Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mungu Amenionyesha Rehema
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Julai 1
    • Mungu Amenionyesha Rehema

      Limesimuliwa na Bolfenk Moc̆nik

      “Jikaze sasa.” Hayo yalikuwa maneno thabiti ya Mama aliponikumbatia. Baada ya wanamgambo kututenganisha, kesi ikaanza. Mwishowe nilihukumiwa kifungo cha miaka mitano gerezani. Huenda watu wengi wangevunjika moyo. Lakini kwa kweli, mwishowe nilihisi amani nyingi ya moyoni. Acheni niwaeleze.

      MATUKIO yanayotajwa hapo juu yalitukia mnamo 1952 huko Slovenia.a Lakini simulizi langu linaanza zaidi ya miaka 20 kabla, katika 1930. Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, walipanga ubatizo kwa ajili ya kikundi cha kwanza katika nchi yetu. Wazazi wangu, Berta na Franz Moc̆nik, walikuwa miongoni mwa wale waliobatizwa. Nilikuwa na umri wa miaka sita, na dada yangu, Majda, alikuwa na umri wa miaka minne. Nyumba yetu ilikuwa kituo cha utendaji wa Kikristo katika jiji la Maribor.

      Adolf Hitler alianza kutawala nchini Ujerumani mnamo 1933 na akaanza kuwatesa Mashahidi. Ili kusaidia kazi ya kuhubiri, Mashahidi wengi Wajerumani walihamia Yugoslavia. Wazazi wangu walifurahia kuwakaribisha wageni waaminifu kama hao. Mgeni mmoja ninayekumbuka vizuri ni Martin Poetzinger, ambaye baadaye alifungwa kwa miaka tisa katika kambi za mateso za Nazi. Baadaye, kuanzia 1977 mpaka kifo chake katika 1988, alitumika akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.

      Sikuzote alipotutembelea, Martin alilala katika kitanda changu, na mimi na dada yangu tulilala kwenye chumba kimoja na wazazi wetu. Alikuwa na ensaiklopidia ndogo yenye rangi mbalimbali ambayo ilinipendeza sana nikiwa mtoto. Nilifurahia kuangalia kurasa mbalimbali za kitabu hicho.

      Wakati wa Majaribu Makali

      Mnamo 1936, utawala wa Hitler ulipokuwa ukiongezeka, wazazi wangu walihudhuria kusanyiko muhimu sana la kimataifa huko Lucerne, Uswisi. Kwa kuwa Baba alikuwa na sauti tamu, wakati huo alichaguliwa arekodi hotuba za Biblia ambazo baadaye zilisikilizwa na wenye nyumba kotekote nchini Slovenia. Muda mfupi baada ya kusanyiko hilo, Mashahidi huko Ulaya walianza kuteswa vibaya. Wengi waliteswa na kufa wakiwa katika kambi za mateso za Nazi.

      Katika Septemba (Mwezi wa 9) 1939, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilianza, na kufikia Aprili (Mwezi wa 4) 1941, majeshi ya Wajerumani yalikuwa yamechukua maeneo fulani ya Yugoslavia. Shule za Kislovenia zilifungwa na watu wakakatazwa kuzungumza lugha hiyo hadharani. Kwa sababu Mashahidi wa Yehova hawaungi mkono upande wowote katika mizozo ya kisiasa, walikataa kuunga mkono vita.b Kwa sababu hiyo, wengi walifungwa gerezani na wengine waliuawa—kutia ndani kijana anayeitwa Franc Drozg, ambaye nilimfahamu vizuri. Kwa kawaida, askari wa Nazi waliwapiga watu risasi karibu na nyumba yetu. Bado ninaweza kumkumbuka Mama akifunga masikio yake na kitambaa, akijaribu kuziba kelele za risasi. Maneno ya mwisho katika barua ya Franc aliyomwandikia rafiki wa karibu yalikuwa, “Tutaonana katika Ufalme wa Mungu.”

      Jambo Ninalojutia Sana

      Nilikuwa na umri wa miaka 19 wakati huo. Hata ingawa nilipendezwa na Franc kwa msimamo wake thabiti, niliogopa. Je, mimi pia ningekufa? Imani yangu haikuwa yenye nguvu, na sikuwa na uhusiano wa karibu na Yehova Mungu. Kisha nikaitwa niende jeshini. Woga wangu ulikuwa mwingi kuliko imani yangu, kwa hiyo nikakubali kwenda jeshini.

      Nilitumwa nikapigane dhidi ya Urusi. Baada ya muda niliwaona wenzangu wakifa kwa wingi. Vita vilitisha na vilikuwa vyenye ukatili. Dhamiri yangu ilinisumbua zaidi na zaidi. Nilimwomba Yehova msamaha na nguvu ili niweze kutembea katika njia inayofaa. Shambulizi kali la kivita liliposababisha mvurugo kambini mwetu, nilipata fursa ya kutoroka.

      Nilijua kwamba ikiwa ningekamatwa, ningeuawa. Katika miezi saba iliyofuata, nilijificha katika maeneo mbalimbali. Hata nilifaulu kumtumia Majda kadi yenye maneno haya: “Nimemwacha mwajiri wangu na sasa ninamfanyia mwajiri mwingine kazi.” Nilimaanisha kwamba nilitaka kumfanyia Mungu kazi sasa, lakini muda ulipita kabla ya kufanya hivyo.

      Mnamo Agosti (Mwezi wa 8) 1945, miezi mitatu baada ya Wajerumani kushindwa na Majeshi ya Muungano, nilifaulu kurudi Maribor. Jambo la kupendeza ni kwamba sisi sote, yaani, baba, mama, na dada yangu, tuliokoka vita hivyo vibaya. Hata hivyo, kufikia wakati huo, Wakomunisti walikuwa mamlakani, na walikuwa wakiwatesa Mashahidi wa Yehova. Kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku, lakini Mashahidi waliendelea kuhubiri kwa siri.

      Katika Februari (Mwezi wa 2) 1947, Mashahidi watatu waaminifu—Rudolf Kalle, Dus̆an Mikić, na Edmund Stropnik—walihukumiwa kifo. Hata hivyo, baadaye hukumu hiyo ilibadilishwa na kuwa kifungo cha miaka 20. Mashirika ya habari yalionyesha hayo kwa undani, na hivyo kuwafanya watu wengi wajue jinsi Mashahidi walivyotendwa isivyo haki. Baada ya kusoma habari hizo, nilichomwa moyoni. Nilitambua nilichopaswa kufanya.

      Napata Nguvu za Kiroho

      Nilijua vizuri sana kwamba nilihitaji kuchukua msimamo kwa ajili ya kweli za Biblia, kwa hiyo niliongeza jitihada za kutumiwa katika kazi yetu ya kuhubiri kwa siri. Kwa sababu ya kusoma Biblia kwa uangalifu, nilipata nguvu za kiroho zilizoniwezesha kuacha tabia chafu, kama vile kuvuta sigara.

      Mnamo 1951, nilibatizwa ili kuonyesha wakfu wangu kwa Mungu, na hivyo nikarudia njia ya maisha niliyoacha miaka kumi hivi mapema. Mwishowe, nilianza kuhisi kwamba Yehova ni Baba wa kweli—mwaminifu, mshikamanifu, na mwenye upendo usiokoma. Ingawa nilikuwa nimefanya uamuzi mbaya nikiwa kijana, niliguswa sana na uhakikisho wa Biblia wa msamaha wa Mungu. Akiwa Baba mwenye upendo, Mungu aliendelea kunivuta “kwa kamba za upendo.”—Hosea 11:4.

      Katika kipindi hicho kigumu, tulifanya mikutano ya Kikristo kwa siri katika nyumba za Mashahidi kadhaa, na tuliendelea na kazi ya kuhubiri isivyo rasmi. Hata kabla ya mwaka mmoja kwisha baada ya ubatizo wangu, nilikamatwa. Mama aliniona kwa muda mfupi kabla ya kesi yangu. Kama nilivyotaja mwanzoni, alinikumbatia kwa upendo na kunihimiza: “Jikaze sasa.” Nilipopewa hukumu ya kufungwa gerezani kwa miaka mitano, nilibaki mtulivu na thabiti.

      Nilifungiwa katika chumba kidogo pamoja na wafungwa wengine watatu, kwa hiyo niliweza kushiriki kweli ya Biblia na watu ambao hawangefikiwa kwa njia nyingine. Ingawa sikuwa na Biblia au vichapo vya Biblia, nilishangaa kwamba niliweza kukumbuka maandiko na ufafanuzi wake kutokana na saa nilizotumia katika kujifunza Biblia kibinafsi. Niliwaambia wafungwa wenzangu mara kwa mara kwamba ikiwa nilihitaji kutumika gerezani kwa miaka mitano, Yehova angenipa nguvu za kufanya hivyo. Hata hivyo, huenda angefungua njia mapema. Nilijiambia, ikiwa angefanya hivyo, ni nani angeweza kufunga njia hiyo?

      Kutumika Tukiwa na Uhuru wa Kadiri

      Mnamo Novemba (Mwezi wa 11) 1953, serikali ilitoa msamaha; Mashahidi wa Yehova wote waliokuwa gerezani waliachiliwa. Kisha niligundua kwamba marufuku dhidi ya kazi yetu ilikuwa imeondolewa miezi miwili mapema. Mara moja tulianza kupanga upya makutaniko na kazi yetu ya kuhubiri. Tulipata mahali pa kukutania katika chumba cha chini katika jengo katikati ya Maribor. Tulibandika ishara kwenye ukuta iliyosema: “Mashahidi wa Yehova—Kutaniko la Maribor.” Shangwe ya kumtumikia Yehova kwa uhuru ilifanya mioyo yetu ifurike kwa uthamini.

      Mwanzoni mwa 1961, nilianza utumishi wa wakati wote nikiwa painia.

  • Mungu Amenionyesha Rehema
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Julai 1
    • [Picha katika ukurasa wa 27]

      Kuanzia kushoto kuelekea kulia: Wazazi wangu, Berta na Franz Moc̆nik, Majda, na mimi, huko Maribor, Slovenia, katika miaka ya 1940

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki