-
Kutahini na Kupepeta Kuanzia NdaniMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
1914—Matarajio na Uhalisi
Katika 1876, C. T. Russell aliandika makala ya kwanza kati ya nyingine ambamo alionyesha mwaka 1914 kuwa mwisho wa Nyakati za Mataifa zilizorejezewa na Yesu Kristo. (Luka 21:24, KJ) Katika buku la pili la Millennial Dawn, lililotangazwa katika 1889, Ndugu Russell alionyesha mambo mengi ya kutoa sababu ambayo yangewezesha wasomaji kuona msingi wa Kimaandiko wa yale yaliyosemwa na kujichunguzia wenyewe. Katika kipindi cha karibu karne nne kilichoongoza hadi 1914, Wanafunzi wa Biblia waligawanya mamilioni ya nakala za vichapo vilivyokazia fikira kwenye mwisho wa Nyakati za Mataifa. Vichapo vingine vichache vya kidini vilitambua kronolojia ya Biblia iliyoelekeza kwenye mwaka 1914, lakini ni kikundi gani isipokuwa kile cha Wanafunzi wa Biblia kilichoendelea kuitangaza kimataifa na kuishi katika njia iliyoonyesha kwamba waliamini kwamba Nyakati za Mataifa zingeisha mwaka huo?
Mwaka 1914 ulipokaribia, matarajio yalipanda. Ungeleta nini? Katika The Bible Students Monthly (Buku 6, Na. 1, lililotangazwa mapema katika 1914), Ndugu Russell aliandika: “Ikiwa tuna tarehe na kronolojia sahihi, Nyakati za Mataifa zitakwisha mwaka huu—1914. Maana yake nini? Hatujui kwa uhakika. Tarajio letu ni kwamba utawala wenye utendaji wa Mesiya utaanza karibu na wakati wa mwisho wa kipindi cha utawala cha Mataifa. Tarajio letu, liwe kweli au si kweli, ni kwamba kutakuwako madhihirisho ya ajabu ya hukumu ya Kimungu dhidi ya ukosefu wote wa haki, na kwamba hilo litamaanisha kuvunjwa kwa mifumo mingi ya wakati huu, ikiwa si yote.” Alikazia kwamba hakutazamia “mwisho wa ulimwengu” katika 1914 na kwamba dunia yadumu milele, lakini kwamba utaratibu wa mambo wa sasa, ambao Shetani ndiye mtawala, utapitilia mbali.
Katika toleo lalo la Oktoba 15, 1913, The Watch Tower lilikuwa limesema: “Kulingana na ufahamu bora zaidi wa kronolojia tuwezao, ni karibu wakati huo—iwe ni Oktoba 1914, au baadaye. Bila kushikilia kauli, tunatazamia matukio fulani: (1) Mwisho wa Nyakati za Mataifa—utawala wa Mataifa ulimwenguni—na (2) Kuanzishwa kwa Ufalme wa Mesiya ulimwenguni.”
Hilo lingetukiaje? Ilionekana kuwa yafaa kwa Wanafunzi wa Biblia wakati huo kwamba huko kungetia ndani utukuzo wa wowote walio duniani bado ambao walikuwa wamechaguliwa na Mungu kushiriki katika Ufalme wa kimbingu pamoja na Kristo. Lakini walihisije wakati hilo lilipokosa kutukia katika 1914? The Watch Tower la Aprili 15, 1916, lilisema: “Tunaamini kwamba tarehe zimethibitika kuwa sahihi kikweli. Tunaamini kwamba Nyakati za Mataifa zimekwisha.” Hata hivyo, uliongezea hivi waziwazi: “Bwana hakusema kwamba Kanisa lote lingetukuzwa kufikia 1914. Tulifanya mkataa huo tu na, bila shaka tukakosea.”
Katika jambo hilo walikuwa kama mitume wa Yesu. Mitume walijua na walifikiri waliamini unabii mbalimbali kuhusu Ufalme wa Mungu. Lakini katika nyakati mbalimbali walikuwa na matarajio yenye makosa kuhusu ni jinsi gani na lini hayo yangetimizwa. Hilo lilifanya wengine wakate tamaa.—Luka 19:11; 24:19-24; Mdo. 1:6.
Wakati Oktoba 1914 ulipopita bila badiliko lililotazamiwa la uhai wa kimbingu, Ndugu Russell alijua kwamba kungekuwako kujipekuapekua sana moyo. Katika The Watch Tower la Novemba 1, 1914, aliandika: “Acheni tukumbuke kwamba sisi tumo katika majira ya kutahini. Mitume walikuwa na majira kama hayo wakati wa muda wa kati ya kifo cha Bwana na Pentekoste. Baada ya kufufuliwa kwa Bwana, Yeye alitokea wanafunzi Wake mara chache, na hawakumwona Yeye kwa siku nyingi. Kisha wakakata tamaa na kusema, ‘Hakuna haja ya kungoja’; ‘Ninaenda kuvua samaki,’ mmoja akasema. Wengine wawili wakasema, ‘Tutaenda nawe.’ Walitaka kwenda kwenye biashara ya uvuvi na kuacha kazi ya kuvua watu. Huo ulikuwa wakati wenye kutahini kwa wanafunzi. Vivyo hivyo wakati huo upo sasa. Ikiwa kuna sababu yoyote ambayo ingeongoza yeyote kuacha Bwana na Kweli Yake na kuacha kutoa dhabihu kwa ajili ya Kusudi la Bwana, basi si upendo wa Mungu tu ndani ya moyo ambao umesukuma kupendezwa katika Bwana, bali jambo jingine; labda kutumaini kwamba wakati ulikuwa mfupi; kujitakasa kulikuwa kwa wakati fulani tu.”
Mambo yalionekana kuwa hivyo kwa watu fulani. Fikira na tamaa zao zilikuwa zimekazwa hasa juu ya taraja la kuweza kubadilishwa kwenye uhai wa kimbingu. Hilo lilipokosa kutukia katika wakati uliotarajiwa, walikosa kuona maana ya mambo yenye kushangaza yaliyotukia katika 1914. Walikosa kutambua kweli zote zenye thamani ambazo walikuwa wamejifunza kutoka kwa Neno la Mungu, na wakaanza kuwadhihaki watu ambao walikuwa wamewasaidia kujifunza hizo.
Kwa unyenyekevu, Wanafunzi wa Biblia walichunguza Maandiko tena, ili waache Neno la Mungu libadilishe mtazamo wao. Usadikisho wao kwamba Nyakati za Mataifa zilikuwa zimekwisha mwaka 1914 haukubadilika. Hatua kwa hatua walikuja kuona waziwazi zaidi jinsi Ufalme wa Kimesiya ulivyokuwa umeanza—kwamba ulisimamishwa mbinguni wakati Yehova alipokabidhi mamlaka kwa Yesu Kristo, Mwanae; pia, kwamba hilo halikuhitaji kungojea hadi warithi-washiriki wa Yesu wainuliwe kwenye uhai wa kimbingu bali kwamba wangetukuzwa naye baadaye. Kwa kuongezea, walikuja kuona kwamba kuenezwa kwa uvutano wa Ufalme hakukuhitaji kwanza manabii waaminifu wa zamani wafufuliwe, bali Mfalme angetumia Wakristo waaminifu-washikamanifu wanaoishi sasa kuwa wawakilishi wake kuwatolea watu wa mataifa yote fursa ya kuishi milele wakiwa raia wa kidunia wa Ufalme.
Mwono huo mtukufu ulipofunuka machoni pao, walitahiniwa na kupepetwa zaidi. Lakini wale waliompenda Yehova kikweli na wakafurahi kumtumikia walikuwa wenye shukrani kwa mapendeleo ya utumishi yaliyofunguka kwa ajili yao.—Ufu. 3:7, 8.
Mmoja wao alikuwa A. H. Macmillan. Baadaye aliandika: “Ingawa mataraja yetu kuhusu kuchukuliwa hadi mbinguni hayakutimizwa katika 1914, mwaka huo ndio uliokuwa mwisho wa Nyakati za Mataifa . . . Hatukusikitika sana hasa kwamba kila kitu hakikutukia kama vile tulivyokuwa tumetazamia, kwa sababu tulikuwa wenye shughuli mno na kazi ya Photo-Drama na matatizo yaliyoletwa na vita.” Yeye aliendelea kuwa mwenye shughuli katika utumishi wa Yehova na alisisimuliwa kuona idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme ikiongezeka kufikia zaidi ya milioni moja wakati wa maisha yake.
Akitazama nyuma kwenye mambo aliyoona wakati wa miaka 66 katika tengenezo, yeye alisema: “Nimeona majaribu mengi makali yakikumba tengenezo na kutahiniwa kwa imani ya wale waliomo. Kwa msaada wa roho ya Mungu tengenezo liliokoka na likaendelea kusitawi.” Kuhusu marekebisho ya uelewevu kadiri wakati ulivyopita, yeye aliongeza: “Kweli za msingi tulizojifunza kutoka kwa Maandiko zilibaki vilevile. Kwa hiyo nilijifunza kwamba tunapaswa kukubali makosa yetu na kuendelea kutafuta katika Neno la Mungu ili kupata nuru zaidi. Hata iwe ni mabadiliko gani ambayo tungelazimika kufanya wakati mmoja au mwingine katika maoni yetu, hilo halingebadili uandalizi wa fadhili wa fidia na ahadi ya Mungu ya uhai wa milele.”
-
-
Kutahini na Kupepeta Kuanzia NdaniMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 634]
C. J. Woodworth
Akiandikia mmoja aliyeacha utumishi wa Yehova kwa sababu wafuasi wa Yesu Kristo watiwa-mafuta hawakuchukuliwa hadi mbinguni katika 1914, C. J. Woodworth alisema:
“Miaka 20 iliyopita wewe na mimi tuliamini katika ubatizo wa vitoto; katika haki ya Kimungu ya makasisi kutoa ubatizo huo; kwamba ubatizo ulikuwa wa lazima ili kuepuka mateso ya milele; kwamba Mungu ni upendo; kwamba Mungu aliumba na aendelea kuumba mabilioni ya viumbe katika mfano Wake ambao kwa mihula ya umilele watakuwa kwenye mioto yenye kusonga ya kiberiti chenye kuwaka, wakiomba tone moja la maji lipunguze uchungu wao bila kufanikiwa . . .
“Tuliamini kwamba baada ya mtu kufa, yeye yuko hai; tuliamini kwamba Yesu Kristo hakufa kamwe; kwamba Yeye hangeweza kufa; kwamba hakuna Fidia iliyopata kulipwa au itapata kulipwa; kwamba Yehova Mungu na Kristo Yesu Mwana Wake ni mtu yuleyule mmoja; kwamba Kristo alikuwa ndiye Baba Yake mwenyewe; kwamba Yesu alikuwa ndiye Mwana Wake mwenyewe; kwamba Roho Takatifu ni mtu; kwamba moja kuongeza moja, kuongeza moja, tokeo ni moja; kwamba wakati Yesu alipotundikwa kwenye msalaba na kusema, ‘Mungu Wangu, Mungu Wangu, mbona Umeniacha,’ Yeye alikuwa tu akijisemeza; . . . kwamba falme za sasa ni sehemu ya Ufalme wa Kristo; kwamba Ibilisi amekuwa mbali mahali fulani katika Helo isiyojulikana mahali ipo, badala ya kuwa na umiliki juu ya falme za dunia hii . . .
“Ninamsifu Mungu kwa siku ambayo alileta Kweli ya Sasa mlangoni pangu. Ilikuwa yenye kufaa sana, yenye kuburudisha akili na moyo sana, hivi kwamba niliacha upesi uwongo na mambo ya upuuzi ya zamani na nikatumiwa na Mungu kufungua pia macho yako yaliyopofushwa. Tulishangilia pamoja katika Kweli, tukifanya kazi pamoja kwa miaka kumi na mitano. Bwana alikustahi sana ukiwa msemaji; Sikupata kamwe kumjua mtu ambaye angeweza kufunua uwongo wa Babiloni kama wewe. Katika barua yako unauliza, ‘Ni nini kinachofuata?’ Lo! sasa ndiyo sehemu yenye kuhuzunisha! Kitu kinachofuata ni kwamba unaruhusu moyo wako umchukie yule ambaye kazi zake za upendo na baraka zake kutoka Juu zilileta Kweli kwa mioyo yetu sote wawili. Uliacha tengenezo, na kuchukua kondoo kadhaa pamoja nawe. . . .
“Labda ninaonekana kuwa mpuuzi kwako kwa sababu sikuenda Mbinguni, Oktoba 1, 1914, lakini wewe huonekani kuwa mpuuzi kwangu—la hasha!
“Wakati huu ambapo mataifa kumi makubwa kati ya mataifa ya dunia yanafurukuta katika uchungu mkali wa kifo chayo, kwangu inaonekana kuwa wakati usiofaa hasa kumdhihaki mtu huyo, na mtu pekee, ambaye kwa miaka arobaini amefundisha kwamba Nyakati za Mataifa zingekoma katika 1914.”
Imani ya Ndugu Woodworth haikutikisika wakati matukio ya 1914 yalipokosa kutimiza yale yaliyotarajiwa. Yeye aling’amua tu kwamba kulikuwa na mengi zaidi ya kujifunza. Kwa sababu ya tumaini lake katika kusudi la Mungu, alifungwa miezi tisa gerezani katika 1918-1919. Baadaye alitumikia akiwa mhariri wa magazeti “The Golden Age” na “Consolation.” Alibaki imara katika imani na mwaminifu-mshikamanifu kwa tengenezo la Yehova hadi kufikia kifo chake katika 1951, akiwa mwenye umri wa miaka 81.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 637]
A. H. Macmillan
“Nimeona hekima ya kumngoja Yehova kwa subira ili atueleweshe vizuri zaidi mambo ya Kimaandiko badala ya kukasirika kwa ajili ya wazo jipya. Nyakati nyingine matarajio yetu ya tarehe fulani yalikuwa zaidi ya yale ambayo Maandiko yaliruhusu. Wakati matarajio hayo yalipokosa kutimizwa, hilo halikubadili makusudi ya Mungu.”
-