-
Yehova—Mungu Aliye Hodari kwa Nguvu ZakeMnara wa Mlinzi—2000 | Machi 1
-
-
Yehova—Mungu Aliye Hodari kwa Nguvu Zake
“Kwa ukuu wa uweza wake, na kwa kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake; hapana moja isiyokuwapo mahali pake.”—ISAYA 40:26.
1, 2. (a) Sisi sote hutegemea chanzo gani cha nguvu? (b) Eleza ni kwa nini Yehova ndiye Chanzo kikuu cha nguvu zote.
WENGI wetu hupuuza nguvu. Kwa mfano, sisi hupuuza nguvu za umeme zinazotupa nuru na joto na pia sisi hupuuza kule kuunganisha tu kwenye umeme chombo chochote cha umeme ambacho huenda tukawa nacho. Umeme ukipotea bila kutarajiwa ndipo sisi hutambua kwamba bila nguvu za umeme majiji ya wanadamu yangekoma. Kwa njia isiyo ya moja kwa moja, umeme mwingi tunaotumia hutoka kwenye chanzo cha nguvu ambacho dunia hukitegemea zaidi—jua.a Kwa kila sekunde jua letu hutumia tani milioni tano za fueli ya nyuklia, likitawanyia dunia nishati yenye kuendeleza uhai.
2 Jua hupata wapi nguvu hizo zote? Ni nani aliyeumba jua? Ni Yehova Mungu. Mtunga-zaburi asema hivi akimrejezea kwenye Zaburi 74:16: “Ndiwe uliyeufanya mwanga na jua.” Ndiyo, Yehova ndiye Chanzo kikuu cha nguvu zote, kama alivyo Chanzo cha uhai wote. (Zaburi 36:9) Haitupasi kamwe kupuuza nguvu zake. Kupitia nabii Isaya, Yehova atukumbusha tutazame vitu vinavyoonekana angani, kama jua na nyota, na kutafakari juu ya jinsi vilivyotokea. “Inueni macho yenu juu, mkaone; ni nani aliyeziumba hizi; aletaye nje jeshi lao kwa hesabu; aziita zote kwa majina; kwa ukuu wa uweza wake, na kwa kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake; hapana moja isiyokuwapo mahali pake.”—Isaya 40:26; Yeremia 32:17.
3. Tunanufaikaje na maonyesho ya nguvu za Yehova?
3 Kwa kuwa Yehova ni hodari kwa nguvu zake, tuna hakika kwamba jua litaendelea kutoa nuru na joto ambazo uhai wetu wategemea. Hata hivyo, sisi hutegemea nguvu za Mungu kwa mambo mengi zaidi kuliko mahitaji yetu ya kimwili ya msingi. Ukombozi wetu kutokana na dhambi na kifo, tumaini letu la wakati ujao, na itibari yetu kwa Yehova, zote zinahusiana kabisa na jinsi anavyotumia nguvu zake. (Zaburi 28:6-9; Isaya 50:2) Biblia imejaa mifano inayothibitisha kwamba Yehova ana nguvu za kuumba na kukomboa, za kuokoa watu wake na kuwaangamiza adui zake.
Nguvu za Mungu Ni Dhahiri Katika Uumbaji
4. (a) Daudi aliitikiaje alipotazama anga la usiku? (b) Vitu vya angani vinafunua nini kuhusu nguvu za Mungu?
4 Mtume Paulo alieleza kwamba ‘nguvu za milele za Muumba zafahamiwa wazi kwa vitu alivyovifanya.’ (Waroma 1:20) Karne nyingi awali, mtunga-zaburi Daudi, ambaye akiwa mchungaji ni lazima awe alitazama anga la usiku mara nyingi, aliona utukufu wa ulimwengu na uweza wa Mfanyi wake. Aliandika: “Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota ulizoziratibisha; mtu ni kitu gani hata umkumbuke, na binadamu hata umwangalie?” (Zaburi 8:3, 4) Japo hakujua sana juu ya vitu vya angani, Daudi alifahamu kwamba yeye si kitu akilinganishwa na Muumba wa ulimwengu wetu mkubwa. Leo, wataalamu wa anga wanafahamu zaidi ukubwa wa ulimwengu na nguvu inayoudumisha. Kwa mfano, wao hutuambia kwamba kwa kila sekunde moja jua letu hutoa nishati inayotoshana na mlipuko wa tani milioni mara milioni 100,000 za TNT.b Na ni sehemu ndogo sana ya nguvu hizo inayofikia dunia; nayo inatosha kuendeleza uhai wa viumbe vyote duniani. Isitoshe, jua letu si nyota yenye nguvu zaidi katika mbingu. Nguvu ambazo nyota fulani hutoa kwa sekunde moja tu hutoshana na nguvu ambazo jua hutoa kwa siku nzima. Basi, ebu wazia nguvu za Muumba wa nyota hizo! Hakika, maneno haya ya Elihu yalikuwa kweli: “Yeye mwenyezi hamwezi kumwona; yeye ni mkuu mwenye uweza.”—Ayubu 37:23.
5. Tunapata ushuhuda gani wa nguvu za Yehova katika matendo yake?
5 ‘Tukiyafikiria matendo ya Mungu’ kama alivyofanya Daudi, tutaona uthibitisho wa nguvu zake kila mahali—katika pepo na mawimbi, katika ngurumo na radi, katika mito mikubwa na milima yenye fahari. (Zaburi 111:2; Ayubu 26:12-14) Na zaidi, kama Yehova alivyomkumbusha Yobu, wanyama hushuhudia nguvu Zake. Miongoni mwa wanyama hao mna Behemothi, au kiboko. Yehova alimwambia Yobu: “Nguvu zake ni katika viuno vyake . . . Mbavu zake ni kama vipande vya chuma.” (Ayubu 40:15-18) Katika nyakati za Biblia fahali wa mwitu alijulikana sana kuwa mwenye nguvu za kutisha, na Daudi alisali ili aokolewe kutokana na “kinywa cha simba, na pembe za fahali wa mwitu.”—Zaburi 22:21, NW; Ayubu 39:9-11.
6. Fahali hufananisha nini katika Maandiko, na kwa nini? (Ona kielezi-chini.)
6 Kwa sababu ya nguvu zake, fahali hutumiwa katika Biblia kufananisha uwezo wa Yehova.c Ono la mtume Yohana la kiti cha enzi cha Yehova laonyesha viumbe-hai wanne, na mmojawapo ana uso kama fahali. (Ufunuo 4:6, 7) Inaonekana kwamba mojawapo ya sifa kuu nne za Yehova zinazoonyeshwa na makerubi hao ni nguvu. Sifa nyinginezo ni upendo, hekima, na haki. Kwa kuwa nguvu ni sehemu muhimu sana ya utu wa Mungu, kufahamu vizuri nguvu zake na jinsi anavyozitumia kutatuvuta karibu zaidi naye na kutusaidia kuiga mfano wake kwa kutumia vizuri nguvu zetu.—Waefeso 5:1.
“Yehova wa Majeshi, Mwenye Nguvu”
7. Kwa nini tuna hakika kwamba wema utashinda uovu?
7 Katika Maandiko, Yehova anaitwa “Mungu Mweza-Yote,” mtajo unaotukumbusha kwamba hatupaswi kupuuza nguvu zake au kutilia shaka uwezo wake wa kushinda kabisa adui zake. (Mwanzo 17:1; Kutoka 6:3) Huenda mfumo mwovu wa Shetani ukaonekana kama umeimarika sana, lakini machoni pa Yehova “mataifa ni kama tone la maji katika ndoo, huhesabiwa kuwa kama mavumbi membamba katika mizani.” (Isaya 40:15) Kwa sababu Mungu ana nguvu hizo, hakuna shaka kwamba wema utashinda uovu. Wakati huu ambapo uovu umeenea, twaweza kupata faraja tukijua kwamba “Yehova wa majeshi, Mwenye Nguvu wa Israeli” ataondoa uovu milele.—Isaya 1:24, NW; Zaburi 37:9, 10.
8. Ni majeshi gani ya mbinguni yanayomtumikia Yehova, na ni jambo gani linaloonyesha nguvu zao?
8 Usemi “Yehova wa majeshi,” ambao umetajwa mara 285 katika Biblia (NW), unatukumbusha pia juu ya nguvu za Mungu. “Majeshi” yanayotajwa hapa ni viumbe-roho wanaomtumikia Yehova. (Zaburi 103:20, 21; 148:2) Katika usiku mmoja tu, mmoja wa malaika hao aliwaua wanajeshi 185,000 wa Ashuru ambao walikuwa wakitisha Yerusalemu. (2 Wafalme 19:35) Tukitambua nguvu za majeshi ya mbinguni ya Yehova, wapinzani hawatatutisha kwa urahisi. Nabii Elisha hakutishika walipozingirwa na kikosi kizima cha wanajeshi ambao walikuwa wakimtafuta kwa sababu, tofauti na mtumishi wake, yeye angeweza kuona kupitia imani kikosi kikubwa sana cha majeshi ya mbinguni kilichomwunga mkono.—2 Wafalme 6:15-17.
9. Kama Yesu, kwa nini tuwe na hakika katika ulinzi wa Mungu?
9 Vilevile, Yesu alijua kwamba anaungwa mkono na malaika alipokabili umati wa watu waliokuwa na mapanga na marungu katika bustani ya Gethsemane. Baada ya kumwambia Petro arudishe upanga wake mahali pake, Yesu alimwambia kwamba ikiwa lazima, anaweza kumwomba Baba yake “malejioni zaidi ya kumi na mawili ya malaika.” (Mathayo 26:47, 52, 53) Sisi pia tukifahamu kwamba Mungu anaweza kutumia majeshi ya mbinguni, tutaitibari kabisa kwamba atatutegemeza. Mtume Paulo aliandika: “Basi, tutasema nini kuhusu mambo haya? Ikiwa Mungu yuko upande wetu, nani atakayekuwa dhidi yetu?”—Waroma 8:31.
10. Yehova hutumia nguvu zake kwa niaba ya akina nani?
10 Basi tuna sababu nyingi za kuitibari ulinzi wa Yehova. Sikuzote yeye hutumia nguvu zake kwa njia yenye kuleta manufaa na kwa kupatana na sifa zake nyinginezo—haki, hekima, na upendo. (Ayubu 37:23; Yeremia 10:12) Ingawa watu wenye uwezo huwakandamiza maskini na wanyenyekevu ili kujinufaisha kibinafsi, Yehova ‘humwinua mnyonge kutoka mavumbini’ na yeye ni “hodari wa kuokoa.” (Zaburi 113:5-7; Isaya 63:1) Kama alivyoelewa Maria, mama ya Yesu aliyekuwa mwenye kiasi na mpole, “Mwenye nguvu” hutumia nguvu zake bila ubinafsi kwa niaba ya wale wanaomhofu, akiwadhalilisha wenye kiburi na kuwainua wenye hali ya chini.—Luka 1:46-53.
Yehova Aonyesha Watumishi Wake Nguvu Zake
11. Waisraeli waliona uthibitisho gani wa nguvu za Mungu mwaka wa 1513 K.W.K.?
11 Yehova aliwaonyesha watumishi wake uweza wake katika pindi kadhaa. Mojawapo ya pindi kama hizo ilikuwa kwenye Mlima Sinai mwaka wa 1513 K.W.K. Katika mwaka huo tayari Waisraeli walikuwa wameona uthibitisho mkubwa sana wa nguvu za Mungu. Mapigo kumi mazito sana yalionyesha jinsi Yehova alivyokuwa na nguvu na jinsi miungu ya Misri ilivyokuwa bure. Punde tu baadaye, kule kuvuka Bahari Nyekundu na kuangamizwa kwa majeshi ya Farao kulithibitisha hata zaidi nguvu za Mungu. Miezi mitatu baadaye, chini ya Mlima Sinai, Yehova aliwaalika Waisraeli wawe ‘tunu kwake kuliko makabila yote ya watu.’ Waisraeli nao wakaahidi: “Hayo yote aliyoyasema BWANA tutayatenda.” (Kutoka 19:5, 8) Kisha, Yehova akadhihirisha wazi nguvu zake. Kulikuwa na ngurumo na radi, na sauti kubwa ya baragumu huku Mlima Sinai ukitoa moshi na kutetemeka. Watu waliokuwa wamesimama mbali kidogo waliogofywa. Lakini Musa akawaambia kwamba mambo hayo waliyoona yapasa kuwafundisha kumhofu Mungu, hofu ambayo ingewasukuma wamtii Mungu wao Yehova, aliye wa pekee na wa kweli na ambaye ni mweza-yote.—Kutoka 19:16-19; 20:18-20.
12, 13. Ni hali zipi zilizomfanya Eliya aache mgawo wake, lakini Yehova alimwimarishaje?
12 Karne kadhaa baadaye, wakati wa Eliya, Mungu alionyesha nguvu zake tena kwenye Mlima Sinai. Tayari nabii huyo alikuwa ameshuhudia nguvu za Mungu. Kwa miaka mitatu na nusu, Mungu ‘alizifunga mbingu zisiwe na mvua’ kwa sababu taifa la Israeli liliasi. (2 Mambo ya Nyakati 7:13) Katika ukame uliofuata, kunguru walimlisha Eliya katika kijito cha Kerithi, na baadaye unga kidogo na mafuta kidogo ya mjane mmoja zikaendelezwa kimuujiza ili kumlisha Eliya. Yehova hata alimpa Eliya nguvu za kumfufua mwana wa mjane huyo. Hatimaye, katika jaribu lenye kutokeza la Uungu kwenye Mlima Karmeli, moto ukatoka mbinguni na kuteketeza dhabihu ya Eliya. (1 Wafalme 17:4-24; 18:36-40) Hata hivyo, punde tu baadaye, Eliya akaogopa na kuvunjika moyo Yezebeli alipotisha kumwua. (1 Wafalme 19:1-4) Alitoroka nchi hiyo, akifikiri kwamba kazi yake ya unabii ilikuwa imekwisha. Ili kumfariji na kumwimarisha, kwa fadhili Yehova mwenyewe alimwonyesha Eliya nguvu zake.
13 Eliya alipokuwa amejificha katika pango, aliona wonyesho wenye kustaajabisha sana wa nguvu tatu ambazo Yehova hudhibiti: upepo mkali, tetemeko la ardhi, na hatimaye moto. Lakini Yehova alipozungumza na Eliya, alisema kwa ‘sauti ndogo ya utulivu.’ Yehova alimpa kazi zaidi ya kufanya akimwambia kwamba katika nchi hiyo kungali kuna waabudu 7,000 wa Yehova walio waaminifu. (1 Wafalme 19:9-18) Kama Eliya, tukivunjika moyo kwa sababu ya kukosa matokeo katika huduma yetu, tunaweza kumwomba Yehova atupe “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida”—nguvu iwezayo kutuimarisha kuendelea kuhubiri habari njema bila kuacha.—2 Wakorintho 4:7.
Nguvu za Yehova Huhakikisha Kwamba Ahadi Zake Zatimizwa
14. Jina la Yehova binafsi lamaanisha nini, na nguvu zake zahusianaje na jina lake?
14 Nguvu za Yehova pia zahusiana sana na jina lake na kutekelezwa kwa mapenzi yake. Jina la kipekee la Yehova, linalomaanisha “Yeye Husababisha Iwe,” laonyesha kwamba yeye hujisababisha kuwa Mtimizaji wa ahadi. Hakuna kitu chochote kile ama mtu yeyote yule awezaye kumzuia Mungu asitimize ahadi zake, hata kama wenye kutilia shaka wanaona kama ahadi hizo haziwezi kutimizwa. Ni kama Yesu alivyowaambia mitume wake pindi moja, “kwa Mungu mambo yote yawezekana.”—Mathayo 19:26.
15. Abrahamu na Sara walikumbushwaje kwamba hakuna neno lililo gumu la kumshinda Yehova?
15 Kwa mfano, pindi moja Yehova alimwahidi Abrahamu na Sara kwamba angefanya wazao wao kuwa taifa kubwa. Hata hivyo walikaa bila kupata mtoto kwa miaka mingi. Wote wawili walikuwa wazee sana Yehova alipowaambia kwamba ahadi ile ilikaribia kutimizwa na Sara akacheka. Malaika akajibu: “Kuna neno gani lililo gumu la kumshinda BWANA?” (Mwanzo 12:1-3; 17:4-8; 18:10-14) Karne nne baadaye, hatimaye Musa alipowakusanya wazao wa Abrahamu—sasa wakiwa taifa kubwa—kwenye Uwanda wa Moabu, aliwakumbusha kwamba Mungu alitimiza ahadi yake. Musa alisema: “Kwa sababu [Yehova] aliwapenda baba zenu, kwa sababu hiyo aliwachagua wazao wao baada yao, akakutoa katika Misri kwa kuwako pamoja nawe, kwa uweza wake mwingi, ili kufukuza mbele yako mataifa, walio wakubwa, wenye nguvu kukupita wewe, ili kukuingiza, na kukupa nchi yao iwe urithi, kama ilivyo leo.”—Kumbukumbu la Torati 4:37, 38.
16. Kwa nini Masadukayo walikosea kwa kukana kuwa hakuna ufufuo wa wafu?
16 Karne kadhaa baadaye, Yesu aliwakemea Masadukayo, ambao hawakuamini ufufuo. Kwa nini walikataa kuamini ahadi ya Mungu ya kwamba angewafufua wafu? Yesu aliwaambia: “Hamjui wala Maandiko wala nguvu ya Mungu.” (Mathayo 22:29) Maandiko hutuhakikishia kwamba ‘wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti ya Mwana wa binadamu na kutoka.’ (Yohana 5:27-29) Tukijua isemavyo Biblia juu ya ufufuo, uhakika wetu katika nguvu za Mungu utatusadikisha kwamba wafu watafufuliwa. Mungu ‘atameza mauti hata milele. BWANA amenena hayo.’—Isaya 25:8.
17. Ni katika siku gani katika wakati ujao ambapo itakuwa muhimu sana kuitibari Yehova kwa njia ya pekee?
17 Karibuni, wakati utafika ambapo kila mmoja wetu atahitaji kuitibari nguvu zenye kuokoa za Mungu katika njia ya pekee. Shetani Ibilisi ataanza kushambulia watu wa Mungu, ambao wataonekana kana kwamba hawana ulinzi. (Ezekieli 38:14-16) Kisha Mungu atadhihirisha nguvu zake nyingi kwa niaba yetu, na kila mtu atalazimika kujua ya kwamba yeye ni Yehova. (Ezekieli 38:21-23) Huu ndio wakati wa kujenga imani na uhakika katika Mungu Mweza-Yote ili tuwe imara katika pindi hiyo muhimu.
18. (a) Tunapata manufaa zipi tunapotafakari juu ya nguvu za Yehova? (b) Ni swali gani litakalozungumziwa katika makala ifuatayo?
18 Bila shaka, kuna sababu nyingi za kutafakari juu ya nguvu za Yehova. Tunapotafakari juu ya matendo yake, twasukumwa kwa unyenyekevu kumsifu Muumba wetu Mtukufu na kushukuru kwamba yeye hutumia nguvu zake katika njia yenye hekima na yenye upendo. Hatuwezi kutishika kamwe tukimtumaini Yehova wa majeshi. Imani yetu katika ahadi zake itakuwa imara. Lakini kumbuka kwamba tumeumbwa kwa mfano wa Mungu. Hivyo, hata sisi tuna nguvu—japo kwa kadiri kidogo. Tunaweza kumwigaje Muumba wetu katika njia ambayo tunatumia nguvu zetu? Jambo hilo litazungumziwa katika makala ifuatayo.
[Maelezo ya Chini]
a Wengi wanaamini kwamba fueli zinazopatikana ardhini kama vile mafuta na makaa-mawe—ambazo ndizo hutegemewa sana na vituo vya umeme—hupata nishati kutoka kwenye jua.
b Kwa kulinganisha, bomu la nyuklia lenye nguvu zaidi ambalo limewahi kulipuliwa katika majaribio lilikuwa na nguvu zinazotoshana na tani milioni 57 za TNT.
c Yaelekea kwamba fahali wa mwitu anayetajwa katika Biblia ni auroch (Kilatini urus). Miaka elfu mbili iliyopita, wanyama hawa waliishi Gaul (ambayo sasa ni Ufaransa), na Juliasi Kaisari aliandika hivi juu yao: “Wanyama hao, uri, karibu watoshane na tembo, lakini tabia yao, rangi yao na umbo lao ni kama fahali. Wana nguvu nyingi sana, na wana mbio sana: hawamwachi mtu wala mnyama mara wanapowaona.”
-
-
“Tafuteni Bwana na Nguvu Yake”Mnara wa Mlinzi—2000 | Machi 1
-
-
“Tafuteni Bwana na Nguvu Yake”
“Macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.”—2 MAMBO YA NYAKATI 16:9.
1. Nguvu ni nini, na wanadamu wameitumiaje?
NGUVU inaweza kumaanisha mambo kadhaa, kama kuwa na udhibiti, mamlaka, au uwezo juu ya wengine; au inaweza kuwa uwezo wa kutenda na kupata matokeo; nguvu za kimwili; au uwezo wa kiakili au kimaadili. Wanadamu hawatumii nguvu vizuri. Mwanahistoria Lord Acton alisema hivi kuhusu nguvu za wanasiasa: “Nguvu hufisidi na nguvu kamili hufisidi kabisa.” Historia ya wakati huu imejaa mifano inayoonyesha ukweli wa maneno ya Lord Acton. Katika karne ya 20 ‘binadamu amekuwa na uwezo wa kumkandamiza na kumdhuru binadamu mwenzake’ kuliko wakati mwingine wowote. (Mhubiri 8:9, ZSB) Watawala wa kimabavu walio wafisadi wametumia nguvu zao vibaya sana na kuua mamilioni ya watu. Nguvu inayotumiwa bila upendo, hekima, na haki ni hatari.
2. Eleza jinsi sifa nyinginezo za Mungu zinavyohusika na jinsi ambavyo Yehova hutumia nguvu zake.
2 Tofauti na wanadamu, Mungu hutumia nguvu zake kwa manufaa. “Macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Yehova hudhibiti nguvu zake. Subira humzuia Mungu asiwaangamize waovu ili awape fursa ya kutubu. Upendo humfanya awaangazie jua watu wa namna zote—waadilifu na wasio waadilifu. Hatimaye haki itamfanya atumie nguvu zake zisizo na kikomo kumwangamiza kabisa yule ambaye husababisha kifo, Shetani Ibilisi.—Mathayo 5:44, 45; Waebrania 2:14; 2 Petro 3:9.
3. Kwa nini nguvu za Mungu mweza yote ni sababu nzuri ya kumwitibari?
3 Nguvu zenye kutisha za Baba yetu wa mbinguni zinafanya tuwe na itibari na uhakika katika ahadi zake na ulinzi wake. Mtoto mdogo hujiona salama miongoni mwa watu asiowajua akishika mkono wa babake, kwa kuwa anajua kwamba babake hatamwacha apatwe na madhara yoyote. Vilevile, Baba yetu wa mbinguni, aliye “hodari wa kuokoa,” atatulinda tusipatwe na madhara yoyote ya kudumu tukitembea pamoja naye. (Isaya 63:1; Mika 6:8) Na kama Baba mzuri, sikuzote Yehova hutimiza ahadi zake. Nguvu zake zisizo na kikomo huhakikisha kwamba ‘neno lake halitamrudia bure katika mambo yale analolituma.’—Isaya 55:11; Tito 1:2.
4, 5. (a) Ni nini kilichotokea Mfalme Asa alipomwitibari Yehova kabisa? (b) Ni nini kinachoweza kutendeka tukitegemea masuluhisho ya wanadamu kwa matatizo yetu?
4 Kwa nini ni jambo muhimu sana kuazimia kwamba hatutasahau twalindwa na Baba yetu wa mbinguni? Hii ni kwa sababu tunaweza kushindwa na hali zinazotukabili na kusahau mahali petu penye usalama halisi. Jambo hilo linaonekana katika mfano wa Mfalme Asa, ambaye kwa ujumla alimwitibari Yehova. Wakati wa utawala wa Asa, jeshi lenye nguvu sana la Waethiopia milioni moja lilishambulia Yuda. Akitambua kwamba adui walimzidi, Asa alisali: “BWANA, hapana kuliko wewe aliye wa kusaidia, kati yake yeye aliye hodari, na yeye asiye na nguvu; utusaidie, Ee BWANA, Mungu wetu; kwa kuwa sisi twakutegemea wewe, na kwa jina lako tumekuja juu ya jamii kubwa hii. Ee BWANA, wewe ndiwe Mungu wetu, asikushinde mwanadamu.” (2 Mambo ya Nyakati 14:11) Yehova alikubali maombi ya Asa na kumpa ushindi mkubwa.
5 Lakini, baada ya kutumikia kwa uaminifu kwa miaka mingi, uhakika wa Asa katika nguvu za Yehova za kuokoa ukadhoofika. Ili afanye ufalme wa kaskazini wa Israeli uache kumtisha kijeshi, yeye aliomba Siria msaada. (2 Mambo ya Nyakati 16:1-3) Ingawa alimhonga Mfalme wa Siria Ben-hadadi naye akafanya Israeli liache kutisha Yuda, agano la Asa pamoja na Siria lilionyesha kwamba alikosa uhakika katika Yehova. Nabii Hanani akamwuliza waziwazi: “Je! hao Wakushi na Walubi hawakuwa jeshi kubwa mno, wenye magari na wapanda farasi wengi sana? Lakini, kwa kuwa ulimtegemea BWANA, aliwatia mkononi mwako.” (2 Mambo ya Nyakati 16:7, 8) Hata hivyo, Asa alikataa karipio hilo. (2 Mambo ya Nyakati 16:9-12) Tunapokabili matatizo, tusitegemee masuluhisho ya wanadamu. Badala yake tuwe na hakika na Mungu, kwa sababu kuitibari nguvu za wanadamu bila shaka kutatutamausha.—Zaburi 146:3-5.
Tafuta Nguvu Ambazo Yehova Hutoav
6. Kwa nini tunapaswa ‘kumtafuta BWANA na nguvu yake’?
6 Yehova aweza kuwapa watu wake nguvu na kuwalinda. Biblia hutuhimiza “Tafuteni BWANA na nguvu yake.” (Zaburi 105:4, ZSB) Kwa nini? Kwa sababu tufanyapo mambo kwa nguvu za Mungu, tutatumia nguvu zetu kuwanufaisha wengine badala ya kuwadhuru. Mfano mzuri zaidi wa jambo hilo ni Yesu Kristo, ambaye alifanya miujiza akitumia “nguvu ya Yehova.” (Luka 5:17) Yesu angejitoa kufuatia utajiri, umashuhuri, au hata kuwa mfalme mwenye nguvu sana. (Luka 4:5-7) Badala yake, alitumia nguvu alizopewa na Mungu kuzoeza na kufundisha, kusaidia na kuponya watu. (Marko 7:37; Yohana 7:46) Huo ni mfano mzuri kama nini kwetu!
7. Tunasitawisha sifa gani muhimu tunapofanya mambo kwa nguvu za Mungu badala ya kutumia nguvu zetu wenyewe?
7 Na zaidi, tunapofanya mambo kwa “nguvu ambazo Mungu hutoa,” hilo litatusaidia kuwa wanyenyekevu. (1 Petro 4:11) Wanadamu ambao hutafuta nguvu kwa ajili yao wenyewe hujisifu. Mfano mmoja ni Mfalme wa Ashuru Esar-hadoni, ambaye alitangaza hivi kwa majisifu: “Nina nguvu, nina uweza wote, mimi ni shujaa, mimi ni mkubwa, mimi ni mkubwa mno.” Tofauti na hilo, Yehova “alivichagua vitu dhaifu vya ulimwengu, ili apate kuaibisha vitu vyenye nguvu.” Basi, ikiwa Mkristo wa kweli anajisifu, anajisifu katika Yehova, kwa kuwa anajua kwamba kile ambacho amefanya hakukitimiza kwa nguvu zake mwenyewe. ‘Kujinyenyekeza chini ya mkono wa Mungu wenye uweza’ kutafanya tupate utukuzo wa kweli.—1 Wakorintho 1:26-31; 1 Petro 5:6.
8. Tunapaswa kufanya nini kwanza ili tupokee nguvu za Yehova?
8 Tunaweza kupataje nguvu za Mungu? Kwanza, ni lazima tuombe nguvu hizo kupitia sala. Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba Baba yake angewapa roho takatifu wale wanaomwomba. (Luka 11:10-13) Fikiria jinsi roho hiyo ilivyowapa nguvu wanafunzi wa Kristo wakati walipoamua kumtii Mungu kuliko viongozi wa kidini ambao walikuwa wamewaamuru waache kutoa ushahidi juu ya Yesu. Waliposali wapate msaada wa Yehova, sala yao yenye kutoka moyoni ilijibiwa, na roho takatifu ikawapa nguvu za kuendelea kuhubiri habari njema kwa ujasiri.—Matendo 4:19, 20, 29-31, 33.
9. Taja chanzo cha pili cha nguvu za kiroho, na taja mfano mmoja wa Maandiko wa kuonyesha matokeo yake.
9 Pili, tunaweza kupata nguvu za kiroho katika Biblia. (Waebrania 4:12) Nguvu za neno la Mungu zilikuwa dhahiri wakati wa Mfalme Yosia. Ijapokuwa mfalme huyo wa Yuda tayari alikuwa ameondoa sanamu za kipagani katika nchi hiyo, kugunduliwa kwa Sheria ya Yehova bila kutarajiwa katika hekalu kulimchochea aendeleze hata zaidi mpango huo wa kuisafisha nchi.a Baada ya Yosia mwenyewe kuwasomea watu Sheria, taifa lote lilifanya agano pamoja na Yehova, na kampeni ya pili iliyokuwa kubwa zaidi ikaanzishwa dhidi ya ibada ya sanamu. Matokeo mazuri ya marekebisho yaliyofanywa na Yosia yakawa kwamba “siku zake zote hawakuacha kumfuata BWANA.”—2 Mambo ya Nyakati 34:33.
10. Ni ipi njia ya tatu ya kupata nguvu kutoka kwa Yehova, na kwa nini hiyo ni muhimu?
10 Jambo la tatu, tunapata nguvu kutoka kwa Yehova kupitia ushirika wa Kikristo. Paulo aliwatia moyo Wakristo wahudhurie mikutano kwa ukawaida ili “kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora” na kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25) Petro alipoachiliwa kimuujiza kutoka gerezani, alitaka kuwa pamoja na ndugu zake, hivyo akaenda moja kwa moja kwenye nyumba ya mamake Yohana Marko, ambako “watu wengi walikuwa wamekusanyika na wakisali.” (Matendo 12:12) Bila shaka hao wote wangebaki tu nyumbani kwao na kusali. Lakini waliamua kukutana pamoja ili kusali na kutiana moyo katika pindi hiyo ngumu. Safari ya Paulo ya kuelekea Roma ilipokaribia mwisho, alikutana na ndugu fulani katika Puteoli na baadaye akakutana na wengine waliokuwa wamesafiri kuja kumwona. Alifanya nini? “Alipowaona mara hiyo, Paulo akamshukuru Mungu na kujipa moyo.” (Matendo 28:13-15) Kuwa pamoja na Wakristo tena kulimwimarisha. Sisi pia hupata nguvu tunaposhirikiana na Wakristo wenzetu. Maadamu tuko huru na kuweza kushirikiana na wengine, tusijaribu kamwe kutembea peke yetu katika barabara iliyofinyana iongozayo kwenye uhai.—Mithali 18:1; Mathayo 7:14.
11. Taja baadhi ya hali ambazo “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” inahitajiwa hasa.
11 Kwa kusali kwa ukawaida, kujifunza Neno la Mungu, na kushirikiana na waamini wenzetu, sisi ‘huendelea kujipatia nguvu katika Bwana na katika uwezaji wa nguvu yake.’ (Waefeso 6:10) Bila shaka sisi sote twahitaji “nguvu katika Bwana.” Wengine wana magonjwa yenye kudhoofisha, wengine wanapatwa na madhara ya uzee au wengine wamepoteza mwenzi wao wa maisha. (Zaburi 41:3) Wengine huvumilia upinzani wa mwenzi asiyeamini. Wazazi, na hasa wazazi wasio na wenzi, huenda wakachoka sana kulea familia huku wakifanya kazi wakati wote. Vijana Wakristo wanahitaji nguvu za kukinza mkazo wa marika na kukataa kutumia dawa za kulevya na kukataa ukosefu wa maadili. Mtu yeyote asisite kumwomba Yehova ampe “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili kukabiliana na magumu kama hayo.—2 Wakorintho 4:7.
“Huwapa Nguvu Wazimiao”
12. Yehova hututegemezaje katika huduma ya Kikristo?
12 Na zaidi, Yehova huwapa nguvu watumishi wake wanapotimiza huduma yao. Twasoma hivi kwenye unabii wa Isaya: “Huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo. . . . Wamngojeao BWANA watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.” (Isaya 40:29-31) Mtume Paulo binafsi alipokea nguvu za kutimiza huduma yake. Huduma yake ikawa na matokeo. Paulo aliwaandikia hivi Wakristo katika Thesalonike: “Habari njema tuhubiriyo haikutokea miongoni mwenu kwa usemi pekee bali pia kwa nguvu na kwa roho takatifu.” (1 Wathesalonike 1:5) Mahubiri yake na mafundisho yake yalikuwa na nguvu za kufanya watu waliomsikiliza wafanye mabadiliko makubwa katika maisha yao.
13. Ni nini kilichomwimarisha Yeremia avumilie japo upinzani?
13 Tunapokabili roho ya kutojali katika eneo letu—eneo ambalo huenda tumehubiri kwa kurudia-rudia kwa miaka mingi bila matokeo mazuri—huenda tukavunjika moyo. Yeremia pia alivunjwa moyo na upinzani, dhihaka, na hali ya kutojali aliyopata. “Sitamtaja [Mungu], wala sitasema tena kwa jina lake,” akawaza. Lakini hangeweza kunyamaza. Ujumbe wake ulikuwa “kama moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa [yake].” (Yeremia 20:9) Ni nini kilichompa nguvu mpya za kukabili magumu mengi kama hayo? “BWANA yu pamoja nami, mfano wa shujaa mwenye kutisha,” akasema Yeremia. (Yeremia 20:11) Kutambua kwamba ujumbe na mgawo aliopewa na Mungu ulikuwa muhimu sana kulimfanya Yeremia aitikie kitia-moyo cha Yehova.
Nguvu za Kuumiza na Nguvu za Kuponya
14. (a) Ulimi ni kitu chenye nguvu kadiri gani? (b) Toa mifano ya kuonyesha jinsi ulimi uwezavyo kudhuru.
14 Nguvu zote tulizo nazo hazitokani moja kwa moja na Mungu. Kwa mfano, ulimi una nguvu za kuumiza na kuponya. “Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi,” aonya Solomoni. (Mithali 18:21) Matokeo ya mazungumzo mafupi baina ya Shetani na Hawa yaonyesha jinsi maneno yawezavyo kusababisha madhara makubwa. (Mwanzo 3:1-5; Yakobo 3:5) Sisi pia twaweza kusababisha madhara makubwa kwa ulimi wetu. Maneno yenye kuvunja moyo kuhusu unene wa msichana mdogo yaweza kumfanya awe na matatizo ya kukataa kula. Kurudia-rudia kuzungumzia uchongezi bila kufikiri kwaweza kuharibu urafiki wa muda mrefu. Ndiyo, kuna uhitaji wa kudhibiti ulimi.
15. Tunaweza kutumiaje ulimi wetu kujenga na kuponya?
15 Lakini, ulimi unaweza kujenga na vilevile kudhuru. Mithali ya Biblia yasema: “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; bali ulimi wa mwenye haki ni afya.” (Mithali 12:18) Wakristo wenye hekima hutumia nguvu za ulimi kuwafariji watu ambao wameshuka moyo na wale waliofiwa. Maneno yenye huruma yaweza kuwatia moyo vijana ambao wanapambana na mkazo wa marika wenye kudhuru. Ulimi unaotumiwa kwa uangalifu waweza kuwafariji ndugu na dada wazee kwamba bado wanahitajiwa na wanapendwa. Maneno yenye fadhili yaweza kuboresha siku za watu ambao ni wagonjwa. Zaidi ya yote, tunaweza kutumia ulimi wetu kuhubiria wote wanaosikiliza ujumbe wenye nguvu wa Ufalme. Tuna nguvu za kutangaza Neno la Mungu ikiwa moyo wetu unataka. Biblia yasema: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.”—Mithali 3:27.
Kutumia Nguvu Ifaavyo
16, 17. Wazee, wazazi, waume, na wake wanaweza kumwigaje Yehova wanapotumia mamlaka waliyopewa na Mungu?
16 Ingawa Yehova ni mweza yote, anatawala kutaniko lake kwa upendo. (1 Yohana 4:8) Kwa kumwiga, waangalizi Wakristo hutunza kundi la Mungu kwa upendo—wakitumia mamlaka yao vizuri, wala si vibaya. Ni kweli kwamba nyakati nyingine waangalizi wanahitaji ‘kukaripia, kukemea, na kuhimiza kwa bidii,’ lakini wao hufanya hivyo “kwa ustahimilivu wote na usanifu wa kufundisha.” (2 Timotheo 4:2) Basi wazee hutafakari daima maneno ya mtume Petro aliyowaandikia wale walio na mamlaka kutanikoni: “Lichungeni kundi la Mungu lililo katika utunzaji wenu, si kwa kushurutishwa, bali kwa nia ya kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu; wala si kama kwa kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali mwe vielelezo kwa kundi.”—1 Petro 5:2, 3; 1 Wathesalonike 2:7, 8.
17 Wazazi na waume pia wana mamlaka ambayo Yehova amewapa, na mamlaka hayo yapasa kutumiwa kusaidia, kukuza, na kuwatunza wengine. (Waefeso 5:22, 28-30; 6:4) Mfano wa Yesu waonyesha kwamba mamlaka yaweza kutumiwa vizuri kwa upendo. Nidhamu ikitolewa kwa usawaziko na kwa ukawaida, watoto hawatavunjika moyo. (Wakolosai 3:21) Ndoa huimarishwa wakati waume Wakristo wanapotumia ukichwa wao kwa upendo na wake kustahi sana ukichwa wa waume zao badala ya kupita mpaka wa madaraka waliyopewa na Mungu ili kudhibiti mambo au kupata mambo wanayotaka.— Waefeso 5:28, 33; 1 Petro 3:7.
18. (a) Tunaweza kuigaje mfano wa Yehova katika kudhibiti hasira yetu? (b) Wale wenye mamlaka wanapaswa kujaribu kuchochea nini katika wale walio chini ya usimamizi wao?
18 Wale ambao wana mamlaka katika familia na katika kutaniko wapaswa kuwa waangalifu hasa kudhibiti hasira yao, kwa kuwa hasira hufanya watu wawe na hofu badala ya upendo. Nabii Nahumu alisema: “BWANA si mwepesi wa hasira, ana uweza mwingi.” (Nahumu 1:3; Wakolosai 3:19) Kudhibiti hasira yetu ni ishara ya kwamba tuna nguvu, ilhali kufoka hasira ni uthibitisho wa udhaifu wetu. (Mithali 16:32) Iwe katika familia au kutanikoni, lengo ni kuchochea upendo—kumpenda Yehova, kupendana, na kupenda kanuni zifaazo. Upendo ndio kifungo chenye nguvu zaidi cha muungano na kichocheo chenye nguvu zaidi cha kufanya yaliyo sawa.—1 Wakorintho 13:8, 13; Wakolosai 3:14.
19. Yehova hutoa uhakikisho gani wenye kufariji, nasi twapaswa kuitikiaje?
19 Kumjua Yehova ni kutambua nguvu zake. Yehova alisema hivi kupitia Isaya: “Je! wewe hukujua? hukusikia? Yeye Mungu wa milele, BWANA, Muumba miisho ya dunia, hazimii, wala hachoki.” (Isaya 40:28) Nguvu za Yehova hazina kikomo. Tukimtegemea badala ya kujitegemea, hatatuacha. Anatuhakikishia hivi: “Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu.” (Isaya 41:10) Tunapaswa kuitikiaje utunzi wake wenye upendo? Kama Yesu, sikuzote na tutumie nguvu zozote zile ambazo Yehova anatupa ili kusaidia wengine na kuwajenga. Na tudhibiti ulimi wetu ili uponye badala ya kudhuru. Na sikuzote tubaki tukiwa macho kiroho, tusimame imara katika imani, na kuwa wenye uweza katika nguvu za Muumba wetu Mtukufu, Yehova Mungu.—1 Wakorintho 16:13.
[Maelezo ya Chini]
a Inaonekana Wayahudi waligundua nakala ya awali ya Sheria ya Musa iliyowekwa katika hekalu karne nyingi zilizotangulia.
-