-
Jazeni Kwenye Ujuzi Wenu KujidhibitiMnara wa Mlinzi—2003 | Oktoba 15
-
-
Jazeni Kwenye Ujuzi Wenu Kujidhibiti
“Jazeni . . . kwenye ujuzi wenu kujidhibiti.”—2 PETRO 1:5-8.
1. Matatizo mengi ya wanadamu yanasababishwa na kutoweza kufanya nini?
WAKATI wa kampeni kubwa ya kupinga matumizi ya dawa za kulevya, vijana nchini Marekani walishauriwa hivi: “Kataeni kabisa.” Hali zingekuwa nzuri kama nini iwapo kila mtu angekataa kabisa dawa za kulevya, ulevi, maisha ya kutojali au yasiyo maadilifu, mazoea ya kibiashara yasiyo manyoofu, na “tamaa za mwili”! (Waroma 13:14) Hata hivyo, si rahisi kukataa kabisa mambo hayo.
2. (a) Ni mifano gani ya Biblia inayoonyesha kwamba ilikuwa vigumu hata kwa watu wa zamani kukataa kabisa mambo fulani? (b) Mifano hiyo inapaswa kututia moyo kufanya nini?
2 Kwa kuwa si rahisi kwa wanadamu wote wasio wakamilifu kuonyesha sifa ya kujidhibiti, tunapaswa kutamani kujua jinsi tunavyoweza kushinda udhaifu wowote tulio nao. Biblia hutueleza kuhusu watu wa zamani waliojitahidi kumtumikia Mungu, ingawa wakati mwingine ilikuwa vigumu kwao kukataa kabisa mambo fulani. Kumbuka Daudi na dhambi ya uzinzi aliyofanya pamoja na Bath-sheba. Dhambi hiyo ilisababisha kifo cha watu wawili wasio na hatia, mtoto wao aliyezaliwa kwa uzinzi na pia mume wa Bath-sheba. (2 Samweli 11:1-27; 12:15-18) Au fikiria mtume Paulo, ambaye alikiri hivi waziwazi: “Kwa maana lile jema nitakalo silifanyi, bali lile baya nisilotaka ndilo nazoea kulifanya.” (Waroma 7:19) Je, nyakati nyingine unahisi umekata tamaa kama yeye? Paulo aliendelea kusema: “Kwa kweli napendezwa na sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini mimi naona katika viungo vyangu sheria nyingine ikifanya vita dhidi ya sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu. Mwenye taabu mimi! Ni nani ataniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?” (Waroma 7:22-24) Mifano inayotajwa katika Biblia inapaswa kuimarisha azimio letu la kuendelea na pambano letu la kuwa wenye kujidhibiti zaidi.
Tunapaswa Kujifunza Jinsi ya Kujidhibiti
3. Eleza kwa nini si rahisi kuonyesha sifa ya kujidhibiti.
3 Sifa ya kujidhibiti, ambayo inatia ndani uwezo wa kukataa kabisa mambo fulani, inatajwa kwenye 2 Petro 1:5-7 pamoja na imani, wema wa adili, ujuzi, uvumilivu, ujitoaji-kimungu, shauku ya kidugu, na upendo. Hakuna mtu anayezaliwa akiwa amesitawisha kabisa sifa hizo nyingine zenye kupendeza. Ni lazima zisitawishwe. Tunahitaji kujitahidi sana ili kuzionyesha kwa kadiri kubwa na ndivyo ilivyo na sifa ya kujidhibiti.
4. Kwa nini watu wengi huhisi kwamba hawana tatizo la kuonyesha sifa ya kujidhibiti, lakini jambo hilo linaonyesha nini?
4 Kwa kweli, huenda watu wengi wakahisi hawana tatizo la kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Wao hufanya watakavyo maishani, na kwa kujua au bila kujua, wao hujiendesha kupatana na mwili wao usio mkamilifu bila kujali jinsi wao au watu wengine watakavyoathiriwa na matokeo ya matendo yao. (Yuda 10) Leo, kuliko wakati mwingine wowote, watu wengi wanashindwa au hawataki kukataa kabisa mambo fulani. Kwa kweli, hiyo inaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” ambazo Paulo alizungumzia alipotabiri hivi: “Nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wakufuru, . . . wasio na hali ya kujidhibiti.”—2 Timotheo 3:1-3.
5. Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanapendezwa na habari inayohusu kujidhibiti, na ni shauri gani linalofaa hata leo?
5 Mashahidi wa Yehova wanajua vizuri sana ni vigumu kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Kama Paulo, wanatambua pambano kati ya tamaa ya kumpendeza Mungu kwa kuishi kupatana na viwango vyake, na mwenendo ambao huenda mwili wao usio mkamilifu ukawachochea kuufuata. Kwa sababu hiyo, kwa muda mrefu wametaka kujua jinsi ya kushinda pambano hilo. Mnamo mwaka wa 1916, toleo la mapema la gazeti unalosoma sasa lilizungumzia “njia inayofaa kufuata ili tujidhibiti wenyewe, mawazo yetu, maneno na mwenendo wetu.” Lilidokeza tukumbuke maneno ya andiko la Wafilipi 4:8. Shauri la Mungu katika andiko hilo linafaa hata leo, ingawa liliandikwa miaka 2,000 hivi iliyopita na labda ni vigumu zaidi kulitii sasa kuliko ilivyokuwa wakati huo au katika mwaka wa 1916. Hata hivyo, Wakristo hujitahidi sana kukataa kabisa tamaa za ulimwengu, huku wakitambua kwamba wanapofanya hivyo wanakubali kufanya mapenzi ya Muumba wao.
6. Kwa nini hatupaswi kukata tamaa tunapositawisha sifa ya kujidhibiti?
6 Sifa ya kujidhibiti inatajwa katika andiko la Wagalatia 5:22, 23 kama sehemu ya “matunda ya roho [takatifu].” Tukionyesha sifa hii pamoja na “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, [na] upole,” tutanufaika sana. Kama Petro anavyosema, kufanya hivyo kutatuzuia tusiwe “ama wasiotenda ama wasiozaa matunda” katika utumishi wetu kwa Mungu. (2 Petro 1:8) Lakini hatupaswi kukata tamaa au kujilaumu tunaposhindwa kuonyesha sifa hizo haraka na kwa ukamili kama vile ambavyo tungependa. Labda umeona kwamba shuleni mwanafunzi fulani hujifunza mambo haraka zaidi kuliko mwingine. Au kazini mtu fulani hujifunza kazi haraka zaidi kuliko wafanyakazi wenzake. Vivyo hivyo, watu fulani hujifunza na kuonyesha sifa za Kikristo haraka zaidi kuliko wengine. Hata hivyo, jambo lililo muhimu ni kuendelea kusitawisha sifa za kimungu kadiri tuwezavyo. Tunaweza kufanya hivyo kwa kujinufaisha kikamili na msaada ambao Yehova hutoa kupitia Neno na kutaniko lake. Kuazimia kwa bidii kufanya maendeleo ndilo jambo muhimu zaidi kuliko kufikia mradi wetu haraka.
7. Ni nini kinachoonyesha kwamba sifa ya kujidhibiti ni muhimu?
7 Ingawa sifa ya kujidhibiti ndiyo inayotajwa mwisho katika orodha ya matunda ya roho, hiyo haimaanishi kwamba sifa hiyo si muhimu sana kama sifa zile nyingine. Tunapaswa kukumbuka kwamba tunaweza kuepuka ‘kazi zote za mwili’ kama tungeweza kujidhibiti kikamili. Hata hivyo, wanadamu wasio wakamilifu wana mwelekeo wa kufanya baadhi ya “kazi za mwili . . . uasherati, ukosefu wa usafi, mwenendo mlegevu, ibada ya sanamu, zoea la uwasiliani-roho, uadui, zogo, wivu, hasira za ghafula, magomvi, migawanyiko, mafarakano.” (Wagalatia 5:19, 20) Kwa hiyo, lazima tuendelee kushindana daima, na kuazimia kuondoa kabisa mielekeo isiyofaa kutoka katika akili na moyo.
Ni Vigumu Zaidi kwa Wengine Kuonyesha Sifa ya Kujidhibiti
8. Ni mambo gani ambayo hufanya iwe vigumu kwa wengine kuonyesha sifa ya kujidhibiti?
8 Ni vigumu zaidi kwa Wakristo fulani kuonyesha sifa ya kujidhibiti kuliko wengine. Kwa nini? Huenda ikawa vigumu kwao kuonyesha sifa hiyo kwa sababu ya malezi au mambo yaliyowapata zamani. Tunapaswa kufurahi ikiwa hatuna tatizo la kusitawisha na kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Lakini bila shaka tunapaswa kuwa na huruma na kuelewa hali tunaposhughulika na wale ambao ni vigumu kwao kuonyesha sifa ya kujidhibiti, hata ikiwa tunaumia wanapokosa kuionyesha. Kwa kuwa sisi pia si wakamilifu, ni nani kati yetu aliye na sababu ya kujiona kuwa mwadilifu?—Waroma 3:23; Waefeso 4:2.
9. Wengine wana udhaifu gani, nao udhaifu huo utaondolewa kabisa wakati gani?
9 Kwa mfano: Huenda tunajua kwamba nyakati nyingine baadhi ya Wakristo wenzetu ambao wameacha kutumia tumbaku au dawa za “kujiburudisha” wanaweza bado kuwa na tamaa kubwa ya kutumia vitu hivyo. Au wengine huona ni vigumu kupunguza kiasi cha chakula wanachokula au kileo wanachotumia. Wengine wana shida ya kudhibiti ulimi wao, kwa hiyo mara nyingi wao hujikwaa katika maneno. Tunahitaji kujitahidi sana kusitawisha sifa ya kujidhibiti ili kushughulika na udhaifu huo. Kwa nini? Andiko la Yakobo 3:2 linakiri hivi kwa kufaa: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyu ni mtu mkamilifu, awezaye kuuongoza kwa hatamu mwili wake wote pia.” Hata hivyo, wengine wana tamaa kubwa ya kucheza kamari. Au huenda ikawa vigumu kwao kudhibiti hasira yao. Huenda ikachukua muda kujua jinsi unavyoweza kufanikiwa kukabiliana na udhaifu huo au udhaifu mwingine kama huo. Ingawa tunaweza kufanya maendeleo makubwa sasa, tamaa mbaya zitaondolewa kabisa tutakapofikia ukamilifu. Wakati huu, kujitahidi kuonyesha sifa ya kujidhibiti kutatusaidia tusirudie maisha ya dhambi. Pambano hilo linapoendelea, na tusaidiane ili tusife moyo.—Matendo 14:21, 22.
10. (a) Kwa nini ni vigumu kwa wengine sana kujidhibiti katika mambo ya ngono? (b) Ndugu mmoja alifanya badiliko gani kubwa? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 16.)
10 Sehemu nyingine ambayo wengine wana tatizo la kujidhibiti inahusu mambo ya ngono. Yehova Mungu alituumba tukiwa na hamu ya ngono. Hata hivyo, wengine huona ni vigumu sana kujidhibiti kuhusiana na ngono, kupatana na viwango vya Mungu. Inaweza kuwa vigumu zaidi kwao kwa sababu wana hamu kubwa ya ngono isivyo kawaida. Tunaishi katika ulimwengu ulio na kichaa cha ngono ambao huchochea tamaa hizo katika njia mbalimbali. Hiyo inaweza kufanya iwe vigumu sana kwa Wakristo wanaotaka kubaki waseja—angalau kwa muda—ili kumtumikia Mungu bila vikengeusha-fikira vinavyosababishwa na ndoa. (1 Wakorintho 7:32, 33, 37, 38) Lakini kupatana na amri ya Kimaandiko kwamba “ni bora kuoa na kuolewa kuliko kuwashwa na harara,” huenda wakaamua kufunga ndoa, jambo ambalo bila shaka linaheshimika. Wakati huohuo wameazimia kufunga ndoa “katika Bwana tu,” kama Maandiko yanavyoshauri. (1 Wakorintho 7:9, 39) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hufurahia kuona tamaa yao ya kufuata kanuni zake za uadilifu. Wakristo wenzao hufurahi kushirikiana na waabudu wa kweli wanaofuata viwango vya juu vya maadili na uaminifu-maadili.
11. Tunaweza kumsaidiaje ndugu au dada ambaye anataka kufunga ndoa lakini hajaweza kufanya hivyo?
11 Namna gani ikiwa mtu hawezi kupata mwenzi anayefaa? Wazia jinsi mtu anavyoweza kuvunjika moyo ikiwa anataka kufunga ndoa lakini hajaweza kufanya hivyo! Huenda akaona marafiki wake wakifunga ndoa na kupata furaha ya kadiri fulani, huku akiwa bado anatafuta mwenzi anayefaa. Huenda wengine walio katika hali hiyo wakawa na tatizo la kudumu la kupiga punyeto. Kwa vyovyote vile, hakuna Mkristo yeyote ambaye angependa kumvunja moyo bila kujua Mkristo mwenzake anayejitahidi kudumisha usafi wa kiadili. Huenda tukawavunja wengine moyo bila kukusudia ikiwa tutawauliza swali kama hili bila kufikiri, “Utafunga ndoa wakati gani?” Huenda mtu akauliza hivyo bila nia mbaya, lakini ingekuwa vema sana kama tungejidhibiti kwa kulinda ulimi wetu! (Zaburi 39:1) Tunapaswa kuwapongeza sana waseja walio kati yetu ambao wanadumisha usafi wa kiadili. Badala ya kusema mambo yanayoweza kuwavunja moyo tunaweza kujitahidi kuwatia moyo. Kwa mfano, tunaweza kujitahidi kuwaalika waseja wakati kikundi kidogo cha Wakristo waliokomaa wanapokutana kula pamoja au kufurahia ushirika wa Kikristo unaofaa.
Kujidhibiti Katika Ndoa
12. Kwa nini hata wale waliofunga ndoa wanahitaji kujidhibiti kwa kadiri fulani?
12 Hata kama umefunga ndoa, hiyo haimaanishi kwamba hutahitaji kujidhibiti kuhusiana na ngono. Kwa mfano, huenda mahitaji ya ngono ya mume na mke yakatofautiana sana. Au huenda nyakati nyingine hali ya mwenzi mmoja ikafanya iwe vigumu au isiwezekane kuwa na uhusiano wa ngono. Labda kwa sababu ya mambo yaliyotukia zamani, huenda ikawa vigumu kwa mwenzi mmoja kutii amri hii: “Acha mume ampe mke wake haki yake; lakini acha mke pia afanye hivyohivyo kwa mume wake.” Katika hali kama hiyo, huenda mwenzi yule mwingine akahitaji kujidhibiti zaidi. Lakini wote wawili wanapaswa kukumbuka shauri la Paulo lenye upendo kwa Wakristo waliofunga ndoa: “Msiwe mkinyimana hiyo, ila kwa makubaliano kwa wakati uliowekwa rasmi, ili mpate kutumia wakati kwa sala na mpate kuja pamoja tena, ili Shetani asipate kufuliza kuwashawishi kwa sababu ya kukosa kwenu kujirekebisha.”—1 Wakorintho 7:3, 5.
13. Tunaweza kufanya nini kwa niaba ya wale wanaojitahidi kuonyesha sifa ya kujidhibiti?
13 Wale waliofunga ndoa wanaweza kufurahi sana ikiwa wote wawili wamejifunza kujidhibiti ifaavyo katika uhusiano huo ulio wa karibu sana. Wakati huohuo, wanapaswa kuelewa hali za waabudu wenzao ambao bado wanajitahidi kuonyesha sifa hiyo kuhusiana na ngono. Hatupaswi kamwe kusahau kusali kwa Yehova ili awapatie ndugu zetu wa kiroho ufahamu, ujasiri, na nia ya kuendelea na pambano lao la kuonyesha sifa ya kujidhibiti na kuchukua hatua kushinda tamaa zisizofaa.—Wafilipi 4:6, 7.
Endeleeni Kusaidiana
14. Kwa nini tunapaswa kushughulika na Wakristo wenzetu kwa huruma na kwa kuelewa hali zao?
14 Nyakati nyingine, huenda ikawa vigumu kwetu kuelewa hali za Wakristo wenzetu ambao wanajitahidi kuonyesha sifa ya kujidhibiti kuhusiana na jambo fulani ambalo kwetu si tatizo. Lakini watu wanatofautiana kiasili. Baadhi yao huongozwa na hisia kwa urahisi; nao wengine huzidhibiti. Wengine huona ni rahisi kujidhibiti. Kwao hilo si tatizo kubwa. Wengine huona ni vigumu zaidi kujidhibiti. Hata hivyo, kumbuka kwamba mtu anayejitahidi si mbaya. Tunahitaji kuelewa hali za Wakristo wenzetu na kuwaonyesha huruma. Tunapata furaha tunapoendelea kuwaonyesha huruma wale ambao bado wanajitahidi kuonyesha sifa ya kujidhibiti kwa kiwango kikubwa zaidi. Tunaweza kuona jambo hilo katika maneno ya Yesu kwenye Mathayo 5:7.
15. Kwa nini maneno ya Zaburi 130:3 yanafariji kuhusiana na kujidhibiti?
15 Hatungependa kamwe kumwelewa vibaya Mkristo mwenzetu ambaye huenda pindi fulani akakosa kuonyesha utu wa Kikristo. Inatia moyo kama nini kujua kwamba mbali na kuona pindi moja ambapo labda tulishindwa kuonyesha sifa ya kujidhibiti, Yehova anaona pindi nyingi ambapo tulisimama imara hata ikiwa Wakristo wenzetu hawakuona jambo hilo! Inafariji sana kukumbuka maneno ya Zaburi 130:3: “BWANA, kama wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?”
16, 17. (a) Tunaweza kutumiaje andiko la Wagalatia 6:2, 5 kuhusiana na kujidhibiti? (b) Tutazungumzia mambo gani kuhusu kujidhibiti katika makala inayofuata?
16 Ili kumpendeza Yehova, lazima kila mmoja wetu asitawishe sifa ya kujidhibiti, lakini tunaweza kuwa na hakika kwamba ndugu zetu Wakristo watatusaidia. Ingawa ni lazima kila mmoja wetu abebe mzigo wake wa daraka, tunahimizwa tusaidiane ili kukabiliana na udhaifu mbalimbali. (Wagalatia 6:2, 5) Tunaweza kumthamini sana mzazi, mwenzi wa ndoa, au rafiki anayetuzuia tusiende mahali tusipopaswa kwenda, kutazama vitu tusivyopaswa kutazama, au kufanya mambo tusiyopaswa kufanya. Anatusaidia kuonyesha sifa ya kujidhibiti, yaani uwezo wa kukataa kabisa mambo fulani.
17 Huenda Wakristo wengi wanakubaliana na mambo ambayo tumezungumzia kuhusu sifa ya kujidhibiti, lakini huenda wakahisi kwamba wanapaswa kufanya maendeleo zaidi. Wangependa kuonyesha sifa ya kujidhibiti kikamili zaidi, kwa kadiri ambavyo wanaona inawezekana kwa wanadamu wasio wakamilifu. Je, unahisi hivyo? Hivyo basi, unaweza kufanya nini ili kusitawisha sifa hii ambayo ni mojawapo ya matunda ya roho ya Mungu? Na kufanya hivyo kunaweza kukusaidiaje kutimiza miradi yako ya muda mrefu ukiwa Mkristo? Acheni tuone jambo hilo katika makala inayofuata.
-
-
Iweni Wenye Kujidhibiti Ili Mshinde Tuzo!Mnara wa Mlinzi—2003 | Oktoba 15
-
-
Iweni Wenye Kujidhibiti Ili Mshinde Tuzo!
“Kila mtu anayeshiriki katika shindano hutumia kujidhibiti katika mambo yote.”—1 WAKORINTHO 9:25.
1. Kupatana na andiko la Waefeso 4:22-24, watu wengi wamekubali jinsi gani kufanya mapenzi ya Yehova?
IKIWA ulibatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, ulitangaza hadharani kwamba ulikuwa tayari kushiriki katika pambano ambalo tuzo lake ni uhai wa milele. Ulikubali kufanya mapenzi ya Yehova. Kabla ya kujiweka wakfu kwa Yehova, wengi wetu tulifanya mabadiliko makubwa ili wakfu wetu uwe wa kweli na wenye kukubaliwa na Mungu. Tulifuata shauri hili la mtume Paulo kwa Wakristo: “Mweke mbali utu wa hapo zamani unaofuatana na njia yenu ya kwanza ya mwenendo na ambao unafisidiwa kulingana na tamaa zake za udanganyifu . . . Mvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.” (Waefeso 4:22-24) Yaani, kabla ya kujiweka wakfu kwa Mungu, ilitubidi kuacha mwenendo wa zamani usiofaa.
2, 3. Andiko la 1 Wakorintho 6:9-12 linaonyeshaje kwamba mabadiliko ya aina mbili yanapaswa kufanywa ili kupata kibali cha Mungu?
2 Baadhi ya tabia za utu wa kale ambazo watu wanaotaka kuwa Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuacha zinashutumiwa waziwazi na Neno la Mungu. Paulo aliorodhesha baadhi ya tabia hizo katika barua yake kwa Wakorintho, akisema: “Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume watunzwao kwa makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume walalao pamoja na wanaume, wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawatarithi ufalme wa Mungu.” Kisha akaonyesha kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walifanya mabadiliko mbalimbali kuhusiana na utu wao, na kuendelea kusema: “Hata hivyo baadhi yenu ndivyo mlivyokuwa.” Ona kwamba Wakristo hao walikuwa hivyo, lakini wakabadilika.—1 Wakorintho 6:9-11.
3 Paulo alidokeza kwamba huenda pia ikawa lazima kufanya mabadiliko zaidi, kwa kuwa aliendelea kusema: “Mambo yote yaruhusika kisheria kwangu; lakini si mambo yote yenye faida.” (1 Wakorintho 6:12) Hivyo, leo wengi ambao hutamani kuwa Mashahidi wa Yehova huona uhitaji wa kukataa kabisa hata mambo ambayo, ingawa yanaruhusika kisheria, hayana faida au hayana thamani ya kudumu. Mambo hayo yanaweza kuwapotezea wakati na kuwakengeusha wasifuatie mambo yaliyo muhimu zaidi.
4. Wakristo waliojiweka wakfu wanakubaliana na Paulo katika jambo gani?
4 Mtu hujiweka wakfu kwa Mungu kwa hiari, na si shingo upande kana kwamba kufanya hivyo ni kujidhabihu sana. Wakristo waliojiweka wakfu wanakubaliana na Paulo ambaye alisema hivi baada ya kuwa mfuasi wa Kristo: “Kwa sababu yake [Yesu] nimekubali hasara ya vitu vyote nami naviona kuwa takataka nyingi, ili niweze kupata Kristo.” (Wafilipi 3:8) Paulo alikataa kabisa kwa hiari mambo yasiyo na thamani ili aweze kuendelea kufanya mapenzi ya Mungu.
5. Paulo alishiriki kwa mafanikio katika shindano gani, nasi tunawezaje kufanya hivyo?
5 Paulo alionyesha sifa ya kujidhibiti alipokuwa akikimbia katika shindano lake la kiroho na mwishowe aliweza kusema: “Nimepigana pigano bora, nimekimbia mwendo hadi mwisho, nimeshika imani. Tangu wakati huu na kuendelea kumewekwa akiba kwa ajili yangu taji la uadilifu, ambalo Bwana, aliye hakimu mwadilifu, atanipa kuwa zawadi katika siku ile, lakini si mimi tu, bali pia wale wote ambao wamependa udhihirisho wake.” (2 Timotheo 4:7, 8) Je, siku moja tutaweza kusema kama yeye? Tutafanya hivyo ikiwa kwa imani tunaonyesha sifa ya kujidhibiti tunapokimbia katika shindano letu la Kikristo mpaka mwisho bila kuacha.
Kujidhibiti Kunahitajiwa ili Kufanya Mema
6. Kujidhibiti ni nini, na tunapaswa kuonyesha sifa hiyo katika njia gani mbili?
6 Maneno ya Kiebrania na ya Kigiriki yanayotafsiriwa “kujidhibiti” katika Biblia, kihalisi yanamaanisha kwamba mtu ana uwezo wa kujizuia. Mara nyingi maneno hayo yanadokeza wazo la kujizuia usifanye mabaya. Lakini ni wazi kwamba kujidhibiti kwa kadiri fulani kunahitajiwa pia ikiwa tutafanikiwa kutumia miili yetu kufanya kazi njema. Kwa kawaida wanadamu wasio wakamilifu wana mwelekeo wa kufanya mabaya, kwa hiyo tuna mapambano ya aina mbili. (Mhubiri 7:29; 8:11) Tunapojizuia kufanya mabaya, inatubidi pia tujilazimishe kufanya mema. Kwa kweli, kudhibiti mwili wetu ili kufanya mema ni mojawapo kati ya njia bora zaidi za kuepuka kufanya mabaya.
7. (a) Kama Daudi, tunapaswa kusali kwa ajili ya nini? (b) Tunaweza kuonyesha sifa ya kujidhibiti kwa kadiri kubwa kwa kutafakari mambo gani?
7 Bila shaka kujidhibiti ni muhimu ili kutimiza wakfu wetu kwa Mungu. Tunapaswa kusali kama Daudi: “Ee Mungu, uniumbie moyo safi, uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.” (Zaburi 51:10) Tunaweza kutafakari manufaa ya kuepuka mambo yasiyo maadilifu au yanayotudhoofisha kimwili. Fikiria madhara unayoweza kupata kwa kutoepuka mambo hayo: matatizo mabaya ya afya, mahusiano yaliyoharibika, na hata kifo cha mapema. Kwa upande mwingine, fikiria faida nyingi za kufuata njia ya maisha ambayo Yehova hupendekeza. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba moyo wetu ni mdanganyifu. (Yeremia 17:9) Ni lazima tuazimie kutoruhusu moyo wetu upunguze uzito wa kufuata viwango vya Yehova.
8. Tumejifunza nini kutokana na mambo yaliyotupata? Toa mfano.
8 Kutokana na mambo yaliyotupata, wengi wetu tunajua kwamba mara nyingi mwili usio na nia ya kufanya mema hupunguza bidii na nia yetu ya kufanya yaliyo mema. Kwa mfano, fikiria kazi ya kuhubiri Ufalme. Yehova hupendezwa na nia ya wanadamu ya kutaka kufanya mema kwa kushiriki katika kazi hii inayotoa uhai. (Zaburi 110:3; Mathayo 24:14) Haikuwa rahisi kwa wengi wetu kujifunza kuhubiri hadharani. Tulihitaji na labda bado tunahitaji kudhibiti mwili wetu, ‘kuupiga-piga’ na “kuuongoza kama mtumwa,” badala ya kuuruhusu utuzuie kuhubiri.—1 Wakorintho 9:16, 27; 1 Wathesalonike 2:2.
“Katika Mambo Yote”?
9, 10. Ni nini kinachohusika katika kuonyesha sifa ya “kujidhibiti katika mambo yote”?
9 Shauri la Biblia kuhusu “kujidhibiti katika mambo yote” linaonyesha kwamba kuna mengi zaidi yanayohusika kuliko kudhibiti tu hasira yetu na kujiepusha na mwenendo usio mwadilifu. Huenda tukahisi kwamba tumejidhibiti katika mambo hayo, na ikiwa ndivyo, tunaweza kufurahi kwelikweli. Hata hivyo, namna gani sehemu nyingine za maisha ambazo huenda isionekane waziwazi kwamba tunahitaji kuonyesha sifa ya kujidhibiti? Kwa mfano, tuseme tunaishi katika nchi ambayo ni tajiri kwa kadiri fulani na yenye kiwango cha juu cha maisha. Je, halitakuwa jambo la hekima kujifunza kutotumia pesa kwa vitu visivyo vya lazima? Wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao kutonunua kitu chochote wanachoona kwa sababu tu kinapatikana, kinavutia, au wana pesa za kukinunua. Bila shaka, ili mafundisho hayo yawe yenye matokeo, lazima wazazi waweke mfano mzuri.—Luka 10:38-42.
10 Kujifunza kuishi bila kitu fulani tunachotaka kunaweza kuimarisha azimio letu. Pia kunaweza kufanya tuthamini vitu tulivyo navyo na kuwahurumia zaidi wale wasiokuwa na vitu hivyo, si kwa kupenda kwao, bali kwa sababu hawana pesa za kuvinunua. Naam, kuishi maisha sahili ni kinyume kabisa na maoni ya watu wengi kwamba lazima watu wajijali kupita kiasi au kuona kwamba wao ndio wanaostahili vitu bora zaidi. Wanabiashara huchochea tamaa ya kujitosheleza papo hapo, lakini wao hufanya hivyo ili wapate faida. Huenda hali hiyo ikazuia jitihada zetu za kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Hivi karibuni, gazeti moja la nchi fulani tajiri ya Ulaya lilisema hivi: “Ikiwa wale wanaoishi chini ya hali ngumu sana za umaskini wanahitaji kujitahidi ili kudhibiti tamaa zisizofaa, basi wale wanaoishi katika nchi tajiri wanahitaji kujitahidi hata zaidi katika jamii ya leo yenye utajiri!”
11. Kwa nini kuna manufaa ya kujifunza kuishi bila vitu fulani, na ni nini hufanya jambo hilo liwe gumu?
11 Ikiwa ni vigumu kwetu kutofautisha kati ya vitu tunavyotaka na mahitaji halisi, huenda ikafaa kuchukua hatua ili kuhakikisha kwamba hatutendi bila kufikiri. Kwa mfano, ikiwa tunataka kujizuia tusitumie pesa ovyoovyo, huenda tukaazimia kutonunua vitu kwa mkopo, au kuchukua kiasi hususa cha pesa tunapoenda kununua vitu. Kumbuka kwamba Paulo alisema ‘ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu’ ni “njia ya kupata faida kubwa.” Alitoa hoja hii: “Hatukuleta kitu katika ulimwengu, wala hatuwezi kupeleka kitu chochote nje. Kwa hiyo, tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.” (1 Timotheo 6:6-8) Je, tunaridhika? Kujifunza kuishi maisha sahili, bila kujiingiza katika mambo yanayoweza kutuzuia kufanya mambo yaliyo ya lazima—hata yawe ni nini—huhitaji tuazimie na kujidhibiti. Hata hivyo, kuna manufaa ya kujifunza kufanya hivyo.
12, 13. (a) Mikutano ya Kikristo inahusishaje sifa ya kujidhibiti? (b) Tunapaswa kusitawisha sifa ya kujidhibiti katika sehemu gani nyingine?
12 Kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na makusanyiko kunahusisha kuonyesha sifa ya kujidhibiti kwa njia fulani hususa. Kwa mfano, sifa hiyo ni muhimu ili kuzuia akili yetu isitangetange wakati programu inapoendelea. (Mithali 1:5) Huenda sifa ya kujidhibiti ikahitajiwa ili tusiwasumbue wengine kwa kuwanong’onezea wale walioketi karibu nasi badala ya kumsikiliza msemaji kwa makini. Huenda tukahitaji sifa ya kujidhibiti ili turekebishe ratiba yetu na kufika mapema. Isitoshe, huenda tukahitaji kuonyesha sifa ya kujidhibiti ili kutenga wakati wa kutayarisha na kushiriki katika mikutano.
13 Kuonyesha sifa ya kujidhibiti katika mambo madogo huimarisha uwezo wetu wa kuonyesha sifa hiyo katika mambo makubwa. (Luka 16:10) Kwa hiyo, ni jambo zuri kujitia nidhamu ili kusoma kwa ukawaida Neno la Mungu na vichapo vinavyozungumzia Biblia, kujifunza na kutafakari mambo tunayojifunza. Ni jambo la hekima kama nini kujitia nidhamu kuhusu kazi zisizofaa, urafiki, mitazamo, na tabia fulani au kujitia nidhamu ili kukataa kabisa mambo yanayoweza kutupotezea wakati wenye thamani wa kumtumikia Mungu! Bila shaka, kuwa na shughuli nyingi katika utumishi wa Yehova hutulinda dhidi ya mambo yanayoweza kutuondoa katika paradiso ya kiroho ya kutaniko la Yehova la ulimwenguni pote.
Iweni Wakomavu kwa Kujidhibiti
14. (a) Watoto wanapaswa kujifunzaje kuonyesha sifa ya kujidhibiti? (b) Watoto wanaweza kupata manufaa gani wanapojifunza kuonyesha sifa hiyo mapema maishani?
14 Mtoto mchanga hawezi kujidhibiti. Kijitabu kimoja cha wataalamu wa tabia ya watoto kinasema: “Sifa ya kujidhibiti haitokei tu bila jitihada yoyote. Watoto wanahitaji mwongozo na msaada wa wazazi ili waanze kujifunza kuwa na sifa ya kujidhibiti. . . . Wazazi wanapowafunza, watoto huanza kusitawisha sifa ya kujidhibiti na kuendelea kuionyesha miaka yote wanapokuwa shuleni.” Uchunguzi uliofanywa kuhusu watoto wenye umri wa miaka minne ulionyesha kwamba wale waliojifunza kuonyesha sifa ya kujidhibiti kwa kadiri fulani “kwa ujumla walikua wakawa vijana wenye nidhamu, wenye kupendeza, wajasiri, wenye uhakika na wenye kutegemeka.” Wale ambao hawakuwa wameanza kujifunza sifa hiyo, “yaelekea walikuwa wapweke, wenye kukasirika kwa urahisi, na wakaidi. Walishindwa na mkazo na hawakutaka kukabili magumu.” Bila shaka, ni lazima mtoto ajifunze kuonyesha sifa ya kujidhibiti ili atakapokuwa mtu mzima awe na nidhamu.
15. Kutojidhibiti huonyesha nini, na kunatofautianaje na lengo linalotajwa katika Biblia?
15 Vivyo hivyo, ili tuwe Wakristo waliokomaa, lazima tujifunze jinsi ya kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Kutojidhibiti huonyesha kwamba bado sisi ni watoto kiroho. Biblia inatushauri ‘tuwe watu wazima katika nguvu za kuelewa.’ (1 Wakorintho 14:20) Lengo letu ni ‘kuufikia umoja katika imani na katika ujuzi sahihi wa Mwana wa Mungu, kufikia kuwa mwanamume aliyekua kabisa, kufikia kipimo cha kimo ambacho ni cha ujao wa Kristo.’ Kwa nini? “Ili tusiwe tena vitoto, tukirushwa huku na huku kama vile na mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho kwa njia ya mbinu ya hadaa ya watu, kwa njia ya ujanja katika kutunga kosa.” (Waefeso 4:13, 14) Ni wazi kwamba kujifunza kuonyesha sifa ya kujidhibiti ni muhimu kwa hali yetu ya kiroho.
Kusitawisha Sifa ya Kujidhibiti
16. Yehova hutoaje msaada?
16 Ili kusitawisha sifa ya kujidhibiti, tunahitaji msaada wa Mungu, nao unapatikana. Neno la Mungu ambalo ni kama kioo, hutuonyesha mahali tunapohitaji kufanya marekebisho ya kibinafsi, nalo hutoa shauri la jinsi ya kufanya hivyo. (Yakobo 1:22-25) Pia ndugu zetu wenye upendo ulimwenguni pote wana nia ya kutusaidia. Wazee Wakristo huonyesha kwamba wanaelewa hali za wengine wanapotoa msaada. Yehova mwenyewe hutupatia roho yake takatifu kwa hiari ikiwa tunaiomba katika sala. (Luka 11:13; Waroma 8:26) Kwa hiyo, na tutumie maandalizi hayo kwa furaha. Madokezo kwenye ukurasa wa 21 yanaweza kusaidia.
17. Andiko la Mithali 24:16 linatupa kitia moyo gani?
17 Ni jambo lenye kufariji kama nini kujua kwamba Yehova huthamini jitihada zetu tunapojaribu kumpendeza! Hilo lapaswa kutuchochea kuendelea kujitahidi ili tuzidi kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Hata tujikwae mara nyingi kadiri gani, hatupaswi kamwe kuacha kujitahidi. “Huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, naye hakika atasimama.” (Mithali 24:16, NW) Kila mara tunapofanikiwa kumpendeza Yehova, tunakuwa na sababu ya kufurahi. Pia tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anapendezwa nasi. Shahidi mmoja anasema kwamba kabla hajajiweka wakfu kwa Yehova, kila mara alipojidhibiti kutovuta sigara kwa juma moja, alijithawabisha mwenyewe kwa kununua kitu kizuri akitumia pesa ambazo angetumia kununua sigara.
18. (a) Pambano letu la kusitawisha sifa ya kujidhibiti linahusisha nini? (b) Yehova anatuhakikishia nini?
18 Zaidi ya yote, tunapaswa kukumbuka kwamba kujidhibiti kunahusisha akili na hisia. Tunaweza kuona jambo hilo kutokana na maneno haya ya Yesu: “Kila mtu ambaye hufuliza kumtazama mwanamke ili kuwa na harara kwa ajili yake tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28; Yakobo 1:14, 15) Mtu ambaye amejifunza kudhibiti akili na hisia zake, ataona ni rahisi pia kudhibiti mwili wake wote. Kwa hiyo, acheni tuimarishe azimio letu la kutofanya mabaya na pia kutoyafikiria. Mawazo mabaya yakitokea, yakatae papo hapo. Tunaweza kukimbia kishawishi kwa kusali huku tukimkazia Yesu macho yetu. (1 Timotheo 6:11; 2 Timotheo 2:22; Waebrania 4:15, 16) Tunapojitahidi kufanya yote tuwezayo, tutakuwa tukitii shauri linalopatikana katika Zaburi 55:22: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.”
-
-
Iweni Wenye Kujidhibiti Ili Mshinde Tuzo!Mnara wa Mlinzi—2003 | Oktoba 15
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]
Jinsi ya Kuimarisha Sifa ya Kujidhibiti
• Isitawishe hata katika mambo madogo
• Tafakari manufaa ya sasa na ya wakati ujao ya sifa hiyo
• Epuka kufanya mambo ambayo Mungu anakataa na utendee yale anayotaka
• Kataa mawazo mabaya papo hapo
• Jaza akili yako mawazo ya kiroho yenye kujenga
• Kubali msaada unaoweza kupewa na Wakristo wenzako wakomavu
• Epuka hali zenye kushawishi
• Sali ili upate msaada wa Mungu wakati wa vishawishi
-