‘Ilikuwa Kama Kula Asali’
KATIKATI ya mwaka wa 1993, katika Altus, Oklahoma, Marekani, baba mwenye kuhangaika, msaidizi wa kamanda katika Jeshi la Wanahewa la Marekani, alisali kupata mwongozo ili amsaidie binti yake, ambaye alikuwa na matatizo ya ndoa na alikuwa akifikiria kupata talaka. Asubuhi iliyofuata mmoja wa Mashahidi wa Yehova alifika mlangoni pake na kumtolea toleo la Julai 8, 1993 la Amkeni!, ambalo lilizungumzia somo “Talaka—Je, Ni Mlango wa Kupata Furaha Zaidi?”
Ijapokuwa mwanamume huyo hakuwapenda Mashahidi kamwe, na hakuwa amewasikiliza kamwe kabla ya hapo, alikubali kwa utayari na akasoma gazeti hilo la Amkeni! Baadaye alishiriki maandiko na mawazo kutoka kwalo na binti yake. Alisoma pia nakala ya Mnara wa Mlinzi ambayo ilikuwa imeachwa pamoja na ile ya Amkeni! Ilikuwa na makala iliyomsukuma afikiri kwa uzito kuhusu itikadi aliyokuwa nayo kwa muda mrefu ya Utatu. Aling’amua kwamba sala yake kuhusiana na binti yake ilikuwa ikijibiwa, lakini akastaajabu kwa nini Mungu angetumia watu ambao hawakuitikadi katika Utatu ili kujibu sala zake. Alisababu kwamba kwa kweli Mungu hawatumii watu wasiofunza kweli kujibu sala.
Hivyo alisukumwa kupiga simu kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova ili kupata fasihi fulani zinazoelezea kwa undani itikadi zao kuhusu Utatu. Mwanamume aliyejibu simu alikuwa akihudhuria mkutano wa wazee Wakristo. Msaidizi wa Kamanda wa jeshi la wanahewa alienda mara moja kwenye Jumba la Ufalme, ambapo alipewa kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani na broshua Je! Uamini Utatu?
Usiku huo, mwanamume huyo aliisoma broshua nzima. Alipokuwa akiisoma alisisimuka sana, baadaye alisema kwamba hata ilimbidi kutua na kujiambia, ‘Hebu tulia. Hili haliwezekani. Hili ni nzuri sana kuwa kweli.’ Broshua hiyo ilitokeza kwa wazi uthibitisho wa Biblia dhidi ya fundisho la Utatu hivi kwamba alipoisoma, akaeleza, “ilikuwa kama tu kula asali.” Jioni iliyofuata alihudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova na alipendezwa na yale aliyosikia.
Baada ya funzo la Biblia lake la kwanza pamoja na Mashahidi wa Yehova na mazungumzo kamili juu ya maoni ya Biblia kuhusu uvutaji wa sigareti, aliharibu sigareti zake na hakuvuta sigareti tena kamwe. Funzo la Biblia liliongozwa pamoja naye mara kadhaa kila juma. Miezi mitatu baada ya kusoma broshua ya Utatu, na baada ya kuondoka jeshini, alianza kushiriki katika kazi ya kuhubiri waziwazi pamoja na Mashahidi. Miezi mitatu baadaye alionyesha wakfu wake kwa Yehova Mungu na kubatizwa. Sasa anatumikia akiwa mhudumu wa wakati wote.