-
Kutambua Daraka la Yesu Akiwa Daudi Mkuu Zaidi na Sulemani Mkuu ZaidiMnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 15
-
-
Sala ya Sulemani ya Kuomba Hekima Yajibiwa
12. Sulemani aliomba nini katika sala?
12 Sulemani mwana wa Daudi alimfananisha pia Yesu.c Sulemani alipokuwa mfalme, Yehova alimtokea katika ndoto na kumwambia kwamba Angempa kitu chochote ambacho angeomba. Sulemani angeweza kuomba utajiri zaidi, mamlaka, au maisha marefu zaidi. Badala yake, alimwomba hivi Yehova bila ubinafsi: “Sasa unipe hekima na ujuzi ili nitoke mbele ya watu hawa na ili niingie ndani, kwa maana ni nani anayeweza kuwahukumu hawa watu wako walio wengi?” (2 Nya. 1:7-10) Yehova alijibu sala ya Sulemani.—Soma 2 Mambo ya Nyakati 1:11, 12.
13. Sulemani alikuwa na hekima isiyo na kifani jinsi gani, na ilitoka wapi?
13 Maadamu Sulemani alikuwa mwaminifu kwa Yehova, alisema maneno yenye hekima kuliko watu wote katika siku zake. Sulemani alisema “methali elfu tatu.” (1 Fal. 4:30, 32, 34) Methali zake nyingi ziliandikwa na bado zinathaminiwa sana na watu wanaotafuta hekima. Malkia wa Sheba alisafiri umbali wa kilomita 2,400 ili kuijaribu hekima ya Sulemani kwa “maswali yenye kutatanisha.” Alivutiwa sana na mambo ambayo Sulemani alisema na pia ufanisi wa ufalme wake. (1 Fal. 10:1-9) Biblia inafunua Chanzo cha hekima ya Sulemani inaposema hivi: “Watu wote wa dunia walikuwa wakiutafuta uso wa Sulemani ili wasikie hekima yake ambayo Mungu alikuwa ametia moyoni mwake.”—1 Fal. 10:24.
Mfuate Yule Mfalme Mwenye Hekima
14. Ni katika njia gani Yesu alikuwa “mtu mkuu kuliko Sulemani”?
14 Ni mwanadamu mmoja tu aliyekuwa na hekima nyingi sana kuliko Sulemani. Mwanadamu huyo ni Yesu Kristo, ambaye alisema kwamba alikuwa “mtu mkuu kuliko Sulemani.” (Mt. 12:42) Yesu alisema “maneno ya uzima wa milele.” (Yoh. 6:68) Kwa mfano, Mahubiri ya Mlimani yanaeleza kindani kanuni za methali fulani za Sulemani. Sulemani alieleza mambo mbalimbali yanayomletea furaha mwabudu wa Yehova. (Met. 3:13; 8:32, 33; 14:21; 16:20) Yesu alikazia kwamba furaha ya kweli inatokana na mambo yanayohusiana na ibada ya Yehova na kutimia kwa ahadi za Mungu. Alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mt. 5:3) Wale wanaofuata kanuni zilizo katika mafundisho ya Yesu wanakuwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova, “chemchemi ya uzima.” (Zab. 36:9; Met. 22:11; Mt. 5:8) Kristo anawakilisha “hekima ya Mungu.” (1 Kor. 1:24, 30) Akiwa Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo ana “roho ya hekima.”—Isa. 11:2.
15. Tunaweza kufaidika namna gani kutokana na hekima inayotoka kwa Mungu?
15 Tukiwa wafuasi wa yule Sulemani Mkuu Zaidi, tunaweza kufaidika namna gani kutokana na hekima inayotoka kwa Mungu? Kwa kuwa hekima ya Yehova inafunuliwa katika Neno lake, ni lazima tujitahidi sana kuipata kwa kujifunza Biblia kwa makini, hasa maneno ya Yesu yaliyoandikwa, na kutafakari mambo tunayosoma. (Met. 2:1-5) Kwa kuongezea, tunahitaji kuendelea kumwomba Mungu hekima bila kuchoka. Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba sala zetu za kutoka moyoni za kuomba msaada zitajibiwa. (Yak. 1:5) Kwa msaada wa roho takatifu, tutapata hazina za hekima katika Neno la Mungu ambazo zinaweza kutusaidia kupambana na matatizo na kufanya maamuzi yenye hekima. (Luka 11:13) Sulemani aliitwa pia “mkutanishaji” ambaye “aliendelea kuwafundisha watu ujuzi.” (Mhu. 12:9, 10) Yesu, akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo, pia ni mkutanishaji wa watu wake. (Yoh. 10:16; Kol. 1:18) Kwa hiyo, tunapaswa kuhudhuria mikutano ya kutaniko, ambamo ‘tunaendelea kufundishwa.’
16. Sulemani na Yesu wanalingana katika njia gani?
16 Sulemani alikuwa mfalme mwenye bidii sana. Alipanga programu ya ujenzi katika taifa lote, alisimamia ujenzi wa majumba ya kifalme, barabara, mifereji ya maji, majiji yenye maghala, majiji ya magari ya vita, na majiji ya wapanda-farasi. (1 Fal. 9:17-19) Miradi yake ya ujenzi ilinufaisha ufalme wake wote. Yesu pia ni mjenzi. Alijenga kutaniko lake juu ya “mwamba.” (Mt. 16:18) Yeye pia atasimamia kazi ya ujenzi itakayofanywa katika ulimwengu mpya.—Isa. 65:21, 22.
Mfuate Yule Mfalme wa Amani
17. (a) Utawala wa Sulemani ulikuwa na sifa gani ya pekee? (b) Sulemani hangeweza kufanya nini?
17 Jina Sulemani linatokana na neno linalomaanisha “amani.” Mfalme Sulemani alitawala akiwa Yerusalemu. Jina Yerusalemu linamaanisha “Umilikaji wa Amani Mara Mbili.” Utawala wake wa miaka 40 ulikuwa na amani isiyo na kifani katika taifa la Israeli. Biblia inasema hivi kuhusu miaka hiyo: “Yuda na Israeli wakaendelea kukaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake mwenyewe na chini ya mtini wake mwenyewe, kuanzia Dani mpaka Beer-sheba, siku zote za Sulemani.” (1 Fal. 4:25) Hata hivyo, ingawa Sulemani alikuwa na hekima nyingi sana hakuweza kuwaweka huru raia wake kutoka katika utumwa wa magonjwa, dhambi, na kifo. Lakini, yule Sulemani Mkuu Zaidi, atawaweka huru raia wake kutoka katika utumwa huo wote.—Soma Waroma 8:19-21.
18. Tunafurahia hali gani katika kutaniko la Kikristo?
18 Hata sasa tunafurahia amani katika kutaniko la Kikristo. Kwa hakika, tunafurahia paradiso ya kiroho iliyo ya kweli. Tuna amani pamoja na Mungu na wanadamu wenzetu. Ona kwamba Isaya alitabiri kuhusu baraka ambazo tunafurahia leo: “Nao watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Taifa halitainua upanga juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.” (Isa. 2:3, 4) Tunapotenda kupatana na roho ya Mungu, tunachangia umaridadi wa paradiso hiyo ya kiroho.
19, 20. Tuna sababu gani za kushangilia?
19 Hata hivyo, hali zitakuwa bora hata zaidi wakati ujao. Wanadamu watiifu watakapofurahia amani isiyo na kifani chini ya utawala wa Yesu, ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu’ hatua kwa hatua mpaka watakapofikia ukamilifu wa kibinadamu. (Rom. 8:21) Baada ya kupita mtihani wa mwisho mwishoni mwa utawala wa Miaka Elfu Moja, “wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” (Zab. 37:11; Ufu. 20:7-10) Kwa kweli, utawala wa Kristo Yesu utakuwa bora zaidi kuliko utawala wa Sulemani kwa njia ambazo hatuwezi kamwe kuwazia!
-
-
Kutambua Daraka la Yesu Akiwa Daudi Mkuu Zaidi na Sulemani Mkuu ZaidiMnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 15
-
-
c Inapendeza kwamba jina la pili la Sulemani lilikuwa Yedidia, ambalo linamaanisha “Mpendwa wa Yah.”—2 Sam. 12:24, 25.
-