-
Kuwaelimisha WasikilizajiFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Huenda hotuba unayotoa ina maandiko ambayo wasikilizaji wanayajua. Utatumiaje maandiko hayo kwa njia inayoelimisha? Yafafanue badala ya kuyasoma tu.
Maandiko kama hayo yanaweza kuelimisha ikiwa unayafafanua sehemu-sehemu, ukitenga sehemu zinazohusiana na hotuba yako na kuzifafanua. Ebu ona jinsi unavyoweza kufafanua andiko kama Mika 6:8 katika Biblia ya Union Version. “Haki” ni nini? Tunazungumzia kanuni ya nani ya haki? Unawezaje kuonyesha maana ya “kutenda haki”? Au maana ya “kupenda rehema”? Unyenyekevu ni nini? Unawezaje kutumia habari hii kumhusu mtu aliye mzee kwa umri? Bila shaka habari ambazo utatumia zinategemea mambo kama kichwa kikuu cha hotuba, kusudi la hotuba, wasikilizaji, na wakati uliowekewa.
Ni vizuri kufafanua mambo kwa njia rahisi. Watu wengine hushangaa kujifunza maana ya “ufalme” unaotajwa katika Mathayo 6:10. Ufafanuzi wa jambo hata unaweza kumsaidia Mkristo wa zamani kufahamu vizuri maana ya andiko fulani. Jambo hili ni wazi unaposoma 2 Petro 1:5-8 na kufafanua sifa zinazotajwa katika mistari hiyo: imani, wema wa adili, ujuzi, kujidhibiti, uvumilivu, ujitoaji-kimungu, shauku ya kidugu, na upendo. Ikiwa maneno yanayofanana yanatumiwa katika muktadha uleule, unaweza kuyafafanua ili kutofautisha maana ya neno moja na jingine. Ndivyo ilivyo kuhusu maneno kama hekima, maarifa, ufahamu, na busara ambayo yametumiwa katika Mithali 2:1-6.
Unaweza kuwaelimisha wasikilizaji ukisababu nao kuhusiana na andiko. Watu wengi hushangaa wanapotambua kwa mara ya kwanza kwamba katika tafsiri nyingine za Biblia Mwanzo 2:7 inasema Adamu ni nafsi hai na kwamba Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible, inaonyesha nafsi hufa. Pindi moja, Yesu aliwashangaza Masadukayo aliporejelea Kutoka 3:6, ambalo Masadukayo walidai kuamini, kisha akaliunganisha na ufufuo wa wafu.—Luka 20:37, 38.
Nyakati nyingine inasaidia kuonyesha muktadha wa andiko, hali zilizokuwako wakati wa kuliandika, na kumtaja msemaji au msikilizaji anayetajwa katika andiko hilo. Mafarisayo walifahamu vizuri Zaburi 110. Lakini bado Yesu aliwafundisha jambo fulani muhimu katika mstari wa kwanza. Yesu aliwauliza: “‘Nyinyi mwafikiri nini juu ya Kristo? Yeye ni mwana wa nani?’ Wakamwambia: ‘Wa Daudi.’ Akawaambia: ‘Basi, ni jinsi gani, kwamba Daudi kwa upulizio amwita yeye “Bwana,” akisema, “Yehova alimwambia Bwana wangu: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwekapo maadui wako chini ya miguu yako’”? Kwa hiyo, ikiwa Daudi humwita yeye “Bwana,” ni jinsi gani yeye ni mwana wake?’” (Mt. 22:41-45) Ukisababu kutokana na Maandiko kama Yesu, utawasaidia watu kusoma Neno la Mungu kwa makini zaidi.
Msemaji akitaja wakati kitabu fulani cha Biblia kilipoandikwa au wakati tukio fulani lilipotokea, anapaswa pia kufafanua hali zilizokuwako wakati huo. Kwa njia hiyo, wasikilizaji wataelewa kwa urahisi zaidi umuhimu wa kitabu hicho au tukio hilo.
Kulinganisha mambo kunaweza kufanya jambo unalosema lielimishe. Unaweza kulinganisha mambo ambayo watu wanapenda na maoni ya Biblia. Au unaweza kulinganisha masimulizi mawili ya Biblia yanayolingana. Je, kuna mambo yanayotofautiana katika masimulizi hayo? Kwa nini? Tunajifunza nini katika masimulizi hayo? Ukilinganisha mambo unaweza kuwasaidia wasikilizaji waione habari hiyo kwa njia mpya.
-
-
Kuwaelimisha WasikilizajiFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Unapochunguza maandiko yaliyo katika hotuba yako, jiulize, ‘Kwa nini habari hii imehifadhiwa katika Maandiko hadi siku zetu?’ (Rom. 15:4; 1 Kor. 10:11) Fikiria hali za maisha za wasikilizaji. Fikiria hali hizo ukitumia shauri na kanuni za Maandiko. Katika hotuba yako, sababu kwa kutumia Maandiko ili kuonyesha jinsi kanuni hizo zinavyoweza kumsaidia mtu kutenda kwa hekima katika hali hizo. Usitaje mambo kwa ujumla. Zungumzia hali na matendo hususa.
-