-
Je, Unahitaji Wakati Zaidi?Amkeni!—2010 | Aprili
-
-
Je, Unahitaji Wakati Zaidi?
IKIWA umetia alama jibu la pili au la tatu katika maswali mengi yaliyotajwa, huenda basi unahitaji wakati zaidi. Lakini si wewe tu. Kila mahali watu wanashinikizwa kufanya mambo wanayopaswa kufanya, na huenda mambo hayo yasiwe ya maana sana kwao. Badala yake, huenda mambo hayo yakawa yale ambayo lazima yafanywe wakati huo kama vile, kurekebisha gari, kufanya kazi ambazo mwajiri anataka ufanye, na kushughulikia mambo ambayo hayakuwa yametazamiwa. Unaposhughulikia jambo moja baada ya lingine, huenda ukahisi kwamba huwezi kudhibiti jinsi unavyotumia wakati wako. Huenda hata ukahisi kwamba maisha yako yanapita kwa kasi bila wewe kuyafurahia.
Bila shaka, huenda unajiambia haya ni mambo ya muda tu. Mwishowe, hali itatulia na utakuwa na wakati mwingi zaidi wa kukazia fikira mambo unayoona kuwa ya maana zaidi, mambo ambayo yatafanya maisha yako, ya familia yako, na ya wengine yawe na kusudi na yenye kuridhisha. Lakini hali itatulia wakati gani? Je, utapata wakati leo? Juma hili? Mwezi ujao?
Kusema kweli, hatutazamii pilkapilka za dunia zipungue. Lakini unaweza kuchukua hatua zitakazokusaidia kupata wakati zaidi. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani?
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Ni mara ngapi unapata wakati wa kufanya mambo unayoona kuwa muhimu zaidi?
◯ Kila siku
◯ Mwisho wa juma
◯ Ni vigumu sana
Katika siku ya kawaida, je,
◯ Unafanya kila kitu ulichopangia kufanya?
◯ Wewe hufuata ratiba hususa ambayo inakuzuia kufanya mambo uliyojipangia?
◯ Wewe hufanya chochote kinachotokea hata kama hukuwa umepangia?
Katika siku ya kawaida, je, wewe huhisi
◯ Unaweza kudhibiti mambo yanayotukia katika maisha yako?
◯ Unashinikizwa kutimiza mambo usiyoweza kutimiza?
◯ Unaharakisha kufanya jambo moja baada ya lingine?
Siku inapoisha, je,
◯ Umetimiza mambo muhimu?
◯ Umemaliza kazi uliyopaswa kufanya, ingawa hukuifanya vizuri?
◯ Hukupata wakati wa kufanya mambo ya maana zaidi?
Wewe huhisije mwishoni mwa siku?
◯ Umeridhika na umekamilisha kila kitu
◯ Hukutimiza chochote, umechoka, na una wasiwasi
◯ Umekata tamaa
-
-
Jinsi ya Kutumia Wakati Wako VizuriAmkeni!—2010 | Aprili
-
-
Jinsi ya Kutumia Wakati Wako Vizuri
“Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu.”—Mhubiri 3:1.
ILI uweze kupata wakati wa kufanya mambo ya maana, lazima ufahamu hayo ni mambo gani. Itakuwa rahisi kufanya hivyo ukitambua tofauti kati ya mambo ambayo ni muhimu zaidi kwako, miradi yako, na utendaji ambao utakusaidia kufikia miradi hiyo.
Kwanza, tambua mambo muhimu zaidi kwako. Jaribu kuandika mambo hayo. Yanaweza kutia ndani familia, marafiki, kazi, elimu, mafanikio, sura nzuri, pesa, furaha, ndoa, fadhili, afya nzuri ya kimwili na ya kiroho. Kisha jiulize, ‘Kati ya mambo haya ni gani yaliyo ya maana zaidi kwangu?’
Baada ya hapo fikiria miradi yote unayotaka kutimiza maishani. Kuna tofauti gani kati ya mambo unayoona kuwa ni muhimu na miradi yako? Katika habari hii, tutasema kwamba mambo yaliyo muhimu zaidi kwako hudumu, ilhali mradi hukamilika na unaanza mingine.
Unaweza kujiwekea miradi gani? Je, ungependa kutumia wakati zaidi pamoja na familia yako? Je, ungependa kupata kazi nzuri zaidi? Je, ungependa kuboresha ustadi wako wa kufanya jambo fulani unalopenda au kuanza kufanya jambo jipya? Je, ungependa kusitawisha sifa fulani? Je, ungependa kwenda likizo, kusoma, au kuandika kitabu?
Kisha, amua ni miradi gani ambayo ni muhimu zaidi kwako. Hakikisha kwamba miradi hiyo inapatana na mambo unayoona kuwa muhimu. Kwa mfano, ikiwa umejiwekea mradi wa kuwa tajiri sana, huenda mradi huo utapingana na mambo muhimu kwako.
Fikiria utendaji kadhaa ambao unaweza kukusaidia kufikia kila mradi. Kwa mfano, ikiwa umejiwekea mradi wa kupunguza uzito, kufanya mazoezi kunaweza kukusaidia kufanya hivyo.
Kuandika Kutakusaidia Jinsi Gani?
Ikiwa miradi yako inapatana na mambo unayoona kuwa muhimu zaidi na unafanya mambo yanayoweza kukusaidia kutimiza miradi yako, maisha yako yatakuwa yenye kuridhisha. Utaona kwamba unatumia wakati mwingi zaidi kufanya mambo ambayo ni ya maana kwako. Bila shaka, hilo halimaanishi eti upuuze mahitaji na mapendezi ya wengine. (Wafilipi 2:4) Linamaanisha kwamba utaweza kutambua na kuepuka mambo ambayo si ya maana kwako.
Kwa kweli, kutakuwa na magumu. Huenda mambo fulani yasiwe muhimu lakini lazima yafanywe. Huenda mambo hayo yakachukua sehemu kubwa ya siku yako na kufanya ukose wakati wa kufanya mambo ya maana zaidi kwako. Hali za dharura zinaweza kutukia. Na hali zako maishani zinaweza kubadilika na kuvuruga ratiba yako. Utafanya nini? Lakini unapotumia wakati mwingi zaidi kufanya mambo ya maana, utaona kwamba unadhibiti zaidi wakati na maisha yako.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]
JE, VIFAA VYA ELEKTRONIKI VINAOKOA WAKATI?
Vinawasaidia watu fulani kuokoa wakati lakini vinawafanya wengine wapoteze wakati. Kwa mfano, kifaa cha elektroniki kinachomsaidia mtu kupanga mambo yake ya kibinafsi kinachoitwa PDA, ni kama kompyuta ndogo iliyo na kalenda, orodha ya namba za simu na anwani, orodha ya mambo ya kufanya, kamera, programu inayoweza kuandika na kuhifadhi habari, kutuma barua-pepe na kukuunganisha kwenye Intaneti. Kifaa hicho kinaweza kukusaidia kuokoa wakati ikiwa utakuwa ukiweka habari za karibuni zaidi na kukibeba kila wakati. Hata hivyo, unaweza kupoteza wakati kwa urahisi ukiingia kwenye Intaneti bila kusudi, ukibadili-badili programu, ukinunua-nunua vitu usivyohitaji, au kuruhusu kifaa hicho kivuruge mahusiano au majukumu muhimu kwako.
Dokezo: Fanya utafiti kabla ya kununua kifaa chochote. Ikiwa kifaa kinaharibika kila wakati, utatumia muda mwingi kukirekebisha. Pia, kifaa kitakufaa ikiwa tu unajua kukitumia. Kwa hiyo, ikiwa una kifaa cha elektroniki, kitumie kuokoa wakati, si kuupoteza.
[Picha katika ukurasa wa 4, 5]
Je, unaweza kutenga wakati wa kufanya mambo ya maana kwako?
-
-
Mbinu 20 za Kutafuta Wakati ZaidiAmkeni!—2010 | Aprili
-
-
Kata na Uhifadhi
Mbinu 20 za Kutafuta Wakati Zaidi
“Endeleeni kutembea kwa hekima . . . , mkijinunulia wakati unaofaa.”—Wakolosai 4:5.
BAADA ya kutambua utendaji unaotaka kufanya, changamoto ni kutafuta mbinu ya kutimiza mambo hayo. Madokezo yafuatayo yanaweza kukusaidia kufanya hivyo.
1 KILA SIKU ANDIKA MAMBO UNAYOTAKA KUTIMIZA. Orodhesha mambo kulingana na yale unayotaka kutimiza kwanza. Tia alama mambo utakayohitaji kutumia wakati mwingi zaidi. Tia alama unapomaliza kuyafanya. Tia mambo unayoshindwa kumaliza kwenye orodha ya siku inayofuata.
2 HAKIKISHA KUWA KALENDA ZAKO ZINAPATANA. Usikose kufanya jambo muhimu kwa sababu hukuliandika katika kalenda zako zote. Ikiwa unatumia kalenda iliyo ndani ya kompyuta yako na nyingine katika kifaa cha elektroniki cha kubeba mkononi, hakikisha kwamba zote zinapatana.
3 ANDIKA “MIKAKATI” itakayotia ndani kila hatua ya jambo unalotaka kufanya, na uzipange katika mpangilio unaofaa.
4 PANGIA MAMBO MUHIMU KWANZA. Itakuwa rahisi kupata wakati wa kufanya mambo yasiyo muhimu.
5 JIWEKEE MIRADI AMBAYO UNAWEZA KUTIMIZA. Una uwezo wa kuboresha stadi zako za kazi, lakini huna uwezo wa kuamua ikiwa utakuwa msimamizi wa kampuni.
6 TAMBUA KWAMBA HUTAPATA WAKATI WA KUFANYA KILA KITU. Chagua kufanya mambo yatakayoleta matokeo bora. Vipi kuhusu mambo ambayo yanapaswa kushughulikiwa haraka au ambayo lazima yafanywe tu? Ikiwa hayawezi kuepukwa au kufanywa na mtu mwingine, jaribu kutumia muda mfupi iwezekanavyo kuyafanya. Mambo fulani yasiyo muhimu yanaweza kusubiri kwa miezi kadhaa ikiwezekana, au si lazima yafanywe. Tenga wakati mwingi iwezekanavyo ili ufanye mambo unayoona kuwa ni muhimu zaidi na yanayopatana na miradi yako.
7 ORODHESHA JINSI UNAVYOTUMIA WAKATI WAKO. Andika orodha ya mambo unayofanya kwa juma moja au mawili ili ujue jinsi unavyotumia wakati wako. Je, unapoteza wakati mwingi kwa kufanya mambo yasiyo muhimu? Je, kila wakati shughuli zako huvurugwa na mtu au watu walewale? Je, shughuli zako huvurugwa wakati fulani hususa katika siku au juma? Achana na mambo yanayopoteza wakati wako.
8 RATIBU MAMBO MACHACHE ZAIDI. Huenda ukahisi kwamba unaharakishwa na huenda usifurahie chochote ikiwa utapangia katika siku ileile kununua chakula, kurekebisha gari, kualika wageni, kuona sinema, na kusoma.
9 PUNGUZA MAMBO YANAYOVURUGA SHUGHULI ZAKO. Tenga wakati fulani kila siku ambao hutavurugwa isipokuwa iwe lazima kabisa. Ikiwezekana, zima simu yako wakati huo. Pia, zima programu zozote za kompyuta zinazotokeza habari ghafula kwenye kiwambo chako ikiwa zinavuruga kazi yako.
10 PANGIA KUFANYA KAZI NGUMU ZAIDI WAKATI AMBAPO UNAJUA UNA NGUVU ZAIDI NA UNAWEZA KUWA MAKINI.
11 FANYA KAZI ISIYOPENDEZA ZAIDI HARAKA IWEZEKANAVYO. Unapomaliza kazi hiyo, utajihisi una nguvu za kufanya kazi rahisi zaidi.
12 TENGA WAKATI KWA AJILI YA MAMBO YASIYOTAZAMIWA. Ukihisi unaweza kufika mahali fulani katika muda wa dakika 15, ahidi kwamba utafika baada ya dakika 25. Ukijua kwamba mkutano fulani utachukua saa zima, pangia kutumia saa moja na dakika 20. Tenga wakati fulani wa siku ambao hujapangia kufanya chochote.
13 FANYA JAMBO FULANI UNAPOSUBIRI. Sikiliza habari au rekodi fulani unaponyoa ndevu. Soma huku ukisubiri treni au unaposafiri. Bila shaka, unaweza kutumia wakati huo kupumzika. Lakini usiupoteze kisha baadaye ulalamike kwamba huna wakati.
14 RAHISISHA KAZI. Je, mambo 2 kati ya 10 ndiyo muhimu zaidi katika orodha yako? Ukifanya ile sehemu muhimu ya kazi fulani, je, utakuwa umeikamilisha kazi yote?
15 UNAPOHISI UMELEMEWA NA KAZI, andika kila kazi kwenye kadi ndogo. Kisha gawa kadi hizo katika vikundi hivi viwili: “Mambo ya Kufanya Leo” na “Mambo ya Kufanya Kesho.” Kesho inapofika fanya vivyo hivyo.
16 PUMZIKA MARA KWA MARA UPATE NGUVU TENA. Kurudi kazini ukiwa umetulia kiakili na kimwili kunaweza kunufaisha zaidi kuliko kufanya kazi ya ziada kwa saa nyingi.
17 ANDIKA MAWAZO YAKO. Andika tatizo, fafanua kwa nini linakutatiza, na uorodheshe njia zote za kulisuluhisha unazoweza kufikiria.
18 USITAZAMIE UKAMILIFU. Tambua wakati wa kuacha jambo fulani na kuanza lingine.
19 FANYA KAZI KAMA MTAALAMU. Usisubiri wakati unajihisi vizuri. Anza kufanya kazi mara moja.
20 BADILIKANA NA HALI. Haya ni mapendekezo, si sheria kali. Jaribu mbinu mbalimbali, tambua zile zinazokufaa, na ujaribu kuzitumia.
-
-
Kutafuta Wakati kwa Ajili ya Mambo MuhimuAmkeni!—2010 | Aprili
-
-
Kutafuta Wakati kwa Ajili ya Mambo Muhimu
“Wakati uliobaki umepungua.”—1 Wakorintho 7:29.
“KURUKARUKA na kupigapiga maji hakumaanishi unajua kuogelea,” akaandika Michael LeBoeuf katika kitabu chake Working Smart.
Kwa maneno mengine, kuna tofauti kati ya kutimiza jambo na kulifanya tu. Fikiria utendaji wako wa juma lililopita. Ulitenga wakati wako ili ufanye nini? Ni nini ambacho hukuweza kufanya kwa kuwa ulikuwa na shughuli nyingi? Je, unaona uhitaji wa kutenga wakati zaidi kufanya mambo unayoona kuwa muhimu zaidi?
-