-
Furahia Kujifunza Kibinafsi Neno la MunguMnara wa Mlinzi—2002 | Desemba 1
-
-
Furahia Kujifunza Kibinafsi Neno la Mungu
“Nitaitafakari kazi yako yote; nitaziwaza habari za matendo yako.”—ZABURI 77:12.
1, 2. (a) Kwa nini tutenge wakati wa kutafakari? (b) Kutafakari kunamaanisha nini?
TUKIWA wanafunzi wa Yesu Kristo, mambo yaliyo muhimu zaidi kwetu ni uhusiano wetu pamoja na Mungu na sababu zinazofanya tumtumikie. Hata hivyo, leo, watu wengi wana shughuli nyingi mno hivi kwamba hawapati wakati wa kutafakari. Wanajishughulisha kabisa na ufuatiaji wa vitu vya kimwili, ununuzi wa bidhaa, na kufuatia anasa bila kusudi lolote. Tunawezaje kuepuka shughuli hizo zisizo na kusudi? Kama vile tunavyotenga wakati kila siku kufanya shughuli za lazima, kama kula na kulala, tunapaswa pia kutenga wakati kila siku kutafakari juu ya kazi na matendo ya Yehova.—Kumbukumbu la Torati 8:3; Mathayo 4:4.
2 Je, kuna wakati unapotulia na kutafakari? Kutafakari kunamaanisha nini? Kamusi ya Kiswahili Sanifu inafasiri neno -tafakari kuwa ‘kuzama katika fikira juu ya jambo fulani; kuwaza, kuzingatia.’ Kutafakari ni muhimu kadiri gani kwetu?
3. Kufanya maendeleo ya kiroho kunahusiana moja kwa moja na nini?
3 Kwanza, kutafakari kunapaswa kutukumbusha maneno ambayo mtume Paulo alimwandikia mtumishi mwenzake Timotheo: “Ninapokuwa nikija, endelea kujitahidi mwenyewe kusoma mbele ya watu wote, kuhimiza kwa bidii, kufundisha. . . . Fikiri kwa uzito juu ya mambo haya; vama katika hayo, ili kusonga mbele kwako kupate kuwa dhahiri kwa watu wote.” Naam, Timotheo alitarajiwa asonge mbele, nayo maneno ya Paulo yalionyesha kwamba kufikiri kwa uzito juu ya mambo ya kiroho kunahusiana moja kwa moja na kusonga mbele. Ndivyo ilivyo leo. Ili kupata uradhi unaotokana na kufanya maendeleo ya kiroho, lazima ‘tufikiri kwa uzito juu ya’ na ‘kuvama’ katika mambo yanayohusiana na Neno la Mungu.—1 Timotheo 4:13-15.
4. Ni vifaa gani unavyoweza kutumia ili vikusaidie kutafakari Neno la Yehova kwa ukawaida?
4 Wakati unaokufaa zaidi wa kutafakari hutegemea ratiba yako na ya familia yako. Wengi hutafakari juu ya andiko la Biblia asubuhi wanaposoma kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. Wajitoleaji wapatao 20,000 katika makao ya Betheli ulimwenguni pote huanza siku kwa kuzungumzia andiko la Biblia kwa muda wa dakika 15. Ingawa ni washiriki wachache wa Betheli ambao hutoa maelezo kila asubuhi, wengine hutafakari habari inayosemwa na kusomwa. Mashahidi wengine hutafakari juu ya Neno la Yehova wanaposafiri kuelekea kazini. Wao husikiliza kaseti za usomaji wa Biblia na za gazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ambazo hupatikana katika lugha fulani. Wake wengi wa nyumbani husikiliza usomaji huo wanapofanya kazi nyumbani. Kwa kweli, wanamwiga mtunga-zaburi Asafu, aliyeandika hivi: “Nitayakumbuka matendo ya BWANA; naam, nitayakumbuka maajabu yako ya kale. Pia nitaitafakari kazi yako yote; nitaziwaza habari za matendo yako.”—Zaburi 77:11, 12.
Mtazamo Unaofaa Huwa na Matokeo Mema
5. Kwa nini tuone funzo la kibinafsi kuwa muhimu?
5 Katika nyakati zetu za kisasa ambapo kuna televisheni, video, na kompyuta watu wengi hawasomi sana. Mashahidi wa Yehova hawapaswi kuwa hivyo. Kwa kweli, kusoma Biblia ni kama kamba ya kuokolea inayotuunganisha na Yehova. Maelfu ya miaka iliyopita, Yoshua alichukua mahali pa Musa kuwaongoza Waisraeli. Ili kupata baraka za Yehova, ilimbidi Yoshua asome Neno la Mungu. (Yoshua 1:8; Zaburi 1:1, 2) Tunatakiwa kufanya hivyo hata wakati huu. Hata hivyo, kwa sababu ya elimu ya chini, huenda watu fulani wakaona ugumu kusoma au wakachoshwa na kusoma. Kwa hiyo, ni nini kinachoweza kuchochea hamu yetu ya kusoma na kujifunza Neno la Mungu? Jibu linapatikana katika maneno ya Mfalme Solomoni kwenye andiko la Mithali 2:1-6. Tafadhali fungua Biblia yako na usome mistari hiyo. Kisha tutaizungumzia pamoja.
6. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuelekea kumjua Mungu?
6 Kwanza, tunahimizwa hivi: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; . . .” (Mithali 2:1, 2) Tunajifunza nini kutokana na maneno hayo? Kwamba kila mmoja wetu ana daraka la kujifunza Neno la Mungu. Ona sharti ambalo limewekwa hapa “kama ukiyakubali maneno yangu.” Sharti hilo ni muhimu kwa sababu watu wengi hawajishughulishi kusoma Neno la Mungu. Ili tupate shangwe ya kujifunza Neno la Mungu, lazima tuwe tayari kupokea maneno ya Yehova na kuyaona kama kitu chenye thamani kubwa hivi kwamba hatungependa kukipoteza. Hatupaswi kuruhusu shughuli zetu za kila siku au mambo fulani yatukengeushe fikira na hivyo tukose kupendezwa na Neno la Mungu, au hata kuwa na shaka nalo.—Waroma 3:3, 4.
7. Inapowezekana, kwa nini tunapaswa kuhudhuria na kusikiliza mikutano ya Kikristo?
7 Je, kweli ‘tunatega sikio’ na kusikiliza kwa makini wakati Neno la Mungu linapofafanuliwa katika mikutano yetu ya Kikristo? (Waefeso 4:20, 21) Je, ‘tunauelekeza moyo wetu’ ili tupate ufahamu? Labda msemaji hana uzoefu mwingi, lakini tunapaswa kumsikiliza kwa makini anapozungumzia Neno la Mungu. Bila shaka, ili kusikiliza hekima ya Yehova, lazima tuhudhurie mikutano ya Kikristo wakati wote inapowezekana. (Mithali 18:1) Hebu wazia jinsi mtu yeyote aliyekosa ule mkutano uliofanywa katika chumba cha juu huko Yerusalemu, Pentekoste 33 W.K. alivyovunjika moyo! Ingawa mikutano yetu si ya pekee kama mkutano huo, Biblia, ambayo ni kitabu chetu kikuu cha mafundisho, huzungumziwa. Kwa hiyo, tunaweza kunufaishwa kiroho na kila mkutano ikiwa tutasikiliza na kufungua maandiko yanayosomwa katika Biblia zetu.—Matendo 2:1-4; Waebrania 10:24, 25.
8, 9. (a) Tunapaswa kufanya nini kuhusiana na funzo la kibinafsi? (b) Ungetofautishaje dhahabu na kumjua Mungu?
8 Mfalme mwenye hekima aendelea kusema: “Naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu; . . .” (Mithali 2:3) Maneno hayo hufanya tuwe na mtazamo gani? Bila shaka, yanafanya tuwe na tamaa kubwa ya kuelewa Neno la Yehova! Yanadokeza nia ya kujifunza kwa kusudi la kupata ufahamu, kuelewa mapenzi ya Yehova. Bila shaka, jitihada inahitajiwa ili kufanya hivyo, kama inavyoonyeshwa na maneno na mfano ufuatao wa Solomoni.—Waefeso 5:15-17.
9 Aendelea kusema: “Ukiutafuta [ufahamu] kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; . . .” (Mithali 2:4) Hilo lafanya tufikirie mafanikio ambayo wachimba-migodi wamepata kwa karne nyingi wakitafuta madini yanayoitwa eti yenye thamani kama vile fedha na dhahabu. Watu wamewaua wengine kwa sababu ya dhahabu. Wengine wametumia maisha yao yote wakitafuta dhahabu. Hata hivyo, dhahabu ina thamani gani? Ikiwa ungepotea jangwani na una kiu kali sana, ungechagua nini: kipande cha dhahabu au kikombe cha maji? Hata hivyo, watu wametafuta dhahabu kwa bidii licha ya kwamba thamani yake ni ya kijuujuu tu na hubadilika-badilika!a Tunapaswa kujitahidi sana kutafuta hekima, ufahamu, na uelewevu wa mapenzi ya Mungu! Lakini tutapata manufaa gani kwa kutafuta mambo hayo?—Zaburi 19:7-10; Mithali 3:13-18.
10. Tunaweza kupata nini tukijifunza Neno la Mungu?
10 Solomoni aendelea hivi na maelezo yake: “Ndipo utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu.” (Mithali 2:5) Ni jambo la kushangaza kama nini—kwamba sisi wanadamu wenye dhambi tunaweza kupata ‘kumjua Yehova Mungu,’ Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu! (Zaburi 73:28; Matendo 4:24) Kwa karne nyingi wanafalsafa na wale wanaoitwa eti watu wenye hekima wa ulimwengu wamejaribu kuelewa mambo yenye kutatanisha kuhusu uhai na ulimwengu. Hata hivyo, wameshindwa “kumjua Mungu.” Kwa nini? Ingawa ujuzi huo umekuwako kwa maelfu ya miaka katika Neno la Mungu, Biblia, wanaikataa wakidai kwamba ina habari za kijuujuu tu na hivyo kukosa kuielewa.—1 Wakorintho 1:18-21.
11. Funzo la kibinafsi lina manufaa gani?
11 Solomoni akazia jambo jingine lenye kuchochea: “BWANA huwapa watu hekima; kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu.” (Mithali 2:6) Yehova hutoa hekima, ujuzi, na ufahamu bila malipo kwa yeyote aliye na nia ya kutafuta mambo hayo. Bila shaka, tuna sababu nzuri za kuthamini funzo la kibinafsi la Neno la Mungu, hata kama kufanya hivyo kutahitaji jitihada, nidhamu, na kujidhabihu. Angalau tuna Biblia zilizochapishwa na hatuhitaji kuandika nakala kwa mkono kama watu wa kale walivyofanya!—Kumbukumbu la Torati 17:18, 19.
Kutembea kwa Kumstahili Yehova
12. Tunapaswa kuwa na lengo gani tunapotafuta kumjua Mungu?
12 Tunapaswa kujifunza kibinafsi tukiwa na lengo gani? Je, tunajifunza ili tuonekane kuwa bora kuliko wengine? Je, ni ili tuonekane tuna ujuzi mwingi? Ni ili tuonekane kana kwamba tunajua kila kitu katika Biblia? La. Lengo letu linapaswa kuwa kujizoeza Ukristo kwa maneno na matendo, sikuzote tukiwa tayari kusaidia wengine, kwa kuiga mtazamo wenye kuburudisha wa Kristo. (Mathayo 11:28-30) Mtume Paulo alionya hivi: “Ujuzi hututumuka, lakini upendo hujenga.” (1 Wakorintho 8:1) Kwa hiyo, tunapaswa kuwa wanyenyekevu kama Musa wakati alipomwambia Yehova hivi: “Unionyeshe njia zako, nipate kukujua, ili nipate neema mbele zako.” (Kutoka 33:13) Naam, tunapaswa kutamani kuwa na ujuzi ili tumpendeze Mungu, si wanadamu. Tungependa kuwa watumishi wa Mungu walio wanyenyekevu na wanaostahili. Tunawezaje kutimiza mradi huo?
13. Ni nini kinachohitajiwa ili mtu awe mtumishi wa Mungu anayestahili?
13 Paulo alimshauri Timotheo hivi kuhusu jinsi ya kumpendeza Mungu: “Fanya yote uwezayo kabisa ili ujionyeshe mwenyewe kuwa mwenye kukubaliwa na Mungu, mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli.” (2 Timotheo 2:15) Usemi ‘kutumia sawasawa’ unatokana na kitenzi-ambatani cha Kigiriki ambacho hapo awali kilimaanisha “kukata kwa kunyooka.” (Kingdom Interlinear) Kulingana na wasomi fulani, usemi huo hudokeza wazo la fundi anayekata kitambaa kwa kufuata mshono fulani, au mkulima anayechimba mitaro, na kadhalika. Vyovyote vile, lazima kitambaa kinachokatwa au mtaro unaochimbwa uwe umenyooka. Jambo kuu ni kwamba ili Timotheo awe mtumishi wa Mungu aliyekubaliwa na anayestahili, alipaswa ‘kufanya yote awezayo’ ili kuhakikisha kwamba mafundisho na mwenendo wake ulipatana na neno la kweli.—1 Timotheo 4:16.
14. Funzo letu la kibinafsi linapaswa kuathirije maneno na matendo yetu?
14 Paulo alitaja jambo hilo alipowahimiza Wakristo wenzake huko Kolosai ‘watembee kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili’ kwa “kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.” (Wakolosai 1:10) Hapa Paulo anahusianisha kumstahili Yehova na “kuzaa matunda katika kila kazi njema” na vilevile “kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.” Yaani, jambo ambalo Yehova huliona kuwa muhimu si jinsi tunavyothamini ujuzi bali ni jinsi tunavyotii Neno lake kwa maneno na matendo. (Waroma 2:21, 22) Hii inamaanisha kwamba funzo letu la kibinafsi linapaswa kuathiri fikira zetu na mwenendo wetu iwapo tunataka kumpendeza Mungu.
15. Tunawezaje kulinda na kudhibiti akili na mawazo yetu?
15 Leo, Shetani ameazimia kuharibu hali yetu ya kiroho kwa kuchochea vita inayohusisha akili. (Waroma 7:14-25) Kwa hiyo, lazima tulinde na kudhibiti akili na mawazo yetu ili tustahili mbele za Yehova, Mungu wetu. Tuna silaha ya “ujuzi wa Mungu,” ambao unaweza ‘kuingiza kila fikira katika utekwa ili kuifanya iwe tiifu kwa Kristo.’ Hii ni sababu nyingine inayofanya tuzingatie kujifunza Biblia kila siku, kwa kuwa tunataka kuondoa mawazo ya ubinafsi na ya kimwili kutoka akilini mwetu.—2 Wakorintho 10:5.
Vifaa vya Kutusaidia Tupate Uelewevu
16. Tunaweza kupata manufaa gani kwa kufundishwa na Yehova?
16 Mafundisho ya Yehova hutokeza manufaa ya kiroho na ya kimwili. Si theolojia isiyopendeza na isiyoweza kutumika. Kwa hiyo, tunasoma hivi: “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.” (Isaya 48:17) Yehova hutusaidiaje tutembee katika njia yake inayonufaisha? Kwanza, tuna Neno lake lililoongozwa kwa roho, Biblia Takatifu. Hiki ndicho kitabu chetu kikuu cha mafundisho, tunachokisoma daima ili kupata msaada. Ndiyo sababu inafaa kusikiliza kwa makini na kusoma maandiko wakati wa mikutano ya Kikristo. Tunaweza kuona manufaa ya kufanya hivyo kutokana na simulizi la towashi Mwethiopia linalopatikana katika Matendo sura ya 8.
17. Ni nini kilichotokea kwa towashi Mwethiopia, na jambo hilo linatufunza nini?
17 Towashi Mwethiopia alikuwa amebadili imani yake akawa mfuasi wa Dini ya Kiyahudi. Alikuwa mwamini mnyofu wa Mungu, naye alijifunza Maandiko. Alikuwa akisafiri katika gari lake, huku akisoma andiko la Isaya wakati Filipo alipomfikia na kumwuliza: “Je, wewe kwa hakika wajua unayoyasoma?” Towashi alimjibuje? “‘Kwa kweli, ningewezaje kufanya hivyo, isipokuwa mtu fulani angeniongoza?’ Naye akamsihi Filipo kwa bidii apande na kuketi pamoja naye.” Kisha Filipo, akiongozwa na roho takatifu, akamsaidia towashi huyo aelewe unabii wa Isaya. (Matendo 8:27-35) Jambo hilo linatufunza nini? Kwamba haitoshi tu kujifunza Biblia kibinafsi. Yehova, kupitia roho yake, hutumia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara kutusaidia tuelewe Neno lake kwa wakati unaofaa. Anafanyaje hivyo?—Mathayo 24:45-47; Luka 12:42.
18. Jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara hutusaidiaje?
18 Ingawa jamii ya mtumwa inafafanuliwa kuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” Yesu hakusema kwamba mtumwa huyo hangeweza kukosea. Wakristo hao waaminifu waliotiwa mafuta si wakamilifu. Hata wanapokuwa na makusudi mazuri, wanaweza kueleweka vibaya, kama wenzao katika karne ya kwanza. (Matendo 10:9-15; Wagalatia 2:8, 11-14) Hata hivyo, wana nia safi, naye Yehova anawatumia kutuandalia vifaa vya kutusaidia kujifunza Biblia na kuimarisha imani yetu katika Neno la Mungu na ahadi zake. Kifaa kikuu ambacho mtumwa huyo ametupatia kwa ajili ya funzo la kibinafsi ni tafsiri ya New World Translation of the Holy Scriptures. Sasa inapatikana ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 42, na nakala milioni 114 zimechapishwa katika tafsiri mbalimbali. Tunaweza kuitumiaje kwa njia yenye matokeo tunapojifunza kibinafsi?—2 Timotheo 3:14-17.
19. Ni sehemu gani za tafsiri ya New World Translation—With References zinazoweza kutusaidia katika funzo la kibinafsi?
19 Kwa mfano, fikiria tafsiri ya New World Translation of the Holy Scriptures—With References. Ina safu za marejeleo yanayolingana, vielezi-chini, konkodansi ndogo ambayo imepangwa kama “Faharisi ya Maneno ya Biblia” na “Faharisi ya Vielezi-chini,” na Nyongeza yenye vichwa na habari mbalimbali 43, kutia ndani ramani na chati. Pia kuna “Utangulizi,” wenye maelezo kuhusu vichapo mbalimbali vilivyotumiwa katika tafsiri hii ya pekee ya Biblia. Iwapo inapatikana katika lugha unayoweza kuelewa, jitahidi kadiri uwezavyo kufahamu sehemu hizo na kuzitumia. Vyovyote vile, tunapaswa kuanza programu yetu ya funzo kwa kujifunza Biblia, na tafsiri ya New World Translation, hukazia ifaavyo jina la Mungu na utawala wa Ufalme wa Mungu.—Zaburi 149:1-9; Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10.
20. Ni maswali gani kuhusu funzo la kibinafsi yanayohitaji kujibiwa sasa?
20 Sasa, huenda tukauliza: ‘Ni msaada gani zaidi tunaohitaji ili kuielewa Biblia? Tunawezaje kupata wakati wa kujifunza kibinafsi? Tunawezaje kufanya funzo letu liwe lenye matokeo zaidi? Funzo letu linapaswa kuwaathirije wengine?’ Makala inayofuata itazungumzia mambo hayo muhimu yanayohusu maendeleo yetu ya Kikristo.
[Maelezo ya Chini]
a Tangu mwaka wa 1979 thamani ya dhahabu imeshuka kutoka dola za Marekani 850.00 kwa gramu 31 mwaka wa 1980 hadi dola za Marekani 252.80 kwa gramu 31 mwaka wa 1999.
-
-
Funzo la Kibinafsi Ambalo Hutuandaa Kuwa Walimu BoraMnara wa Mlinzi—2002 | Desemba 1
-
-
Funzo la Kibinafsi Ambalo Hutuandaa Kuwa Walimu Bora
“Fikiri kwa uzito juu ya mambo haya; vama katika hayo, ili kusonga mbele kwako kupate kuwa dhahiri kwa watu wote. Daima kaza uangalifu kwako mwenyewe na kwa kufundisha kwako.”—1 TIMOTHEO 4:15, 16.
1. Ukweli ni nini kuhusu wakati na funzo la kibinafsi?
“KWA kila jambo kuna majira yake,” yasema Biblia katika andiko la Mhubiri 3:1. Bila shaka, hilo lahusu pia funzo la kibinafsi. Wengi huona vigumu kutafakari mambo ya kiroho wakati usiofaa au mahali pasipofaa. Kwa mfano, baada ya kufanya kazi ngumu na kula chakula kingi jioni, je, utataka kujifunza, hasa iwapo umejinyoosha kwenye kiti chako cha kustarehe ukitazama televisheni? La. Kwa hiyo suluhisho ni nini? Bila shaka, tunapaswa kuchagua mahali na wakati wa kujifunza tukiwa na kusudi la kunufaika kikamili na funzo letu.
2. Ni wakati upi unaofaa zaidi kufanya funzo la kibinafsi?
2 Wengi huona kwamba wakati unaofaa zaidi kujifunza ni asubuhi na mapema wakati akili yao inapokuwa chonjo. Wengine hujifunza kwa muda mfupi wakati wa mapumziko ya mchana. Ona wakati unaotajwa wa kufanya mambo muhimu ya kiroho katika mifano inayofuata. Mfalme Daudi wa Israeli la kale aliandika hivi: “Unifanye kusikia fadhili zako asubuhi, kwa maana nimekutumaini Wewe. Unijulishe njia nitakayoiendea, kwa maana nakuinulia nafsi yangu.” (Zaburi 143:8) Nabii Isaya alionyesha uthamini kama huo aliposema: “Bwana MUNGU amenipa ulimi wa hao wafundishwao, nipate kujua jinsi ya kumtegemeza kwa maneno yeye aliyechoka, huniamsha asubuhi baada ya asubuhi; huniamsha, sikio langu lipate kusikia kama watu wafundishwao.” Jambo kuu ni kwamba tunapaswa kujifunza na kuwasiliana na Yehova kindani wakati akili zetu ziko chonjo, hata iwe ni saa ngapi.—Isaya 50:4, 5; Zaburi 5:3; 88:13.
3. Ni hali zipi zinazofaa ili kunufaika na funzo?
3 Jambo jingine linalofanya funzo liwe lenye matokeo ni kutoketi katika kiti chenye kustarehesha sana. Hatuwezi kuwa chonjo tukifanya hivyo. Tunapojifunza, akili yetu inapaswa kuwa chonjo, na hatuwezi kuwa chonjo iwapo tumestarehe sana. Pia inafaa kuwa mahali patulivu pasipo na vikengeusha-fikira ili kujifunza na kutafakari. Huwezi kunufaika na funzo iwapo fikira zako zinakengeushwa na redio, televisheni, au watoto. Yesu alipotaka kutafakari, alienda mahali patulivu. Pia alitaja umuhimu wa kutafuta mahali pa faragha ili kusali.—Mathayo 6:6; 14:13; Marko 6:30-32.
Funzo la Kibinafsi Ambalo Hutuandaa Kujibu Maswali
4, 5. Broshua Anataka inasaidia katika njia gani?
4 Funzo la kibinafsi huridhisha tunapotumia vichapo mbalimbali vinavyoifafanua Biblia ili kufanya utafiti zaidi kuhusu habari fulani, hasa tunapofanya hivyo ili kujibu maswali ambayo mtu ameuliza kwa unyofu. (1 Timotheo 1:4; 2 Timotheo 2:23) Wapya wengi huanza kwa kujifunza broshua Mungu Anataka Tufanye Nini?,a ambayo sasa hupatikana katika lugha 261. Ni kichapo rahisi kueleweka lakini sahihi, nacho kinategemea kabisa Biblia. Kinasaidia wasomaji waelewe upesi matakwa ya Mungu kuhusu ibada ya kweli. Hata hivyo, kwa kuwa hiyo ni broshua, haiwezekani kuzungumzia kila habari kindani. Ikiwa mwanafunzi wako wa Biblia auliza maswali kwa unyofu kuhusu habari fulani za Biblia, utapata wapi habari zaidi itakayomsaidia kujibu maswali hayo?
5 Wale ambao wana Watchtower Library kwenye CD-ROM katika lugha yao, wanaweza kupata habari nyingi kwenye kompyuta. Lakini namna gani wale ambao hawana kifaa hiki? Na tuchunguze masomo mawili katika broshua Anataka ili tuone jinsi tunavyoweza kuzidisha uelewevu wetu na kuweza kujibu kindani zaidi—hasa mtu anapouliza, Mungu ni nani? na kwa kweli Yesu alikuwa mtu wa aina gani?—Kutoka 5:2; Luka 9:18-20; 1 Petro 3:15.
Mungu Ni Nani?
6, 7. (a) Ni swali gani linalotokea kumhusu Mungu? (b) Kasisi mmoja alifanya kosa gani kubwa alipokuwa akitoa hotuba?
6 Somo la 2 katika broshua Anataka hujibu swali hili muhimu, Mungu Ni Nani? Hili ni fundisho muhimu kwa sababu mtu hawezi kumwabudu Mungu wa kweli ikiwa Hamjui au ikiwa labda anatilia shaka kuwepo Kwake. (Waroma 1:19, 20; Waebrania 11:6) Hata hivyo, watu ulimwenguni pote wana maoni mbalimbali kuhusu Mungu. (1 Wakorintho 8:4-6) Kila dini hutoa jibu tofauti kuhusu Mungu ni nani. Dini nyingi zinazojiita eti za Kikristo huamini kwamba Mungu ni Utatu. Kasisi mmoja mashuhuri huko Marekani alitoa hotuba iliyokuwa na kichwa “Je, Unamjua Mungu?” lakini hakutaja jina la Mungu hata kidogo katika hotuba yake, licha ya kwamba alinukuu Maandiko ya Kiebrania mara kadhaa. Bila shaka, alikuwa akisoma tafsiri ya Biblia inayotumia neno “Bwana” ambalo ni neno lililo na maana nyingi na si jina la mtu binafsi badala ya kutumia jina Yehova au Yahweh.
7 Kasisi huyo alikosa kuona jambo muhimu sana aliponukuu andiko la Yeremia 31:33, 34: “Wala hawatamfundisha kila mtu jirani yake, na kila mtu ndugu yake, wakisema, Mjue BWANA [Kiebrania, “Mjue Yehova”]; kwa maana watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema BWANA [Kiebrania, Yehova].” Tafsiri aliyotumia haikutaja jina Yehova, linalomtambulisha Mungu.—Zaburi 103:1, 2.
8. Ni nini kinachoonyesha umuhimu wa kutumia jina la Mungu?
8 Andiko la Zaburi 8:9, NW linaonyesha kwa nini ni muhimu sana kutumia jina la Yehova: “Ee Yehova Bwana wetu, jina lako ni lenye utukufu kama nini katika dunia yote!” Linganisha tafsiri hiyo na: “Ee BWANA, Bwana wetu, jina lako ni lenye utukufu duniani mwote!” (Zaire Swahili Bible) Hata hivyo, kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, tunaweza kupata “kumjua Mungu” tukiruhusu Neno lake lituelimishe. Lakini ni kifaa gani cha kujifunzia Biblia kitakachojibu maswali yetu moja kwa moja kuhusu umuhimu wa jina la Mungu?—Mithali 2:1-6.
9. (a) Ni kichapo gani kinachoweza kutusaidia kueleza umuhimu wa kutumia jina la Mungu? (b) Watafsiri wengi wamekosaje kuonyesha heshima kwa jina la Mungu?
9 Tunaweza kupata msaada katika broshua Jina la Mungu Litakaloendelea Milele, ambayo imetafsiriwa katika lugha 69.b Sehemu yenye kichwa “Jina la Mungu—Maana Yalo na Linavyotamkwa” (ukurasa wa 6-11) inaonyesha waziwazi kwamba ile Tetragramatoni ya Kiebrania (Tetragramatoni inamaanisha “herufi nne” katika Kigiriki) inapatikana karibu mara 7,000 katika maandishi ya awali ya Kiebrania. Hata hivyo, makasisi na watafsiri wa Dini ya Kiyahudi na dini zinazojiita eti za Kikristo wameliondoa kimakusudi katika tafsiri zao za Biblia.c Wanawezaje kudai kwamba wanamjua Mungu na wawe na uhusiano mzuri pamoja naye ikiwa hawataki kumwita kwa jina lake? Jina lake la kweli husaidia watu waelewe makusudi yake na utu wake. Zaidi ya hayo, ile sehemu katika sala ya kielelezo ya Yesu “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako litakaswe” ina thamani gani ikiwa jina la Mungu halitumiwi?—Mathayo 6:9; Yohana 5:43; 17:6.
Yesu Kristo Ni Nani?
10. Tunawezaje kupata habari kamili kuhusu maisha na huduma ya Yesu?
10 Somo la 3 katika broshua Anataka lina kichwa “Yesu Kristo Ni Nani?” Katika mafungu sita tu, inatoa muhtasari mfupi kuhusu Yesu, mwanzo wake, na kusudi lake la kuja duniani. Hata hivyo, mbali na vitabu vya Injili unaweza pia kupata habari kamili kuhusu maisha yake katika kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi ambacho kinapatikana katika lugha 111.d Kitabu hiki kinatoa habari kamili kwa kufuata utaratibu wa miaka na matukio kuhusu maisha na mafundisho ya Kristo, kupatana na zile Injili nne. Sura zake 133 zinazungumzia maisha na huduma ya Yesu. Ukitaka habari inayochanganua kindani Yesu Kristo, unaweza kusoma kitabu Insight, Buku la 2, chini ya kichwa “Jesus Christ.”
11. (a) Imani ya Mashahidi wa Yehova kuhusu Yesu inatofautianaje na ya wengine? (b) Ni maandiko gani ya Biblia ambayo hupinga fundisho la Utatu waziwazi, na ni kichapo gani ambacho hutusaidia kuelewa habari hiyo?
11 Katika dini zinazojiita eti za Kikristo kuna ubishi wa kama Yesu ni “Mwana wa Mungu” na vilevile “Mungu Mwana”—yaani, ubishi ambao kichapo Catechism of the Catholic Church huuita “fumbo kuu la imani ya Kikristo,” Utatu. Mashahidi wa Yehova ambao ni tofauti na dini zinazojiita eti za Kikristo wanaamini kwamba Yesu aliumbwa na Mungu, naye si Mungu. Maelezo mazuri sana kuhusu habari hii yanapatikana katika broshua Je, Uamini Utatu?, ambayo imetafsiriwa katika lugha 95.e Baadhi ya maandiko mengi ambayo yametumiwa katika broshua hiyo kupinga fundisho la Utatu ni Marko 13:32 na 1 Wakorintho 15:24, 28.
12. Ni swali gani jingine tunalopaswa kulifikiria?
12 Habari iliyotajwa juu kuhusu Mungu na Yesu Kristo inaonyesha njia mbalimbali tunazoweza kutumia kufanya funzo la kibinafsi tukiwa na kusudi la kusaidia wale ambao hawafahamu kweli ya Biblia wapate ujuzi sahihi. (Yohana 17:3) Hata hivyo, namna gani wale ambao wamekuwa wakishirikiana na kutaniko la Kikristo kwa miaka mingi? Kwa kuwa wana ujuzi mwingi wa Biblia, je, bado wanahitaji kujifunza Neno la Yehova kibinafsi?
Kwa Nini ‘Tukaze Uangalifu Daima’?
13. Ni maoni gani yasiyofaa ambayo huenda watu wengine wakawa nayo kuhusu funzo la kibinafsi?
13 Huenda wengine ambao wamekuwa washiriki wa kutaniko kwa miaka mingi wakawa na zoea la kutegemea tu ujuzi wa Biblia waliopata miaka michache ya kwanza wakiwa Mashahidi wa Yehova. Ni rahisi mtu kuwaza hivi: “Si lazima nijifunze kwa bidii kama wapya. Kwani, kwa miaka mingi nimeisoma Biblia na vichapo vinavyozungumzia Biblia mara nyingi.” Hii ingekuwa sawa na kusema: “Kwa kweli sihitaji kukazia uangalifu sana kiasi cha chakula ninachokula sasa, kwani nimekula mara nyingi sana muda uliopita.” Tunajua kwamba mwili unapaswa kulishwa kwa ukawaida chakula kinachofaa, kilichopikwa vizuri, ili uwe na nguvu na afya. Tunapaswa kufanya vivyo hivyo iwapo tunataka kuendelea kuwa wenye afya na nguvu kiroho.—Waebrania 5:12-14.
14. Kwa nini tunapaswa kukaza uangalifu daima kwetu wenyewe?
14 Kwa hiyo, sisi sote, tuwe tumejifunza Biblia kwa muda mrefu au la, tunahitaji kutii shauri la Paulo kwa Timotheo, ambaye wakati huo alikuwa mwangalizi aliyekomaa kiroho: “Kaza uangalifu kwako mwenyewe na kwa kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivi utajiokoa wewe mwenyewe na wale wakusikilizao pia.” (1 Timotheo 4:15, 16) Kwa nini tuzingatie sana shauri la Paulo? Kumbuka, pia kwamba Paulo alisema tuna pigano dhidi ya “mbinu [“matendo ya hila”] za Ibilisi” na “dhidi ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” Naye mtume Petro alionya kwamba Ibilisi ‘anatafuta sana kunyafua mtu fulani,’ na ‘mtu’ huyo anaweza kuwa yeyote kati yetu. Anaweza kupata fursa ya kutushambulia iwapo hatujali hatari hiyo.—Waefeso 6:11, 12; 1 Petro 5:8.
15. Ni kinga gani ya kiroho tuliyo nayo, nasi tunaweza kuidumishaje?
15 Kwa hiyo, tuna kinga gani? Mtume Paulo anatukumbusha hivi: “Chukueni suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu, ili mpate kuweza kukinza katika siku ya uovu na, baada ya nyinyi kuwa mmefanya mambo yote kikamili, kusimama imara.” (Waefeso 6:13) Ili suti hiyo kamili ya silaha itukinge, tunapaswa kuitunza kwa ukawaida badala ya kuiachilia katika hali yake ya awali. Kwa hiyo, suti hiyo kamili ya silaha kutoka kwa Mungu lazima itie ndani ujuzi wa sasa kutoka kwa Neno la Mungu. Hilo lakazia umuhimu wa kwenda sambamba na uelewevu wa ile kweli ambao Yehova hufunua kupitia Neno lake na kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Ili tudumishe suti yetu ya silaha kamili za kiroho, tunapaswa kujifunza Biblia kwa ukawaida pamoja na vichapo vinavyozungumzia Biblia.—Mathayo 24:45-47; Waefeso 6:14, 15.
16. Tunaweza kufanya nini ili tuhakikishe kwamba “ngao [yetu] kubwa ya imani” imetunzwa vizuri?
16 Paulo anakazia sehemu muhimu ya silaha zetu za ulinzi “ngao kubwa ya imani,” inayoweza kutusaidia kuzuia na kuzima mishale yenye moto ya Shetani ambayo ni mashtaka bandia na mafundisho ya waasi-imani. (Waefeso 6:16) Kwa hiyo ni muhimu kuchunguza ngao yetu ya imani ina nguvu kadiri gani na ni hatua gani tunazopaswa kuchukua ili kuitunza na kuiimarisha. Kwa mfano, huenda ukajiuliza: ‘Ninatayarishaje funzo la Biblia la kila juma kwa kutumia Mnara wa Mlinzi? Je, nimejifunza vya kutosha kuweza ‘kuwachochea wengine kwenye upendo na kazi zilizo bora’ kwa kutoa majibu yaliyofikiriwa vizuri wakati wa mkutano? Je, mimi hufungua Biblia na kusoma maandiko yaliyotajwa tu bila kunukuliwa? Je, ninawatia moyo wengine kwa kutoa maelezo kwa shauku?’ Chakula chetu cha kiroho ni kigumu, na kinahitaji kusagwa ifaavyo ili tunufaike kikamili.—Waebrania 5:14; 10:24.
17. (a) Shetani anatumia sumu gani kudhoofisha hali yetu ya kiroho? (b) Dawa ya sumu ya Shetani ni nini?
17 Shetani anajua udhaifu wetu sisi wanadamu wasio wakamilifu, naye hutumia mbinu za hila. Mojawapo ya mbinu anazotumia kueneza uvutano wake mwovu ni kufanya ponografia (picha na habari chafu) ipatikane kwa urahisi kwenye televisheni, Internet, video, na vichapo. Wakristo fulani wameruhusu sumu hiyo ipenye na kuwadhoofisha, na imefanya wapoteze mapendeleo kutanikoni au hata kupatwa na madhara mabaya zaidi. (Waefeso 4:17-19) Dawa ya sumu hiyo ya Shetani ni nini? Hatupaswi kuacha kujifunza Biblia kwa ukawaida, wala mikutano yetu ya Kikristo, na suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu. Mambo hayo yote hutupatia uwezo wa kutofautisha kati ya mema na mabaya na kuchukia mambo ambayo Mungu huchukia.—Zaburi 97:10; Waroma 12:9.
18. “Upanga wa roho” unaweza kutusaidiaje katika vita yetu ya kiroho?
18 Tukiendelea kujifunza Biblia kwa ukawaida, ujuzi sahihi wa Neno la Mungu utatupatia nguvu za kujikinga, na pia tutafanikiwa kufanya mashambulizi tukitumia “upanga wa roho, yaani, neno la Mungu.” Neno la Mungu ni “lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili na hudunga hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na uloto wavyo, na ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.” (Waefeso 6:17; Waebrania 4:12) Tukiwa stadi katika kutumia “upanga,” huo basi tunapokabili vishawishi, tutaweza kutambua waziwazi mambo ambayo huenda yakaonekana kuwa hayana madhara, au hata yanayoonekana kuwa yenye kuvutia, na kuyaona kuwa mtego wa waovu unaoweza kusababisha kifo. Ujuzi wa Biblia pamoja na uelewevu tulio nao utatusaidia kukataa maovu na kutenda mema. Kwa hiyo sote tunapaswa kujiuliza: ‘Je, upanga wangu ni mkali, au una kutu? Je, mimi huona ni vigumu kukumbuka maandiko ya Biblia yanayoweza kunipa nguvu za kushambulia?’ Na tudumishe mazoea mazuri ya kujifunza Biblia kibinafsi na hivyo kumpinga Ibilisi.—Waefeso 4:22-24.
19. Tunaweza kupata manufaa gani kwa kujifunza kibinafsi kwa bidii?
19 Paulo aliandika hivi: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.” Tukizingatia maneno ambayo Paulo alimwambia Timotheo, tunaweza kuimarisha hali yetu ya kiroho na kufanya huduma yetu iwe yenye matokeo zaidi. Wazee na watumishi wa huduma wanaweza kunufaisha sana kutaniko, na sisi sote tunaweza kudumu tukiwa thabiti katika imani.—2 Timotheo 3:16, 17; Mathayo 7:24-27.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa kawaida, mtu mwenye kupendezwa anayejifunza broshua Anataka atajifunza kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, baada ya kumaliza broshua hiyo. Vichapo vyote viwili vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova. Madokezo yaliyotolewa hapa yatasaidia kuondoa mambo yoyote yanayoweza kumzuia mtu asifanye maendeleo ya kiroho.
b Kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova. Wale ambao wana kitabu Insight on the Scriptures katika lugha yao wanaweza kutazama Buku la 2, chini ya kichwa, “Jehovah.”
c Baadhi ya tafsiri za Kiswahili zinatumia Tetragramatoni za Kiebrania “Yahweh” na “Yehova.”
d Imechapishwa na Mashahidi wa Yehova.
e Imechapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-