-
Funzo Lina FaidaFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Jinsi ya Kujifunza
Badala ya kuanza moja kwa moja na fungu la 1 na kuendelea hadi mwisho, kwanza angalia funzo zima au sura nzima. Anza kwa kuchunguza maneno ya kichwa kikuu. Hilo ndilo jambo kuu la habari utakayojifunza. Kisha chunguza kwa makini jinsi vichwa vidogo vinavyohusiana na jambo kuu. Chunguza picha zozote zile, chati, au masanduku ya maswali ambazo zinaambatana na habari. Jiulize: ‘Nitarajie kujifunza nini kulingana na pitio hili la kimbele? Itanisaidia kwa njia gani?’ Kufanya hivyo hufanya funzo liwe na kusudi.
Fahamu vichapo vya kufanyia utafiti katika lugha unazofahamu
Sasa soma habari kamili. Funzo la Mnara wa Mlinzi na baadhi ya vitabu vina maswali yaliyochapishwa. Unaposoma kila fungu, inafaa kutia alama kwenye majibu. Hata kama hakuna maswali ya funzo, bado unaweza kutia alama mambo makuu ambayo unataka kukumbuka. Ukiona jambo ambalo ni jipya kwako, tumia muda zaidi kulichunguza ili uhakikishe umelielewa vizuri. Uwe macho kuona mifano au njia za kusababu ambazo zitakusaidia katika huduma ya shambani au ambazo unaweza kutumia katika hotuba utakayotoa. Fikiria watu fulani-fulani ambao imani yao inaweza kuimarishwa ukiwaeleza habari unayojifunza. Tia alama mambo ambayo unataka kutumia, na uyapitie tena unapomaliza kujifunza.
Unapojifunza, soma maandiko yaliyotajwa. Chunguza jinsi kila andiko linavyohusiana na mawazo ya fungu hilo.
Huenda ukapata mambo ambayo huyaelewi kwa urahisi au yale ambayo ungependa kuchunguza zaidi. Badala ya kuacha mambo hayo yakukengeushe, andika kifupi kwamba utayachunguza baadaye. Mara nyingi mambo hueleweka wazi unapoendelea kusoma habari hiyo. Kama sivyo, unaweza kufanya utafiti wa ziada. Unaweza kuandika mambo gani ili uyachunguze baadaye? Labda huelewi vizuri andiko fulani ambalo limenukuliwa. Au huenda usiweze kutambua mara moja jinsi linavyohusu habari inayozungumziwa. Labda unahisi kwamba unaelewa habari fulani lakini huielewi kwa kiasi cha kuweza kuwaelezea wengine. Badala ya kupuuza tu mambo hayo, huenda ikawa jambo la hekima kuyafanyia utafiti baada ya kumaliza kusoma.
Soma maandiko
Mtume Paulo alipowaandikia Wakristo Waebrania barua yenye mambo mengi, alitua katikati akasema: “Jambo kuu ni hili.” (Ebr. 8:1) Je, wewe hujikumbusha hivyo pindi kwa pindi? Ebu ona sababu iliyomfanya Paulo afanye hivyo. Katika sura zinazotangulia za barua yake iliyopuliziwa, tayari ameonyesha kwamba Kristo akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu aliye mkuu ameingia katika mbingu yenyewe. (Ebr. 4:14–5:10; 6:20) Lakini kwa kutenga jambo kuu na kulikazia mwanzoni mwa sura ya 8, Paulo alitayarisha akili za wasomaji ili wafikirie kwa uzito jinsi jambo hilo linavyohusu maisha yao. Alitaja kwamba Kristo alikuwa ametokea mbele ya Mungu kwa niaba yao na alikuwa amewafungulia njia ya kuingia “mahali patakatifu” mbinguni. (Ebr. 9:24; 10:19-22) Uhakika wa tumaini lao ungesaidia kuwafanya watumie mashauri mengine ya barua hii ambayo yanahusu imani, uvumilivu, na mwenendo wa Kikristo. Vivyo hivyo, kukazia akili mambo makuu tunapojifunza kutatusaidia kutambua jinsi kichwa kinavyofafanuliwa na kuingiza akilini mwetu sababu nzuri za kutenda kwa kupatana nayo.
Je, funzo lako la binafsi litakuchochea utende? Swali hili ni muhimu. Unapojifunza jambo, jiulize: ‘Jambo hili linahusuje mtazamo wangu na miradi yangu maishani? Naweza kutumiaje habari hii kusuluhisha tatizo, kufanya uamuzi, au kufikia mradi fulani? Naweza kuitumiaje habari hii katika familia, katika huduma ya shambani, na kutanikoni?’ Yafikirie maswali haya kwa njia ya sala, ukitafakari hali halisi za maisha ambazo katika hizo unaweza kutumia ujuzi huo.
Baada ya kumaliza sura moja au makala moja, pitia kwa ufupi habari uliyosoma. Je, unaweza kukumbuka mambo makuu na sababu zinazotolewa kuyathibitisha. Hiyo itakusaidia kukumbuka habari hiyo ukaitumie wakati ujao.
-