-
Kufanya Kazi Katika “Shamba” Kabla ya MavunoMnara wa Mlinzi—2000 | Oktoba 15
-
-
Mwaka wa 1837, George Storrs mwenye umri wa miaka 40 alipata nakala moja kwenye garimoshi. Storrs alikuwa mzaliwa wa Lebanon, New Hampshire, lakini wakati huo alikuwa anaishi Utica, New York.
Alikuwa mhudumu mashuhuri sana katika Kanisa la Methodisti-Episkopali. Aliposoma kijitabu hicho, alivutiwa kuona jinsi hoja nzuri zilivyotolewa kupinga mafundisho ya msingi ya Jumuiya ya Wakristo, ambayo hakuwa amepata kuyatilia shaka. Hakujua mwandishi wa kijitabu hicho, na alikuja kukutana tu na Henry Grew miaka kadhaa baadaye, mwaka wa 1844, wakati ambapo wote wawili walikuwa wanaishi Philadelphia, Pennsylvania. Hata hivyo, Storrs alichunguza jambo hilo mwenyewe kwa miaka mitatu, na kulizungumzia tu na wahudumu wengine.
Hatimaye, kwa kuwa hakuna mtu aliyeweza kukanusha mambo aliyokuwa akijifunza, George Storrs aliamua kwamba hangeweza kuwa mwaminifu kwa Mungu kama angeendelea kushirikiana na Kanisa la Methodisti. Alijiuzulu mwaka wa 1840 na kuhamia Albany, New York.
Katika masika ya mwanzo-mwanzo wa mwaka wa 1842, kwa muda wa majuma sita, Storrs alitoa mfululizo wa hotuba sita wenye kichwa “Uchunguzi—Je, Waovu Ni Wasioweza Kufa?” Watu walipendezwa sana na hotuba hizo hivi kwamba alizisahihisha na kuzichapisha, na kwa miaka 40 iliyofuata, nakala 200,000 ziligawanywa Marekani na Uingereza. Storrs na Grew walifanya mijadala pamoja kupinga fundisho la kutokufa kwa nafsi. Grew aliendelea kuhubiri kwa bidii hadi alipokufa Agosti 8, 1862, huko Philadelphia.
Muda mfupi tu baada ya Storrs kutoa hotuba zile sita zilizotoka tu kutajwa, alipendezwa na mahubiri ya William Miller, aliyekuwa akitarajia kurudi kwa Kristo kunakoonekana mwaka wa 1843. Kwa miaka miwili hivi, Storrs alijihusisha sana katika kuhubiri ujumbe huo kotekote katika kaskazini-mashariki mwa Marekani. Baada ya 1844, hakuunga mkono tena kuweka tarehe yoyote ya kurudi kwa Kristo, hata hivyo hakupinga wale waliotaka kuchunguza kronolojia. Storrs aliamini kwamba kurudi kwa Kristo kulikuwa karibu na kwamba ilikuwa muhimu Wakristo waendelee kuwa macho kiroho, wakiwa tayari kwa ajili ya siku ya kukaguliwa. Lakini aliacha kushirikiana na kikundi cha Miller kwa sababu kilikubali mafundisho yasiyo ya Kimaandiko, kama vile kutokufa kwa nafsi, kuchomwa kwa ulimwengu, na kwamba wale wanaokufa kabla ya kujifunza hawana tumaini lolote la kuishi milele.
Upendo wa Mungu Ungeongoza Kwenye Nini?
Storrs alichukizwa na wazo la Waadventisti kwamba Mungu atafufua waovu akiwa na kusudi pekee la kuwaua tena. Hakupata uthibitisho wowote katika Maandiko kwamba Mungu angeweza kufanya tendo la aina hiyo lisilo na msingi na la kutaka kulipiza kisasi. Storrs na washiriki wake walishikilia maoni yaliyokuwa kinyume kabisa cha hayo na kukata kauli kwamba waovu hawatafufuliwa kamwe. Ingawa ilikuwa vigumu kwao kueleza maandiko fulani yaliyorejezea ufufuo wa wasio waadilifu, waliona mkataa wao kuwa unapatana zaidi na upendo wa Mungu. Punde si punde wangechukua hatua nyingine ya kuelewa kusudi la Mungu.
Mwaka wa 1870, Storrs akawa mgonjwa sana na hakuweza kufanya kazi kwa miezi kadhaa. Katika kipindi hicho, aliweza kuchunguza upya yote aliyokuwa amejifunza katika miaka yake yote 74. Alikata kauli kwamba alikuwa amekosa kusudi muhimu la Mungu kuhusu wanadamu kama lionyeshwavyo katika agano la Kiabrahamu—kwamba ‘familia zote za dunia zitabarikiwa kwa sababu Abrahamu alisikiliza sauti ya Mungu.’— Mwanzo 22:18; Matendo 3:25.
Jambo hilo lilimpa wazo jipya. Ikiwa “familia zote” zingebarikiwa, je, watu wote hawangehitaji kusikia habari njema? Wangeisikiaje? Je, mamilioni hawakuwa wamekufa tayari? Kwa kuchunguza Maandiko zaidi, alifikia mkataa kwamba kuna vikundi viwili vya watu “waovu” waliokufa: wale waliokataa katakata upendo wa Mungu na wale waliokufa kabla ya kujifunza.
Storrs alifikia mkataa kwamba kikundi cha pili kingehitaji kufufuliwa kutoka kwa wafu na kupewa fursa ya kunufaika na dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu. Wale ambao wangeikubali wangeishi milele duniani. Wale ambao wangeikataa wangeharibiwa. Naam, Storrs aliamini kwamba hakuna mtu ambaye angefufuliwa na Mungu bila kupewa tumaini naye. Hatimaye, hakuna mtu ambaye angekufa kutokana na dhambi ya Adamu isipokuwa Adamu! Lakini namna gani wale wanaoishi wakati wa kurudi kwa Bwana Yesu Kristo? Hatimaye Storrs aliona kwamba kampeni ya kuhubiri ulimwenguni pote ingehitaji kufanywa ili kuwafikia. Hakujua kwa vyovyote jinsi ambavyo kazi hiyo ingefanywa, lakini aliandika hivi kwa imani: “Watu wengi sana, wasipoelewa jinsi jambo fulani linavyopasa kufanywa hulikataa, kana kwamba Mungu hawezi kulifanya kwa sababu hawawezi kuona hatua hiyo.”
George Storrs alikufa Desemba 1879, nyumbani kwake Brooklyn, New York, majengo machache tu kutoka sehemu ambayo ingekuja kuwa kitovu cha kampeni ya kuhubiri ulimwenguni pote aliyokuwa ameitazamia kwa hamu.
-
-
Kufanya Kazi Katika “Shamba” Kabla ya MavunoMnara wa Mlinzi—2000 | Oktoba 15
-
-
Nuru Zaidi Ilihitajiwa
Je, watu kama vile Henry Grew na George Storrs walielewa ile kweli waziwazi kama tunavyoielewa leo? La. Walifahamu pambano lao kama alivyosema Storrs mwaka wa 1847: “Twapaswa kukumbuka kwamba tumetoka tu kwenye enzi za giza za kanisa; na hatutashangaa hata kidogo tukitambua kwamba tunaona mafundisho fulani ya Babiloni kuwa kweli.”
-
-
Kufanya Kazi Katika “Shamba” Kabla ya MavunoMnara wa Mlinzi—2000 | Oktoba 15
-
-
Vivyohivyo, George Storrs hakuelewa kwa usahihi mambo fulani muhimu. Aliweza kutambua mafundisho bandia yaliyofundishwa na makasisi, lakini nyakati fulani alichukua msimamo ulio kinyume kabisa. Kwa mfano, yaonekana baada ya kukasirishwa sana na imani inayokubaliwa na makasisi kuhusu Shetani, Storrs alipinga wazo la kwamba Ibilisi ni mtu halisi. Alikataa Utatu; hata hivyo, hakuwa na uhakika kama roho takatifu ni mtu ama sivyo hadi alipokaribia kufa. Ingawa George Storrs alitarajia kwamba kurudi kwa Kristo hakungeonekana hapo kwanza, hatimaye alifikiri kwamba kungeonekana.
-