wanasayansi au wanadini, kutafuta ukweli kwa bidii katika pande zote mbili. Katika makutaniko yao, Mashahidi huwatia watu moyo kuheshimu sayansi na uthibitisho wa kisayansi kwa njia inayofaa na pia kuamini kabisa kwamba ukweli wa kidini unaweza kupatikana tu katika Biblia, ambayo inasema waziwazi na kwa uthibitisho mwingi kwamba hiyo ni Neno la Mungu. Mtume Paulo alisema hivi: “Mlipopokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.
Kwa wazi, sawa na sayansi, uwongo na mazoea yenye kudhuru yameingizwa katika dini. Kwa hiyo, kuna dini ya kweli na dini ya uwongo. Hiyo ndiyo sababu watu wengi wameacha dini za kawaida na kuwa washiriki wa kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova. Wamekata tamaa kwa sababu dini walizoshirikiana nazo hapo awali zilikataa kufuata ukweli na badala yake kufuata mapokeo na mafundisho ya uwongo ya wanadamu.
Zaidi ya hilo, Wakristo wa kweli hupata kusudi halisi maishani kwa kutegemea ujuzi mwingi kumhusu Muumba na makusudi yake kwa ajili ya wanadamu na dunia yetu, kama inavyoelezwa katika Biblia. Mashahidi wa Yehova wameridhika na majibu ya Biblia yenye kupatana na akili kuhusu maswali kama vile, Kwa nini tuko hai? Wakati ujao utakuwaje? Watafurahi sana kukueleza habari hizo.
[Maelezo ya Chini]
a Ona kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Sanduku katika ukurasa wa 10]
Je, Kila Siku ya Uumbaji Ilikuwa na Saa 24 Tu?
Watu fulani wenye imani kali ya kidini wanasema kwamba vitu vyote vinavyoonekana viliumbwa katika kipindi cha siku sita tu kati ya miaka 6,000 na 10,000 iliyopita, na kila siku ilikuwa na saa 24. Lakini kwa kufanya hivyo, wanaendeleza fundisho lisilopatana na Maandiko ambalo limewafanya watu wengi kuidharau Biblia.
Je, kila wakati ambapo Biblia inataja siku moja huwa inamaanisha kipindi cha saa 24? Mwanzo 2:4 inasema kuhusu “siku ile BWANA Mungu alipoziumba mbingu na nchi.” Siku hiyo moja inatia ndani siku zote sita za uumbaji zinazotajwa kwenye Mwanzo sura ya 1. Biblia hutumia neno siku kuonyesha kipindi cha wakati kilicho na urefu fulani na kinaweza kuwa cha miaka elfu moja au maelfu mengi ya miaka. Inawezekana kwamba kila siku ya uumbaji inayotajwa katika Biblia ilikuwa na maelfu ya miaka. Isitoshe, tayari dunia ilikuwepo hata kabla ya siku za uumbaji kuanza. (Mwanzo 1:1) Kwa hiyo, simulizi la Biblia linapatana na sayansi ya kweli katika jambo hilo.—2 Petro 3:8.
Akizungumzia kuhusu maoni ya kwamba siku za uumbaji zilikuwa saa 24 tu, mwanabiolojia wa molekuli Francis Collins anasema hivi: ‘Ile dhana ya kwamba kila siku ya uumbaji ilikuwa na saa 24 tu imepotosha sana imani ya watu wenye akili kuliko kitu kingine chochote hivi karibuni.’
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
Je, Sayansi Ndiyo Yenye Maadili Bora Zaidi?
Inaeleweka ni kwa nini watu wengi wanaopenda sayansi wamekataa dini kwa sababu ya jinsi ambavyo imepinga maendeleo ya kisayansi, matendo yake mabaya, na unafiki na ukatili wake. Profesa wa elimu ya vijiumbe John Postgate anasema hivi: ‘Dini za ulimwengu zimesababisha uovu mwingi kupitia kuua wanadamu kama dhabihu, vita vitakatifu, maangamizi makubwa ya jamii mbalimbali, na mabaraza ya kuwahukumu waasi. Katika ulimwengu wa sasa, uovu huo wa dini umekuwa hatari. Kwani, dini si kama sayansi kwa sababu inaweza kuunga mkono upande wowote.’
Akilinganisha jambo hilo na vile ambavyo sayansi inaonekana kuwa yenye busara, isiyopendelea, na yenye utulivu, Postgate anasema kwamba “sasa sayansi ndiyo yenye maadili bora zaidi.”
Je, kweli sayansi ina maadili bora zaidi? La. Postgate mwenyewe anakubali kwamba ‘wanasayansi huwa na wivu, pupa, na ubaguzi.’ Anaongeza kwamba “wanasayansi wachache wamekuwa tayari kuua kwa sababu ya utafiti, kama ilivyotukia katika Ujerumani ya Nazi na katika kambi za magereza huko Japani.” Na wakati jarida la National Geographic lilipomtuma mwandishi wa habari kupeleleza jinsi habari za kisukuku bandia zilivyoingia katika jarida hilo, mwandishi huyo alitaja mambo kama vile “kuweka siri isivyofaa, kuamini watu wabaya, migogoro mikali kati ya watu walioshikilia kauli zao binafsi, watu waliojifanya kuwa wa maana sana, kuwazia mambo yasiyokuwapo, makisio ya kipumbavu, makosa, ukaidi, kubadili mambo kwa ujanja ili kujifaidi, kusengenyana, kusema uwongo, [na] ufisadi.”
Na ni wazi kwamba wanasayansi ndio wamewatengenezea wanadamu silaha hatari za vita, kama vile viini vya magonjwa vinavyotumiwa kama silaha, gesi yenye sumu, makombora, mabomu yanayoongozwa na miangaza maalumu, na mabomu ya nyuklia.
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Wingu la mavumbi la “Ant Nebula” (Menzel 3), kama lilivyoonekana kwenye Darubini ya Angani ya Hubble
[Hisani]
NASA, ESA and The Hubble Heritage Team (STScI/AURA)
[Picha katika ukurasa wa 9]
Uvumbuzi wa sayansi umeonyesha wazi kwamba ulimwengu ulibuniwa na mtu mwenye akili
[Picha katika ukurasa wa 10]
Mashahidi wa Yehova huwatia watu moyo waheshimu sayansi ya kweli na kuamini Biblia
-