Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Paradiso ya Kiroho Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Machi 1
    • Neno la Kiswahili “paradiso” linahusiana na maneno ya Kigiriki, Kiajemi, na Kiebrania ambayo yote huwa yana maana ya bustani, mahali pa starehe pa mapumziko. Biblia yaahidi kwamba siku moja dunia itakuwa paradiso halisi, makao ya kibustani kwa jamii ya wanadamu isiyo na dhambi. (Zaburi 37:10, 11) Tukikumbuka hilo, twaona kwamba paradiso ya kiroho ni mazingira yanayopendeza macho na yenye kuburudisha, yanayofanya mtu afurahie amani pamoja na mwanadamu mwenzake na pamoja na Mungu.

  • Paradiso ya Kiroho Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Machi 1
    • Paradiso ya Kiroho Ni Nini?

      Jambo moja linalofanya Mashahidi wa Yehova wawe tofauti ni uthamini wao wa ujuzi wa Biblia. Wanaamini kwamba Biblia ni ya kweli na kwamba ni Neno la Mungu. Kwa sababu hiyo, hawatosheki kujua tu mambo ya msingi ya dini yao. Wana ratiba yenye kuendelea ya funzo la kibinafsi na usomaji wa Biblia. Kadiri mtu aendeleavyo kushirikiana na Mashahidi wa Yehova, ndivyo ajifunzavyo zaidi kuhusu Mungu na mapenzi Yake yanayoonyeshwa katika Biblia.

      Ujuzi huo huwaweka Mashahidi wa Yehova huru kutokana na mambo yanayonyang’anya watu wengi furaha, kama vile ushirikina na mawazo yenye kudhuru. Yesu alisema: “Kweli itawaweka nyinyi huru,” na Mashahidi wa Yehova wamethibitisha jambo hilo. (Yohana 8:32) Fernando, ambaye wakati mmoja alizoea kuwasiliana na roho waovu, asema hivi: “Kujifunza juu ya uhai udumuo milele kulikuwa msaada mkubwa sana. Nilikuwa na hofu ya kwamba ama mimi au wazazi wangu tungekufa.” Kweli ilimweka Fernando huru kutokana na hofu yake ya ulimwengu wa roho na yale yaitwayo eti maisha baada ya kifo.

      Katika Biblia, ujuzi kuhusu Mungu wahusiana sana na paradiso. Nabii Isaya alisema: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

      Bila shaka, ujuzi pekee hautoshi kuleta amani iliyotabiriwa na Isaya. Lazima mtu atende kulingana na yale anayojifunza. Fernando alitoa maelezo haya: “Mtu asitawishapo matunda ya roho, yeye huchangia paradiso ya kiroho.” Fernando alikuwa akirejezea maneno ya mtume Paulo, ambaye aliziita sifa nzuri ambazo Mkristo apaswa kusitawisha “matunda ya roho.” Aliyaorodhesha kuwa “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.”—Wagalatia 5:22, 23.

      Waweza kuona ni kwa nini kushirikiana na jamii ya watu ambao hujitahidi kusitawisha sifa hizo kwa kweli kungekuwa kama kuwa katika paradiso? Paradiso ya kiroho iliyotabiriwa na nabii Sefania ingekuwako miongoni mwa watu hao. Yeye alisema hivi: “Hawatatenda uovu, wala kusema uongo; wala ulimi wa hadaa hautaonekana kinywani mwao; kwa maana watakula na kulala, wala hapana mtu atakayewaogofya.”—Sefania 3:13.

      Umuhimu wa Upendo

      Huenda umeona kwamba tunda la kwanza la roho linalotajwa na Paulo ni upendo. Hiyo ni sifa ambayo Biblia huongea sana juu yake. Yesu alisema hivi: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Ni kweli kwamba, Mashahidi wa Yehova si wakamilifu. Mara nyingine wana matatizo ya kutoafikiana miongoni mwao wenyewe kama walivyokuwa mitume wa Yesu. Lakini kwa kweli wanapendana sana, nao husali wasaidiwe na roho takatifu wanapositawisha sifa hiyo.

      Tokeo ni kwamba, ibada yao haina kifani. Hakuna ukabila wala ubaguzi wa kitaifa wenye kuleta migawanyiko miongoni mwao. Mashahidi wa Yehova ambao wamejipata katikati ya mauaji ya kimakusudi ya makabila na maangamizi ya jamii nzimanzima miaka ya mwishomwisho ya karne ya 20 walilindana hata wakahatarisha maisha zao. Ijapokuwa ‘wanatoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha,’ wanafurahia umoja ambao ni vigumu kuuwazia hadi unapoushiriki mwenyewe.—Ufunuo 7:9.

      Paradiso Miongoni mwa Wale Wafanyao Mapenzi ya Mungu

      Paradiso ya kiroho hairuhusu pupa, ukosefu wa adili, na ubinafsi. Wakristo waambiwa hivi: “Komeni kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe umbo kwa kufanya upya akili yenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Tunapoishi maisha safi, yenye maadili na kufanya mapenzi ya Mungu katika njia nyingine, twasaidia kujenga paradiso ya kiroho na twajiletea wenyewe furaha. Carla aliona hilo kuwa la kweli. Anasema: “Baba yangu alinifundisha kufanya kazi kwa bidii ili nijitegemee kifedha. Lakini ingawa masomo yangu ya chuo kikuu yalinipa usalama, nilikosa umoja wa familia na usalama ambao huletwa tu na ujuzi kutoka katika Neno la Mungu.”

      Bila shaka, kufurahia paradiso ya kiroho hakuondoi matatizo ya maisha. Wakristo huwa wagonjwa. Taifa wanaloishi huenda likawa na zogo la kiraia. Wengi huvumilia umaskini. Hata hivyo, kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova Mungu—ambao ni sehemu muhimu ya paradiso ya kiroho—humaanisha kwamba twamtegemea kupata msaada. Kwa kweli, yeye hutualika ‘tumtwike mizigo yetu,’ na wengi wanaweza kusema juu ya njia ya ajabu ambayo amewategemeza wakati wa hali ngumu zaidi. (Zaburi 55:22; 86:16, 17) Mungu anaahidi kuwa pamoja na waabudu wake hata katika “bonde la uvuli wa mauti.” (Zaburi 23:4) Uhakika wa kwamba Mungu yuko tayari kututegemeza hudumisha ‘amani yetu ya Mungu izidiyo fikira yote,’ ambayo ni ufunguo wa paradiso ya kiroho.—Wafilipi 4:7.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki